Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Upendo hutuchochea kutanguliza mahitaji ya wengine badala ya mahitaji yetu

Jinsi ya Kuwaonyesha Wengine Upendo

Jinsi ya Kuwaonyesha Wengine Upendo

Tukiwa wazao wa mwanadamu wa kwanza Adamu, sisi sote ni familia moja. Ingawa washiriki wa familia wanapaswa kupendana na kuheshimiana, leo ni vigumu kupata upendo wa aina hiyo. Mungu wetu mwenye upendo anataka tupendane.

MAANDIKO MATAKATIFU YANASEMA NINI KUHUSU UPENDO?

“Ni lazima umpende mwenzako kama unavyojipenda mwenyewe.”​—MAMBO YA WALAWI 19:18.

“Endeleeni kuwapenda adui zenu.”​—MATHAYO 5:44.

KUWAPENDA WANADAMU WENZETU KUNAMAANISHA NINI?

Chunguza jinsi Mungu anavyofafanua upendo katika Neno lake kwenye 1 Wakorintho 13:4-7:

“Upendo ni wenye subira na fadhili.”

Fikiria jambo hili: Wewe utahisije ikiwa wengine wanakutendea kwa subira na fadhili na hawakasiriki unapofanya makosa?

“Upendo hauna wivu.”

Fikiria jambo hili: Unahisije wengine wanapokutilia shaka kupita kiasi au wanakuonea wivu?

Upendo “hautafuti faida zake wenyewe.”

Fikiria jambo hili: Unahisije wengine wanapoheshimu maoni yako na sikuzote wako tayari kukubali maoni ya wengine?

Upendo “hauweki hesabu ya ubaya.”

Fikiria jambo hili: Mungu yuko tayari kutusamehe ikiwa tumetenda dhambi na kutubu kikweli. “Hatatafuta makosa sikuzote, wala hataendelea kuwa na hasira.” (Zaburi 103:9) Sisi tunafurahi sana tunapoona mtu tuliyemkosea anatusamehe. Hivyo, tunapaswa kuwa tayari kuwasamehe wengine wanapotukosea.​—Zaburi 86:5.

Upendo “haushangilii ukosefu wa uadilifu.”

Fikiria jambo hili: Tunapopatwa na mambo mabaya, hatungependa wengine wafurahie. Hivyo, hatushangilii wengine wanapopatwa na mambo mabaya, hata ikiwa watu hao walitukosea.

Ili tupate baraka za Mungu, tunapaswa kuwapenda wengine licha ya umri wao, nchi yao, au dini yao. Njia moja ya kuonyesha tunawapenda wengine ni kuwasaidia wanapopatwa na matatizo.