Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Ambayo Watu Huuliza Mara Nyingi

Maswali Ambayo Watu Huuliza Mara Nyingi

Maswali Ambayo Watu Huuliza Mara Nyingi

Kwa nini watu fulani husema mambo mabaya kuwahusu Mashahidi wa Yehova?

Watu wengi hawajaambiwa ukweli kuwahusu Mashahidi wa Yehova. Huenda wengine hawapendi kazi ya kueneza Injili ambayo Mashahidi wanafanya. Hata hivyo, ukweli ni kwamba Mashahidi hufanya kazi hiyo kwa sababu wanawapenda majirani, wakijua kuwa “kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.”—Waroma 10:13.

Je, Mashahidi wa Yehova ni Waprotestanti, Wakristo wenye imani kali, au ni madhehebu?

Mashahidi wa Yehova ni Wakristo, na si Waprotestanti kwa sababu ileile inayowafanya wasiwe Wakatoliki—wanatambua kuwa baadhi ya mafundisho ya dini hizo hayapatani na Maandiko. Kwa mfano, Biblia haifundishi kuwa Mungu mwenye upendo anawatesa watu katika moto wa mateso. Wala haifundishi kuwa wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa au Wakristo wanapaswa kujihusisha na siasa.—Ezekieli 18:4; Yohana 15:19; 17:14; Waroma 6:23. *

The World Book Encyclopedia kinasema kuwa “Wakristo wenye imani kali ni kikundi kikubwa cha Waprotestanti huko Marekani.” Baadhi ya vikundi hivyo vyenye imani kali “vimetumia vibaya mistari fulani ya Biblia ili kujihusisha katika mambo fulani ya kijamii na ya kisiasa.” Mashahidi wa Yehova hawafanyi hivyo. Kama ilivyotajwa mapema, wao hujiepusha na siasa na hawawalazimishi watu wakubali maoni yao kwa kutumia njia ya kisiasa au njia nyingine yoyote. Badala yake, wao hujadiliana na watu moja kwa moja na kutoa uthibitisho wenye kusadikisha, wakiwaiga Wakristo wa karne ya kwanza.—Matendo 19:8.

Madhehebu ni kikundi kilichojitenga na dini nyingine na kuanzisha dini mpya. Mashahidi wa Yehova hawakutokana na kanisa fulani. Wao si madhehebu.

Wao hufanya nini katika mikutano yao?

Mikutano yao ambayo mtu yeyote anaweza kuhudhuria, huwa ni ya kujifunza Biblia, na wasikilizaji hushiriki mikutano hiyo kwa kutoa maelezo. Mojawapo ya mikutano yao ya kila juma ni Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ambayo huwasaidia washiriki wa kutaniko kusitawisha uwezo wa kufundisha, kusoma, na kufanya utafiti. Mkutano mwingine ni hotuba ya dakika 30 inayotegemea Biblia ambayo huzungumzia kichwa kimoja cha habari kinachowafaa wasikilizaji ambao si Mashahidi wa Yehova. Hotuba hiyo hufuatiwa na funzo la Biblia linalotegemea Mnara wa Mlinzi. Mikutano huanza na kumalizwa kwa wimbo na sala, na hakuna pesa zinazokusanywa wala sahani inayopitishwa kukusanya sadaka.—2 Wakorintho 8:12.

Mashahidi wa Yehova hugharamia kazi yao jinsi gani?

Kazi yao hutegemea michango ya hiari. Mashahidi hawatozi pesa zozote kwa ajili ya huduma kama vile kubatiza, harusi, maziko, au huduma nyingine za kidini. Wala hawatoi fungu la kumi. Mtu yeyote anayetaka kutoa mchango, anaweza kufanya hivyo katika masanduku yaliyowekwa kwenye Jumba la Ufalme. Mashahidi wa Yehova huchapisha vitabu vinavyotegemea Biblia na hivyo kupunguza gharama, na pia Majumba yao ya Ufalme na ofisi za tawi hujengwa hasa na wajitoleaji.

Je, Mashahidi wa Yehova wanakubali matibabu?

Ndiyo. Bila shaka, wao hutafuta matibabu bora kwa ajili yao na wapendwa wao. Isitoshe, Mashahidi wengi hufanya kazi katika taaluma ya tiba wakiwa wauguzi, wahudumu wa hali za dharura, madaktari, na hata wapasuaji. Hata hivyo, Mashahidi hukataa kutiwa damu mishipani. ‘Jiepushe . . . na damu,’ Biblia inasema. (Matendo 15:28, 29) Jambo la kupendeza ni kwamba madaktari wengi sasa wanakubali kuwa matibabu yasiyohusisha damu ndiyo matibabu bora zaidi, kwa kuwa yanawaepusha wagonjwa na matatizo yanayotokezwa na damu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Unaweza kupata maoni ya Biblia kuhusu vichwa hivi na vichwa vingine muhimu katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

WAKAZI WANAOISHI PAMOJA KWA KUHESHIMIANA

Mji wa Bejucal de Ocampo ulio kusini mwa Mexico ni mji wa kipekee. “Wengi wa wakazi wa mji huo ni Mashahidi wa Yehova,” inasema ripoti moja katika gazeti Excélsior, na ikaongezea kusema: “Wakazi wa eneo hilo huheshimu maoni ya kidini na ya kisiasa ya majirani wao. . . . Wakazi wa mji huo wameacha kunywa pombe na kuvuta sigara na badala yake sasa wao wanamsifu Mungu kwa nyimbo na kusoma Biblia. Pia wanaheshimu mamlaka.”

Ingawa kuna dini mbalimbali katika mji huo, “hakuna mizozo ya kidini wala ugomvi wowote ambao umewahi kuzuka,” inasema ripoti hiyo. Pia inaendelea kusema: “Hakuna uhasama kati ya wakazi hao, na ingawa wakazi hao ni wa dini mbalimbali, hilo haliwazuii kusalimiana . . . Kila familia hufuata dini yake lakini hilo haliwazuii kuishi pamoja kwa amani. Haishangazi kwamba Mashahidi wa Yehova wana uvutano mkubwa huko Bejucal.” Zaidi ya hilo, watoto wao ‘huvalia kwa kiasi, wanapita mitihani, na wanajiendesha vizuri darasani,’ anasema mwalimu wa shule ya sekondari ambaye si Shahidi.