Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

A4

Jina la Mungu Katika Maandiko ya Kiebrania

Jina la Mungu katika herufi za Kiebrania cha zamani zenye zilitumiwa mbele ya uhamisho wa Babiloni

Jina la Mungu katika herufi za Kiebrania cha zamani zenye zilitumiwa kisha uhamisho wa Babiloni

Jina la Mungu, lenye linaandikwa kwa herufi ine (4) za Kiebrania יהוה, linapatikana karibu mara 7000 katika Maandiko ya Kiebrania. Katika tafsiri hii herufi hizo ine, zenye kujulikana kuwa Tetragramatoni, zimetafsiriwa “Yehova.” Hilo ndilo jina lenye linapatikana mara nyingi zaidi katika Biblia. Hata kama waandikaji wa Biblia wenye waliongozwa na roho ya Mungu walimutaja Mungu kwa kutumia majina mengi ya cheo na maneno mengine ya kueleza mambo, kama vile “Mweza-Yote,” “Mwenye Kuwa Juu Zaidi,” na “Bwana,” Tetragramatoni tu ndilo jina la pekee lenye walitumia ili kumutambulisha Mungu.

Yehova Mungu mwenyewe aliongoza waandikaji wa Biblia watumie jina lake. Kwa mufano, alimuongoza nabii Yoeli kupitia roho yake aandike hivi: “Kila mutu mwenye anaitia jina la Yehova ataokolewa.” (Yoeli 2:32) Na Mungu alimuongoza mwandikaji mumoja wa zaburi kuandika hivi: “Wajue kwamba wewe, mwenye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Mwenye Kuwa Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” (Zaburi 83:18) Kwa kweli, jina la Mungu linapatikana karibu mara mia saba (700) katika kitabu cha Zaburi peke yake​—kitabu cha maandishi ya kishairi yenye yalipaswa kuimbwa na kurudiliwa-rudiliwa na watu wa Mungu. Basi, sababu gani jina la Mungu linakosekana katika tafsiri nyingi za Biblia? Sababu gani tafsiri hii inatumia jina “Yehova”? Na jina la Mungu, Yehova, linamaanisha nini?

Sehemu za kitabu cha Zaburi katika Kitabu cha Kukunjwa cha Bahari ya Chumvi za tangu nusu ya kwanza ya karne ya kwanza (1-100) K.K.Y. Maandishi hayo yanaandikwa kwa kutumia herufi za Kiebrania zenye zilikuwa zinatumiwa sana kisha uhamisho wa Babiloni, lakini Tetragramatoni inaonekana mahali pengi katika herufi za Kiebrania cha zamani

Sababu gani jina la Mungu linakosekana katika tafsiri nyingi za Biblia? Kuko sababu nyingi. Watu fulani wanafikiri kama Mungu Mweza-Yote hana lazima ya kuwa na jina la pekee lenye kumutambulisha. Inaonekana wengine wamechochewa na desturi ya Wayahudi ya kuepuka kutumia jina hilo, pengine kwa sababu ya kuogopa kulichafua. Kuko pia wengine wenye wanaamini kama kwa kuwa hakuna mutu mwenye anajua kwa uhakika namna jina la Mungu lilitamukwa kabisa, ni muzuri zaidi kutumia tu jina la cheo, kama vile “Bwana” ao “Mungu.” Lakini, mawazo hayo hayana musingi kwa sababu zenye kufuata:

  • Wale wenye wanasema kama Mungu Mweza-Yote hana lazima ya kuwa na jina la pekee wanasahau kwamba kopi za kwanza-kwanza za Neno lake, kutia ndani zile zenye zililindwa tangu mbele ya wakati wa Kristo, ziko na jina la pekee la Mungu. Kama vile ilionyeshwa pale juu, Mungu aliongoza mambo ili jina lake liwekwe katika Neno lake karibu mara 7000. Ni wazi kwamba, anataka tujue na tutumie jina lake.

  • Watafsiri wenye kuondoa jina la Mungu kwa sababu ya kuheshimia desturi ya Wayahudi wanakosa kutambua jambo moja la musingi. Hata kama waandishi fulani Wayahudi walikataa kutamuka jina la Mungu, hawakuliondoa katika kopi zao za Biblia. Vitabu vya kukunjwa vya zamani vyenye vilipatikana katika Qumran, karibu na Bahari ya Chumvi, viko na jina hilo mahali pengi. Watafsiri fulani wa Biblia wanaonyesha kwamba jina la Mungu lilipatikana katika maandishi ya kwanza kwa kuandika jina la heshima “BWANA” kwa herufi kubwa. Lakini bado ulizo ni hili, Sababu gani watafsiri hao walijipatia uhuru wa kubadilisha ao kuondoa jina la Mungu katika Biblia hata kama wanakubali kwamba linapatikana katika maandishi ya Biblia mara maelfu? Wanaamini ni nani aliwapatia mamlaka ya kufanya mabadiliko hayo? Wao tu ndio wanajua.

  • Lakini wale wenye wanasema kwamba jina la Mungu halipaswe kutumiwa kwa sababu namna ya kulitamuka haijulikane kabisa hawasite kutumia jina Yesu. Hata hivyo, wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza (1-100) walitamuka jina lake tofauti sana na namna Wakristo wengi wanalitamuka leo. Kwa Wakristo Wayahudi, inawezekana jina Yesu lilitamukwa Ye·shuʹa‛. Na jina la cheo “Kristo” lilitamukwa Ma·shiʹach, ao “Masiya.” Wakristo wenye kuzungumuza Kigiriki walimuita I·e·sousʹ Khri·stosʹ, na Wakristo wenye kuzungumuza Kilatini walimuita Ieʹsus Chriʹstus. Kupitia uongozi wa roho ya Mungu, tafsiri ya Kigiriki ya jina lake iliandikwa katika Biblia, na hilo linaonyesha kama kwa busara Wakristo wa karne ya kwanza (1-100) walitumia jina hilo namna lilikuwa linatamukwa na watu wengi katika luga yao. Vilevile, Halmashauri ya Kutafsiri Biblia ya Ulimwengu Mupya inaamini kama ni muzuri kutumia jina “Yehova,” hata kama haiko vile kabisa jina la Mungu lilitamukwa katika Kiebrania cha zamani.

Sababu gani Tafsiri ya Ulimwengu Mupya inatumia jina “Yehova”? Katika Swahili (Congo), herufi ine (4) za Tetragramatoni (יהוה) zinaandikwa kwa herufi YHWH. Kama vile ilikuwa kuhusu maneno yote yenye yaliandikwa katika Kiebrania cha zamani, Tetragramatoni haikukuwa na herufi za sauti. Katika matamushi yao ya kila siku, wasomaji Waebrania waliingiza kwa vyepesi herufi za sauti zenye zilifaa.

Miaka karibu elfu moja kisha Maandiko ya Kiebrania kumalizika, Wayahudi wenye elimu nyingi waliunda alama za matamushi za kusaidia kuonyesha ni herufi gani za sauti zenye zinapaswa kutumiwa wakati wa kusoma Kiebrania. Lakini wakati huo, Wayahudi wengi walikuwa na mawazo ya ushirikina kwamba ilikuwa kosa kusema kwa sauti jina la pekee la Mungu, kwa hiyo walitumia majina mengine. Hivyo, inaonekana kwamba wakati waliandika Tetragramatoni, walichanganya herufi za sauti zenye walitumia katika majina mengine na zile herufi ine (4) zenye kuonyesha jina la Mungu. Kwa hiyo, maandishi yenye kuwa na alama za matamushi hayasaidie kutambua namna jina hilo lilikuwa linatamukwa zamani katika Kiebrania. Watu fulani wanafikiri kwamba jina la Mungu lilikuwa linatamukwa ­“Yahweh,” lakini wengine wanapendekeza njia zingine tofauti. Kitabu kimoja cha kukunjwa cha Bahari ya Chumvi chenye kuwa na sehemu ya kitabu cha Mambo ya Walawi katika Kigiriki kinatafsiri jina la Mungu kuwa Iao. Zaidi ya namna hiyo, waandikaji wa zamani wa Kigiriki wanapendekeza pia matamushi Iae, I·a·beʹ, ao I·a·ou·eʹ. Lakini, hakuna sababu ya kuweka sheria. Kwa kweli, hatujue namna watumishi wa Mungu wa zamani walitamuka jina hilo katika Kiebrania. (Mwanzo 13:4; Kutoka 3:15) Tunajua tu kwamba Mungu alitumia mara nyingi jina lake wakati alikuwa anazungumuza na watu wake, kwamba walitumia jina hilo ili kuzungumuza naye, na kwamba walilitumia kwa uhuru wakati walikuwa wanazungumuza na wengine.​—Kutoka 6:2; 1 Wafalme 8:23; Zaburi 99:9.

Basi, sababu gani tafsiri hii inatumia jina “Yehova”? Ni kwa sababu jina hilo limetumiwa tangu zamani katika luga ya Swahili (Congo).

Jina la Mungu katika Mwanzo 15:2 katika tafsiri ya William Tyndale ya Pantateki, 1530

Jina la pekee la Mungu lilitumiwa kwa mara ya kwanza katika Biblia ya Kiingereza katika mwaka wa 1530 katika tafsiri ya William Tyndale ya Pantateki. Alitumia jina “Iehouah.” Kisha, luga ya Kiingereza ilibadilika, na jina la Mungu lilianza kuandikwa kwa njia mupya. Kwa mufano, katika mwaka wa 1612, Henry Ainsworth alitumia jina “Iehovah” katika tafsiri yake yote ya kitabu cha Zaburi. Kisha, katika mwaka wa 1639, wakati tafsiri hiyo ilirekebishwa na kuchapishwa pamoja na Pantateki, jina “Jehovah” lilitumiwa. Katika mwaka wa 1901, watafsiri wenye walitokeza Biblia ya American Standard Version walitumia jina “Jehovah” mahali jina la Mungu lilionekana katika maandishi ya Kiebrania.

Wakati alieleza sababu gani alitumia jina “Jehovah” kuliko kutumia jina “Yahweh” katika kitabu chake Studies in the Psalms cha mwaka wa 1911, mutu mwenye elimu nyingi ya Biblia mwenye kuheshimiwa, Joseph Bryant Rotherham alisema kama alitaka kutumia “jina lenye kujulikana zaidi (na kukubaliwa kabisa) na wasomaji wengi wa Biblia.” Katika mwaka wa 1930, mutu mwenye elimu nyingi A. F. ­Kirkpatrick alitoa wazo kama hilo kuhusu matumizi ya jina “Jehovah.” Alisema hivi: “Wasomi wa luga wa siku hizi wanasema kwamba linapaswa kusomwa Yahveh ao Yahaveh; lakini inaonekana kwamba jina JEHOVAH ndilo limetumiwa sana katika luga ya Kiingereza, na jambo la maana kabisa haiko namna jina hilo linapaswa kutamukwa kabisa, lakini ni kukubali kama ni Jina la Pekee, hapana tu jina la cheo kama vile ‘Bwana.’”

Tetragramatoni, YHWH: “Yeye Anafanya Kuwa”

Kitenzi HWH: “kuwa”

Jina Yehova linamaanisha nini? Katika Kiebrania, jina Yehova linatokana na kitenzi (verbe) chenye kumaanisha “kuwa,” na watu wengi wenye elimu nyingi wanafikiri kwamba hilo linaonyesha hali ya kitenzi hicho cha Kiebrania ya kufanya jambo fulani litendeke. Kwa hiyo, Halmashauri ya Kutafsiri Biblia ya Ulimwengu Mupya inaelewa kama jina la Mungu linamaanisha “Yeye Anafanya Kuwa.” Watu wenye elimu nyingi wako na maoni yenye kutofautiana, kwa hiyo hatuwezi kuweka sheria kwamba hiyo ndiyo maana pekee ya jina hilo. Lakini, maana hiyo inapatana kabisa na daraka la Yehova akiwa Muumbaji wa vitu vyote na Mutimizaji wa kusudi lake. Yeye hakufanya tu ulimwengu wenye kuonekana na viumbe vyenye akili vikuwe, lakini kama vile matukio yanaonyesha, anaendelea kufanya mapenzi yake na kusudi lake vitimie.

Kwa hiyo, maana ya jina Yehova haielezwe tu na kitenzi (verbe) chenye kupatikana katika andiko la Kutoka 3:14, lenye linasema: “Nitakuwa Kile Ninachagua Kuwa” ao, “Nitakuwa Kile Nitakuwa.” Kwa kweli kabisa, maneno hayo hayatoe maana kamili ya jina la Mungu. Lakini, yanafunua sehemu moja ya utu wa Yehova, yakionyesha kwamba anakuwa kile chenye kinahitajika katika kila hali ili kutimiza kusudi lake. Kwa hiyo, hata kama jina Yehova linaweza kutia ndani wazo hilo, jina hilo halimaanishe tu kile anachagua kuwa. Linamaanisha pia kile chenye anafanya kikuwe kuhusiana na uumbaji wake na kutimizwa kwa kusudi lake.