Kutoka 3:1-22

  • Musa na kichaka cha miiba kilichowaka moto (1-12)

  • Yehova aeleza maana ya jina Lake (13-15)

  • Yehova ampa Musa maagizo (16-22)

3  Musa akawa mchungaji wa kondoo wa Yethro,+ baba mkwe wake, kuhani wa Midiani. Alipokuwa akiwaongoza kondoo kuelekea upande wa magharibi wa nyika, hatimaye alifika kwenye mlima wa Mungu wa kweli ulioitwa Horebu.+  Kisha malaika wa Yehova akamtokea katika mwali wa moto katikati ya kichaka cha miiba.+ Musa alipoendelea kutazama, aliona kwamba kichaka hicho cha miiba kilikuwa kikiwaka moto, lakini hakikuteketea.  Basi Musa akasema: “Nitaenda kuchunguza jambo hili la ajabu, nione kwa nini kichaka kile cha miiba hakiteketei.”  Yehova alipoona akienda kukitazama, Mungu akamwita kutoka katika kichaka cha miiba: “Musa! Musa!” naye akajibu: “Mimi hapa.”  Akamwambia: “Usikaribie zaidi. Vua viatu vyako, kwa sababu mahali unaposimama ni ardhi takatifu.”  Akaendelea kusema: “Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Abrahamu,+ Mungu wa Isaka,+ na Mungu wa Yakobo.”+ Ndipo Musa akauficha uso wake, kwa sababu aliogopa kumtazama Mungu wa kweli.  Kisha Yehova akasema: “Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walio Misri, nami nimesikia kilio chao kwa sababu ya wale wanaowalazimisha kufanya kazi; ninajua vema maumivu yao.+  Nitashuka huko ili niwaokoe kutoka mikononi mwa Wamisri+ na kuwapandisha kutoka katika nchi hiyo na kuwapeleka katika nchi nzuri na kubwa, nchi inayotiririka maziwa na asali,+ eneo la Wakanaani, Wahiti, Waamori, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi.+  Sasa tazama! Kilio cha Waisraeli kimenifikia, nami nimeona pia jinsi Wamisri wanavyowakandamiza kwa ukatili.+ 10  Sasa njoo, nitakutuma kwa Farao, nawe utawatoa watu wangu Waisraeli kutoka Misri.”+ 11  Hata hivyo, Musa akamwambia Mungu wa kweli: “Mimi ni nani hata niende kwa Farao na kuwatoa Waisraeli nchini Misri?” 12  Mungu akamwambia: “Nitathibitika kuwa pamoja nawe,+ na hii ndiyo ishara itakayoonyesha kwamba ni mimi niliyekutuma: Baada ya kuwatoa Waisraeli nchini Misri, ninyi mtanitumikia* mimi, Mungu wa kweli, kwenye mlima huu.”+ 13  Lakini Musa akamwambia Mungu wa kweli: “Tuseme niende kwa Waisraeli na kuwaambia, ‘Mungu wa mababu zenu amenituma kwenu,’ nao waniulize, ‘Jina lake ni nani?’+ Niwaambie nini?” 14  Basi Mungu akamwambia Musa: “Nitakuwa Kile Ninachochagua* Kuwa.”*+ Kisha akasema: “Hivi ndivyo unavyopaswa kuwaambia Waisraeli, ‘Nitakuwa amenituma kwenu.’”+ 15  Tena Mungu akamwambia Musa: “Hivi ndivyo unavyopaswa kuwaambia Waisraeli, ‘Yehova Mungu wa mababu zenu, Mungu wa Abrahamu,+ Mungu wa Isaka,+ na Mungu wa Yakobo,+ amenituma kwenu.’ Hilo ndilo jina langu milele,+ na hivyo ndivyo ninavyopaswa kukumbukwa kizazi baada ya kizazi. 16  Sasa nenda, uwakusanye wazee wa Israeli na kuwaambia, ‘Yehova Mungu wa mababu zenu amenitokea, Mungu wa Abrahamu, Isaka, na Yakobo, naye alisema: “Hakika nimewatazama+ na nimeona mambo mnayotendewa nchini Misri. 17  Kwa hiyo ninasema, nitawatoa katika mateso+ mnayopata mikononi mwa Wamisri na kuwapeleka katika nchi ya Wakanaani, Wahiti, Waamori,+ Waperizi,+ Wahivi, na Wayebusi, nchi inayotiririka maziwa na asali.”’+ 18  “Hakika wataisikiliza sauti yako,+ nawe utaenda, wewe pamoja na wazee wa Israeli, kwa mfalme wa Misri, nanyi mnapaswa kumwambia: ‘Yehova Mungu wa Waebrania+ amewasiliana nasi. Kwa hiyo, tafadhali, turuhusu tusafiri kwa siku tatu nyikani ili tumtolee Yehova Mungu wetu dhabihu.’+ 19  Lakini mimi mwenyewe ninajua vema kwamba mfalme wa Misri hatawaruhusu kwenda asipolazimishwa kwa mkono wenye nguvu.+ 20  Kwa hiyo nitalazimika kuunyoosha mkono wangu na kuipiga Misri kwa matendo yangu yote ya ajabu nitakayofanya nchini humo, kisha atawaruhusu mwondoke.+ 21  Nami nitawafanya watu hawa wapate kibali machoni pa Wamisri, nanyi mtakapoondoka, hamtaondoka kamwe mikono mitupu.+ 22  Kila mwanamke anapaswa kumwomba jirani yake na mwanamke anayeishi nyumbani mwake vito vya fedha na vya dhahabu na pia mavazi, nanyi mtawavika wana wenu na mabinti wenu; nanyi mtachukua mali za Wamisri.”+

Maelezo ya Chini

Au “mtaniabudu.”
Au “Nitathibitika Kuwa Kile Nitakachothibitika Kuwa.” Angalia Nyongeza A4.
Au “Ninachotaka.”