Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unajua Nini Kuhusu Mashahidi wa Yehova?

Unajua Nini Kuhusu Mashahidi wa Yehova?

Unatuona tukihubiri. Huenda umesoma habari kutuhusu au umesikia mambo kadhaa kutoka kwa watu. Lakini kweli unawajua vizuri Mashahidi wa Yehova?

PIMA UJUZI WAKO

Tia alama kuonyesha ikiwa sentensi zifuatazo ni kweli au si kweli.

KWELI SI KWELI

  1. Mashahidi wa Yehova ni Wakristo.

  2. Mashahidi wa Yehova wanaamini dunia iliumbwa kwa siku sita zenye urefu wa saa 24.

  3. Mashahidi wa Yehova hawakubali matibabu.

  4. Mashahidi wa Yehova huamini Biblia nzima.

  5. Mashahidi wa Yehova hutumia tu tafsiri yao ya Biblia.

  6. Mashahidi wa Yehova wamebadili Biblia yao ifaane na mambo wanayoamini.

  7. Mashahidi wa Yehova hawajihusishi na shughuli za kijamii.

  8. Mashahidi wa Yehova hudharau dini nyingine.

Ili kupata majibu, soma kurasa zifuatazo.

  1. 1 KWELI. Tunajitahidi kufuata mafundisho na mwenendo wa Yesu Kristo. (1 Petro 2:21) Hata hivyo, kuna tofauti mbalimbali kati yetu na vikundi vingine vya kidini vya Kikristo. Kwa mfano, tunaamini kwamba Biblia inafundisha kuwa Yesu ni Mwana wa Mungu, si sehemu ya Utatu. (Marko 12:29) Tunaamini kwamba nafsi inaweza kufa na kwamba hakuna msingi wowote wa Kimaandiko wa kusema kwamba Mungu huwatesa watu milele katika moto wa mateso. Pia, tunaamini kwamba wale wanaoongoza katika mambo ya kidini hawapaswi kuwa na majina ya cheo yanayowainua juu ya watu wengine.—Mhubiri 9:5; Ezekieli 18:4; Mathayo 23:8-10.

  2. 2 SI KWELI. Tunaamini kwamba Mungu ndiye aliyeumba kila kitu. Lakini hatuamini kwamba dunia iliumbwa kwa siku sita zenye urefu wa saa 24. Kwa sababu gani? Kwa sababu wazo hilo linapingana na Biblia. Kwa mfano, watu fulani wanaamini kwamba siku sita za uumbaji zilikuwa na urefu wa saa 24. Lakini katika Biblia, neno “siku” linaweza kurejelea muda mrefu. (Mwanzo 2:4; Zaburi 90:4) Watu fulani wanafundisha kwamba dunia imekuwapo kwa maelfu kadhaa ya miaka. Hata hivyo, kulingana na Biblia, dunia na anga zilikuwepo hata kabla ya zile siku sita za uumbaji kuanza. 1Mwanzo 1:1.

  3. 3 SI KWELI. Tunakubali njia mbalimbali za matibabu. Hata wengine miongoni mwetu ni madaktari, kama alivyokuwa Luka, Mkristo wa karne ya kwanza. (Wakolosai 4:14) Hata hivyo, hatukubali matibabu yoyote yanayopingana na kanuni za Biblia. Kwa mfano, hatukubali kutiwa damu mishipani kwa sababu Biblia inakataza kutumia damu.—Matendo 15:20, 28, 29.

    Tunajitahidi kutafuta matibabu bora kwa kadiri inavyowezekana kwa ajili yetu na familia zetu. Kwa kweli, matibabu yasiyohusisha damu yamewasaidia si Mashahidi tu, bali pia watu wengine. Sasa katika nchi nyingi, mgonjwa yeyote anaweza kuchagua matibabu yasiyohusisha damu ili kuepuka magonjwa yanayosababishwa na kutiwa damu, au makosa ya kibinadamu.

  4. 4 KWELI. Tunaamini kwamba Biblia nzima ‘imeongozwa na roho ya Mungu na ni yenye faida.’ (2 Timotheo 3:16) Biblia nzima inatia ndani maandiko yanayojulikana kama Agano la Kale na Agano Jipya. Kwa kawaida, sisi huita sehemu hizo Maandiko ya Kiebrania na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Tunaziita hivyo ili watu wasiwe na wazo la kwamba sehemu fulani za Biblia zimepitwa na wakati au si muhimu.

  5. 5 SI KWELI. Tunatumia tafsiri mbalimbali za Biblia kujifunza neno la Mungu. Hata hivyo, katika lugha ambazo inapatikana, sisi hupenda kutumia Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kwa sababu inatumia jina la Mungu, ni sahihi, na inaeleweka kwa urahisi. Fikiria kuhusu matumizi ya jina la Mungu, Yehova. Kwenye utangulizi wa tafsiri moja ya Biblia kuna orodha ya majina 79 ya watu ambao kwa njia fulani walichangia kutafsiriwa kwa Biblia hiyo. Hata hivyo, kwenye Biblia hiyo jina la Mtungaji—Yehova Mungu—limeondolewa kabisa! Kinyume na hilo, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imelirudisha jina la Mungu katika maelfu ya sehemu ambapo jina hilo lilipatikana katika maandishi ya awali. 2

  6. 6 SI KWELI. Mara tu tunapogundua kwamba jambo fulani tunaloamini halipatani na yale ambayo Biblia inasema, tunaacha kuamini jambo hilo. Miaka mingi hata kabla ya kuchapisha Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika mwaka wa 1950, tulitumia tafsiri za Biblia zilizokuwepo kutegemeza mafundisho yetu.

  7. 7 SI KWELI. Huduma yetu huwanufaisha wengi katika jamii. Tumewasaidia watu wengi kushinda mazoea yenye uraibu kama vile matumizi mabaya ya dawa za kulevya na kileo. Madarasa yetu ya kujifunza kusoma na kuandika yamewasaidia maelfu ya watu kujua kusoma na kuandika. Pia, misiba inapotokea sisi hutoa msaada kwa Mashahidi na watu ambao si Mashahidi. Tunajitahidi kuwasadia waathiriwa kihisia na kiroho, msaada ambao wao huhitaji sana wakati huo. 3

  8. 8 SI KWELI. Tunatii shauri la Biblia kwamba ‘tuwaheshimu watu wote’—haidhuru wana imani gani ya kidini. (1 Petro 2:17, Biblia Habari Njema) Kwa mfano, katika nchi fulani kuna mamia ya maelfu ya Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, hatujaribu kuwashinikiza wanasiasa au wabunge wazuie au kupiga marufuku kazi ya vikundi vingine vya kidini. Wala hatujaribu kufanya kampeni ili sheria zitungwe zinazowalazimisha watu katika jamii wafuate imani yetu ya kidini na ya kiadili. Badala yake, tunaheshimu haki za wengine, kama vile tu tungependa wao waheshimu haki zetu.—Mathayo 7:12.

Makala hii ina habari zilizo katika tovuti yetu rasmi, jw.org/sw. Ili kupata habari zaidi, tembelea KUTUHUSU › MASWALI YANAYOULIZWA MARA NYINGI.

^ 1. Kwa sababu hiyo, Mashahidi wa Yehova hawapingi utafiti unaotegemeka wa kisayansi unaoonyesha kwamba dunia imekuwapo kwa mabilioni ya miaka—kama wanavyosema watu wanaoamini dunia iliumbwa kwa siku sita zenye urefu wa saa 24.

^ 2. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatofautiana kwa njia nyingine na tafsiri nyingine za Biblia: Inatolewa bila malipo. Kwa sababu hiyo mamilioni ya watu wanaweza kusoma Biblia katika lugha zao za asili. Sasa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inapatikana katika lugha 130. Pia, unaweza kuisoma katika Intaneti kwenye www.pr418.com/sw.

^ 3. Njia moja ambayo michango tunayopata hutumika ni kuwapatia kitulizo waliokumbwa na misiba. (Matendo 11:27-30) Kwa kuwa kazi hiyo hufanywa na wajitoleaji wasiolipwa, pesa tunazopata hutumiwa hasa kutoa msaada na si kulipa mishahara.