Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Praslin, Shelisheli, mahali ambapo Jenerali Gordon alipata bustani yake ya Edeni mwaka wa 1881

Paradiso Duniani​—Je, Ni Jambo Halisi au la Kuwaziwa tu?

Paradiso Duniani​—Je, Ni Jambo Halisi au la Kuwaziwa tu?

Paradiso! Broshua zenye kupendeza zinazoonyesha maeneo mazuri ya kutembelea hutushawishi twende kwenye maeneo hayo yanayofanana na “paradiso,” ili tukapumzike na kusahau matatizo na mahangaiko yetu yote. Hata hivyo, kama tujuavyo, tunaporudi nyumbani mambo huwa vilevile tulivyoyaacha.

Ingawa hivyo, bado tunasisimuka sana tunapofikiria kuhusu paradiso. Hilo hufanya tujiulize: ‘Je, “paradiso” ni jambo la kuwaziwa tu? Ikiwa ndivyo, kwa nini linawasisimua watu wengi? Na je, kweli kutawahi kuwa na paradiso?’

HADITHI KUHUSU PARADISO

Kwa karne nyingi, wazo la paradiso limewapendeza watu. Wengi wao walianza kufikiria kuhusu paradiso waliposoma simulizi la Biblia kuhusu “bustani katika Edeni, kuelekea mashariki.” Ni nini kilifanya bustani hiyo ivutie sana? Simulizi hilo linasema hivi: “Yehova Mungu akachipusha katika nchi kila mti wenye kutamanika kwa macho ya mtu na ulio mwema kwa ajili ya chakula.” Bustani hiyo ilikuwa ni mahali pazuri na yenye kupendeza. Zaidi ya yote, kulikuwa “pia [na] mti wa uzima katikati ya bustani na mti wa ujuzi wa mema na mabaya.”​—Mwanzo 2:​8, 9.

Kwa kuongezea, simulizi la Mwanzo linataja mito minne iliyotoka katika bustani hiyo. Mito miwili kati ya hiyo inafahamika hadi leo hii. Mito hiyo ni Tigri (au, Hidekeli) na Efrati. (Mwanzo 2:​10-​14) Mito hiyo miwili inamwaga maji yake kwenye Ghuba ya Uajemi kupitia eneo ambalo lilikuwa sehemu ya milki ya kale ya Uajemi na sasa ni nchi ya Iraki.

Kwa kufaa, wazo la dunia paradiso ni sehemu ya utamaduni wa Uajemi. Zulia la Uajemi la karne ya 16, lililohifadhiwa kwenye Jumba la Sanaa la Makumbusho la Philadelphia huko Pennsylvania, nchini Marekani, lina picha ya bustani iliyozungushiwa ukuta, ambayo ina miti na maua. Maana nyingine ya neno la Kiajemi linalotafsiriwa “bustani iliyozungushiwa ukuta,” ni “paradiso,” na picha iliyo kwenye zulia hilo inafanana na simulizi la Biblia kuhusu bustani ya Edeni iliyokuwa nzuri na maridadi.

Hadithi kuhusu paradiso zinasimuliwa katika lugha na tamaduni nyingi duniani kote. Kadiri wanadamu walivyohamia maeneo mbalimbali duniani, walienda na habari kuhusu bustani ya awali ya Edeni, na hivyo, hatua kwa hatua ikawa sehemu ya imani na hekaya zilizositawi katika maeneo yao. Hadi leo, baadhi ya watu wana mazoea ya kuita maeneo yenye kuvutia sana, paradiso.

KUITAFUTA PARADISO

Baadhi ya wavumbuzi walidai kwamba wameipata paradiso iliyopotea. Kwa mfano, jenerali wa jeshi la Uingereza, Charles Gordon, alipotembelea visiwa vya Shelisheli mwaka wa 1881, alivutiwa sana na mandhari maridadi ya Vallée de Mai, eneo ambalo sasa ni moja ya maeneo yanayostahili Kuhifadhiwa Ulimwenguni, na kusema kwamba eneo hilo ndio bustani ya Edeni. Katika karne ya 15, baharia Mwitaliano Christopher Columbus alihisi kwamba ameipata bustani ya Edeni alipowasili kwenye kisiwa cha Hispaniola, ambacho sasa ni eneo la Jamhuri ya Dominika na Haiti.

Kitabu cha kisasa cha historia, Mapping Paradise, kinataja kuhusu ramani zaidi ya 190 za kale, na nyingi kati ya ramani hizo zinawaonyesha Adamu na Hawa wakiwa Edeni. Kati ya hizo kuna ramani ya pekee kutoka kwenye nakala ya hati ya karne ya 13 ya Beatus wa Liébana. Katika sehemu ya juu ya ramani hiyo kuna kisanduku kidogo ambacho katikati yake kuna paradiso. Mito minne inayoitwa “Tigri,” “Efrati,” “Pishoni,” na “Gihoni” inatoka kwenye paradiso hiyo, kila mmoja ukipita kwenye pembe moja kati ya zile nne za kisanduku hicho, huenda kuashiria jinsi ambavyo Ukristo ulienea katika pembe nne za dunia. Picha kama hizo zinaonyesha kwamba ingawa mahali hususa ambapo Paradiso ya awali ilikuwa hapajulikani, bado watu huwazia picha maridadi kuihusu.

Mshairi wa Uingereza wa karne ya 17, John Milton, anafahamika sana kwa shairi lake Paradise Lost (Paradiso Iliyopotea) linalotegemea simulizi la kitabu cha Mwanzo kuhusu dhambi ya Adamu na kufukuzwa kwake Edeni. Katika shairi hilo alitaja kuhusu ahadi ya wanadamu kurudishiwa uzima wa milele duniani, na kusema hivi: “Kwa maana wakati huo dunia yote itakuwa Paradiso.” Baadaye, Milton aliandika sehemu ya pili ya shairi hilo iliyokuwa na kichwa Paradise Regained (Paradiso Iliyorudishwa).

MTAZAMO UMEBADILIKA

Ni wazi kwamba, katika historia yote ya wanadamu, watu wamevutiwa na habari kuhusu paradiso. Hivyo basi, kwa nini jambo hilo limepuuzwa? Kama kitabu Mapping Paradise kinavyoonyesha, sababu kuu ni kwamba “wanatheolojia . . . wamelifumbia macho kimakusudi suala la mahali ilipokuwa paradiso.”

Waumini wengi wa makanisa wanafundishwa kwamba hatma ya wanadamu ni kuishi mbinguni, na si katika dunia paradiso. Hata hivyo, Biblia inasema hivi katika andiko la Zaburi 37:29: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” Kwa kuwa dunia si paradiso leo, ni nini kinachoweza kututhibitishia kwamba ahadi hiyo itatimizwa? *

TUMAINI LA DUNIA PARADISO NI HAKIKA

Yehova Mungu, ambaye aliiumba Paradiso ya awali, ameahidi kuirudisha. Jinsi gani? Kumbuka kwamba Yesu alitufundisha tusali: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:​10) Ufalme huo ni serikali ya ulimwenguni pote inayotawaliwa na Yesu Kristo ambayo itachukua mahali pa tawala zote za wanadamu. (Danieli 2:​44) Chini ya utawala wa Ufalme huo, mapenzi ya Mungu kuhusu dunia paradiso ‘yatatendeka.’

Nabii Isaya aliongozwa na roho ya Mungu kueleza hali zitakavyokuwa katika Paradiso iliyoahidiwa, wakati ambapo misuguano na migogoro yote inayowakabili wanadamu leo haitakuwepo. (Isaya 11:​6-9; 35:​5-7; 65:​21-​23) Tunakutia moyo utenge dakika chache usome Maandiko hayo kwenye Biblia yako. Kufanya hivyo kutakusaidia uamini mambo ambayo Mungu amepanga kuwafanyia wanadamu watiifu. Wale watakaoishi wakati huo watafurahia paradiso na kibali cha Mungu, mambo ambayo Adamu alipoteza.​—Ufunuo 21:3.

Kwa nini tuna uhakika kwamba tumaini la dunia Paradiso ni halisi na si jambo la kuwaziwa tu? Kwa sababu Biblia inasema hivi: “Mbingu ni mbingu za Yehova, bali dunia amewapa wana wa binadamu.” Tumaini la Paradiso duniani ni jambo ambalo “Mungu, asiyeweza kusema uwongo, aliahidi nyakati za zamani za kale.” (Zaburi 115:16; Tito 1:2) Naam, Biblia inatupatia tumaini zuri kwelikweli la Paradiso!

^ fu. 15 Inapendeza pia kwamba Kurani inasema hivi kwenye mstari wa 105 wa sura ya 21, Al-Anbiya’ [Manabii]: “Wale walio waadilifu kati ya watumishi Wangu watairithi dunia.”