Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Uamini Utatu?

Je, Uamini Utatu?

Zaidi ya watu bilioni mbili wanadai kuwa Wakristo. Wengi wao wanashirikiana na makanisa yanayofundisha Utatu—fundisho la kwamba Baba, Mwana, na roho takatifu ni Mungu mmoja. Utatu ulikuwaje fundisho rasmi? Zaidi ya hilo, je fundisho hilo linapatana na Biblia?

BIBLIA ilikamilishwa katika karne ya kwanza W.K. Mafundisho yaliyoongoza kwenye kuanzishwa kwa fundisho la Utatu yalianza kubuniwa katika mwaka wa 325 W.K. katika baraza fulani katika jiji la Nisea huko Asia Ndogo, ambalo leo linaitwa Iznik, nchini Uturuki. Hiyo ilikuwa zaidi ya karne mbili baada ya Biblia kukamilishwa. Kulingana na kitabu New Catholic Encyclopedia (Ensaiklopedia Mpya ya Katoliki), imani hiyo iliyoanzishwa na Baraza la Nisea ilitoa ufafanuzi rasmi wa kwanza kuhusu mafundisho ya msingi ya kanisa, kutia ndani ufafanuzi kumhusu Mungu na Kristo. Hata hivyo, kwa nini ilionekana kuwa muhimu kutoa ufafanuzi kumhusu Mungu na Kristo karne kadhaa baada ya Biblia kukamilishwa? Kwani Biblia haitoi ufafanuzi wa wazi kuhusu mambo hayo muhimu?

JE, YESU NI MUNGU?

Konstantino alipoanza kuwa mtawala pekee wa Milki ya Roma, watu waliodai kuwa Wakristo walikuwa wamegawanyika kuhusu uhusiano uliopo kati ya Mungu na Kristo. Je, Yesu alikuwa Mungu? Au je, aliumbwa na Mungu? Ili kutatua jambo hilo, Konstantino aliwakutanisha viongozi wa kanisa kule Nisea, si kwa sababu alitaka kupata kweli ya kidini, bali kwa sababu hakutaka dini igawe milki yake.

“Kwetu sisi Mungu ni mmoja tu, aliye Baba.”1 Wakorintho 8:6, Union Version

Konstantino aliwaomba maaskofu hao wafikie kauli moja, lakini hawakuweza kukubaliana. Kisha akapendekeza kwamba baraza hilo likubali wazo lisiloeleweka wazi kwamba Yesu alikuwa “wa asili moja” (homoousios) pamoja na Baba. Neno hilo linalotokana na falsafa ya Kigiriki ambalo halipatikani katika Biblia likaweka msingi wa fundisho la Utatu kama lilivyokuja kujulikana katika imani za kanisa. Kwa kweli, kufikia mwisho wa karne ya nne, fundisho la Utatu lilikuwa limeanza kueleweka kama linavyoeleweka leo, kutia ndani sehemu ya tatu, yaani, roho takatifu.

KWA NINI HABARI HII IKUPENDEZE?

Yesu alisema kwamba “waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa . . . kweli.” (Yohana 4:23) Kweli hiyo inapatikana katika  Biblia. (Yohana 17:17) Je, Biblia inafundisha kwamba Baba, Mwana, na roho takatifu ni watu watatu katika Mungu mmoja?

Kwanza kabisa, neno “Utatu” halipatikani katika Biblia. Pili, Yesu hakuwahi kudai kwamba yuko sawa na Mungu. Badala yake, Yesu alimwabudu Mungu. (Luka 22:41-44) Jambo la tatu ni uhusiano wa Yesu na wafuasi wake. Hata baada ya kufufuliwa akiwa na mwili wa roho, Yesu aliwaita wafuasi wake “ndugu zangu.” (Mathayo 28:10) Je, walikuwa ndugu za Mungu Mweza-Yote? Bila shaka la! Lakini kupitia imani yao katika Kristo—Mwana mzaliwa kwanza wa Mungu—wao pia walikuja kuwa wana wa huyo Baba mmoja. (Wagalatia 3:26) Linganisha maandiko fulani ya ziada pamoja na maneno yafuatayo kutoka kwa orodha ya imani zilizoanzishwa na Baraza la Nisea.

Imani ya Nisea inasema hivi:

“Tunaamini . . . katika Bwana mmoja Yesu Kristo, . . . [aliye] kwa asili ya Baba, Mungu kutoka kwa Mungu, Nuru kutoka kwa Nuru, Mungu wa kweli kutoka kwa Mungu wa kweli.”

Biblia inasema hivi:

  • “Baba ni mkuu kuliko mimi [Yesu].”Yohana 14:28. *

  • “Ninapaa [Yesu] kwenda kwa Baba yangu naye ni Baba yenu, kwa Mungu wangu naye ni Mungu wenu.”Yohana 20:17.

  • “Kwetu sisi Mungu ni mmoja tu, aliye Baba.”1 Wakorintho 8:6.

  • “Ahimidiwe Mungu, Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo.”1 Petro 1:3.

  • “Haya ndiyo anenayo yeye aliye Amina [Yesu], . . . mwanzo wa kuumba kwa Mungu.”Ufunuo 3:14. *

^ fu. 13 Italiki ni zetu. Manukuu yote katika sehemu hii yametolewa kwenye tafsiri ya Union Version.

^ fu. 17 Kitabu cha kujifunzia Biblia chenye kichwa Biblia Inafundisha Nini Hasa? kina sura hizi mbili: “Ukweli Kumhusu Mungu?” na “Yesu Kristo Ni Nani?” Unaweza kujipatia nakala kutoka kwa Mashahidi wa Yehova au ukisome kwenye tovuti ya www.pr418.com/sw.