Kulingana na Mathayo 20:1-34

  • Wafanyakazi katika shamba la mizabibu wapokea mshahara unaolingana (1-16)

  • Kifo cha Yesu chatabiriwa tena (17-19)

  • Ombi la kupewa vyeo katika Ufalme (20-28)

    • Yesu atoa fidia kwa ajili ya wengi (28)

  • Wanaume wawili vipofu waponywa (29-34)

20  “Kwa maana Ufalme wa mbinguni ni kama bwana mwenye nyumba aliyetoka asubuhi na mapema kwenda kuajiri wafanyakazi kwa ajili ya shamba lake la mizabibu.+  Baada ya kukubaliana na wafanyakazi hao awalipe dinari* moja kwa siku, akawatuma katika shamba lake la mizabibu.  Akatoka pia karibu saa tatu,* akaona wengine wamesimama sokoni bila kazi;  akawaambia, ‘Ninyi pia, nendeni katika shamba la mizabibu, nami nitawalipa haki yenu.’  Basi wakaenda. Tena akatoka karibu saa sita* na saa tisa* na kufanya vivyo hivyo.  Mwishowe, akatoka karibu saa kumi na moja,* akakuta wengine wakiwa wamesimama tu, naye akawauliza, ‘Mbona mmesimama hapa mchana kutwa bila kazi?’  Wakamjibu, ‘Kwa sababu hakuna mtu aliyetuajiri.’ Akawaambia, ‘Ninyi pia nendeni katika shamba la mizabibu.’  “Ilipofika jioni, mwenye shamba la mizabibu akamwambia msimamizi wake, ‘Waite wafanyakazi uwalipe mshahara wao,+ ukianza na wa mwisho na kumalizia na wa kwanza.’  Wale watu wa saa 11 walipokuja, wakapokea kila mmoja dinari* moja.⁠ 10  Basi, wale wa kwanza walipokuja, walidhani wangepokea zaidi; lakini wao pia wakalipwa dinari* moja. 11  Walipoipokea wakaanza kumlalamikia bwana mwenye nyumba 12  na kusema, ‘Watu hawa wa mwisho walifanya kazi kwa saa moja tu; na bado umewalipa sawa na sisi tuliofanya kazi ngumu mchana kutwa kwenye jua kali!’ 13  Lakini akamjibu mmoja wao, akasema, ‘Mwenzangu, sijakukosea. Tulikubaliana dinari* moja, sivyo?+ 14  Chukua mshahara wako uende. Ninataka kumpa huyu wa mwisho sawa na wewe. 15  Je, sina haki ya kufanya kile ninachotaka na vitu vyangu? Au jicho lako lina wivu* kwa sababu mimi ni mwema?’*+ 16  Vivyo hivyo, wa mwisho watakuwa wa kwanza, na wa kwanza watakuwa wa mwisho.”+ 17  Alipokuwa akipanda kwenda Yerusalemu, Yesu akawaita faraghani wale wanafunzi 12 na kuwaambia wakiwa barabarani:+ 18  “Tazama! Tunapanda kwenda Yerusalemu, na Mwana wa binadamu atatiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani na waandishi. Nao watamhukumia kifo+ 19  na kumtia mikononi mwa watu wa mataifa ili wamdhihaki, wampige mijeledi, na kumuua kwenye mti;+ na siku ya tatu atafufuliwa.”+ 20  Ndipo mama ya wana wa Zebedayo+ akamjia akiwa na wanawe, akamsujudia* na kumwomba jambo fulani.+ 21  Yesu akamuuliza: “Unataka nini?” Akamjibu: “Toa agizo kwamba hawa wanangu wawili waketi mmoja upande wako wa kuume na mwingine upande wako wa kushoto, katika Ufalme wako.”+ 22  Yesu akajibu: “Hamjui kile mnachoomba. Je, mnaweza kunywa kikombe ambacho niko karibu kukinywa?”+ Wakamwambia: “Tunaweza.” 23  Akawaambia: “Kwa kweli mtakunywa kikombe changu,+ lakini kuketi upande wangu wa kuume na upande wangu wa kushoto si haki yangu kutoa, bali wataketi wale ambao Baba yangu amewatayarishia.”+ 24  Wale wengine kumi waliposikia jambo hilo, wakawakasirikia hao ndugu wawili.+ 25  Lakini Yesu akawaita, akawaambia: “Mnajua kwamba watawala wa mataifa hupiga ubwana juu yao na wakuu hutumia mamlaka juu yao.+ 26  Haipaswi kuwa hivyo kati yenu;+ bali yeyote anayetaka kuwa mkubwa kati yenu lazima awe mhudumu wenu,+ 27  na yeyote anayetaka kuwa wa kwanza kati yenu lazima awe mtumwa wenu.+ 28  Kama vile Mwana wa binadamu alivyokuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu+ na kutoa uhai wake* uwe fidia badala ya wengi.”+ 29  Walipokuwa wakitoka Yeriko umati mkubwa ukamfuata. 30  Na tazama! wanaume wawili vipofu waliokuwa wameketi kando ya barabara waliposikia kwamba Yesu anapitia hapo, wakapaza sauti: “Bwana, Mwana wa Daudi, tuhurumie!”*+ 31  Hata hivyo, umati ukawakemea na kuwaambia wanyamaze; lakini wakapaza sauti hata zaidi, wakisema: “Bwana, Mwana wa Daudi, tuhurumie!”* 32  Basi Yesu akasimama, akawaita na kuwauliza: “Mnataka niwafanyie nini?” 33  Wakamjibu: “Bwana, tunaomba macho yetu yafunguliwe.” 34  Yesu akawasikitikia, akayagusa macho yao,+ na mara moja wakaanza kuona, nao wakamfuata.

Maelezo ya Chini

Yaani, karibu saa 3 asubuhi.
Yaani, karibu saa 6 mchana.
Yaani, karibu saa 9 alasiri.
Yaani, karibu saa 11 jioni.
Tnn., “ni baya; lina uovu.”
Au “mkarimu.”
Au, “akamwinamia.”
Au “nafsi yake.”
Au “tuonyeshe rehema!”
Au “tuonyeshe rehema!”