Matendo ya Mitume 5:1-42

  • Anania na Safira (1-11)

  • Mitume wafanya ishara nyingi (12-16)

  • Wafungwa gerezani, kisha waachiliwa huru (17-21a)

  • Washtakiwa mbele ya Sanhedrini tena (21b-32)

    • ‘Kumtii Mungu badala ya wanadamu’ (29)

  • Ushauri wa Gamalieli (33-40)

  • Kuhubiri nyumba kwa nyumba (41, 42)

5  Hata hivyo, mwanamume fulani aliyeitwa Anania, pamoja na Safira mke wake, waliuza mali.  Lakini akajiwekea kisiri kiasi fulani, mke wake pia akijua jambo hilo, naye akaleta sehemu fulani tu na kuiweka miguuni pa mitume.+  Lakini Petro akamuuliza: “Anania, kwa nini Shetani amekupa ujasiri wa kuidanganya+ roho takatifu+ ukajiwekea kisiri kiasi fulani cha bei ya shamba?  Kabla ya kuliuza, je, halikuwa mali yako? Na baada ya kuliuza, je, pesa hizo hazikuwa mikononi mwako? Kwa nini umewaza tendo kama hili moyoni mwako? Umedanganya si wanadamu, bali Mungu.”  Anania aliposikia maneno hayo, akaanguka chini akafa. Na wote waliosikia jambo hilo wakaogopa sana.  Basi vijana wakasimama, wakamfunga kwa vitambaa, wakamtoa nje, na kumzika.  Sasa baada ya muda wa saa tatu hivi, mke wake akaingia bila kujua kilichokuwa kimetokea.  Petro akamuuliza: “Niambie, je, ninyi wawili mliuza shamba kwa kiasi hiki?” Akajibu: “Ndiyo, kwa kiasi hicho.”  Kwa hiyo Petro akamwambia: “Kwa nini ninyi wawili mlikubaliana kuijaribu roho ya Yehova?* Tazama! Miguu ya wale waliomzika mume wako, ipo mlangoni, nao watakubeba na kukutoa nje.” 10  Papo hapo akaanguka chini miguuni pa Petro akafa. Wale vijana walipoingia walikuta amekufa, wakamtoa nje na kumzika kando ya mume wake. 11  Basi kutaniko lote na wote waliosikia kuhusu mambo hayo wakaogopa sana. 12  Isitoshe, kupitia mikono ya mitume ishara nyingi na mambo ya ajabu* yakaendelea kutukia kati ya watu;+ na wote walikuwa wakikutana kwenye Safu ya Nguzo za Sulemani.+ 13  Kwa kweli, hakuna yeyote kati ya wale wengine aliyekuwa na ujasiri wa kujiunga nao; hata hivyo, watu walikuwa wakiwasifu. 14  Isitoshe, wale waliomwamini Bwana wakazidi kuongezeka, idadi kubwa ya wanaume na wanawake.+ 15  Hata wakawaleta wagonjwa kwenye njia kuu na kuwalaza kwenye vitanda vidogo na mikeka, ili Petro akipita hapo, angalau kivuli chake kiwaangukie baadhi yao.+ 16  Pia, umati kutoka kwenye majiji yaliyokuwa karibu na Yerusalemu ukazidi kuja, ukiwa umewabeba wagonjwa na wale waliosumbuliwa na roho waovu, nao wote wakaponywa. 17  Lakini kuhani mkuu akasimama, na wote waliokuwa pamoja naye, ambao walikuwa wafuasi wa madhehebu ya Masadukayo, nao walikuwa wamejaa wivu. 18  Basi wakawakamata mitume na kuwafunga katika jela ya watu wote.+ 19  Lakini usiku, malaika wa Yehova* akaifungua milango ya gereza,+ akawatoa nje na kuwaambia: 20  “Nendeni mkasimame hekaluni, na mwendelee kuwaambia watu maneno yote kuhusu maisha haya.” 21  Baada ya kusikia hilo, wakaingia hekaluni wakati wa mapambazuko na kuanza kufundisha. Basi kuhani mkuu na wale waliokuwa pamoja naye walipofika, wakakusanya Sanhedrini na kusanyiko lote la wazee wa wana wa Israeli, nao wakawatuma watu kwenye jela ili wawalete mitume mbele yao. 22  Lakini wale maofisa walipofika huko, hawakuwakuta gerezani. Basi wakarudi na kutoa taarifa, 23  wakisema: “Tuliikuta jela ikiwa imefungwa kabisa na walinzi wakiwa wamesimama kwenye milango, lakini tulipoifungua hatukumkuta mtu yeyote ndani.” 24  Basi, kapteni wa hekalu na wakuu wa makuhani waliposikia maneno hayo, walifadhaika sana kwa kuwa hawakujua jambo hilo lingekuwa na matokeo gani. 25  Lakini mtu fulani akaja na kuwaambia: “Tazameni! Wale watu mliowafunga gerezani wako hekaluni, wakiwa wamesimama wakiwafundisha watu.” 26  Ndipo kapteni akaenda pamoja na maofisa wake na kuwaleta bila kutumia nguvu, kwa maana waliogopa watu watawapiga mawe.+ 27  Basi wakawaleta na kuwasimamisha mbele ya Sanhedrini. Kisha kuhani mkuu akawahoji 28  akisema: “Tuliwakataza kabisa msifundishe kwa msingi wa jina hili,+ na bado tazama! mmejaza Yerusalemu fundisho lenu, nanyi mmeazimia kuileta damu ya mtu huyu juu yetu.”+ 29  Petro na wale mitume wengine wakajibu: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.+ 30  Mungu wa mababu zetu alimfufua Yesu, ambaye ninyi mlimuua, kwa kumtundika kwenye mti.+ 31  Mungu alimwinua huyo kuwa Wakili Mkuu+ na Mwokozi+ kwenye mkono wake wa kuume,+ ili kuwapa Israeli toba na msamaha wa dhambi zao.+ 32  Nasi ni mashahidi wa mambo hayo,+ na pia roho takatifu,+ ambayo Mungu amewapa wale wanaomtii akiwa mtawala.” 33  Waliposikia hayo, wakakasirika sana* nao wakataka kuwaangamiza. 34  Lakini Farisayo mmoja aitwaye Gamalieli+ akasimama katika Sanhedrini; alikuwa mwalimu wa Sheria aliyeheshimiwa na watu wote, naye akaamuru watu hao watolewe nje kwa muda mfupi. 35  Kisha akawaambia: “Wanaume wa Israeli, iweni waangalifu kuhusu jambo mnalokusudia kuwatendea watu hawa. 36  Kwa mfano, kabla ya siku hizi Theuda alisimama akidai kwamba yeye ni mtu wa maana, na wanaume kadhaa, karibu 400, wakajiunga na chama chake. Lakini aliangamizwa, na wafuasi wake wote wakatawanyika na kwisha. 37  Baada yake, Yuda Mgalilaya akainuka katika zile siku za uandikishaji, naye akawa na wafuasi. Mtu huyo pia aliangamia, na wafuasi wake wote wakatawanyika. 38  Basi chini ya hali zilizopo, ninawaambia, msiingilie mambo ya watu hawa, bali waacheni. Kwa maana, ikiwa mpango huu au kazi hii ni ya wanadamu, itaangamizwa; 39  lakini ikiwa imetoka kwa Mungu, hamtaweza kuwaangamiza.+ La sivyo, huenda ikawa mnapigana na Mungu mwenyewe.”+ 40  Ndipo wakasikiliza ushauri wake, wakawaita mitume, wakawapiga viboko,+ na kuwaagiza waache kusema kwa msingi wa jina la Yesu, kisha wakawaacha waende. 41  Basi wakatoka mbele ya Sanhedrini, wakishangilia+ kwa sababu walikuwa wamestahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake. 42  Na kila siku hekaluni na nyumba kwa nyumba+ wakaendelea kufundisha na kutangaza habari njema kumhusu Kristo Yesu bila kuacha.+

Maelezo ya Chini

Au “miujiza.”
Au “wakahisi wamechomwa.”