Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 12

Kazi Yetu ya Kuhubiri Ufalme Hufanywaje?

Kazi Yetu ya Kuhubiri Ufalme Hufanywaje?

Hispania

Belarus

Hong Kong

Peru

Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alisema: “Habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Lakini kazi hiyo ya kuhubiri ulimwenguni pote ingetimizwa jinsi gani? Ingetimizwa kwa kufuata kielelezo ambacho Yesu aliweka alipokuwa duniani.—Luka 8:1.

Tunajitahidi kuhubiri nyumba kwa nyumba. Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kuhubiri habari njema nyumba kwa nyumba. (Mathayo 10:11-13; Matendo 5:42; 20:20) Wanafunzi hao walipewa maeneo hususa ya kuhubiri. (Mathayo 10:5, 6; 2 Wakorintho 10:13) Vivyo hivyo leo, kazi yetu ya kuhubiri inafanywa kwa utaratibu, na kila kutaniko huwa na eneo lake la kuhubiri. Utaratibu huo hutuwezesha kutimiza amri ya Yesu ya ‘kuwahubiria watu na kutoa ushahidi kamili.’—Matendo 10:42.

Tunajitahidi kuwafikia watu mahali popote walipo. Yesu alituwekea mfano kwa kuwahubiria watu katika maeneo mbalimbali yenye watu wengi kama vile kwenye ufuo wa bahari au kisimani. (Marko 4:1; Yohana 4:5-15) Sisi pia huzungumza na watu kuhusu Biblia popote walipo—iwe ni barabarani, katika maeneo ya biashara, kwenye mabustani, au kupitia simu. Pia, tunawahubiria majirani, wafanyakazi, wanafunzi, na watu wetu wa ukoo tunapopata fursa. Jitihada zote hizo zimefanya iwezekane kwa mamilioni ya watu ulimwenguni pote kusikia “habari njema za wokovu.”—Zaburi 96:2.

Je, kuna mtu yeyote ambaye ungependa kuzungumza naye kuhusu habari njema za Ufalme wa Mungu, na jinsi anavyoweza kufaidika wakati ujao? Zungumza naye mara tu upatapo fursa!

  • Ni “habari njema” zipi zinazohitaji kutangazwa?

  • Mashahidi wa Yehova wanaigaje mbinu ya Yesu ya kuhubiri?