Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAONI YA BIBLIA

Kuteseka

Kuteseka

Baadhi ya watu hufikiri kwamba Mungu ndiye anayesababisha kuteseka au hajali hata anapoona watu wakiteseka. Lakini Biblia inafundisha nini? Biblia inatoa majibu tofauti.

Je, Mungu ndiye anayesababisha mateso?

“Kwa kweli, Mungu hatendi kwa uovu.”Ayubu 34:12.

WATU HUSEMA NINI?

Baadhi ya watu husema kwamba kila jambo linalotokea ni mapenzi ya Mungu. Kwa hiyo wanaamini kwamba kuteseka kwa wanadamu ni mapenzi ya Mungu. Kwa mfano, majanga yanapotokea, wanafikiri kwamba mambo hayo ni njia ya Mungu ya kuwaadhibu watenda dhambi.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia inasema wazi kwamba Mungu hasababishi mateso yanayowapata wanadamu. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba tunapopatwa na matatizo, si sahihi kusema: “Mungu ananijaribu.” Kwa nini? Kwa sababu “Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Kwa kweli, Mungu hasababishi kamwe majaribu au mateso tunayopata. Kufanya hivyo kungemfanya awe mwovu, lakini tofauti na hilo Biblia inasema “Mungu hatendi kwa uovu.”—Ayubu 34:12.

Ikiwa si Mungu, ni nini au ni nani basi anayesababisha mateso ya wanadamu? Kwa kusikitisha, mara nyingi wanadamu wameteswa na wanadamu wenzao. (Mhubiri 8:9) Kwa kuongezea, tunaweza kupatwa na majanga kwa sababu ya “wakati na tukio lisilotazamiwa,” yaani, kuwa mahali pasipofaa wakati usiofaa. (Mhubiri 9:11) Biblia inafundisha kwamba “mtawala wa ulimwengu huu,” Shetani Ibilisi, ndiye chanzo kikuu cha mateso ya wanadamu, kwa sababu “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (Yohana 12:31; 1 Yohana 5:19) Kwa hiyo, Mungu hasababishi mateso ya wanadamu. Shetani ndiye anayesababisha watu wateseke.

Je, Mungu anatujali tunapoteseka?

“Wakati wa taabu zao zote hilo lilimtaabisha.”Isaya 63:9.

WATU HUSEMA NINI?

Wengine hufikiri kwamba Mungu hajali tunapoteseka. Kwa mfano, mwandishi mmoja alisema kwamba Mungu “hana huruma hata kidogo wala hawasikitikii wanaoteseka.” Anachosema ni kwamba ikiwa Mungu yupo, basi “hawajali wanadamu.”

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia haisemi kwamba Mungu hana huruma au kwamba hajali, badala yake inafundisha kwamba Mungu anatuhurumia tunapoteseka—na hivi karibuni ataondoa matatizo yetu. Fikiria ahadi tatu zinazotufariji zinazopatikana katika Biblia.

Mungu anajua mateso yetu. Tangu mwanzo wa mateso ya wanadamu, hakuna hata tone moja la machozi ya wanadamu ambalo Yehova * amelipuuza, kwa sababu “macho yake yanayong’aa” yanaona kila kitu. (Zaburi 11:4; 56:8) Kwa mfano, wakati watumishi wake wa zamani walipokuwa wakiteswa, Mungu alisema hivi: “Pasipo shaka nimeyaona mateso ya watu wangu.” Lakini je, unafikiri Mungu alielewa mateso yao kwa kina? Ndiyo, kwa sababu anaendelea kusema hivi: “Nayajua vizuri maumivu waliyo nayo.” (Kutoka 3:7) Watu wengi wamefarijika baada ya kujua ukweli huo—kwamba Mungu anatambua kuteseka kwetu, hata kama wanadamu wenzetu hawazijui wala hawazielewi hali zetu.—Zaburi 31:7; Methali 14:10.

Mungu anatuhurumia tunapoteseka. Zaidi ya kutambua mateso yetu, Mungu pia anatuhurumia. Kwa mfano, Mungu alihuzunika watumishi wake wa zamani walipopatwa na matatizo. Biblia inasema hivi: “Wakati wa taabu zao zote hilo lilimtaabisha.” (Isaya 63:9) Ingawa Mungu ni mkuu sana kuliko wanadamu, yeye huwahurumia wanapoteseka—ni kana kwamba maumivu yao yako moyoni mwake! Kwa kweli, “Yehova ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.” (Yakobo 5:11) Kwa kuongezea, Yehova hutusaidia kukabiliana na mateso.—Wafilipi 4:12, 13.

Mungu ataondoa mateso yote yanayowapata wanadamu. Biblia inafundisha kwamba Mungu ataondoa mateso ya wanadamu wote duniani. Kupitia Ufalme wake wa mbinguni, Yehova atabadilisha kabisa hali za wanadamu na kuzifanya ziwe bora. Kuhusu wakati huo, Biblia inaahidi kwamba Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:4) Vipi kuhusu wale ambao wamekufa? Mungu atawafufua ili wao pia wafurahie maisha duniani bila mateso yoyote. (Yohana 5:28, 29) Je, kuna mtu yeyote atakayeumia kwa sababu ya kumbukumbu za mateso ya zamani? Hapana, kwa sababu Yehova anaahidi hivi: “Mambo ya zamani hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni.”—Isaya 65:17. *

^ fu. 13 Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa katika Biblia.

^ fu. 15 Ili ujue kwa nini Mungu ameruhusu wanadamu wateseke na pia jinsi atakavyoyaondoa mateso hayo, tafadhali soma sura ya 8 na sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.