Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA MAKUMI MBILI NA MBILI

Alibaki Mushikamanifu Ijapokuwa Majaribu

Alibaki Mushikamanifu Ijapokuwa Majaribu

1, 2. Yesu anapofundisha katika Kapernaumu, mutume Petro anatazamia nini, lakini matokeo yanakuwa namna gani?

PETRO anatazama huku na huku na kwa wasiwasi anaangalia sura za watu wanaomusikiliza Yesu. Wako katika sinagogi huko Kapernaumu. Petro anaishi katika muji huu; ni hapo anafanya kazi yake ya kuvua na kuuzisha samaki, upande wa kaskazini mwa Bahari ya Galilaya; marafiki wake wengi, watu wa jamaa, na watu wanaofanya kazi ya kuvua pamoja naye wanaishi hapo. Bila shaka, Petro ni mwenye kutumainia kwamba watu wa muji wao watamuona Yesu kuwa Masiya kama vile yeye anavyomuona, na kwamba watafurahia kufundishwa mambo yanayohusu Ufalme wa Mungu na mwalimu mukubwa zaidi kuliko walimu wote. Lakini siku hiyo, mambo hayatokee kama alivyotumainia.

2 Wengi hawapendi kumusikiliza Yesu. Wengine wananungunika-nungunika kwa sauti, wanapinga ujumbe wa Yesu. Lakini, jambo linalomusumbua Petro zaidi, ni kuona wanafunzi fulani wa Yesu nao, wanakuwa na mashaka. Sura zao zinaonyesha kama hawafurahie tena mambo mapya kuhusu kweli ambayo Yesu anawafundisha. Na sasa, wanaonekana kuwa wenye kuvunjika moyo na hata wanakasirika. Wengine wanasema waziwazi, wanamuambia Yesu kama maneno yake yanawaumiza. Hawapendi tena kumusikiliza, na kwa hiyo, wanatoka katika sinagogi na wanaacha kuwa wafuasi wake.—Soma Yohana 6:60, 66.

3. Imani ya Petro inamusaidia mara nyingi kufanya nini?

3 Ni wakati mugumu kwa Petro na kwa mitume wenzake. Ni kweli kwamba Petro pia haelewe kabisakabisa maana ya yale ambayo Yesu alisema siku hiyo. Yeye pia anaona kwamba maneno hayo yanaweza kukwaza watu ikiwa hayafasiriwe. Petro atafanya nini? Hii si mara yake ya kwanza kuona ushikamanifu wake kwa Bwana wake unajaribiwa hivyo; wala si mara ya mwisho. Acheni basi tuone namna gani imani ya Petro inamusaidia kupambana na majaribu hayo na kubaki mushikamanifu.

Anabaki Mushikamanifu Kuliko Wengine

4, 5. Namna gani Yesu anatenda tofauti na yale ambayo watu wanatazamia?

4 Mara nyingi, Petro alikuwa anashangazwa na matendo na maneno ya Yesu. Kila siku, yale Bwana wake alikuwa anafanya na kusema yalikuwa tofauti na yale watu walikuwa wanatazamia. Siku moja tu mbele ya hapo, Yesu alilisha maelfu ya watu kimuujiza, na watu hao walipenda kumufanya awe mufalme. Lakini anawashangaza wengi, anakimbia na anawaomba wafuasi wake waingie katika mashua na waende upande wa Kapernaumu. Wanafunzi wake wanaposafiri kwa mashua usiku, Yesu anawashangaza tena, anatembea juu ya Bahari ya Galilaya yenye zoruba. Wakati huo Petro anajifunza jambo la maana kuhusu imani.

5 Inapokuwa asubuhi, wanatambua kwamba watu walipanda pia katika mashua zao na kuwafuata. Hata hivyo, inaonekana wazi kwamba, watu wanafanya hivyo kwa sababu wanapenda Yesu awalishe tena kimuujiza, wala si kwa sababu wana hamu ya kusikiliza mafundisho yake. Yesu anawakaripia kwa sababu ya roho hiyo ya kupenda tu vitu vya kimwili. (Yoh. 6:25-27) Mazungumuzo hayo yanaendelea katika sinagogi la Kapernaumu, mahali ambapo kweli ya maana sana ambayo Yesu anawafundisha inawaumiza.

6. Yesu anatoa mufano gani, na wasikilizaji wake wanaonyesha hali gani?

6 Yesu anapenda watu hao wasimuone tu kama mutoaji wa chakula cha kimwili, lakini kama mutoaji wa chakula cha kiroho kinachotoka kwa Mungu, ni kusema, wajue kama yeye ndiye ametumwa na Mungu, ili kupitia uzima wake na kifo chake wengine waweze kupata uzima wa milele. Kwa hiyo, anawapa mufano mumoja, na katika mufano huo anajilinganisha na mana, mukate uliotoka mbinguni katika siku za Musa. Wasikilizaji wengine wanapinga, kwa hiyo, anatumia mufano unaokazia jambo hilo: anawaonyesha kwamba inafaa kula mwili wake na kunywa damu yake ili kupata uzima. Anaposema maneno hayo, wasikilizaji wake wanakasirika sana. Wamoja wanasema: ‘Maneno hayo yanashitua, ni nani ambaye anaweza kuyasikiliza?’ Wanafunzi wake wengi wanaamua kumuacha. *Yoh. 6:48-60, 66.

7, 8. (a) Ni jambo gani ambalo bado Petro hajaelewa kumuhusu Yesu? (b) Namna gani Petro anajibia ulizo ambalo Yesu anauliza mitume?

7 Mutume Petro atafanya nini? Inaonekana kwamba yeye pia anavurugika sana na maneno ya Yesu. Bado, hajaelewa kwamba ni lazima Yesu akufe ili atimize mapenzi ya Mungu. Je, Petro anajaribu kumuacha Yesu kama wale wanafunzi wengine wanavyofanya siku hiyo? Hapana; mutume Petro ana sifa fulani ya maana sana inayomutofautisha na wale wengine. Ni sifa gani hiyo?

8 Yesu anawaangalia mitume wake na anawauliza: ‘Je, ninyi pia munataka kuenda?’ (Yoh. 6:67) Anawauliza mitume wake 12, lakini ni Petro anayejibu kama ilivyokuwa kawaida yake. Inawezekana, ni Petro aliye na umri mukubwa kuwapita wote. Iwe hivyo ao hapana, ni yeye aliyekuwa akisema waziwazi kati ya mitume; kwa kawaida hakuwa anasita kusema mambo aliyokuwa anafikiri. Wakati huo, mawazo anayofikiri ni yale maneno mazuri yasiyosahaulika: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.”—Yoh. 6:68.

9. Namna gani Petro alionyesha ushikamanifu wake kwa Yesu?

9 Je, maneno hayo hayaguse moyo wako? Petro alimuamini kabisa Yesu, na imani yake ilimusaidia akomalishe sifa ya maana sana: ushikamanifu. Petro alielewa wazi kwamba ni Yesu tu ndiye Mwokozi ambaye Yehova ametuma na kwamba Yesu anaokoa watu kupitia maneno yake, ni kusema, mafundisho yake kuhusu Ufalme wa Mungu. Petro alijua kama ijapokuwa kuna mambo fulani ambayo hajaelewa, hakuna mahali pengine ambapo angeweza kuenda ikiwa anataka kukubaliwa na Mungu na kupata uzima wa milele.

Ni lazima tushikamane na mafundisho ya Yesu, hata ikiwa hayapatane na mambo tunayotazamia ao mapendezi yetu

10. Namna gani tunaweza kuiga ushikamanifu wa mutume Petro leo?

10 Je, ni hivyo unavyojisikia? Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, wengi katika ulimwengu wa leo wanadai kwamba wanamupenda Yesu, lakini wanashindwa kubaki washikamanifu kwake. Ili kubaki washikamanifu kwa Kristo tunapaswa kupenda mafundisho yake kama vile Petro. Tunapaswa kujua mafundisho hayo, kuelewa maana yake, na kuishi kulingana nayo hata ikiwa hatuyaelewe ao hayapatane na yale tunayotazamia ao mapendezi yetu. Yesu anataka tupate uzima wa milele, na tunaweza kutumainia kupata uzima huo ikiwa tunabaki washikamanifu kwake.Soma  Zaburi 97:10.

Anabaki Mushikamanifu Hata Kisha Kukaripiwa

11. Yesu anawapeleka wafuasi wake wapi? (Soma pia maelezo yaliyo chini.)

11 Muda mufupi kisha wakati huo wenye shuguli nyingi, Yesu anafunga safari ndefu pamoja na mitume wake na pia wanafunzi wake na kuwapeleka upande wa kaskazini. Mulima Hermoni unapatikana mbali zaidi kwenye mupaka wa upande wa kaskazini wa Inchi ya Ahadi; unaonekana kutoka Bahari ya Galilaya yenye maji ya kijani, na wakati mwengine sehemu ya juu ya mulima huo ni yenye kuwa na teluji. Polepole, kadiri wanavyoukaribia mulima huo, unaonekana kuwa mukubwa; wanapanda eneo lenye kuinuka na kuelekea vijiji fulani karibu na Kaisaria Filipi. * Wakiwa katika mahali hapo penye kuvutia, ambapo wanaweza kuona sehemu kubwa ya Inchi ya Ahadi upande wa kusini, Yesu anawauliza wafuasi wake ulizo fulani la maana.

12, 13. (a) Sababu gani Yesu anataka kujua yale watu wanawaza juu yake? (b) Namna gani jibu la Petro linaonyesha kwamba ana imani ya kweli?

12 Anapenda kujua jambo fulani, kwa hiyo anawauliza hivi: ‘Watu wanasema mimi ni nani?’ Unaweza kuwazia namna Petro anavyomuangalia sana Yesu katika macho na kutambua wema wake, nguvu na akili yake kubwa. Yesu anataka kujua yale ambayo wasikilizaji wake wanawaza juu yake kutokana na mambo wanayoona na kusikia. Wanafunzi wa Yesu wanajibu, wanamuonyesha mawazo fulani yasiyofaa ambayo watu wanayo kumuhusu. Lakini Yesu anataka kujua mengi zaidi. Anataka kujua ikiwa wafuasi wake, wanaomufuata, wana pia mawazo kama hayo yenye makosa. Kwa hiyo, anawauliza: ‘Ingawa hivyo, ninyi munasema mimi ni nani?’—Lu. 9:18-20.

13 Mara hii tena, Petro anajibu haraka. Anataja wazi na kwa ujasiri yale wengine wanawaza katika mioyo yao. Anajibu hivi: “Wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.” Tunaweza kuwazia namna Yesu anavyocheka kidogo ili kuonyesha kama anakubaliana na jibu hilo la Petro na anamupongeza kwa uchangamufu. Yesu anamukumbusha Petro kwamba ni Yehova Mungu, wala si mwanadamu, ndiye anawafunulia kweli hiyo ya maana sana, wao walio na imani ya kweli. Yehova anamusaidia Petro kutambua moja ya kweli ya maana sana kati ya mambo ambayo Yehova alikuwa bado hajawafunulia, ni kusema, kumutambua yule aliyeahidiwa tangu zamani sana kuwa yeye ndiye Masiya ao Kristo!—Soma Mathayo 16:16, 7.

14. Yesu anamupatia Petro mapendeleo gani ya maana sana?

14 Huyo Kristo ndiye unabii mbalimbali wa zamani ulizungumuzia kuwa jiwe ambalo wajengaji wangekataa. (Zab. 118:22; Lu. 20:17) Yesu anafikiria unabii huo anapofunua kwamba Yehova atajenga kutaniko juu ya jiwe lenyewe (ao mwamba), ambalo Petro anatoka kutambulisha kuwa Kristo. Kwa hiyo anamutolea Petro mapendeleo fulani ya maana sana katika kutaniko hilo. Yesu hamufanye Petro kuwa mukubwa juu ya mitume wengine, kama vile dini fulani zinavyofundisha, lakini anamupatia tu kazi ya zaidi ao madaraka. Anamupatia Petro “funguo za ufalme.” (Mt. 16:19) Petro anapata pendeleo la kufungulia vikundi vitatu vya wanadamu tumaini la kuingia katika Ufalme wa Mungu: kwanza Wayahudi, kisha Wasamaria, na mwishowe Watu wa Mataifa, ao Watu Wasio Wayahudi.

15. Petro anamukemea Yesu namna gani, na kwa nini anafanya hivyo?

15 Hata hivyo, baadaye Yesu anasema kama wale wanaopewa mengi watadaiwa mengi, na Petro anajionea ukweli wa maneno hayo. (Lu. 12:48) Yesu anaendelea kufunua kweli za maana kuhusu Masiya, kama vile kuteswa na kufa kwake huko Yerusalemu. Petro hapendi kusikia mambo kama hayo, yanamusumbua sana. Anamupeleka Yesu pembeni na kumukemea, akisema: ‘Jitendee kwa fazili, Bwana; wewe hautapatwa hata kidogo na jambo hili.’​—Mt. 16:21, 22.

16. Namna gani Yesu alimurekebisha Petro, na ni shauri gani linalofaa ambalo sisi wote tunapata kupitia maneno ya Yesu?

16 Kwa kusema hivyo Petro hakuwa na mawazo mabaya, lakini, bila shaka jibu la Yesu litamushangaza. Anamugeuzia Petro mugongo na anawaangalia wanafunzi wengine, ambao labda wana pia mawazo kama hayo ya Petro, kisha anasema: ‘Enda nyuma yangu, Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa sababu wewe unafikiri, si fikira za Mungu, bali za wanadamu.’ (Mt. 16:23; Mk. 8:32, 33) Maneno hayo ya Yesu yana mashauri yanayoweza kutusaidia sisi wote leo. Ni vyepesi sana kuacha mawazo ya kibinadamu yachukue nafasi ya mawazo ya Mungu. Tukiruhusu jambo hilo, hata wakati tunapofikiri kwamba tunatoa musaada, bila kujua tunaweza kufikia kuunga mukono kusudi la Shetani kuliko kuunga mukono kusudi la Mungu. Kwa hiyo basi, Petro anafanya nini?

17. Yesu anamaanisha nini anapomuambia Petro ‘aende nyuma’ yake?

17 Petro anajua kama Yesu hamuite Shetani Ibilisi kwa njia halisi. Ni kweli kwamba Yesu haseme na Petro namna alivyosema na Shetani. Aliposema na Shetani, Yesu alimuambia: ‘Enda zako’; lakini anaposema na Petro, anamuambia: ‘Enda nyuma yangu.’ (Mt. 4:10) Yesu hamukatae mutume huyo, alikwisha kuona mambo mengi mazuri ndani yake, lakini anaonyesha tu kwamba Petro alikuwa na mawazo mabaya kuhusiana na jambo hilo. Ni rahisi kuona kwamba Petro anajikaza asiwe kama jiwe la kukwaza mbele ya Bwana wake, lakini anajikaza kuwa mufuasi wake mushikamanifu.

Tunaweza kuendelea kumukaribia Yesu Kristo na Baba yake Yehova, ikiwa tu tunakubali kwa unyenyekevu mashauri yao na kufaidika nayo

18. Namna gani Petro anaonyesha ushikamanifu wake, na namna gani tunaweza kumuiga?

18 Je, Petro anafanya ubishi ao anakasirikia Yesu? Hapana; anakubali kwa unyenyekevu kurekebishwa. Kwa hiyo, anaonyesha ushikamanifu wake tena. Wote wanaomufuata Kristo watakuwa na lazima ya kurekebishwa wakati mwengine. Tunaweza kuendelea kumukaribia Yesu Kristo na Baba yake Yehova, ikiwa tu tunakubali kwa unyenyekevu mashauri yao na kufaidika nayo.—Soma Methali 4:13.

Petro alibaki mushikamanifu hata kisha kukaripiwa

Anabarikiwa kwa Sababu ya Ushikamanifu Wake

19. Yesu anasema maneno gani yenye kushangaza, na labda Petro anawaza nini?

19 Yesu anasema jambo lingine lenye kushangaza: ‘Kwa kweli ninawaambia ninyi kwamba kuna wengine kati ya wale wanaosimama hapa ambao hawataonja kifo kamwe mupaka kwanza wamuone Mwana wa binadamu akija katika ufalme wake.’ (Mt. 16:28) Bila shaka Petro anapenda kujua maana ya maneno hayo. Lakini, labda Petro anawaza kama hatapata pendeleo hilo kwa sababu ya karipio kali ambalo Yesu alimutolea.

20, 21. (a) Eleza maono ambayo Petro anajionea. (b) Namna gani mazungumuzo ya wale watu watatu yanarekebisha maoni ya Petro?

20 Kisha juma moja, Yesu anachukua Yakobo, Yohana, na Petro na anaenda kwenye mulima murefu, labda Mulima Hermoni, unaopatikana kwenye umbali wa kilometre 25. Inawezekana ni usiku kwa kuwa wanaume hao watatu wanapigana na usingizi. Yesu anaposali, jambo moja linatokea ambalo linakimbiza usingizi wa hao wanaume watatu.​—Mt. 17:1; Lu. 9:28, 29, 32.

21 Yesu anaanza kubadilika mbele yao. Sura yake inaanza kuangaa, mupaka wakati anangaa kama jua. Mavazi yake yanakuwa meupe peee. Kisha watu wawili wenye kugeuzwa sura wanatokea na kuanza kuzungumuza na Yesu, mumoja anamuwakilisha Musa na mwengine Eliya. Wanazungumuza na Yesu kuhusu “kuondoka kwake ambako angetimiza huko Yerusalemu”​—bila shaka, ni kuhusu kifo chake na ufufuo wake. Petro anatambua kwamba alikosea kabisa kufikiri kwamba Yesu hatateseka wala kufa!​—Lu. 9:30, 31.

22, 23. (a) Namna gani Petro anaonyesha kuwa yeye ni mutu mwenye fazili na roho ya moto-moto? (b) Petro, Yakobo, na Yohana wanapata baraka gani ingine?

22 Petro anajisikia kuwa anapaswa kushiriki kwa njia fulani katika maono hayo yenye kushangaza. Inaonekana kama Musa na Eliya wanamuacha Yesu. Kwa hiyo Petro anasema: “Mwalimu, ni vizuri kwetu kuwa hapa, kwa hiyo na tusimamishe mahema matatu, moja lako na moja la Musa na moja la Eliya.” Bila shaka, watu wawili hao wanaofananisha watumishi wawili wa Mungu wa zamani hawana lazima ya mahema. Kwa kweli, Petro hatambue analosema. Hata hivyo, tunavutiwa na Petro kwa sababu ni mutu mwenye fazili na roho ya moto-moto.—Lu. 9:33.

Petro, Yohana, na Yakobo walibarikiwa kwa kuona maono yenye kuvutia sana

23 Petro, Yakobo, na Yohana wanapata baraka ingine usiku huo. Wingu linatokea na kukaa juu yao kwenye mulima. Sauti inatoka katika wingu hilo na wanasikia sauti ya Yehova Mungu! Anasema: ‘Huyu ni Mwanangu, ambaye amechaguliwa. Mumusikilize.’ Kisha maono hayo yanakwisha, na wanabaki wenyewe kwenye mulima pamoja na Yesu.—Lu. 9:34-36.

24. (a) Namna gani maono ya kugeuzwa sura yalimusaidia Petro? (b) Namna gani sisi leo tunaweza kufaidika na maono hayo?

24 Maono ya kugeuzwa sura yalikuwa baraka kubwa kwa Petro na ni baraka kubwa kwetu leo! Miaka mingi baadaye, Petro aliandika kuhusu pendeleo alilopata usiku huo la kuwa mumoja kati ya “mashahidi wa kujionea fahari yake,” ni kusema, kumuona Yesu mbele ya wakati namna atakavyokuwa Mufalme mwenye utukufu mbinguni. Maono hayo yalihakikisha unabii mwingi wa Neno la Mungu na kutia nguvu imani ya Petro kuhusiana na majaribu ambayo yalikuwa mbele yake. (Soma 2 Petro 1:16-19.) Maono hayo yanaweza kuwa na matokeo hayo pia kwetu, ikiwa tunabaki waaminifu kwa Bwana wetu, ambaye Yehova ameweka juu yetu, kwa kujifunza juu yake, kukubali mashauri yake na kuendelea kumufuata kwa unyenyekevu siku baada ya siku.

^ fu. 6 Tunaweza kusema kwamba watu waliokuwa hapo kwenye sinagogi walikuwa wageugeu ao wasio na musimamo tunapolinganisha jinsi wanavyotenda wanaposikia maneno ya Yesu wakati huo, na jinsi walivyosema siku iliyotangulia. Siku hiyo, kwa kuchangamuka sana walitangaza kwamba Yesu ni nabii wa Mungu.​—Yoh. 6:14.

^ fu. 11 Kikundi hicho kinatoka sehemu za Bahari ya Galilaya inayopatikana kwenye metre 210 hivi chini ya usawa wa bahari na kupitia maeneo yenye kuvutia sana ya muendo wa kilometre 50, ili kufikia eneo linalopatikana kwenye metre 350 hivi juu ya usawa wa bahari.