Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JE, KUNA FAIDA YOYOTE TUNAPOSALI?

Kwa Nini Mungu Hutuhimiza Tusali?

Kwa Nini Mungu Hutuhimiza Tusali?

Mungu anataka tuwe rafiki zake.

Marafiki huwasiliana ili kuwa na uhusiano mzuri. Vivyo hivyo, Mungu hutuhimiza tusali ili tuwe na urafiki wa karibu naye. Anasema hivi: “Mtaniita na kuja na kusali kwangu, nami nitawasikiliza.” (Yeremia 29:12) Kadiri unavyoongea na Mungu, ndivyo ‘utakavyomkaribia [yeye], naye atakukaribia.’ (Yakobo 4:8) Biblia inatuhakikishia hivi: “Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia.” (Zaburi 145:18) Tunavyoendelea kusali kwa Mungu ndivyo uhusiano wetu pamoja naye utakavyozidi kuimarika.

“Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia.”—Zaburi 145:18

Mungu anataka kukusaidia.

Yesu alisema hivi: “Ni nani kati yenu ambaye mwana wake akimwomba mkate—je, atampa jiwe? Au, labda, akiomba samaki—je, atampa nyoka? Kwa hiyo, ikiwa ninyi . . . mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo nzuri, je, Baba yenu aliye mbinguni hatawapa hata zaidi vitu vyema wale wanaomwomba?” (Mathayo 7:9-11) Naam, Mungu anakuhimiza usali kwake kwa sababu ‘anakujali’ na anataka kukusaidia. (1 Petro 5:7) Pia, anataka umwambie matatizo yako. Biblia inatuambia hivi: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu.”—Wafilipi 4:6.

Wanadamu wana uhitaji wa kiroho.

Wataalamu wa masomo ya asili ya mwanadamu wamegundua kwamba watu wengi wanahisi kuna uhitaji wa kusali. Hata wale wanaoamini kwamba hakuna Mungu au wanaoamini kwamba mambo yake hayawezi kujulikana wanahisi hivyo pia. * Hilo linathibitisha kwamba wanadamu waliumbwa wakiwa na uhitaji wa kiroho. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Njia moja ya kutosheleza uhitaji huo ni kwa kuwasiliana na Mungu kwa ukawaida.

Tutapata faida gani tukisali kwa Mungu?

^ fu. 8 Kulingana na uchunguzi uliofanywa na kituo cha utafiti cha Pew Research Center katika mwaka wa 2012, asilimia 11 ya watu nchini Marekani wanaoamini kwamba hakuna Mungu au wanaoamini kwamba mambo yake hayawezi kujulikana, husali angalau mara moja kwa mwezi.