Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KUMI NA SITA

Alitenda kwa Hekima, Ujasiri na kwa Kujinyima

Alitenda kwa Hekima, Ujasiri na kwa Kujinyima

1-3. (a) Hali iko namna gani Esta anapomukaribia bwana yake mwenye kukaa kwenye kiti cha ufalme? (b) Mufalme anakubali Esta amukaribie ao hapana?

ESTA anajongelea polepole kiti cha mufalme, moyo wake unapigapiga. Wazia namna chumba kikubwa cha mufalme wa Perse huko Shushani kilivyo kimya kabisa, kiasi cha kwamba Esta anaweza kusikia mulio wa miguu yake anapotembea na mulio wa mavazi yake ya kifalme. Haruhusu akengeushwe na utukufu wa nyumba ya mufalme, nguzo zilizopambwa vizuri sana, dari lenye kutengenezwa kwa mbao za miti ya mierezi iliyotoka mbali huko Liban. Esta anakazia fikira zake yule mwanaume anayekaa kwenye kiti cha ufalme, ambaye anaweza kuamua ikiwa Esta ataendelea kuishi ao hapana.

2 Esta anamujongelea mufalme, naye mufalme anamukazia macho na kisha anamunyooshea fimbo yake ya kifalme ya zahabu. Ni tendo ndogo tu, lakini linaokoa uzima wa Esta, kwa sababu kwa kumunyooshea fimbo yake, mufalme anaonyesha kwamba amesamehe kosa ambalo Esta amefanya, ni kusema, kuingia mahali mufalme iko bila kuitwa. Esta anakaribia kiti cha ufalme, ananyoosha mukono wake na kugusa fimbo ya kifalme. Esta ni mwenye shukrani kabisa.—Esta 5:1, 2.

Kwa unyenyekevu, Esta alimushukuru mufalme kwa sababu alimuonyesha rehema

3 Mufalme Ahasuero anaonekana kabisa kuwa mutu tajiri na mwenye mamlaka makubwa. Inajulikana kwamba mavazi ya kifalme ambayo wafalme wa Perse wa siku hizo walikuwa wanavaa yalikuwa ya bei sana, kiasi cha mamia ya mamilioni ya dolare. Hata hivyo, Esta anaangalia macho ya bwana yake, anaona kama anamuchangamukia, kwa hiyo anajua kama anamupenda. Ahasuero anamuuliza: “Una nini, Ee, Esta, malkia, na ombi lako ni nini? Hata nusu ya ufalme—na upewe wewe!”—Esta 5:3.

4. Ni kazi gani ngumu inamungojea Esta?

4 Hiyo si mara ya kwanza Esta anaonyesha imani na ujasiri wenye kushangaza; mbele ya hapo alikuwa ameingia kumuona mufalme ili kuwatetea watu wake wasiuawe. Mupaka hapo alifanikiwa, lakini hata ikiwa mufalme anakubali aingie ili kumuona, bado ana kazi ngumu inayomungojea. Anapaswa kumusadikisha mutawala huyo mwenye kiburi kwamba mushauri wake ambaye anatumainia zaidi ni mutu muovu ambaye amemudanganya ili aagize watu wa Esta wauawe. Atafanya nini ili amusadikishe, na mufano wa Esta wa imani unaweza kutufundisha nini?

Anachagua kwa Hekima “Wakati wa Kusema”

5, 6. (a) Namna gani Esta anatumia kanuni inayopatikana katika andiko la Mhubiri 3:1, 7? (b) Namna gani Esta anaonyesha hekima anapozungumuza na bwana yake?

5 Je, Esta atamufunulia mufalme shida yake mbele ya kila mutu aliye hapo? Kufanya hivyo kunaweza kumupatisha mufalme haya na kumupatia Hamani nafasi ya kupinga mashitaka. Esta atafanya nini? Miaka mingi zamani, Mufalme mwenye hekima Sulemani aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu, . . . wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema.” (Mhu. 3:1, 7) Tunawazia kuwa mwanaume mwaminifu Mordekai hakukosa kumufundisha Esta, binti yake kijana, kanuni kama hizo alipokuwa anakomaa. Bila shaka, Esta alisikia ulazima wa kuchagua kwa uangalifu “wakati wa kusema.”

6 Esta anamujibu hivi: ‘Mufalme akiona vema, mufalme na aje leo pamoja na Hamani kwenye karamu ambayo nimemuandalia [ao nimemutayarishia].’ (Esta 5:4) Mufalme anakubali na anaagiza wamuite Hamani. Je, unaona namna Esta anavyozungumuza kwa hekima? Hamukosee bwana yake heshima na pia anataka amufunulie bwana yake shida yake mahali panapofaa na wakati unaofaa.—Soma Methali 10:19.

7, 8. Karamu ya kwanza ambayo Esta anatayarisha iko namna gani, hata hivyo, sababu gani hapendi kumujulisha mufalme shida yake mara moja?

7 Bila shaka, Esta alitayarisha karamu hiyo kwa kufikiria sana kila jambo ambalo bwana yake anafurahia. Anatayarisha divai nzuri ili wawe wenye furaha. (Zab. 104:15) Ahasuero anafurahia kabisa karamu hiyo, kwa hiyo, anamuuliza tena Esta ni nini anachotaka kumuomba. Je, huo ndio kweli wakati unaofaa wa kusema?

8 Esta hafikiri hivyo. Kuliko kufanya hivyo, anamualika mufalme na pia anamualika tena Hamani kwenye karamu, siku inayofuata. (Esta 5:7,8) Sababu gani anakawisha mambo hivyo? Usisahau kwamba watu wote wa Esta walikuwa wanangojea kuuawa, kwa sababu Hamani alikuwa ameruhusiwa na mufalme kutangaza sheria ya kuwamaliza Wayahudi wote. Kwa sababu ya hatari hiyo kubwa, Esta anapaswa kuhakikisha kwamba wakati anaochagua ndio wakati unaofaa, akikosea, watu wengi watapoteza maisha yao. Kwa hiyo, anangojea na anatayarisha nafasi hiyo nyingine ili kumuonyesha bwana yake kama anamuheshimu sana na anapenda kabisa kumufurahisha.

9. Je, uvumilivu ni wa lazima kabisa, na namna gani tunaweza kumuiga Esta katika jambo hilo?

9 Uvumilivu ni sifa ya lazima sana ambayo watu wengi hawana. Hata ikiwa Esta anahangaishwa na anataka kabisa kumuambia mufalme yale yaliyo moyoni, Esta anajionyesha kuwa muvumilivu, anangojea wakati unaofaa. Mufano wake unaweza kutufundisha mambo mengi, mara nyingi sisi wote tunaona mambo fulani ambayo hayaendeke na ambayo ingefaa yatengenezwe haraka. Ikiwa tunataka kumusadikisha mutu fulani mwenye mamlaka ashugulikie tatizo fulani, labda inatuomba kumuiga Esta na kuwa wavumilivu. Andiko la Methali 25:15 linasema hivi: ‘Kwa subira [ao uvumilivu] kiongozi anashawishiwa, na ulimi wa upole unaweza kuvunja mufupa.’ Ikiwa tunangojea kwa uvumilivu wakati unaofaa, na kusema jambo kwa upole, kama Esta, tunaweza hata kumutuliza mutu ambaye ni mupinzani sana. Je, Yehova, Mungu wa Esta, alibariki uvumilivu na hekima yake?

Uvumilivu Unaongoza Kwenye Haki

10, 11. Kisha kutoka kwenye karamu ya kwanza, ni nini inayomufanya Hamani akasirike, na marafiki wake na bibi yake wanamushauria afanye nini?

10 Uvumilivu wa Esta unaongoza kwenye mufululizo wa matukio makubwa. Hamani anaondoka kwenye karamu ya kwanza mwenye kuchangamuka sana, mwenye “shangwe na furaha moyoni,” anafikiri kwamba anapendwa sana na mufalme na malkia wake kuliko watu wote. Hamani anapitia kwenye lango la jumba la mufalme, anamuona Mordekai, Muyahudi ambaye bado anakataa kumuinamia. Kama tulivyoona katika Sura ya15, Mordekai hafanye hivyo ili kumukosea Hamani heshima, lakini ni kwa sababu ya zamiri yake na uhusiano wake pamoja na Yehova Mungu. Basi, ‘upesi Hamani anajawa na gazabu.’—Esta 5:9.

11 Wakati Hamani anawaambia marafiki wake na bibi yake kuhusu tendo hilo la Mordekai, wanamushauria atengeneze muti mukubwa, wenye urefu wa metre 22, kisha amuombe mufalme ruhusa ili amutundike Mordekai juu ya muti huo. Hamani anafurahia wazo lao na mara moja anamuomba mutu fulani atengeneze muti huo.—Esta 5:12-14.

12. Sababu gani mufalme anaomba asomewe kwa sauti maandishi ya serikali kuhusu mambo ya taifa, na anafikia kujua nini kupitia usomaji huo?

12 Wakati huohuo, usiku mufalme hapate usingizi. Biblia inasema: ‘Usingizi wa mufalme ulimutoka,’ basi anaomba asomewe kwa sauti maandishi ya serikali kuhusu mambo ya taifa. Anaposomewa, anasikia habari kuhusu mupango mubaya uliovumbuliwa wa kumuua. Anakumbuka jambo hilo; wale waliotaka kufanya hivyo, walikamatwa na kuuawa. Lakini, walimufanyia nini yule mwanaume aliyefunua mupango huo, ni kusema Mordekai? Kwa gafula, mufalme anauliza ikiwa Mordekai alipewa zawadi gani. Anajibiwa kwamba hakupewa kitu chochote.—Soma Esta 6:1-3.

13, 14. (a) Namna gani mambo yanaanza kumugeukia Hamani? (b) Marafiki wa Hamani na bibi yake wanamuambia nini?

13 Mufalme anakasirika, na anatambua kwamba hilo ni kosa, anajiuliza ni nani kati ya wakubwa walio hapo atamusaidia kutengeneza jambo hilo. Anapojiuliza hivyo, Hamani ndiye iko katika uwanja wa jumba la mufalme, amekuja asubuhi mapema, inaonekana kwamba ana hamu sana ya kupata ruhusa ya mufalme ili kumutundika Mordekai. Lakini, mbele hajatoa ombi lake, mufalme anamuita na kumuuliza ni nini mufalme anaweza kumufanyia mutu ambaye anapendezwa naye ili kumuheshimu kwa namna iliyo bora zaidi. Hamani anafikiri mutu huyo ni yeye tu na si mwengine, na anamuambia mufalme heshima kubwa inayopaswa kutolewa mutu kama huyo: Avalishwe mavazi ya kifalme, apewe mutumishi wa mufalme wa cheo cha juu amupandishe juu ya farasi ya mufalme, amutembeze kuzunguka Shushani na kumusifu kwa sauti ili watu wote wasikie. Wazia katika akili yako namna uso wa Hamani unavyobadilika anapoambiwa kwamba mutu huyo ni Mordekai! Na unajua mufalme anamupatia nani kazi ya kumusifu Mordekai kwa nyimbo? Anamupatia Hamani!—Esta 6:4-10.

14 Hamani anafanya kwa kinyongo kazi hiyo yenye kumuchukiza, kisha anaenda haraka nyumbani kwake, ni mwenye huzuni kabisa. Marafiki wake na bibi yake wanamuambia kwamba ikiwa mambo yamegeuka hivyo, ni ishara ya kwamba atapatwa na jambo mbaya, atashindwa mbele ya Mordekai na Wayahudi.—Esta 6:12, 13.

15. (a) Uvumilivu wa Esta ulizaa jambo gani nzuri? (b) Sababu gani ni hekima kwetu kuonyesha hali ya ‘kungojea’?

15 Kwa sababu Esta alikuwa muvumilivu kungojea siku moja zaidi ili kutoa ombi lake kwa mufalme, hilo lilimupatia Hamani wakati wa kufanya mambo yaliyoongoza kwenye kuanguka kwake. Na inawezekana ni Yehova aliyefanya mufalme huyo akose usingizi, sivyo? (Met. 21:1) Haishangaze ikiwa Neno la Mungu linatutia moyo tuwe katika hali ya ‘kungojea’! (Soma Mika 7:7.) Tunapomutumainia Mungu na kumungojea atende, tunaweza kufikia kutambua kwamba njia yake ya kutatua matatizo ndio nzuri zaidi kuliko njia zetu.

Anasema kwa Ujasiri

16, 17. (a) Ni wakati gani Esta anaona kuwa sasa ni “wakati wa kusema?” (b) Esta na Vashti, wanatofautiana namna gani?

16 Esta hapaswe kuendelea kumuacha mufalme katika wasiwasi kuhusu kile anachotaka; kwenye karamu anayotayarisha siku ya pili anapaswa kumuambia mambo yote. Lakini, ni wakati gani kabisa atamuambia? Bila kutazamia, mufalme anamuuliza tena ikiwa ombi lake ni nini, naye Esta anatumia nafasi hiyo ili kujieleza. (Esta 7:2) Sasa ‘wakati wa Esta wa kusema’ umefika.

17 Unaweza kuwazia namna Esta anavyofanya sala fupi kwa Mungu wake mbele ya kusema maneno haya: ‘Ikiwa nimepata kibali machoni pako, Ee mufalme, na mufalme akiona vema, na nipewe nafsi yangu mwenyewe kuwa ombi langu na watu wangu kuwa haja yangu.’ (Esta 7:3) Katika maneno hayo, unaona kwamba anamuheshimu mufalme, anamuhakikishia kwamba ataheshimu uamuzi wake kadiri anavyoona kuwa ni hivyo. Esta anatofautiana kabisa na Vashti ambaye alimupatisha bwana yake haya kimakusudi! (Esta 1:10-12) Tena, Esta hamuseme mufalme vibaya kwa sababu ya tendo lake la upumbavu la kumuaminia Hamani. Kuliko kufanya hivyo, anamulilia mufalme amulinde na hali inayohatarisha uzima wake.

18. Namna gani Esta anamufunulia mufalme tatizo lake?

18 Bila shaka, mufalme anashangazwa na anaguswa moyo na ombi hilo. Ni nani huyo anayetaka kuhatarisha maisha ya malkia wake? Esta anamujibu: ‘Tumeuzishwa, mimi na watu wangu, tuangamizwe, tuuawe na kuharibiwa. Basi ikiwa tungaliuzishwa tuwe watumwa na wajakazi, ningalinyamaza kimya. Lakini taabu hii haifae ikiwa inamuletea mufalme hasara.’ (Esta 7:4) Unaona kwamba Esta ameonyesha tatizo waziwazi, hata hivyo, anaongeza kwamba ingekuwa ni jambo tu la kuuzishwa kuwa watumwa hangesema lolote. Lakini, kwa kuwa mauaji hayo makubwa yangemuletea mufalme mwenyewe hasara kubwa, kwa hiyo hawezi kubaki kimya.

19. Mufano wa Esta unatufundisha nini kuhusu ufundi wa kumufanya mutu akubali yale unayomuambia?

19 Mufano wa Esta unatufundisha mambo mengi kuhusu ufundi wa kumufanya mutu akubali yale unayomuambia. Ikiwa una tatizo nzito na ni lazima umuambie mutu unayemupenda ao mutu fulani mwenye mamlaka tatizo hilo, ili kumusadikisha ni vizuri kuwa na uvumilivu, heshima na kusema tatizo hilo waziwazi.—Met. 16:21, 23.

20, 21. (a) Namna gani Esta anaonyesha waziwazi mupango wa Hamani, na hilo linamutia mufalme katika hali gani? (b) Hamani anafanya nini inapoonekana wazi kuwa yeye ni mutu mudanganyifu?

20 Mufalme anauliza: ‘Ni nani huyo, na iko wapi mutu huyo ambaye amejipatia ujasiri wa kufanya hivyo?’ Katika akili yako unaweza kuona namna Esta anavyoonyesha kidole chake na kusema: ‘Mutu huyo, mupinzani na adui, ni huyu Hamani mutu mubaya.’ Hamani ameshitakiwa. Anaogopa sana. Uso wa mufalme unabadilika kwa sababu ya hasira, anatambua sasa kwamba mushauri wake anayetumainia, amemudanganya kwa kumufanya atie sinyatire sheria ambayo ingemuangamiza bibi yake mupendwa! Mufalme anatoka kwa hasira na kuenda katika bustani ili atulie.—Esta 7:5-7.

Kwa ujasiri, Esta anafunua ubaya wa Hamani

21 Hamani anaona sasa kwamba inaonekana wazi kuwa yeye ni mutu mudanganyifu na mwoga, anainama kulilia kwenye miguu ya malkia ili kuomba huruma. Mufalme anaporudi anamuona Hamani karibu ya Esta kwenye kiti kirefu kilicho kama kitanda; mufalme anakasirika tena zaidi na kumushitaki Hamani kwamba anataka kumulala malkia kinguvu katika nyumba ya mufalme. Maneno hayo ni kifo cha Hamani. Anapelekwa akiwa mwenye kufunikwa uso. Mumoja wa watumishi wa mufalme anapaza sauti na kumuambia mufalme kuhusu muti ambao Hamani alitayarisha ili kumutundika Mordekai. Mara moja, Ahasuero anaamuru kwamba Hamani atundikwe juu ya muti huo.​—Esta 7:8-10.

22. Namna gani mufano wa Esta unaweza kutufundisha kuwa na tumaini, kutokuasi, ao kuwa na imani tunapoonewa ao kupatwa na mambo ya kukosa haki?

22 Katika ulimwengu huu usio na haki, ni vigumu kuwazia kwamba siku fulani kutakuwa na haki. Wewe pia umekwisha kuwa na wazo hilo? Esta hakukata tumaini, hakuasi, wala kukosa imani. Wakati ulipojitokeza, alisema kwa ujasiri ili kutetea haki, na alimutumainia Yehova. Sisi pia acheni tufanye hivyohivyo! Tangu wakati wa Esta, Yehova hajabadilika. Bado ana uwezo wa kuwanasa waovu na watu wadanganyifu katika mitego yao wenyewe, kama Hamani.—Soma Zaburi 7:11-16.

Alijinyima kwa Ajili ya Yehova na Ndugu Zake

23. (a) Mufalme anamupatia Mordekai na Esta zawadi gani? (b) Namna gani unabii ambao Yakobo alitoa alipokuwa kwenye kitanda mbele ya kufa kumuhusu Benyamini ulitimia? (Soma kisanduku, “Utimizo wa Unabii.”)

23 Mwishowe, mufalme anajua kwamba Mordekai, mwanaume mwaminifu, ndiye aliyemuponyesha na mipango ya kumuua, na anajua pia kwamba yeye ndiye baba mulezi wa Esta. Ahasuero anamupa Mordekai cheo cha Hamani, anakuwa waziri mukubwa. Kisha anamupa Esta nyumba ya Hamani na utajiri wake mwingi. Na Esta anamufanya Mordekai kuwa musimamizi wa nyumba hiyo.—Esta 8:1, 2.

24, 25. (a) Sababu gani Esta hapumuzike hata ikiwa mupango wa Hamani unafunuliwa wazi? (b) Namna gani Esta anahatarisha tena uzima wake?

24 Kwa kuwa sasa hakuna tena hatari juu ya Esta na Mordekai, je, malkia anapaswa sasa kupumuzika? Hawezi kufanya hivyo, yeye ni mutu anayefikiria sana wengine. Wakati huo, sheria ya Hamani ya kuwaua Wayahudi ilikuwa imetumwa katika utawala wote wa Perse. Hamani alipiga kura, ao Puri, ambayo ni namna ya uchawi ya kuzungumuza na pepo, ili kujua siku inayofaa ya kutimiza mauaji hayo. (Esta 9:24-26) Kulikuwa bado miezi ya kutosha mbele ya kufikia siku hiyo, lakini ilikaribia sana. Je, ingewezekana kuepuka musiba huo?

25 Kwa kuwa Esta ana moyo wa kujinyima, anahatarisha tena maisha yake, anaenda tena kumuona mufalme bila kuitwa. Mara hii anatoa hata machozi kwa ajili ya watu wake, anamulilia bwana yake afute sheria hiyo mbaya. Lakini, sheria zilizopitishwa katika jina la mufalme wa Perse haziwezi kufutwa. (Dan. 6:12, 15) Kwa hiyo, mufalme anamupa Esta na Mordekai mamlaka ya kuandika sheria mupya. Kwa hiyo, tangazo la pili linatumwa, ambalo linawapa Wayahudi haki ya kujilinda ili wasishambuliwe. Wapanda-farasi wanaenda mbio katika kila sehemu ya utawala wa Perse, wanawapelekea Wayahudi habari hiyo njema. Sasa Wayahudi wanapata tena tumaini. (Esta 8:3-16) Katika akili yako unaweza kuona namna Wayahudi hao wanavyochukua silaha na kujitayarisha kupigana, jambo ambalo hawangefanya ikiwa sheria hiyo mupya haingetolewa. Hata hivyo, ulizo la lazima ni hili, je, “Yehova wa majeshi” atakuwa pamoja na watu wake?—1 Sam. 17:45.

Esta na Mordekai wanatuma tangazo kwa Wayahudi walio katika utawala wa Perse

26, 27. (a) Maadui wa watu wa Yehova waliharibiwa kwa kiasi gani, na je, watu wa Yehova walifikia mwisho wa ushindi wao? (b) Wakati watoto wa Hamani waliuawa, ni unabii gani ulitimia?

26 Siku hiyo iliyochaguliwa inapofika, watu wa Mungu wako tayari. Hata watumishi wengi wa mufalme katika utawala wa Perse wanaposikia kwamba Mordekai, Muyahudi, anakuwa waziri mukubwa, wanaunga Wayahudi mukono. Yehova aliwapatia watu wake ushindi mukubwa. Bila shaka, Yehova anawalinda watu wake ili wasishambuliwe tena wakati mwengine, na kwa hiyo anafanya maadui wao washindwe kabisa. *Esta 9:1-6.

27 Jambo lingine ni hili: Mordekai hatajisikia kuwa salama ikiwa atasimamia nyumba ya Hamani na bado watoto wanaume kumi wa mwanaume huyo muovu wangali wazima. Kwa hiyo, wao pia wanauawa. (Esta 9:7-10) Kwa kufanya hivyo, unabii wa Biblia unatimia, kwa sababu zamani Mungu alikuwa amesema kwamba Waamaleki walipaswa kuangamizwa kabisa, kwa sababu walijifanya kuwa maadui wa watu wa Mungu. (Kum. 25:17-19) Inaonekana kwamba watoto wa Hamani ndio waliokuwa watu wa mwisho wa taifa hilo lililohukumiwa.

28, 29. (a) Sababu gani ilikuwa ni mapenzi ya Mungu kwamba Esta na watu wake wafanye vita ya kimwili? (b) Sababu gani mufano wa Esta ni baraka kwetu leo?

28 Esta alichukua madaraka mazito ijapokuwa alikuwa angali kijana, kama vile kutolewa kwa sheria za mufalme zilizowaruhusu Wayahudi kupigana na kuua maadui wao. Haikuwa jambo rahisi. Lakini, ili mapenzi ya Yehova yatimie, iliomba watu wake walindwe. Taifa la Israeli lilipaswa kutokeza Masiya, tumaini pekee la wanadamu wote! (Mwa. 22:18) Leo, watumishi wa Mungu wanafurahi kujua kwamba yule Masiya, Yesu, alipokuja duniani, aliwakataza wafuasi wake, kuanzia wakati huo, kupigana vita ya kimwili.—Mt. 26:52.

29 Hata hivyo, Wakristo wanapigana vita ya aina nyingine, ni kusema, vita ya kiroho; Shetani amekusudia kabisa kuharibu imani yetu katika Yehova Mungu. (Soma 2 Wakorintho 10:3, 4.) Kuwa na mufano wa Esta ni baraka kubwa kabisa! Kama yeye, sisi pia tunapaswa kuonyesha imani kwa kuwa wavumilivu na wenye hekima tunaposadikisha watu kwa ujasiri, na kuwa tayari kujinyima ili kuwatetea watu wa Mungu.

^ fu. 26 Mufalme aliwapatia Wayahudi siku zingine mbili ili waendelee kupigana na adui zao na kuwashinda kabisa. (Esta 9:12-14) Hata leo, Wayahudi wanakumbuka ushindi huo kwenye sikukuu ya Purimu inayofanywa kila mwaka katika mwezi wa Adar, ni kusema, mwisho wa Mwezi wa 2 na mwanzoni mwa Mwezi wa 3, kulingana na kalendari yetu. Jina Purimu linatokana na kura ambayo Hamani alipiga ili kujua namna atawaangamiza Waisraeli..