Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 9

Jinsi Familia Yako Inavyoweza Kuwa na Furaha

Jinsi Familia Yako Inavyoweza Kuwa na Furaha

1. Kufunga ndoa kunachangiaje furaha ya familia?

Habari njema hutoka kwa Yehova, Mungu mwenye furaha, ambaye anataka familia ziwe na furaha. (1 Timotheo 1:11) Yeye ndiye aliyeanzisha ndoa. Ndoa halali kisheria ni muhimu ili familia iwe yenye furaha kwa sababu inaandaa mazingira salama ambayo watoto watalelewa. Wakristo wanapaswa kuheshimu sheria za nchi zao zinazohusu kuandikisha ndoa.​—Soma Luka 2:1, 4, 5.

Mungu anaionaje ndoa? Anataka ndoa iwe muungano wa kudumu kati ya mume na mke. Yehova anataka waume na wake wawe waaminifu kwa wenzi wao wa ndoa. (Waebrania 13:4) Anachukia talaka. (Malaki 2:16) Hata hivyo, anamruhusu Mkristo kutaliki na kuoa au kuolewa tena ikiwa tu mwenzi wake amefanya uzinzi.​—Soma Mathayo 19:3-6, 9.

2. Mume na mke wanapaswa kutendeana jinsi gani?

Yehova aliwaumba wanaume na wanawake ili wakamilishane katika ndoa. (Mwanzo 2:18) Akiwa kichwa cha familia, mume anapaswa kuiandalia familia yake mahitaji ya kimwili na kuifundisha kumhusu Mungu. Anapaswa kumpenda mke wake na kujidhabihu kwa ajili yake. Waume na wake wanapaswa kupendana na kuheshimiana. Kwa kuwa hakuna mume au mke aliye mkamilifu, ni muhimu kujifunza kusameheana ili ndoa iwe yenye furaha.​—Soma Waefeso 4:31, 32; 5:22-25, 33; 1 Petro 3:7.

3. Ikiwa ndoa yenu haina furaha, je, umwache mwenzi wako wa ndoa?

Ikiwa mna matatizo katika ndoa yenu, nyote wawili mnapaswa kujitahidi kutendeana kwa upendo. (1 Wakorintho 13:4, 5) Neno la Mungu halipendekezi kutengana kama njia ya kutatua matatizo ambayo ni ya kawaida katika ndoa.​—Soma 1 Wakorintho 7:10-13.

4. Watoto, Mungu anataka muwe na maisha ya aina gani?

Yehova anataka muwe wenye furaha. Anawapa mashauri bora kuhusu jinsi mnavyoweza kufurahia ujana wenu. Anataka mnufaike na hekima na uzoefu wa wazazi wenu. (Wakolosai 3:20) Pia, Yehova anataka mpate shangwe inayotokana na kumtumikia Yeye na Mwana wake.​—Soma Mhubiri 11:9–12:1; Mathayo 19:13-15; 21:15, 16.

5. Wazazi, watoto wenu wanahitaji nini ili wawe wenye furaha maishani?

Mnapaswa kufanya kazi kwa bidii ili kuwaandalia watoto wenu chakula, makao, na mavazi. (1 Timotheo 5:8) Lakini ili watoto wenu wawe wenye furaha, mnahitaji pia kuwafundisha wampende Mungu na wajifunze kutoka kwake. (Waefeso 6:4) Kielelezo chenu cha kumpenda Mungu kinaweza kuwachochea sana watoto wenu. Mkitegemea Neno la Mungu, maagizo mnayowapa yanaweza kuwasaidia wawe na mtazamo unaofaa.​—Soma Kumbukumbu la Torati 6:4-7; Methali 22:6.

Watoto hunufaika mnapowatia moyo na kuwapongeza. Wanahitaji pia kurekebishwa na kutiwa nidhamu. Kuwazoeza kwa njia hiyo kutawasaidia waepuke mwenendo unaoweza kuwafanya wakose furaha. (Methali 22:15) Hata hivyo, nidhamu haipaswi kamwe kutolewa kwa ukali au kwa ukatili.​—Soma Wakolosai 3:21.

Mashahidi wa Yehova wamechapisha vitabu kadhaa ambavyo vimekusudiwa hasa kuwasaidia wazazi na watoto. Vitabu hivyo vinategemea Biblia.​—Soma Zaburi 19:7, 11.