Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KUMI NA MUNANE

Alifikiri na Kuamua Katika Moyo Wake

Alifikiri na Kuamua Katika Moyo Wake

1, 2. Safari ya Maria iko namna gani, na sababu gani Maria ana matatizo ya kukaa vizuri juu ya punda.

MARIA amesafiri kwa muda murefu juu ya punda, lakini yeye ana matatizo ya kukaa vizuri juu ya punda huyo. Yosefu iko mbele, anashika kamba inayofunga punda, anatembea katika njia inayowaongoza Bethlehemu mbali sana. Mara nyingine, Maria anasikia kitoto kikichezacheza ndani ya tumbo lake.

2 Mimba yake imekwisha kukomaa; Biblia inasema kwamba wakati huo ‘alikuwa karibu kuzaa.’ (Lu. 2:5) Wakati Yosefu na Maria wanapitia karibu-karibu ya mashamba, labda walimaji fulani wanaacha kwanza kulima ao kupanda, wanawatazama na wanajiuliza sababu gani mwanamuke aliye katika hali kama hiyo anaweza kukubali kufunga safari hiyo. Sababu gani Maria anafunga safari hiyo ndefu kutoka Nazareti, nyumbani kwao?

3. Maria alikuwa amepewa mugao gani, na tutajifunza nini kumuhusu Maria?

3 Mambo yote yalianza kumekwisha kupita miezi fulani wakati mwanamuke huyo alipopewa mugao wa pekee ambao hakuna mwanadamu yeyote amekwisha kupewa. Maria anapaswa kuzaa mutoto atakayekuwa yule Masiya aliyekuwa anangojewa, Mwana wa Mungu! (Lu. 1:35) Kadiri wakati wa kuzaa unakaribia, ndivyo safari hiyo inakuwa ya lazima sana. Katika safari hiyo, Maria anakutana na mambo mengi yanayojaribu imani yake. Basi, acha tuone ni nini iliyomusaidia kubaki nguvu kiroho.

Safari Kuelekea Bethlehemu

4, 5. (a) Sababu gani Yosefu na Maria wanajielekeza Bethlehemu? (b) Amri ya Kaisari inatimiza unabii gani?

4 Katika safari yao, Yosefu na Maria wanasafiri pia na watu wengine. Kaisari Auguste ametoa amri kwamba watu wote katika inchi wajiandikishe, na kwa hiyo watu walipaswa kusafiri mupaka kwenye muji wao wa kuzaliwa ili wajiandikishe. Yosefu alifanya nini? Tunasoma hivi katika Biblia: ‘Yosefu pia akapanda kutoka Galilaya, kutoka jiji la Nazareti, akaingia Yudea, kwenye jiji la Daudi, linaloitwa Bethlehemu, kwa sababu alikuwa mushiriki wa nyumba na familia ya Daudi.’—Lu. 2:1-4.

5 Ikiwa Mufalme Kaisari alitoa amri hiyo kwa wakati huo, hilo halikuwa jambo lisilotazamiwa. Unabii ulioandikwa miaka karibu 700 mbele, ulitabiri kwamba Masiya atazaliwa Bethlehemu. Sasa, ilifikia kwamba kwenye umbali wa kilometre 11 tu kutoka Nazareti kulikuwa na muji unaoitwa Bethlehemu. Lakini unabii wa Biblia ulisema waziwazi kwamba Masiya atazaliwa “Bethlehemu Efratha.” (Soma Mika 5:2.) Ili kufika kwenye kijiji hicho kidogo cha Nazareti, watu wanatembea kilometre 150 hivi, kwenye barabara za milimani kupitia Samaria. Hiyo ndiyo Bethlehemu ambako Yosefu anapaswa kuenda kujiandikisha, kwa sababu ndicho kijiji cha ukoo wa Mufalme Daudi; Yosefu na bibi yake, wote wawili ni wa ukoo wa Daudi.

6, 7. (a) Sababu gani kufunga safari kuelekea Bethlehemu haikuwa rahisi kwa Maria? (b) Kwa kuwa sasa Maria ni bibi ya Yosefu, maamuzi yake yalitegemea nini? (Soma pia maelezo yaliyo chini, ukurasa wa 155.)

6 Yosefu anaazimia kutii sheria hiyo ya Kaisari, je, Maria atamuunga mukono? Yeye ana mimba yenye kukomaa na kwa hiyo, safari itakuwa ngumu sana kwake. Inaonekana ilikuwa ni mwanzo wa kipindi cha mvua kwa sababu kipindi cha jua kali kilikuwa kinaanza kumalizika polepole. Zaidi ya hilo, maneno “akapanda kutoka Galilaya” yanafaa, kwa sababu muji wa Bethlehemu unapatikana juu kwenye metre zaidi ya 760 kulinganishwa na usawa wa bahari; kwa hiyo, safari ya siku nyingi ili kupanda huko Bethlehemu ilipaswa kuwa safari ngumu na yenye kuchokesha sana kwa Maria. Labda safari hiyo inapaswa kuchukua wakati murefu kuliko kawaida, kwa kuwa Maria ana lazima ya kupumuzika mara nyingi kwa sababu ya hali yake. Zaidi ya hayo, wakati kama huo kila mwanamuke anayekaribia kuzaa angependa kubaki nyumbani, karibu na watu wa familia na marafiki wake ambao wanaweza kuwa tayari kumusaidia wakati uchungu wa kuzaa unaanza. Kwa kweli, inamuomba Maria kuwa na ujasiri ili kukubali safari kama hiyo.

Kufunga safari kuenda Bethlehemu haikuwa jambo rahisi

7 Hata hivyo, Luka anaandika kwamba Yosefu alienda “kuandikishwa pamoja na Maria.” Pia, anaandika kwamba Yosefu ‘alikuwa amemuoa Maria kama ilivyoahidiwa.’ (Lu. 2:4, 5) Maria alikuwa tayari bibi ya Yosefu na kwa hiyo maamuzi yake yalitegemea sana maoni ya bwana yake. Anamuona bwana yake kuwa kichwa cha familia yao, na hivyo anamuunga mukono katika maamuzi anayochukua ili kuonyesha kwamba anakubali daraka alilopewa na Mungu la kuwa musaidizi wake. * Kwa hiyo, Maria alikuwa tayari kutii bwana yake, na kwa njia hiyo alionyesha kwamba ana imani kabisa.

8. (a) Labda ni jambo gani lingine linalomuchochea Maria kufunga safari pamoja na Yosefu ili kuenda Bethlehemu? (b) Ni katika jambo gani Maria ni mufano muzuri sana kwa watu waaminifu?

8 Ni jambo gani lingine linalomuchochea Maria kutii? Je, anajua unabii uliosema kwamba Masiya atazaliwa Bethlehemu? Biblia haiseme lolote. Hata hivyo, inawezekana anajua, kwa sababu jambo hilo linajulikana sana na viongozi wa kidini na watu kwa ujumla. (Mt. 2:1-7; Yoh. 7:40-42) Kuhusu Maandiko, Maria pia anayajua vizuri kabisa. (Lu. 1:46-55) Kwa vyovyote, iwe Maria anakubali kufunga safari hiyo kwa kumutii bwana yake, iwe ni kwa kutii sheria ya Kaisari, ao ni kwa sababu ya unabii wa Yehova, ao ni kwa sababu hizo zote tatu, mwanamuke huyo alituachia mufano muzuri kabisa. Yehova anafurahia sana wanaume na wanawake walio na roho ya unyenyekevu na ya utii. Leo, mutu mwenye sifa ya kujitiisha anaonekana kuwa mutu wa bure, kwa hiyo, Maria ni mufano muzuri sana kwa watu waaminifu kila mahali.

Kuzaliwa kwa Kristo

9, 10. (a) Inawezekana Maria na Yosefu wanakumbuka nini wanapokaribia Bethlehemu? (b) Yosefu na Maria wanaenda kupitisha usiku wapi na kwa nini?

9 Bila shaka, Maria anapoona kwa mbali Bethlehemu, anasikia moyo wake unatulizana. Wanapopanda milima kupitia mashamba ya mizabibu, mimea ya mwisho inayopaswa kuvunwa, labda Maria na Yosefu wanakumbuka historia ya kijiji hicho kidogo. Ni kijiji kidogo sana hivi kwamba hakihesabiwe kati ya miji ya Yuda kama nabii Mika alivyosema; lakini ni hapo Boazi na Naomi walizaliwa na kisha Daudi pia alizaliwa hapo, zaidi ya miaka elfu moja iliyokuwa imepita.

10 Maria na Yosefu wanapofika, wanakuta kijiji hicho kinajaa watu. Watu wengine walifika mbele yao ili kujiandikisha, kwa hiyo, hawapate nafasi katika chumba cha kulala cha wageni. * Basi wanalazimika kupitisha usiku mahali wanyama wanapolalishwa. Katika akili tunaweza kuona namna Yosefu anavyohangaika anapomuona bibi yake katika uchungu mukali wa kuzaa unaozidi kuongezeka. Ni mahali hapo pasipofaa kabisa ambapo Maria anaanza kusikia uchungu wa kuzaa.

11. (a) Sababu gani wanawake duniani pote wanaweza kuelewa jinsi Maria alivyojisikia? (b) Yesu ni ‘muzaliwa wa kwanza’ katika maana gani?

11 Wanawake duniani pote wanaweza kuelewa jinsi Maria alivyojisikia. Miaka 4 000 hivi iliyokuwa imepita, Yehova alikuwa amesema kwamba, kwa sababu ya kuriti zambi, wanawake wangezaa watoto kwa uchungu. (Mwa. 3:16) Hakuna jambo linaloonyesha kwamba Maria hakupatwa na uchungu huo. Luka hakuzungumuzia uchungu ambao Maria alisikia, lakini anaandika tu hivi: ‘Akamuzaa mwana wake, muzaliwa wa kwanza.’ (Lu. 2:7) Ndiyo, ‘muzaliwa wake wa kwanza,’ kwa sababu baadaye Maria alizaa watoto wengine 7. (Mk. 6:3) Lakini, mwana huyu atakuwa tofauti kabisa na wengine. Ni kweli kwamba alikuwa muzaliwa wa kwanza wa Maria, lakini pia ‘muzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote’ vya Yehova, Mwana muzaliwa​-pekee wa Mungu!​—Kol. 1:15.

12. Maria alimulalisha mutoto mahali gani, na hilo linatofautiana namna gani na michezo, michoro na mambo mbalimbali yanayoonyesha kuzaliwa kwa Yesu?

12 Sasa ni hapa ndipo habari hiyo inataja jambo fulani linalojulikana sana: ‘Akamufunga vitambaa na kumulaza katika hori [ao sanduku la kulishia wanyama].’ (Lu. 2:7) Michezo, michoro na mambo mbalimbali yanayofanywa mahali pote ili kuonyesha kuzaliwa kwa Yesu yanakazia sana tukio hilo kwa kupitisha kiasi na kwa njia isiyo ya kweli. Ukweli ni huu: Yesu alilazwa katika sanduku la kulishia wanyama. Usisahau kwamba familia hiyo ilienda kupitisha usiku mahali wanyama wanalalishwa, kwa kawaida hapo ni mahali penye harufu mbaya na pasipo na hewa safi. Kwa kweli, ni muzazi gani ambaye anaweza kuchagua kumuzaa mutoto wake mahali kama hapo ikiwa ana mahali pazuri zaidi? Kwa kawaida, wazazi wanataka kuwapatia watoto wao kilicho kizuri zaidi, sivyo? Bila shaka, Maria na Yosefu wangetaka pia Mwana wa Mungu azaliwe mahali pazuri zaidi!

13. (a) Namna gani Maria na Yosefu wanafanya yale yanayolingana na uwezo wao? (b) Namna gani leo wazazi wenye hekima wanaweza kuiga mufano wa Yosefu na Maria?

13 Hata hivyo, hawaruhusu hali hiyo mbaya iwakoseshe furaha; wanafanya tu yale yanayolingana na uwezo wao. Kwa mufano, ona kwamba Maria yeye mwenyewe anahangaikia kitoto chake, anakifunga nguo za kitoto ili kiwe na joto, kisha anakilalisha kwa uangalifu katika sanduku ili kilale vizuri, na anahakikisha kwamba kiko salama. Maria haruhusu hali hiyo imuvunje moyo na kumukengeusha kiasi cha kutofanya kile anaweza kufanya juu ya kitoto chake. Kwa upande mwengine, wao wawili wanajua kwamba jambo nzuri zaidi ambalo wanaweza kufanya juu ya mutoto huyo ni kumusaidia akomae vizuri kiroho. (Soma Kumbukumbu la Torati 6:6-8.) Leo, wazazi wenye hekima wanatia mambo ya kiroho pa nafasi ya kwanza wanapowalea watoto wao katika dunia hii isiyoona faida za kumutumikia Mungu.

Maria na Yosefu Wanatiwa Moyo na Wachungaji wa Kondoo

14, 15. (a) Sababu gani wachungaji walitamani sana kumuona mutoto huyo? (b) Kisha wachungaji hao kumuona Yesu katika sanduku la kulishia wanyama, walifanya nini?

14 Kwa gafula amani iliyokuwapo inavurugwa. Wachungaji wa kondoo wanaingia mahali hapo, wanapenda kuiona familia hiyo, zaidi sana yule mutoto. Ni wenye kuchangamuka sana na nyuso zao zinangaa kwa furaha. Wamekuja kwa haraka sana kutoka milimani mahali walikuwa wanachunga kondoo zao. * Wanawaambia wazazi hao wenye kushangaa kuhusu jambo fulani la ajabu lililowafikia. Katikati ya usiku walipokuwa wanachunga kondoo zao, huko kwenye milima, malaika aliwatokea kwa gafula. Utukufu wa Yehova uliwaangazia kuzunguka pande zote, na malaika aliwaambia kwamba yule Kristo, ao Masiya, amezaliwa Bethlehemu na kwamba watakuta mutoto huyo amelazwa katika sanduku la kulishia wanyama, amefungwa katika nguo za kitoto. Tena, kulikuwa na jambo fulani la ajabu zaidi lililotokea: kulikuwa na jeshi kubwa la malaika wenye kuimba utukufu wa Mungu!—Lu. 2:8-14.

15 Kwa hiyo, si jambo la kushangaza kwamba wachungaji hao wanyenyekevu wanakuja Bethlehemu wakikimbia! Bila shaka, wanachangamuka sana kukuta kitoto hicho kichanga kinalazwa katika sanduku kama malaika alivyowaambia. Hawafiche habari hiyo njema. ‘Walisema mambo yaliyokuwa yamesemwa. . . . Na wote waliosikia walistaajabu juu ya mambo waliyoambiwa na wachungaji.’ (Lu. 2:17, 18) Inajulikana kwamba viongozi wa kidini wa siku hizo walikuwa wanawazarau wachungaji wa kondoo. Lakini ni wazi kwamba Yehova aliwaona wachungaji hao wanyenyekevu na waaminifu kuwa watu wa maana kabisa. Maria alifaidika namna gani kwa kutembelewa na wachungaji?

Ni wazi kwamba Yehova aliwaona wachungaji hao wanyenyekevu na waaminifu kuwa watu wa maana kabisa

16. Ni nini inayoonyesha kwamba Maria ni mwanamuke anayefikiria mambo kwa uzito, na ni nini sababu kubwa iliyomufanya awe na imani yenye nguvu?

16 Bila shaka, Maria ni mwenye kuchoka sana kisha kuzaa, hata hivyo anasikiliza kila neno kwa uangalifu sana. Na anafanya zaidi ya hilo: ‘Maria akaanza kuyahifazi [ao kuyachunga] maneno hayo yote, akikata kauli [ao kufikiri na kuamua] katika moyo wake.’ (Lu. 2:19) Kwa kweli, mwanamuke huyo ni mwanamuke anayefikiria mambo kwa uzito. Anajua kwamba ujumbe huo wa malaika ulikuwa wa lazima sana. Yehova, Mungu wake, alitaka ajue kama mwana ambaye amezaa ni nani na daraka la lazima ambalo mwana huyo atatimiza. Ndiyo sababu Maria hasikilize tu, lakini pia anayachunga maneno hayo katika moyo wake, ili aweze kuyakumbuka na kuyatafakari tena na tena katika miezi na miaka ijayo. Hiyo ndiyo sababu kubwa iliyomufanya Maria aendelee kuwa na imani yenye nguvu katika maisha yake.—Soma Waebrania 11:1.

Maria aliwasikiliza wachungaji kwa uangalifu sana, na alichunga maneno yao katika moyo wake

17. Namna gani tunaweza kuiga mufano wa Maria kuhusiana na mafundisho ya Biblia?

17 Je, utauiga mufano wa Maria? Yehova amejaza Neno lake na mafundisho mengi ya kweli ya lazima sana. Hata hivyo, mafundisho hayo yanaweza kutufaidi ikiwa tu tunayasikiliza kwa uangalifu. Tutafanya hivyo kwa kusoma Biblia kwa ukawaida, si kama kitabu cha hadisi lakini kama Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake. (2 Tim. 3:16) Kisha, kama Maria, tunapaswa kuyachunga mambo hayo ya kiroho katika mioyo yetu, kuyakumbuka na kuyatafakari. Ikiwa tunatafakari mambo tunayosoma katika Biblia, na kufikiri namna tunaweza kutumia mashauri ya Yehova vizuri zaidi, tunaipatia imani yetu mambo inayohitaji ili ikomae.

Anaambiwa Maneno Mengine na Anayachunga Katika Moyo

18. (a) Namna gani Maria na Yosefu wanatii Sheria ya Musa siku chache tu kisha kuzaliwa kwa Yesu? (b) Namna gani matoleo ambayo Yosefu na Maria wanaleta kwenye hekalu yanafunua hali yao ya maisha?

18 Mutoto anapofanya siku munane, Maria na Yosefu wanamufanya atahiriwe kulingana na Sheria ya Musa, na wanamupa jina Yesu, kama walivyoagizwa. (Lu. 1:31) Kisha, siku ya 40, wanamupeleka mutoto kwenye hekalu huko Yerusalemu, umbali wa kilometre 10 hivi kutoka Bethlehemu, ili kutoa matoleo ya kujitakasa ambayo Sheria iliwaomba masikini kutoa: njiwa​-tetere wawili ao hua wawili. Hata ikiwa wanasikia haya kwa sababu hawakutoa kondoo​-dume na njiwa​-tetere kama wazazi wengine waliokuwa na uwezo, hawajiache kuvurugwa akili na jambo hilo. Jambo la lazima kwao ni kwamba walitiwa moyo sana walipokuwa huko.—Lu. 2:21-24.

19. (a) Simeoni alimuambia Maria maneno mengine gani ya kuchunga katika moyo wake? (b) Nabii mwanamuke Ana alipomuona Yesu, alifanya nini?

19 Mwanaume muzee anayeitwa Simeoni anawakaribia na anamuambia Maria mambo mengine ambayo anapaswa kuchunga katika moyo wake. Muzee huyo alikuwa ameahidiwa kwamba atamuona Masiya mbele ya kufa, na roho takatifu ya Yehova ilimuonyesha kwamba mutoto huyo anayeitwa Yesu ndiye Mwokozi aliyeahidiwa. Tena, Simeoni anamujulisha Maria kuhusu uchungu ambao siku moja anapaswa kuvumilia. Anamuambia kwamba itakuwa kama upanga murefu unaomupita katika mwili. (Lu. 2:25-35) Hata ikiwa maneno hayo ni yenye kuogopesha, yalimusaidia Maria kuvumilia wakati huo mugumu ulipofika, miaka 33 kisha. Simeoni alipomaliza kusema, nabii mwanamuke anayeitwa Ana alianza naye kumuambia kila mutu aliyekuwa na tumaini la kukombolewa kwa Yerusalemu juu ya mutoto Yesu.—Soma Luka 2:36-38.

Maria na Yosefu walitiwa moyo huko Yerusalemu kwenye hekalu la Yehova

20. Sababu gani kumuleta Yesu kwenye hekalu huko Yerusalemu ulikuwa uamuzi muzuri kabisa?

20 Yosefu na Maria walichukua uamuzi muzuri kabisa kwa kumuleta mutoto wao huko Yerusalemu, kwenye hekalu la Yehova! Matukio hayo yalikuwa mwanzo kwa mwana wao kuzoea kuenda kwenye hekalu la Yehova. Huko, wao wenyewe walitoa yote waliyokuwa nayo kulingana na uwezo wao, nao walipata maagizo na kutiwa moyo. Bila shaka, siku hiyo Maria alitoka katika hekalu imani yake ikiwa tayari imetiwa nguvu, na moyo wake ukiwa wenye kujaa mawazo ya kiroho ambayo atatafakari na kuwajulisha wengine.

21. Tunaweza kufanya nini ili imani yetu iwe nguvu zaidi kama ile ya Maria?

21 Ni jambo linalopendeza kabisa kuona wazazi leo wanafuata mufano huo. Kwa uaminifu, wazazi Mashahidi wa Yehova wanawapeleka watoto wao kwenye mikutano ya Kikristo. Wazazi kama hao wanafanya yote wanayoweza, wanawatia moyo ndugu na dada zao Wakristo. Na wanaporudi nyumbani kutoka kwenye mikutano hiyo, wanakuwa na nguvu na furaha zaidi, na pia wanajaa na mambo mengi mazuri ya kuwaambia wengine. Ni jambo lenye kufurahisha sana kukutana na wazazi hao! Ukifanya hivyo, utaona kwamba imani yako itakuwa nguvu zaidi kama ile ya Maria.

^ fu. 7 Ona tofauti kati ya andiko hilo na habari inayozungumuzia safari aliyofanya hapo mbele: “Maria akaondoka . . . akaenda” kumutembelea Elisabeti. (Lu. 1:39) Wakati huo Maria alikuwa mwanamuke mwenye kuchumbiwa, lakini si mwenye kuolewa kabisa, kwa hiyo, angeweza kufanya safari hiyo bila uamuzi wa Yosefu. Lakini, kisha kuolewa, inaonekana kwamba ni Yosefu ndiye aliyechukua uamuzi wa kufanya safari yao, wala si Maria.

^ fu. 10 Siku hizo ilikuwa kawaida katika muji kutayarisha chumba kimoja cha kulala kwa ajili ya watu wanaosafiri pamoja.

^ fu. 14 Kwa kuwa wakati huo wachungaji hao walikuwa wanaishi inje na kondoo zao, hilo linahakikisha kile Biblia inasema kuhusu wakati Yesu alizaliwa: Kristo hakuzaliwa Mwezi wa 12 wakati ambapo wanyama wa kufugwa wangelindwa vizuri karibu na nyumba, lakini alizaliwa mwanzoni mwa Mwezi wa 10.