Ezekieli 18:1-32

  • Kila mutu anapaswa kubeba hatia ya zambi zake mwenyewe (1-32)

    • Nafsi yenye inatenda zambi itakufa (4)

    • Mwana hatalipia zambi ya baba yake (19, 20)

    • Sifurahie kifo cha mutu muovu (23)

    • Kutubu kunalinda uzima (27, 28)

18  Na neno la Yehova likakuja tena kwangu, na kusema:  “Mezali hii yenye munataja katika inchi ya Israeli inamaanisha nini, ‘Baba wamekula zabibu chachu, lakini meno ya wana ndiyo yanatiwa ukakasi’?*+  “‘Kama vile hakika ninaishi,’ ni vile Bwana Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi Yehova anasema, ‘hamutaendelea kutaja usemi huo katika Israeli.  Angalia! Nafsi zote*—ni zangu. Kama vile nafsi ya baba ni vile pia nafsi ya mwana—ni zangu. Nafsi* yenye inatenda zambi ndiyo itakufa.*  “‘Wazia kama mutu ni mwenye haki na anatenda mambo ya haki na yenye kuwa sawa.  Hakule zabihu zenye zinatolewa kwa sanamu kwenye milima;+ haangalie sanamu zenye kuchukiza* za nyumba ya Israeli; hamuchafue bibi ya jirani yake+ ao kulala na mwanamuke mwenye kuwa katika siku zake za kuona mwezi;*+  hamutendee mubaya mutu yeyote,+ lakini anarudisha kitu chenye mwenye kuwa na deni lake aliwekesha kwa ajili ya mukopo;+ hamunyanganye mutu yeyote,+ lakini anapatia chakula chake mwenye njaa+ na anamufunika nguo mwenye kuwa uchi;+  haombe faida wala kulipisha faida ya juu sana,+ lakini anajizuia ili asitende bila haki;+ anatenda haki ya kweli katikati ya mutu na mwenzake;+  na anaendelea kutembea katika sheria zangu na kushika maamuzi yangu ya hukumu ili kutenda kwa uaminifu. Mutu huyo ni mwenye haki na hakika ataendelea kuishi,’+ ni vile Bwana Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi Yehova anasema. 10  “‘Lakini kama amezaa mwana mwenye kuwa munyanganyi+ ao muuaji*+ ao mwenye kufanya jambo lolote kati ya mambo haya mengine 11  (hata kama baba hajafanya jambo lolote kati ya mambo hayo)—anakula zabihu zenye zilitolewa kwa sanamu kwenye milima, anamuchafua bibi ya jirani yake, 12  anatendea mubaya wenye uhitaji na maskini,+ anakamata vitu kwa unyanganyi, harudishe kitu chenye kiliwekeshwa kwa ajili ya mukopo; anaangalia sanamu zenye kuchukiza,+ anajiingiza katika mazoea yenye kuchukiza,+ 13  analipisha faida ya juu sana na kuomba faida+⁠—⁠basi mwana huyo hataendelea kuishi. Kwa sababu ya mambo hayo yote yenye kuchukiza yenye amefanya, hakika atauawa. Damu yake mwenyewe itakuwa juu yake. 14  “‘Lakini kama baba iko* na mwana mwenye anaona zambi zote zenye baba yake amefanya, na hata kama anaziona, yeye hafanye mambo kama hayo. 15  Hakule zabihu zenye zilitolewa kwa sanamu kwenye milima; haangalie sanamu zenye kuchukiza za nyumba ya Israeli; hamuchafue bibi ya jirani yake; 16  hamutendee mutu yeyote mubaya; hanyanganye kitu chenye kiliwekeshwa kwa ajili ya mukopo; hakamate kitu chochote kwa unyanganyi; anapatia chakula chake mwenye njaa na anamufunika nguo mwenye kuwa uchi; 17  anaepuka kukandamiza maskini; halipishe faida ya juu sana wala kuomba faida; na anashika maamuzi yangu ya hukumu na kutembea katika sheria zangu. Mutu huyo hatakufa kwa sababu ya kosa la baba yake. Hakika ataendelea kuishi. 18  Lakini kwa sababu baba yake alizoea kupunja, alimunyanganya ndugu yake, na alifanya mambo ya mubaya kati ya watu wake, atakufa kwa sababu ya kosa lake. 19  “‘Lakini mutasema: “Sababu gani mwana hana hatia kwa sababu ya kosa la baba yake?” Kwa kuwa mwana ametenda haki na uadilifu,* ameshika sheria zangu zote na kuzitenda, hakika ataendelea kuishi.+ 20  Nafsi yenye inatenda zambi ndiyo itakufa.*+ Mwana hatakuwa na hatia kwa sababu ya kosa la baba yake, na baba hatakuwa na hatia kwa sababu ya kosa la mwana wake. Haki ya mwenye haki itahesabiwa kwake mwenyewe, na uovu wa muovu utahesabiwa kwake mwenyewe.+ 21  “‘Sasa kama mutu muovu anageuka na kuacha zambi zote zenye amefanya na anashika sheria zangu na kutenda haki na uadilifu,* hakika ataendelea kuishi. Hatakufa.+ 22  Hakuna kosa lolote kati ya makosa yenye ametenda lenye litahesabiwa* kwake.+ Ataendelea kuishi kwa sababu ya kutenda haki.’+ 23  “‘Je, ninafurahia kabisa kifo cha mutu muovu?’+ ni vile Bwana Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi Yehova anasema. ‘Je, mimi sifurahie kwamba aache njia zake naye aendelee kuishi?’+ 24  “‘Lakini wakati mwenye haki anaacha haki yake na kufanya mabaya,* na kufanya mambo yote yenye kuchukiza yenye waovu wanafanya, je ataishi? Hakuna tendo lolote lenye litakumbukwa kati ya matendo yenye haki yenye alifanya.+ Atakufa kwa sababu ya ukosefu wake wa uaminifu na zambi yenye alitenda.+ 25  “‘Lakini mutasema: “Njia ya Yehova haiko ya haki.”+ Tafazali sikiliza, Ee nyumba ya Israeli! Je, njia yangu ndiyo haiko ya haki?+ Je, haiko njia zenu ndizo haziko za haki?+ 26  “‘Wakati mwenye haki anaacha haki yake na kufanya mabaya na anakufa kwa sababu ya ubaya huo, atakufa kwa sababu ya makosa yake mwenyewe. 27  “‘Na wakati mutu muovu anageuka na kuacha uovu wenye ametenda na kuanza kutenda haki na uadilifu,* atalinda uzima wake.*+ 28  Wakati anatambua na kuacha makosa yote yenye ametenda, hakika ataendelea kuishi. Hatakufa. 29  “‘Lakini nyumba ya Israeli itasema: “Njia ya Yehova haiko ya haki.” Je, kweli njia zangu ndizo haziko za haki, Ee nyumba ya Israeli?+ Je, haiko njia zenu ndizo haziko za haki?’ 30  “‘Kwa hiyo, nitamuhukumu kila mumoja wenu kulingana na njia zake,+ Ee nyumba ya Israeli,’ ni vile Bwana Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi Yehova anasema. ‘Muache, ndiyo, muache kabisa makosa yenu yote, ili yasikuwe kikwazo chenye kinaleta hatia juu yenu. 31  Mujiondolee makosa yenu yote yenye mumefanya+ na mujipatie* moyo mupya na roho mupya,+ kwa maana sababu gani mukufe,+ Ee nyumba ya Israeli?’ 32  “‘Sifurahie hata kidogo kifo cha mutu yeyote,’+ ni vile Bwana Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi Yehova anasema. ‘Kwa hiyo mugeuke na kuishi.’”+

Maelezo ya Chini

Tnn., “ganzi.”
Ao “uzima.” Angalia Maana ya Maneno.
Ao “Mutu.” Angalia Maana ya Maneno.
Ao “Mutu mwenye anatenda zambi ndiye atakufa.”
Pengine neno la Kiebrania lenye linatumiwa hapa linahusiana na maneno “mavi ya wanyama” na linatumiwa ili kuonyesha zarau.
Ao “hezi.”
Tnn., “mutu mwenye kumwanga damu.”
Ao “eko.”
Ao “Mutu mwenye anatenda zambi ndiye atakufa.”
Tnn., “litakumbukwa.”
Ao “anakosa kutenda haki.”
Ao “nafsi yake.” Angalia Maana ya Maneno.
Tnn., “mujifanyie.”