Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

A5

Jina la Mungu Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo

Watu wenye elimu nyingi ya Biblia wanakubali kwamba jina la pekee la Mungu, kama vile linaandikwa na Tetragramatoni (יהוה), linapatikana karibu mara 7000 katika maandishi ya kwanza ya Maandiko ya Kiebrania. Lakini, watu wengi wanawaza kama halikupatikana katika maandishi ya kwanza ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kwa sababu hiyo, Biblia nyingi za sasa za Swahili (Congo) hazitumie jina Yehova katika tafsiri ya maandiko yenye kuitwa Agano Jipya. Hata wakati wanatafsiri maneno yenye yalichukuliwa katika Maandiko ya Kiebrania yenye ndani yake Tetragramatoni inapatikana, watafsiri wengi wanatumia jina “Bwana” kuliko kutumia jina la pekee la Mungu.

Biblia​Tafsiri ya Ulimwengu Mupya haifuate zoea hilo la watafsiri wengi. Inatumia jina Yehova mara mia mbili makumi tatu na saba (237) katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Ili kuamua kufanya vile, watafsiri walifikiria mambo haya mbili ya maana: (1) Maandishi ya Kigiriki yenye tuko nayo leo haiko ndiyo ya kwanza kabisa. Kati ya maelfu ya kopi zenye zinapatikana leo, nyingi ziliandikwa miaka mia mbili (200) hivi kisha maandishi ya kwanza kuandikwa. (2) Wakati huo, wale wenye walikuwa wanaandika kopi za maandishi walibadilisha Tetragramatoni na Kyʹri·os, neno la Kigiriki lenye maana yake ni “Bwana,” ao waliandika kopi za maandishi kwenye jina hilo lilikuwa tayari limeondolewa.

Halmashauri ya Kutafsiri Biblia ya Ulimwengu Mupya iliona kwamba kuko mambo ya hakika yenye kuonyesha kuwa Tetragramatoni ilipatikana katika maandishi ya kwanza ya Kigiriki. Uamuzi wao ulitegemea uhakika huu:

  • Kopi za Maandiko ya Kiebrania zenye zilitumiwa katika siku za Yesu na mitume wake zilikuwa na Tetragramatoni katika maandishi yote. Zamani, hesabu kidogo ya watu walikataa jambo hilo. Sasa kwa kuwa kopi za Maandiko ya Kiebrania za tangu karne ya kwanza (1-100) zimevumbuliwa katika Qumran, jambo hilo limehakikishwa bila mashaka yoyote.

  • Katika siku za Yesu na mitume wake, Tetragramatoni ilipatikana pia katika tafsiri za Kigiriki za Maandiko ya Kiebrania. Kwa mamia ya miaka, watu wenye elimu nyingi walifikiri kama Tetragramatoni haikukuwa katika maandishi ya tafsiri ya Kigiriki ya Septante ya Maandiko ya Kiebrania. Kisha, katikati ya karne ya 20 (1901-​2000), watu wenye elimu nyingi walivumbua vipande fulani vya zamani sana vya toleo la Kigiriki la Septante lenye lilikuwa katika siku za Yesu. Vipande hivyo viko na jina la pekee la Mungu, likiwa limeandikwa katika herufi za Kiebrania. Kwa hiyo katika siku za Yesu, kopi za Maandiko katika Kigiriki zilikuwa na jina la Mungu. Hata hivyo, kuanzia karne ya 4 (301-​400) K.K.Y., maandishi mengi ya Septante ya Kigiriki, kama vile Kodeksi ya Vatikani na Kodeksi ya Sinai, hazikukuwa na jina la Mungu katika vitabu kuanzia Mwanzo mupaka Malaki (kwenye lilikuwa katika maandishi ya mbele ya wakati huo). Kwa hiyo, haishangaze kwamba katika maandishi yenye yalilindwa kuanzia wakati huo, jina la Mungu halipatikane katika ile yenye kuitwa Agano Jipya, ao sehemu ya Biblia ya Maandiko ya Kigiriki.

    Yesu alisema hivi waziwazi: “Nimekuja katika jina la Baba yangu.” Pia, alikazia kwamba alifanya kazi zake katika “jina la Baba” yake

  • Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yenyewe yanasema kama mara nyingi Yesu alitaja jina la Mungu na kulijulisha wengine. (Yohana 17:6, 11, 12, 26) Yesu alisema hivi waziwazi: “Nimekuja katika jina la Baba yangu.” Pia alikazia kwamba alifanya kazi zake katika “jina la Baba” yake.​—Yohana 5:43; 10:25.

  • Kwa kuwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yenye yaliongozwa na roho ya Mungu yaliongezwa kwenye Maandiko Matakatifu ya Kiebrania, kukosekana bila kutazamia kwa jina la Yehova katika maandishi hayo kungefanya ionekane kuwa sehemu hizo mbili hazipatane. Karibu katikati ya karne ya kwanza (1-​100) K.K.Y., mwanafunzi Yakobo aliambia hivi wazee katika Yerusalemu: “Simioni ameeleza kikamili namna Mungu kwa mara ya kwanza alielekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kati yao watu kwa ajili ya jina lake.” (Matendo 15:14) Yakobo hangesema maneno hayo ikiwa hakuna mutu katika karne ya kwanza (1-100) mwenye alijua ao kutumia jina la Mungu.

  • Jina la Mungu linapatikana katika kifupi chake katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kwenye Ufunuo 19:1, 3, 4, 6, jina la Mungu linapatikana katika neno “Haleluya.” Hilo linatokana na neno la Kiebrania lenye neno kwa neno linamaanisha “Mumusifu Yah.” “Yah” ni kifupi cha jina Yehova. Majina mengi yenye yalitumiwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalitokana na jina la Mungu. Kwa kweli, vitabu fulani vinaeleza kwamba jina la Yesu mwenyewe linamaanisha “Yehova Ni Wokovu.”

  • Maandishi ya zamani ya Kiyahudi yanaonyesha kama Wakristo Wayahudi walitumia jina la Mungu katika maandishi yao. Maandishi yenye kuitwa Tosefta yenye kuwa mukusanyo wa sheria za Wayahudi, yenye yalimalizwa karibu mwaka wa 300 K.K.Y., yanasema hivi kuhusu maandishi ya Kikristo yenye yaliteketezwa katika siku ya Sabato: “Vitabu vya Waeneza-injili na vitabu vya minim [watu wenye wanawaziwa kuwa ni Wakristo Wayahudi] haviokolewe kutokana na moto. Lakini vinaachwa viteketezwe kwa moto mahali vinapatikana, pamoja na nafasi zake zenye kuwa na Jina la Mungu.” Maandishi yaleyale yanataja Rabi Yosé Mugalilaya, mwenye aliishi kwenye mwanzo wa karne ya pili (101-​200) K.K.Y., akisema kama katika siku zingine za juma, “mutu anakata nafasi zenye kuwa na Jina la Mungu ndani ya hayo [inaeleweka kuwa anazungumuzia maandishi ya Kikristo] na kuziweka mahali fulani, na maandishi yenye yanabakia yanateketezwa kwa moto.”

  • Watu fulani wenye elimu nyingi ya Biblia wanakubali kwamba inaonekana kuwa jina la Mungu lilipatikana katika Maandiko ya Kiebrania yenye yalitajwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Katika habari yenye kichwa “Tetragramatoni Katika Agano Jipya,” kitabu kimoja kinasema hivi: “Kuko uhakika fulani wa kwamba Tetragramatoni, Jina la Mungu, Yahweh, lilipatikana katika maneno fulani ao maneno yote ya A[gano] la K[ale] yenye yalitajwa katika A[gano] J[ipya] wakati vitabu vya AJ viliandikwa kwa mara ya kwanza.” (The Anchor Bible Dictionary) Mutu mwenye elimu nyingi George Howard anasema hivi: “Kwa kuwa Tetragramu ilikuwa ingali yenye kuandikwa katika kopi za tafsiri ya Biblia ya Kigiriki [Septante] yenye ilifanyiza Maandiko ya kanisa la kwanza-kwanza, ni jambo lenye kufaa kuamini kwamba waandikaji wa A[gano] J[ipya], wakati wa kutaja Andiko, walilinda Tetragramu katika maandishi ya Biblia.”

  • Watafsiri wa Biblia wenye kujulikana wametumia jina la Mungu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Wengi kati ya watafsiri hao walifanya vile zamani mbele hata ya Tafsiri ya Ulimwengu Mupya kutokezwa. Kati ya watafsiri hao na kazi zao tunaweza kutaja: A Literal Translation of the New Testament . . . From the Text of the Vatican Manuscript, ya Herman Heinfetter (1863); The Emphatic Diaglott ya Benjamin Wilson (1864); The Epistles of Paul in Modern English, ya George Barker Stevens (1898); St. Paul’s Epistle to the Romans, ya W. G. Rutherford (1900); The New Testament Letters, ya J.W.C. Wand, Askofu wa Londres (1946). Zaidi ya hayo, katika tafsiri moja ya Kihispania ya mwanzo wa karne ya 20 (1901-​2000), mutafsiri Pablo Besson alitumia “Jehová” kwenye Luka 2:15 na Yuda 14, na karibu maelezo mia moja (100) ya chini katika tafsiri yake yanapendekeza jina la Mungu kuwa lingetumiwa pale. Zamani mbele ya tafsiri hizo, matoleo ya Kiebrania ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo tangu karne ya 16 (1501-​1600) na kuendelea yalitumia Tetragramatoni katika maandiko mengi. Katika luga ya Kijerumani peke yake, tafsiri karibu kumi na moja (11) zinatumia “Jehovah” (ao tafsiri ya jina la Kiebrania “Yahweh”) katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na watafsiri ine (4) wanaongeza jina la Mungu katika paranteze kisha jina la cheo “Bwana.” Tafsiri za Kijerumani zaidi ya makumi saba (70) zinatumia jina la Mungu katika maelezo ya chini ao maelezo mengine.

  • Tafsiri za Biblia katika luga mbalimbali zaidi ya mia moja ziko na jina la Mungu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Luga nyingi za Afrika, za kienyeji za Amerika, za Asia, Ulaya, na visiwa vya Pasifiki zinatumia sana jina la Mungu. (Ona oroza kwenye ukurasa wa 1742 na 1743.) Watafsiri wa matoleo hayo waliamua kutumia jina la Mungu kwa sababu zenye kufanana na zile zenye zimetajwa pale juu. Tafsiri fulani kati ya tafsiri hizo za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zimetokea hivi karibuni, kama vile tafsiri ya Rotuman Bible (1999), yenye inatumia “Jihova” mara makumi tano na moja (51) katika mistari makumi ine na munane (48), na tafsiri ya Batak (Toba) (1989) kutoka Indonesia, yenye inatumia “Jahowa” mara mia moja na kumi (110).

Jina la Mungu kwenye Marko 12:29, 30 katika tafsiri moja ya luga ya Hawaii

Bila shaka, kuko musingi muzuri wa kurudisha jina la Mungu, Yehova, katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Hilo kabisa ndilo jambo lenye watafsiri wa Tafsiri ya Ulimwengu Mupya wamefanya. Wanaheshimia sana jina la Mungu na wako na woga wenye kufaa wa kuondoa jambo lolote lenye lilikuwa katika maandishi ya kwanza.​—Ufunuo 22:18, 19.