Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KUMI NA SABA

“Tazama! Mimi Ni “Kijakazi wa Yehova!”

“Tazama! Mimi Ni “Kijakazi wa Yehova!”

1, 2. (a) Mugeni anamusalimia Maria namna gani? (b) Maria anapaswa kuchukua uamuzi gani na namna gani hilo litabadilisha maisha yake yote?

MARIA anainua macho na kutazama kwa mushangao mugeni anayeingia nyumbani kwao. Mugeni huyo hamuulize kuhusu baba yake wala mama yake, kwa sababu amekuja kumuona yeye! Namna mugeni huyo anavyoonekana, Maria iko hakika kwamba mutu huyo si mukaaji wa Nazareti. Katika muji mudogo kama Nazareti, ni vyepesi kutambua wageni. Kwa sababu mugeni huyu ni tofauti kabisa, kila mutu angemutambua hivyo. Namna anavyomusalimia Maria, hakuna mutu alikwisha kumusalimia hivyo, anamusalimia hivi: ‘Siku njema, uliyependelewa sana, Yehova iko pamoja nawe.’—Soma Luka 1:26-28.

2 Hivyo ndivyo Biblia inaanza kuzungumuza juu ya Maria, binti ya Heli, anayeishi Galilaya katika muji wa Nazareti. Habari ya Maria katika Biblia inaanza wakati anapaswa kuchukua uamuzi wa maana sana katika maisha yake. Yeye ni muchumba wa Yosefu ambaye ni seremala wala si mutu tajiri, lakini ni mwanaume aliye na imani yenye nguvu katika Mungu. Kwa hiyo, Maria anaona tayari namna maisha yake yatakavyokuwa: maisha ya hali ya chini ya mwanamuke anayefanya kazi ili kumusaidia bwana yake, na pia kulea watoto wao. Lakini, kwa gafula, anajikuta mbele ya mugeni anayemupa mugao unaotoka kwa Mungu, ambao utabadilisha maisha yake yote.

3, 4. Ikiwa tunapenda kumujua Maria vizuri, inatufaa kuachana na mawazo gani, na tunapaswa kukazia fikira zetu nini?

3 Watu wengi wanashangaa kuona kwamba Biblia haizungumuzie mambo mengi kuhusu Maria. Haiseme mengi kuhusu malezi yake, inasema machache tu kuhusu sifa zake, na haiseme chochote kuhusu sura yake. Hata hivyo, machache tu ambayo Neno la Mungu linasema kumuhusu yanatufundisha mambo mengi kabisa.

4 Ikiwa tunapenda kumujua Maria vizuri, inatufaa kuachana na mawazo mbalimbali ambayo dini zimefundisha kumuhusu. Basi, tusifikirie yule Maria anayeonyeshwa kwenye picha ao sanamu zilizochorwa na kutengenezwa kwa vitu mbalimbali. Pia, tuondoe katika akili mafundisho ya kidini ambayo yanamutukuza kupita kiasi mwanamuke huyo munyenyekevu kwa kumuita “Mama ya Mungu” na “Malkia wa Mbinguni.” Kwa hiyo, acheni tukazie fikira yale Biblia inafundisha juu yake. Biblia inatusaidia kuona imani yake kubwa sana na namna gani tunaweza kuiiga.

Malaika Anamutembelea

5. (a) Maria anafanya nini malaika anapomuambia kwamba anapendelewa sana? (b) Mufano wa Maria unaweza kutufundisha nini?

5 Mugeni wa Maria si mwanadamu, ni malaika Gabrieli. Anapomuambia Maria kwamba ‘anapendelewa sana,’ Maria ‘anashitushwa sana’ na maneno hayo, na anajiuliza maana ya salamu hiyo isiyo ya kawaida. (Lu. 1:29) Anapendelewa sana na nani? Maria hatazamie kupendelewa hivyo na wanadamu. Lakini malaika anazungumuza kuhusu kupendelewa na Yehova Mungu. Na Maria anaona kupendelewa hivyo kuwa ndilo jambo la lazima sana. Hata hivyo, Maria hajivune kwamba tayari amekwisha kupendelewa na Mungu. Mufano wa Maria unatufundisha kwamba tunapaswa kujikaza ili tukubaliwe na Mungu, na hatupaswe kuwaza mara moja kwa kiburi kwamba tayari Mungu anatupenda. Mungu anawapinga watu wenye majivuno, lakini anawapenda na kuwategemeza watu wa hali ya chini na wanyenyekevu.—Yak. 4:6.

Maria hajivune kwamba tayari amekwisha kupendelewa na Mungu

6. Malaika anamutolea Maria pendeleo gani?

6 Maria ana lazima ya unyenyekevu kama huo, kwa sababu pendeleo ambalo malaika anamutolea ni pendeleo la pekee, ni kusema, pendeleo la kuzaa mutoto ambaye atakuwa mutu wa lazima sana kuliko wanadamu wote. Malaika Gabrieli anamuambia hivi: ‘Yehova Mungu atamupa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, naye atatawala akiwa mufalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho.’ (Lu. 1:32, 33) Bila shaka, Maria anajua ahadi ambayo Mungu alimupatia Daudi kumekwisha kupita miaka zaidi ya elfu moja, kwamba mumoja wa wazao wake atatawala milele. (2 Sam. 7:12, 13) Kwa hiyo, ni mutoto wake ndiye atakuwa Masiya ambaye watu wa Mungu walikuwa wanangojea kwa muda wa miaka mingi!

Malaika Gabrieli anamutolea Maria pendeleo la pekee

7. (a) Ulizo ambalo Maria anamuuliza malaika waziwazi linafunua nini kuhusu Maria mwenyewe? (b) Mufano wa Maria unaweza kuwafundisha vijana nini leo?

7 Zaidi ya hilo, malaika anamuambia Maria kwamba mutoto huyo “ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi.” Inawezekana namna gani mwanamuke wa kibinadamu azae mwana wa Mungu? Na jambo lingine ni hili, Maria ni muchumba wa Yosefu na bado hawajaoana, namna gani atazaa mutoto? Maria anamuuliza malaika ulizo hilo waziwazi: ‘Hilo litawezekanaje, kwa kuwa silale na mwanaume?’ (Lu. 1:34) Unaona jinsi Maria anazungumuzia ubikira wake bila kusikia haya hata kidogo? Anajivunia hali yake ya kuwa bado bikira. Leo, vijana wengi wanaharibu haraka ubikira wao na kisha wanaanza kuwacheka wale ambao bado wanachunga ubikira wao. Ni wazi kwamba ulimwengu umebadilika. Lakini, Yehova hajabadilika. (Mal. 3:6) Bado anaendelea kupendezwa na wale wanaoshikamana na sheria zake kuhusu mwenendo safi, kama ilivyokuwa katika siku za Maria.—Soma Waebrania 13:4.

8. Kwa kuwa Maria ni mwanadamu asiye mukamilifu, namna gani inawezekana azae mutoto mukamilifu?

8 Maria anamutumikia Mungu kwa uaminifu, lakini yeye ni mwanadamu asiye mukamilifu. Kwa hiyo, namna gani yeye atazaa mutoto mukamilifu, Mwana wa Mungu? Gabrieli anamufasiria jinsi jambo hilo litafanyika: “Roho takatifu itakuja juu yako, na nguvu za Aliye Juu Zaidi zitakufunika. Kwa sababu hiyo pia, kile kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.” (Lu. 1:35) Kitu kitakatifu ni kitu “safi,” “chenye kutakata.” Kwa kawaida, watoto wanariti hali ya kukosa kukamilika, ao ya zambi kwa wazazi wao. Lakini kuhusu kuzaliwa kwa mutoto huyu, Yehova anataka kufanya muujiza ambao haujawahi kufanyika na hautafanyika tena. Anahamisha uzima wa Mwana wake aliye mbinguni na kuuingiza katika tumbo la uzazi la Maria, na kisha anatumia roho yake takatifu, ni kusema, nguvu yake ya utendaji, ‘kumufunika’ Maria, ili kumulinda mutoto huyo asiambukizwe na zambi hata kidogo. Je, Maria anaamini ahadi ya malaika? Anasema nini?

Maria Anamujibu Gabrieli

9. (a) Sababu gani watu wenye mashaka wanakosea, wanapokataa kuamini habari kuhusu Maria? (b) Namna gani Gabrieli anaitia imani ya Maria nguvu?

9 Watu wengi wenye mashaka na hata wanateolojia fulani wa dini zinazojiita za Kikristo hawaamini kwamba bikira aliweza kuzaa mutoto. Hata ikiwa wamejifunza mambo mengi, wameshindwa kuelewa kweli hiyo rahisi. Malaika Gabrieli anamuambia Maria, “kwa Mungu hakuna tangazo [ao neno] lolote lisilowezekana.” (Lu. 1:37) Maria hatilie shaka ukweli wa maneno ya Gabrieli, kwa sababu yeye ni kijana mwanamuke mwenye imani kubwa. Hata hivyo, hakuamini tu hivihivi bila musingi wowote. Anaamini maneno ya Gabrieli kwa sababu ya usadikisho ambao anamutolea na kwa hiyo Gabrieli anamutolea usadikisho zaidi. Anamuambia kuhusu Elisabeti, mutu wa ukoo wake ambaye amezeeka, na ambaye kwa muda murefu anajulikana kuwa tasa. Kwa muujiza Mungu amefanya awe na mimba!

10. Hata ikiwa ni pendeleo kuzaa Mwana wa Mungu, sababu gani jambo hilo si rahisi kwa Maria?

10 Sasa Maria atafanya nini? Amepewa mugao na ana usadikisho kwamba Mungu atafanya yote ambayo Gabrieli alimuambia. Tusifikiri kwamba pendeleo hilo halimuogopeshe ao halina tatizo lolote. Tatizo la kwanza, anafikiria uchumba wake na Yosefu. Atakapojua kwamba ana mimba, je, atakubali tena kumuoa? Tatizo lingine, mugao wenyewe bila shaka unaonekana kuwa wenye kuogopesha. Maria anapaswa kuchunga uzima wa kiumbe chenye bei sana kati ya viumbe vyote vya Mungu, ni kusema, Mwana mupendwa wa Mungu! Anapaswa kumutunza akiwa bado kitoto na kumulinda kabisa anapokomaa katika ulimwengu muovu. Kwa kweli, hilo ni daraka nzito!

11, 12. (a) Wanaume fulani wenye nguvu na waaminifu walifanya nini wakati Mungu aliwapa migao? (b) Jibu la Maria kwa Gabrieli linafunua nini juu yake mwenyewe?

11 Biblia inaonyesha kwamba wakati fulani hata wanaume waaminifu walisita kukubali migao migumu waliyopewa na Mungu. Musa alijiona hastahili kuwa musemaji wa Mungu kwa sababu hajue kusema vizuri. (Kut. 4:10) Yeremia alitaka kukataa mugao wake, kwa sababu yeye ni kijana sana, ‘muvulana tu.’ (Yer. 1:6) Na Yona alikimbia mugao wake! (Yona 1:3) Lakini, Maria atafanya nini?

12 Maneno aliyomuambia Gabrieli, maneno yenye kuonyesha unyenyekevu na utii, hata leo yanakumbukwa na watu wengi wenye imani. Anamuambia hivi: “Tazama! [Mimi ni] kijakazi wa Yehova! Na itendeke kwangu kulingana na tangazo [ao neno] lako.” (Lu. 1:38) Kijakazi alikuwa mutumishi wa chini sana kati ya watumishi wote kwa sababu maisha yake yalikuwa mikononi mwa bwana wake. Hivyo ndivyo Maria anavyojiona mbele ya Bwana wake, Yehova. Anajua kwamba Yehova ni mushikamanifu kwa wale walio washikamanifu kwake, kwa hiyo anajisikia salama mikononi mwake, na kwamba atamubariki ikiwa anafanya yake yote ili kutimiza mugao huo mugumu.​—Zab. 18:25.

Maria anajua kwamba Yehova Mungu wake ni mushikamanifu, kwa hiyo anajisikia salama mikononi mwake

13. Ikiwa kufanya jambo ambalo Mungu anatuomba inaonekana kuwa ni vigumu ao hata haiwezekane, namna gani mufano wa Maria unaweza kutusaidia?

13 Wakati fulani Mungu anaweza kutuomba tufanye jambo ambalo linaonekana kuwa ngumu ao hata haliwezekane. Lakini, katika Neno lake anatupatia sababu nyingi za kumutumainia, kujiacha katika mikono yake, kama Maria. (Met. 3:5, 6) Je, tutafanya hivyo? Tukifanya hivyo, atatubariki sana, na jambo hilo litatutolea sababu nyingi zitakazoongeza imani yetu kwake.

Maria Anamutembelea Elisabeti

14 Maria anatiwa moyo na maneno ambayo Gabrieli anamuambia kuhusu Elisabeti. Maria anajua kama kati ya wanawake wote duniani ni Elisabeti ndiye anaweza kuelewa hali yake vizuri kabisa. Kwa hiyo, kwa haraka anaenda katika eneo la milima-milima la inchi ya Yuda, safari hiyo inamuchukua karibu siku tatu ao ine. Anapoingia katika nyumba ya kuhani Zekaria na Elisabeti, Yehova anamupatia usadikisho mwengine ili kutia imani yake nguvu. Elisabeti anaposikia tu salamu ya Maria, mara moja anasikia kitoto kilicho katika tumbo lake kinaruka kwa furaha. Elisabeti anajaa na roho takatifu na anamuita Maria “mama ya Bwana wangu.” Mungu alimufunulia Elisabeti kwamba mutoto wa Maria atakuwa Bwana wake, yule Masiya. Zaidi ya hilo, Elisabeti anaongozwa na roho ya Mungu kumupongeza Maria kwa sababu ya imani yake na utii wake, anasema hivi: “Mwenye furaha pia ni yule aliyeamini.” (Lu. 1:39-45) Ndiyo, kila jambo ambalo Mungu alimuahidi Maria litatimia!

Maria na Elisabeti waliona urafiki wao kuwa ni baraka kabisa

14, 15. (a) Namna gani Yehova anamupatia Maria usadikisho mwengine ili kutia imani yake nguvu? (b) Maneno ya Maria yanayopatikana katika andiko la Luka 1:46-55 yanafunua nini juu yake?

15 Kisha Maria naye anasema. Maneno aliyosema yamechungwa vizuri katika Neno la Mungu. (Soma Luka 1:46-55.) Maneno hayo ndio mazungumuzo marefu ya Maria katika Biblia, na yanafunua mengi juu yake. Maneno yake yanaonyesha namna anavyomusifu Yehova ili kuonyesha shukrani yake na kuonyesha kwamba anasamini pendeleo analomutolea la kuwa mama ya Masiya. Yanaonyesha kwamba Maria ana imani kubwa: anasema kwamba Yehova anawashusha wenye majivuno na wenye nguvu na kuwasaidia watu wa hali ya chini na masikini wanaotaka kumutumikia. Pia, yanaonyesha kwamba Maria ana ujuzi sana wa maandiko. Inakadiriwa kwamba alitaja Maandiko ya Kiebrania zaidi ya mara 20! *

16, 17. (a) Ni sifa gani Maria na mwana wake walionyesha ambayo tunapaswa kuiga? (b) Maria kumutembelea Elisabeti kunatukumbusha jambo gani kuhusu faida ya urafiki?

16 Ni wazi kwamba Maria ni mwanamuke mwenye kutafakari sana juu ya Neno la Mungu. Hata hivyo, yeye anabaki tu munyenyekevu, anaacha Maandiko yaseme kuliko kujitungia mambo ya kusema. Mutoto aliyekuwa katika tumbo lake alipokomaa, alionyesha pia unyenyekevu huohuo, alisema hivi: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.” (Yoh. 7:16) Kwa hiyo, ni vizuri kujiuliza: “Je, ninaliogopa na kuliheshimu Neno la Mungu hivyo? Ao je, ninapendelea kufundisha mawazo yangu mwenyewe?” Maria kwa upande wake alikuwa na maoni yanayofaa.

17 Maria anaendelea kukaa na Elisabeti kwa miezi mitatu hivi, bila shaka anapata vitia-moyo vingi na anamutolea pia Elisabeti vitia-moyo. (Lu. 1:56) Habari hiyo yenye kufurahisha kuhusu matembezi hayo inatukumbusha kwamba kuwa na rafiki ni baraka kabisa. Tukifanya urafiki na watu wanaomupenda kabisa Mungu wetu Yehova, tutakuwa pia marafiki wazuri wa Yehova na tutakuwa na hali nzuri ya kiroho. (Met. 13:20) Mwishowe, wakati wa Maria kurudi nyumbani unafika. Sasa Yosefu atasema nini atakapojulishwa hali ya Maria?

Maria na Yosefu

18. Maria anamuambia Yosefu nini, naye Yosefu anajisikia namna gani?

18 Inaonekana kwamba Maria hangojee watu waone kama ana mimba ili amujulishe Yosefu jambo hilo. Labda mbele ya kuzungumuza na Yosefu, anajiuliza namna mwanaume huyo mwema, anayemuogopa Mungu atakavyojisikia wakati atamujulisha habari hiyo. Hata hivyo, anaenda kumuona na kumuelezea mambo yote yaliyomufikia. Je, katika akili yako unaweza kuona namna Yosefu ni mwenye kuvurugika sana? Anafanya nguvu ya kuamini yale binti huyo mupendwa wake anamuambia, lakini anaona kwamba binti huyo si mwaminifu kwake. Biblia haieleze ni mawazo gani yalimuvuruga Yosefu ao ni nini alikuwa anafikiri, lakini inasema tu kwamba aliamua kuvunja ndoa. Ni hivyo, kwa sababu wakati huo watu waliochumbiana walionekana kuwa kama wameoana. Yosefu hataki kumupatisha Maria haya mbele ya watu ao kumufanya aazibiwe, kwa hiyo, anaamua kuvunja ndoa hiyo kwa siri. (Mt. 1:18, 19) Bila shaka, Maria anahuzunishwa sana kuona namna mwanaume huyu mwema anavyohangaishwa na hali hiyo isiyo ya kawaida. Lakini, Maria hamulaumu Yosefu kwa sababu Yosefu hamuamini.

19. Namna gani Yehova anamusaidia Yosefu kuchukua uamuzi unaofaa?

19 Kwa upendo Yehova anamusaidia Yosefu kuchukua uamuzi unaofaa. Katika ndoto, malaika wa Mungu anamuambia kwamba mimba ya Maria kwa kweli ilikuwa ya kimuujiza. Bila shaka, hilo linamutuliza kabisa Yosefu! Sasa Yosefu anafanya kama vile Maria alivyofanya hapo mwanzoni, ni kusema, anatenda kama vile Yehova anavyomuagiza. Anamuoa Maria, na anajitayarisha kutimiza daraka la pekee la kumulea Mwana wa Yehova.—Mt. 1:20-24.

20, 21. Maisha ya Yosefu na Maria yanaweza kuwafundisha nini wale waliokwisha kufunga ndoa na wale wanaotazamia kufunga ndoa?

20 Ndoa ya Yosefu na Maria, watu walioishi kumepita miaka 2 000, inaweza kuwafundisha mengi wale waliokwisha kufunga ndoa, na wale wanaotazamia kufunga ndoa. Yosefu anapoona namna bibi yake ambaye bado ni kijana anavyotimiza daraka lake la mama, bila shaka anafurahi kuona kwamba malaika wa Yehova alimuongoza. Hakika Yosefu aliona ulazima wa kumutegemea Yehova wakati mutu anataka kuchukua maamuzi mazito. (Zab. 37:5; Met. 18:13) Yosefu aliendelea kubaki mwangalifu na mwenye fazili katika maamuzi yote aliyokuwa anachukua kuhusu familia yake.

21 Kwa upande mwengine, tunaweza kujifunza nini tunapoona kwamba Maria anakubali Yosefu amuoe hata ikiwa Yosefu hakuamini haraka yale aliyomuambia? Hata ikiwa hapo mwanzoni Yosefu hakumuelewa, Maria hakuvunjika moyo haraka, alingojea ili aone namna gani mwanaume huyo ataamua, kwa sababu ni mwanaume huyo ndiye atakuwa kichwa cha familia yao. Bila shaka, Maria aliona ulazima wa kuwa muvumilivu, na hilo ni somo nzuri sana kwa dada Wakristo leo. Mwishowe, mambo ambayo Yosefu na Maria walipitia yaliwafundisha mengi kuhusu ulazima wa kuzungumuza waziwazi katika familia na kuaminiana.—Soma Methali 15:22.

22. Sababu gani ndoa ya Yosefu na Maria ilikuwa na musingi muzuri, nao walifurahia sana tumaini gani?

22 Bila shaka, Yosefu na Maria walifanya ndoa yao iwe na musingi muzuri tangu mwanzo. Wote wawili walimupenda Yehova Mungu kuliko kila kitu, na zaidi ya hilo, walitamani sana kumupendeza katika daraka lao la kuwa wazazi wenye kuhangaikia familia yao. Kwa kweli, walibarikiwa sana, lakini pia walipambana na matatizo mengi. Walifurahia sana tumaini la kumulea Yesu atakapozaliwa, na kisha kumukomalisha yule ambaye alikuja kuwa mutu mukubwa zaidi ya watu wote waliopata kuishi.

^ fu. 15 Kati ya maandiko hayo ambayo Maria alitaja, inaonekana kwamba aliyachukua katika maneno ya Hana, mwanamuke mwenye imani ambaye pia Yehova alibariki na akazaa mutoto.​—Soma kisanduku “Sala Mbili Zisizo za Kawaida,” Sura ya 6.