Kulingana na Yohana 8:12-59

  • Baba hutoa ushahidi kumhusu Yesu (12-30)

    • Yesu ndiye “nuru ya ulimwengu” (12)

  • Watoto wa Abrahamu (31-41)

    • “Kweli itawaweka ninyi huru” (32)

  • Watoto wa Ibilisi (42-47)

  • Yesu na Abrahamu (48-59)

8  12  Kisha Yesu akawaambia tena: “Mimi ndiye nuru ya ulimwengu.+ Yeyote anayenifuata hatatembea kamwe gizani, bali atakuwa na nuru+ ya uzima.” 13  Basi Mafarisayo wakamwambia: “Wewe unatoa ushahidi juu yako mwenyewe; ushahidi wako si wa kweli.” 14  Yesu akawajibu: “Hata ikiwa ninatoa ushahidi juu yangu mwenyewe, ushahidi wangu ni wa kweli, kwa sababu ninajua nilikotoka na ninakoenda.+ Lakini ninyi hamjui nilikotoka wala ninakoenda. 15  Ninyi mnahukumu kulingana na mwili;*+ mimi simhukumu mtu yeyote kamwe. 16  Hata nikihukumu, hukumu yangu ni ya kweli, kwa sababu siko peke yangu, bali Baba aliyenituma yuko pamoja nami.+ 17  Pia, katika Sheria yenu imeandikwa: ‘Ushahidi wa watu wawili ni wa kweli.’+ 18  Mimi ninatoa ushahidi juu yangu mwenyewe, na Baba aliyenituma hutoa ushahidi kunihusu.”+ 19  Kisha wakamuuliza: “Baba yako yuko wapi?” Yesu akajibu: “Ninyi hamnijui mimi wala Baba yangu.+ Kama mngenijua mimi, mngemjua Baba yangu pia.”+ 20  Alisema maneno hayo katika chumba cha hazina+ alipokuwa akifundisha hekaluni. Lakini hakuna mtu aliyemkamata, kwa sababu saa yake haikuwa imefika.+ 21  Kwa hiyo, akawaambia tena: “Ninaenda zangu, nanyi mtanitafuta, na bado mtakufa katika dhambi zenu.+ Ninakoenda hamwezi kuja.”+ 22  Basi Wayahudi wakaanza kuulizana: “Je, atajiua? Kwa sababu anasema, ‘Ninakoenda hamwezi kuja.’” 23  Akaendelea kuwaambia: “Ninyi mnatoka katika makao ya chini; mimi ninatoka katika makao ya juu.+ Ninyi mnatoka katika ulimwengu huu; mimi sitoki katika ulimwengu huu. 24  Ndiyo maana niliwaambia: Mtakufa katika dhambi zenu. Kwa maana msipoamini kwamba mimi ndiye, mtakufa katika dhambi zenu.” 25  Kwa hiyo wakaanza kumuuliza: “Wewe ni nani?” Yesu akawajibu: “Kwa nini hata ninazungumza nanyi? 26  Nina mambo mengi ya kusema kuwahusu na mengi ya kuhukumu. Kwa hakika, Yule aliyenituma ni wa kweli, na mambo niliyoyasikia kutoka kwake ninayasema ulimwenguni.”+ 27  Hawakuelewa kwamba alikuwa akiwaambia kumhusu Baba. 28  Kisha Yesu akasema: “Baada ya kumwinua Mwana wa binadamu,+ ndipo mtakapojua kwamba mimi ndiye+ na kwamba sifanyi jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe;+ bali mambo ambayo Baba amenifundisha, ndiyo ninayosema. 29  Na Yule aliyenituma yuko pamoja nami; naye hakuniacha peke yangu, kwa sababu sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza.”+ 30  Alipokuwa akisema mambo hayo, wengi wakamwamini. 31  Basi Yesu akawaambia Wayahudi waliokuwa wamemwamini: “Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, 32  nanyi mtaijua kweli,+ nayo kweli itawaweka ninyi huru.”+ 33  Wakamjibu: “Sisi ni uzao wa Abrahamu na hatujawahi kuwa watumwa wa mtu yeyote. Kwa nini basi unasema tutakuwa huru?” 34  Yesu akawajibu: “Kwa kweli ninawaambia, kila mtu anayetenda dhambi ni mtumwa wa dhambi.+ 35  Isitoshe, mtumwa habaki nyumbani milele; lakini mwana hubaki milele. 36  Kwa hiyo, Mwana akiwaweka ninyi huru, kwa kweli mtakuwa huru. 37  Ninajua kwamba ninyi ni uzao wa Abrahamu. Lakini mnataka kuniua, kwa sababu neno langu halifanyi maendeleo kati yenu. 38  Ninasema mambo niliyoona nilipokuwa na Baba yangu,+ lakini ninyi mnafanya mambo mliyosikia kutoka kwa baba yenu.” 39  Wakamwambia: “Baba yetu ni Abrahamu.” Yesu akawaambia: “Kama mngekuwa watoto wa Abrahamu,+ mngefanya kazi za Abrahamu. 40  Lakini sasa mnataka kuniua, mimi ambaye nimewaambia kweli niliyosikia kutoka kwa Mungu.+ Abrahamu hakufanya hivyo. 41  Mnafanya kazi za baba yenu.” Wakamwambia: “Hatukuzaliwa kutokana na uasherati;* tuna Baba mmoja tu, Mungu.” 42  Yesu akawaambia: “Kama Mungu angekuwa Baba yenu, mngenipenda,+ kwa maana nilitoka kwa Mungu nami nipo hapa. Sikuja kwa uamuzi wangu mwenyewe, bali Yeye ndiye aliyenituma.+ 43  Kwa nini hamwelewi mambo ninayosema? Kwa sababu hamwezi kusikiliza neno langu. 44  Ninyi mmetoka kwa baba yenu Ibilisi, nanyi mnataka kufanya tamaa za baba yenu.+ Alikuwa muuaji alipoanza,*+ naye hakusimama imara katika kweli, kwa sababu kweli haimo ndani yake. Anaposema uwongo, yeye husema kulingana na mwelekeo wake mwenyewe, kwa sababu yeye ni mwongo na ndiye baba ya uwongo.+ 45  Lakini kwa sababu mimi ninawaambia kweli, hamniamini. 46  Ni nani kati yenu anayeweza kunihukumu kwamba nina dhambi? Ikiwa ninasema kweli, kwa nini hamniamini? 47  Yule anayetoka kwa Mungu husikiliza maneno ya Mungu.+ Kwa sababu hiyo, ninyi hamsikilizi, kwa kuwa hamtoki kwa Mungu.”+ 48  Wayahudi wakamjibu: “Je, hatusemi kweli tunaposema, ‘Wewe ni Msamaria+ na una roho mwovu’?”+ 49  Yesu akajibu: “Mimi sina roho mwovu bali ninamheshimu Baba yangu, lakini ninyi mnanivunjia heshima. 50  Hata hivyo, mimi sijitafutii utukufu;+ kuna Yule anayetafuta na kuhukumu. 51  Kwa kweli ninawaambia, yeyote akishika maneno yangu, hataona kifo kamwe.”+ 52  Wayahudi wakamwambia: “Sasa tunajua una roho mwovu. Abrahamu alikufa, na manabii vilevile, lakini wewe unasema, ‘Yeyote akishika maneno yangu hataonja kifo kamwe.’ 53  Wewe si mkuu kuliko Abrahamu baba yetu ambaye alikufa, sivyo? Manabii pia walikufa. Unafikiri wewe ni nani?” 54  Yesu akajibu: “Nikijitukuza mwenyewe, utukufu wangu si kitu. Baba yangu ambaye mnasema ni Mungu wenu, ndiye anayenitukuza.+ 55  Ninyi bado hamjamjua,+ lakini mimi ninamjua.+ Kama ningesema simjui, ningekuwa mwongo kama ninyi. Lakini mimi ninamjua, na ninalishika neno lake. 56  Baba yenu Abrahamu alishangilia sana tazamio la kuona siku yangu, naye aliiona na kushangilia.”+ 57  Kisha Wayahudi wakamuuliza: “Wewe hujafika umri wa miaka 50, na bado umemwona Abrahamu?” 58  Yesu akawaambia: “Kwa kweli ninawaambia, mimi nimekuwapo kabla Abrahamu hajakuwapo.”+ 59  Ndipo wakaokota mawe ili wampige, lakini Yesu akajificha na kuondoka hekaluni.

Maelezo ya Chini

Au “kwa viwango vya wanadamu.”
Neno la Kigiriki, por·neiʹa. Angalia Kamusi.
Au “tangu mwanzoni.”