Kulingana na Mathayo 22:1-46

  • Mfano wa karamu ya ndoa (1-14)

  • Mungu na Kaisari (15-22)

  • Swali kuhusu ufufuo (23-33)

  • Amri mbili zilizo kuu zaidi (34-40)

  • Je, Kristo ni mwana wa Daudi? (41-46)

22  Yesu akasema tena nao akitumia mifano, akawaambia:  “Ufalme wa mbinguni ni kama mfalme aliyemwandalia mwanawe karamu ya ndoa.+  Akawatuma watumwa wake wawaite wale walioalikwa kwenye karamu ya ndoa, lakini hawakutaka kuja.+  Tena akawatuma watumwa wengine, akasema, ‘Waambieni wale walioalikwa: “Tazameni! Nimetayarisha chakula changu cha mchana, ng’ombe dume wangu na wanyama waliononeshwa wamechinjwa, na vitu vyote viko tayari. Njooni kwenye karamu ya ndoa.”’  Lakini wakapuuza na kwenda zao, wengine kwenye mashamba yao, na wengine kwenye biashara zao;+  lakini wengine wakawakamata wale watumwa wakawatendea kwa dharau na kuwaua.  “Mfalme akakasirika sana, akatuma majeshi yake yakawaue wauaji hao na kulichoma jiji lao.+  Kisha akawaambia watumwa wake, ‘Karamu ya ndoa iko tayari, lakini walioalikwa hawakustahili.+  Kwa hiyo, nendeni kwenye barabara zinazotoka jijini, na kumwalika kwenye karamu ya ndoa mtu yeyote mtakayemwona.’+ 10  Basi watumwa wakaenda barabarani na kuwaalika wote waliowaona, waovu na wema; na chumba cha sherehe za harusi kikajaa wageni.* 11  “Mfalme alipoingia kuwakagua wageni, akamwona mtu ambaye hakuwa amevaa vazi la ndoa. 12  Basi akamuuliza, ‘Mwenzangu, umeingiaje humu bila vazi la ndoa?’ Akakosa la kusema. 13  Ndipo mfalme akawaambia watumishi wake, ‘Mfungeni mikono na miguu, kisha mmtupe nje gizani. Huko ndiko atalia na kusaga meno yake.’ 14  “Kwa maana kuna wengi walioalikwa, lakini waliochaguliwa ni wachache.” 15  Ndipo Mafarisayo wakaenda kupanga njama pamoja ili wamtege Yesu kwa maneno yake.+ 16  Basi wakawatuma wanafunzi wao kwake, pamoja na wafuasi wa chama cha Herode.+ Wakamwambia: “Mwalimu, tunajua wewe husema ukweli nawe hufundisha njia ya Mungu katika kweli, na hutafuti kibali cha yeyote, kwa maana huangalii sura ya nje ya mtu. 17  Basi tuambie, unaonaje? Je, ni halali* au si halali kumlipa Kaisari kodi?”* 18  Lakini Yesu akijua uovu wao, akasema: “Kwa nini mnanijaribu, ninyi wanafiki? 19  Nionyesheni sarafu ya kodi.” Wakamletea dinari.* 20  Akawauliza: “Sura hii na maandishi haya ni ya nani?” 21  Wakajibu: “Ni ya Kaisari.” Ndipo akawaambia: “Basi, mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, na Mungu vitu vya Mungu.”+ 22  Waliposikia hilo, wakashangaa, wakamwacha na kwenda zao. 23  Siku hiyo, Masadukayo ambao husema hakuna ufufuo,+ wakaja na kumuuliza:+ 24  “Mwalimu, Musa alisema: ‘Mtu yeyote akifa bila kupata watoto, ndugu yake anapaswa kumwoa mke wake ili kumwinulia ndugu yake uzao.’+ 25  Basi kulikuwa na ndugu saba kati yetu. Wa kwanza akaoa kisha akafa, na kwa sababu hakuwa na watoto, akamwachia ndugu yake mke wake. 26  Ikawa vivyo hivyo kwa yule wa pili na wa tatu, na kwa wote saba. 27  Mwishowe, yule mwanamke akafa. 28  Basi, katika ufufuo, atakuwa mke wa nani kati ya wale saba? Kwa maana aliolewa na wote.” 29  Yesu akawajibu: “Ninyi mmekosea, kwa sababu hamjui Maandiko wala nguvu za Mungu;+ 30  kwa maana katika ufufuo, wanaume hawaoi, wala wanawake hawaolewi, bali wao ni kama malaika mbinguni.+ 31  Kuhusu ufufuo wa wafu, je, hamkusoma mliloambiwa na Mungu, aliposema: 32  ‘Mimi ni Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo’?+ Yeye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai.”+ 33  Umati uliposikia hilo, ukashangazwa na mafundisho yake.+ 34  Mafarisayo waliposikia kwamba Yesu amewanyamazisha Masadukayo, wakaja wakiwa kikundi kimoja. 35  Na mmoja wao aliyekuwa na ujuzi wa Sheria, akamuuliza swali ili kumjaribu: 36  “Mwalimu, ni amri gani iliyo kuu zaidi katika Sheria?”+ 37  Akamwambia: “‘Lazima umpende Yehova* Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi* yako yote na kwa akili yako yote.’+ 38  Hii ndiyo amri ya kwanza na iliyo kuu zaidi. 39  Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.’+ 40  Sheria yote na Manabii hutegemea amri hizo mbili.”+ 41  Basi Mafarisayo walipokuwa wamekusanyika, Yesu akawauliza:+ 42  “Mna maoni gani kuhusu Kristo? Ni mwana wa nani?” Wakamwambia: “Wa Daudi.”+ 43  Akawauliza: “Basi, kwa nini Daudi akiongozwa na roho+ anamwita Bwana, akisema, 44  ‘Yehova* alimwambia Bwana wangu: “Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwaweke maadui wako chini ya miguu yako”’?+ 45  Basi ikiwa Daudi anamwita Bwana, anawezaje kuwa mwanawe?”+ 46  Na hakuna mtu aliyeweza kumjibu neno, na tangu siku hiyo hakuna mtu aliyethubutu tena kumuuliza swali.

Maelezo ya Chini

Au “wale waliokuwa wameketi mezani.”
Au “sawa.”
Au “kodi ya kichwa.”
Angalia Kamusi.