Hamia kwenye habari

Je, Mashahidi wa Yehova Wana Biblia Yao Wenyewe?

Je, Mashahidi wa Yehova Wana Biblia Yao Wenyewe?

 Mashahidi wa Yehova wametumia tafsiri mbalimbali za Biblia kujifunza neno la Mungu. Hata hivyo, katika lugha ambazo inapatikana, sisi hupenda kutumia Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kwa sababu inatumia jina la Mungu, ni sahihi, na inaeleweka kwa urahisi.

  •   Jina la Mungu. Baadhi ya wachapishaji wa Biblia wameshindwa kumpa utukufu Mtungaji wa Biblia. Kwa mfano, tafsiri moja ya Biblia ina orodha ya majina zaidi ya 70 ya watu ambao kwa njia fulani walichangia kutafsiriwa kwa Biblia hiyo. Hata hivyo, kwenye Biblia hiyo jina la Mtungaji​—Yehova Mungu​—limeondolewa kabisa!

     Kinyume na hilo, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imelirudisha jina la Mungu katika maelfu ya sehemu ambapo jina hilo lilipatikana katika maandishi ya awali, lakini haitaji majina ya halmashauri iliyohusika katika kuitafsiri.

  •   Usahihi. Si tafsiri zote zinazopitisha kwa usahihi ujumbe wa awali wa Biblia. Kwa mfano, tafsiri moja ya Biblia hutafsiri hivi maneno ya Yesu kwenye Mathayo 16:​24: “Mtu yeyote akitaka kuwa mfuasi wangu, lazima ajikane mwenyewe, auchukue msalaba wake, anifuate.” Kwa karne nyingi kabla ya Kristo kuja duniani, wapagani walitumia msalaba kama mfano wa kidini katika ibada yao. Kufikia karne ya tatu W.K. makanisa yalianza kutumia mfano huo kuwakilisha msalaba wa Kristo. Huenda watafsiri waliotafsiri mstari huo waliingiza wazo hilo la “msalaba” kwa sababu waliamini kwamba Yesu alikufa juu ya msalaba. Hata hivyo, neno lililotumiwa katika maandishi ya awali linatafsiriwa “mti,” na si “msalaba.” Hii ndiyo sababu Biblia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inasema hivi katika mstari huo: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuuchukua mti wake wa mateso na kunifuata sikuzote.”

  •   Kueleweka kwa urahisi. Tafsiri nzuri inapaswa kuwa sahihi na pia ieleweke kwa urahisi. Fikiria mfano mmoja. Kwenye andiko la Mathayo 5:3, Yesu alitumia usemi ambao kihalisi unamaanisha “wenye furaha ni wale walio maskini wa roho.” Kwa kuwa usemi huo hauna maana yoyote katika Kiingereza cha kisasa, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imetumia maneno yanayoweza kueleweka kwa urahisi katika mstari huo. Tafsiri hiyo ya Biblia inasema “wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”

 Pamoja na kwamba inatumia jina la Mungu, ni sahihi, na inaeleweka kwa urahisi, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatofautiana kwa njia nyingine na tafsiri nyingine za Biblia: Inatolewa bila malipo. Kwa sababu hiyo mamilioni ya watu wanaweza kusoma Biblia katika lugha zao za asili​—hata wale ambao hawangeweza kununua Biblia.