Ona video zinazopatikana

Wanamuke Wenye Kuzungumuziwa mu Biblia Wanatufundisha Nini?

Wanamuke Wenye Kuzungumuziwa mu Biblia Wanatufundisha Nini?

Jibu la Biblia

 Biblia inataja majina ya wanamuke wengi. Kujifunza juu ya maisha ya wale wanamuke inaweza kutufundisha mambo ya mingi ya lazima. (Waroma 15:4; 2 Timoteo 3:16, 17) Hii habari inazungumuzia tu kwa kifupi wanamuke fulani wenye Biblia inataja. Wengi kati yao walikuwa mifano ya muzuri yenye tunaweza kufuata, lakini wengine walikuwa mifano ya mubaya yenye hatupendi kufuata.​—1 Wakorinto 10:11; Waebrania 6:12.

  Abigaili

 Abigaili alikuwa nani? Alikuwa bibi ya Nabali, mwanaume tajiri, lakini mwenye alikuwa mukali sana. Abigaili yeye, alikuwa na utambuzi na munyenyekevu. Alikuwa na sura na umbo ya muzuri, na masifa yenye kumufurahisha Yehova.​—1 Samweli 25:3.

 Alifanya nini? Abigaili alitenda kwa hekima na kwa utambuzi juu ya kuepuka musiba. Yeye na bwana yake Nabali waliishi mu eneo yenye Daudi, mwenye angekuwa mufalme wa Israeli, alikimbilia juu ya kujificha. Wakati Daudi na wanaume wake walikuwa wanaishi kule, walikuwa wanalinda makundi ya kondoo ya Nabali ili wanyanganyi wasiikamate. Lakini wakati Daudi alituma wanaume wake kwa Nabali juu awapatie chakula kidogo, Nabali aliwajibu kwa zarau na alikatala kuwapatia chakula yenye waliomba. Daudi alikasirika sana. Kwa hiyo, yeye na wanaume wake walienda kwa Nabali juu ya kumuua na kuua wanaume wote wa mu nyumba yake.​—1 Samweli 25:10-12, 22.

 Wakati alisikia mambo yenye bwana yake alifanya, Abigaili alitenda haraka. Alipatia watumishi wake chakula ya kumupelekea Daudi na wanaume wake. Na yeye mwenyewe aliwafuata juu ya kumuomba Daudi huruma. (1 Samweli 25:14-19, 24-31) Wakati Daudi aliona zawadi zenye Abigaili alimuletea, namna alitenda kwa unyenyekevu, na wakati Daudi alisikiliza mashauri yake ya hekima, akatambua kama ni Mungu njo alituma ule mwanamuke juu ya kumuepusha kufanya mambo ya mubaya. (1 Samweli 25:32, 33) Wakati kidogo kisha pale, Nabali alikufa na Abigaili akakuwa bibi ya Daudi.​—1 Samweli 25:37-41.

 Mufano wa Abigaili unaweza kutufundisha nini? Hata kama alikuwa na sura na umbo ya muzuri, na hata kama alikuwa tajiri, Abigaili hakujiona kuwa wa maana sana. Juu ya kuendelesha amani, Abigaili alikuwa tayari kuomba musamaha hata kama haiko yeye njo alikosea. Juu ya kumaliza hali ya nguvu, Abigaili alitumia akili na akatenda kwa utulivu, busara, na uhodari.

  •  Juu ya kujua mambo ya mingi kuhusu Abigaili, soma habari yenye kichwa “Alitenda kwa Busara.”

  Bibi ya Loti

 Bibi ya Loti alikuwa nani? Biblia haitaje jina yake. Lakini inasema kama alikuwa na watoto wanamuke wawili na kama yeye na watu wa familia yake waliishi mu muji wa Sodoma.​—Mwanzo 19:1, 15.

 Alifanya nini? Alikosa kutii Amri ya Mungu. Mungu aliamua kuharibu muji wa Sodoma na miji yenye ilikuwa pembeni juu watu wa mu ile miji walikuwa na tabia ya kufanya uasherati. Juu Mungu alimupenda Loti, mutu mwenye haki, na familia yake, wenye walikuwa wanaishi mu muji wa Sodoma, alituma malaika wawili ili kuwatosha mu muji na kuwapeleka fasi yenye ilikuwa salama.​—Mwanzo 18:20; 19:1, 12, 13.

 Wale malaika waliambia watu wa familia ya Loti wakimbie na wasiangalie nyuma; kama wanaangalia nyumba wangekufa. (Mwanzo 19:17) Bibi ya Loti “akaanza kuangalia nyuma, naye akakuwa nguzo ya chumvi.”​—Mwanzo 19:26.

 Mufano wa bibi ya Loti unaweza kutufundisha nini? Habari yake inaonyesha hatari ya kupenda vitu vya kimwili mupaka kufikia kukosa kumutii Mungu. Yesu alionyesha kama bibi ya Loti alikuwa mufano mubaya. Alisema hivi: “Mukumbuke bibi ya Loti.”​—Luka 17:32.

  Debora

 Debora alikuwa nani? Alikuwa nabii mwanamuke mwenye Yehova, Mungu wa Israeli, alitumia juu ya kuambia watu wake mambo yenye alipenda wafanye. Tena, Mungu alimutumia juu ya kusaidia kumaliza matatizo kati ya Waisraeli.​—Waamuzi 4:4, 5.

 Alifanya nini? Kwa uhodari nabii mwanamuke Debora alitegemeza watu wenye walimuabudu Mungu. Kwa muongozo wa Mungu, alimuita Baraka ili aongoze Waisraeli mu vita juu ya Wakanaani wenye walikuwa wanawatesa. (Waamuzi 4:6, 7) Wakati Baraka alimuomba Debora aende naye ku vita, hakuogopa wala hakukatala kuenda, lakini kuliko kufanya vile aliitika na akaenda naye.​—Waamuzi 4:8, 9.

 Kisha Mungu kuwapatia ushindi mukubwa, Debora alitunga sehemu ya wimbo yenye aliimba na Baraka juu ya kueleza namna mambo ilikuwa. Mu ile wimbo, alionyesha mambo yenye Yaeli, mwanamuke mwingine mwenye kuwa hodari, alifanya ili wapate ushindi juu ya Wakanaani.​—Waamuzi, sura ya 5.

 Mufano wa Debora unaweza kutufundisha nini? Debora alikuwa na uhodari na alikuwa tayari kujitoa. Alitia watu moyo wafanye mambo yenye Mungu anaona kuwa ya muzuri. Na wakati watu walifanya vile, aliwapongeza sana.

  Delila

 Delila alikuwa nani? Alikuwa mwanamuke mwenye Samsoni, muamuzi Muisraeli, alipenda.​—Waamuzi 16:4, 5.

 Alifanya nini? Aliitika makuta ya wakubwa Wafilisti juu ya kumusaliti Samsoni, mwenye Mungu alikuwa anatumia ili kuokoa Waisraeli kutoka kwa Wafilisti. Wafilisti walishindwa kumukamata juu alikuwa na nguvu ya ajabu yenye ilitoka kwa Mungu. (Waamuzi 13:5) Kwa hiyo, wakubwa wa Wafilisti walimuomba Delila awasaidie.

 Wafilisti walimupatia Delila makuta juu atafute kujua kwenye kunatokaka nguvu ya ajabu yenye Samsoni anakuaka nayo. Delila aliitika, na kisha kumuuliza mara mingi, alifikia kuvumbula siri ya Samsoni. (Waamuzi 16:15-17) Kisha aliambia Wafilisti ile siri, na wakamukamata Samsoni na kumutia mu gereza.​—Waamuzi 16:18-21.

 Mufano wa Delila unaweza kutufundisha nini? Delila alikuwa mufano mubaya. Juu alikuwa na pupa ya makuta, alimutendea mutumishi wa Yehova Mungu kwa udanganyifu, kwa kukosa ushikamanifu, na kwa uchoyo.

  Esta

 Esta alikuwa nani? Alikuwa mwanamuke Muyahudi mwenye Mufalme Ahasuero wa Uajemi alichagua juu akuwe Malkia wake.

 Alifanya nini? Malkia Esta alitumia cheo yake ili kuzuia mauaji makubwa juu ya watu wake. Alivumbula kama Mufalme alitoa agizo yenye ilionyesha siku yenye Wayahudi wote wenye kuishi mu utawala wa Uajemi walipaswa kuuawa. Ile mupango ya mubaya ilitoka kwa mwanaume mwenye alikuwa waziri mukubwa, jina yake ilikuwa Hamani. (Esta 3:13-15; 4:1, 5) Juu binamu (ao cousin) yake Mordekai, mwenye alikuwa na miaka mingi kuliko yeye, alimusaidia; na juu alitia maisha yake mu hatari, Esta alimufunulia bwana yake, Mufalme Ahasuero ile mupango ya mubaya. (Esta 4:10-16; 7:1-10) Kwa hiyo Ahasuero alimuruhusu Esta na Mordekai watangaze agizo ingine yenye kuruhusu Wayahudi wapiganie uzima wao. Wayahudi waliwashinda kabisa maadui wao.​—Esta 8:5-11; 9:16, 17.

 Mufano wa Esta unaweza kutufundisha nini? Malkia Esta alituachia mufano muzuri sana wa uhodari, unyenyekevu, na kiasi. (Zaburi 31:24; Wafilipi 2:3) Hata kama alikuwa na sura na umbo ya muzuri, na hata kama alikuwa na cheo ya juu; aliomba mashauri na musaada. Wakati alizungumuza na bwana yake, alifanya vile kwa busara, kwa heshima na kwa uhodari. Na wakati Wayahudi walikuwa mu hatari sana, kwa uhodari alijitambulisha kuwa mumoja wao.

  Eva

 Eva alikuwa nani? Alikuwa mwanamuke wa kwanza kabisa ku dunia na ni yeye njo mwanamuke wa kwanza mwenye Biblia inataja.

 Alifanya nini? Eva alikosa kutii agizo yenye kuwa wazi yenye Mungu alitoa. Sawa tu Adamu, bwana yake, Eva alikuwa mukamilifu wakati aliumbwa na alikuwa na uhuru wa kuchagua. Pia alikuwa na uwezo wa kukomalisha sifa za Mungu, kama vile, upendo na hekima. (Mwanzo 1:27) Eva alijua kama Mungu alimwambia Adamu kuwa ikiwa wangekula matunda ya muti fulani, wangekufa. Lakini alidanganywa na akawaza kama hatakufa. Kusema kweli, Shetani alimufanya awaze kama ikiwa anakosa kumutii Mungu, atakuwa na maisha ya muzuri. Kwa hiyo, alikula tunda ya muti yenye Mungu alikataza na akamuchochea bwana yake naye akule.​—Mwanzo 3:1-6; 1 Timoteo 2:14.

 Mufano wa Eva unaweza kutufundisha nini? Mufano mubaya wa Eva unaonyesha hatari ya kuendelea kuwaza juu ya mambo ya mubaya. Hata kama agizo ya Mungu ilikuwa wazi, Eva alikomalisha tamaa yenye ilifikia kuwa nguvu sana na ikamusukuma kukamata kitu yenye haikukuwa yake.​—Mwanzo 3:6; 1 Yohana 2:16.

  Hana

 Hana alikuwa nani? Alikuwa bibi ya Elkana na mama ya Samweli, mwenye alifikia kuwa nabii mwenye kujulikana sana mu Israeli ya zamani.​—1 Samweli 1:1, 2, 4-7.

 Alifanya nini? Juu Hana hakukuwa anazala, alimuomba Mungu amufariji. Bwana ya Hana alikuwa na bibi wawili. Bibi yake mwingine, Penina, alikuwa na watoto, lakini Hana yeye alibakia tasa kwa wakati murefu kisha yeye kuolewa. Kila mara Penina alikuwa anamuchokoza, lakini Hana alisali juu Mungu amufariji. Alifanya naziri na kumulaga Mungu kama akimupatia mutoto mwanaume, atamutolea ule mutoto na kufanya mipango juu atumike ku tabenakulo, hema yenye ilikuwa inaamishwa na yenye Waisraeli walitumia juu ya kuabudu.​—1 Samweli 1:11.

 Mungu alijibia sala ya Hana, na akamuzala Samweli. Hana alitimiza naziri yake kwa kumupeleka Samweli ku tabenakulo wakati alikuwa angali mutoto kidogo. (1 Samweli 1:27, 28) Kila mwaka, mama yake alikuwa anamutengenezea na kumupelekea koti yenye haina mikono. Kisha wakati fulani, Mungu alimubariki Hana na akazala watoto wengine tano, ni kusema, watoto wanaume watatu, na watoto wanamuke wawili.​—1 Samweli 2:18-21.

 Mufano wa Hana unaweza kutufundisha nini? Hana alitoa sala ya kutoka ku moyo, na ile ilimusaidia avumilie majaribu. Sala ya shukrani yenye alitoa yenye kuwa mu kitabu ya 1 Samweli 2:1-10 inaonyesha kama alikuwa na imani ya nguvu kwa Mungu.

  •  Juu ya kujua mambo ya mingi kuhusu Hana, soma habari yenye kichwa “Alimufungulia Mungu Moyo Katika Sala.”

  •  Juu ya kujua sababu zenye zilifanya Mungu aruhusu mwanaume kuwa na bibi wengi kati ya watu wake wa zamani, soma habari yenye kichwa “Je, Mungu Anakubali Ndoa ya Wanawake Wengi?

  Kijana mwanamuke Mushulami

 Kijana mwanamuke Mushulami alikuwa nani? Alikuwa kijana mwanamuke mwenye sura na umbo ya muzuri mwenye aliishi mu eneo ya mashamba na ni yeye njo anazungumuziwa sana mu kitabu ya Biblia yenye kuitwa Wimbo wa Sulemani. Biblia haitaje jina yake.

 Alifanya nini? Kijana mwanamuke Mushulami alibakia mushikamanifu kwa muchungaji wake mwenye alikuwa anapenda. (Wimbo wa Sulemani 2:16) Sura na umbo yake ya muzuri sana ilimuvutia Mufalme Sulemani mwenye alikuwa tajiri. Na Sulemani alipenda kuiba moyo wake. (Wimbo wa Sulemani 7:6) Hata kama watu wengine walimusukuma amuchague Sulemani, kijana Mushulami alikatala. Alimupenda na alibakia mushikamanifu kwa ule muchungaji wake mwenye alikuwa mutu wa hali ya chini.​—Wimbo wa Sulemani 3:5; 7:10; 8:6.

 Mufano wa kijana mwanamuke Mushulami unaweza kutufundisha nini? Hata kama alikuwa na sura na umbo ya muzuri, na hata kama watu walianza kupendezwa naye, kijana Mushulami hakuanza kujiona kuwa wa maana sana. Tena, hata kama watu walimukaza amuchague Sulemani, na hata kama Sulemani alimupatia ahadi ya kuwa tajiri na mwenye kujulikana sana, ile haikufanya aache kumupenda ule muchungaji. Alilinda hisia zake na akaendelea kuwa na mwenendo safi.

  Lea

 Lea alikuwa nani? Alikuwa bibi wa kwanza wa muzee wa ukoo Yakobo. Mudogo yake, Raheli, alikuwa bibi wa pili wa Yakobo.​—Mwanzo 29:20-29.

 Alifanya nini? Lea alimuzalia Yakobo watoto sita wanaume. (Rutu 4:11) Kusudi ya Yakobo ilikuaka kumuoa Raheli, hapana Lea. Lakini, Labani baba ya wale wanamuke wawili, alifanya mupango juu Lea aolewe pa nafasi ya Raheli. Wakati Yakobo alitambua kama Labani alimudanganya kwa kumupatia Lea, alikasirika na akaenda kuzungumuza naye. Labani akamuambia kama mu desturi yao, mutoto mudogo hawezi kuolewa mbele ya dada yake mukubwa. Kisha juma moja, Yakobo akamuoa Raheli.​—Mwanzo 29:26-28.

 Yakobo alimupenda sana Raheli kuliko Lea. (Mwanzo 29:30) Njo maana Lea alimusikilia dada yake wivu na akaanza kufanya naye mashindano juu afikie kuiba moyo wa Yakobo. Mungu aliona namna Lea alikuwa anajisikia na akamubariki kwa kumuwezesha kupata watoto saba, ni kusema, wanaume sita na mwanamuke mumoja.​—Mwanzo 29:31.

 Mufano wa Lea unaweza kutufundisha nini? Lea alimutegemea Mungu kwa kusali. Na hata kama alikuwa na magumu mu familia yake, hakuacha ile imufanye ashindwe kuona namna Mungu alikuwa anamusaidia. (Mwanzo 29:32-35; 30:20) Habari ya maisha yake inaonyesha waziwazi magumu yenye inakuaka mu ndoa ya bibi wengi, yenye Mungu aliruhusu kwa wakati fulani. Mupango wenye Mungu anakubali ni ndoa kati ya mwanaume mumoja na mwanamuke mumoja tu.​—Matayo 19:4-6.

  •  Juu ya kujua mambo ya mingi kuhusu Lea, soma habari yenye kichwa “Dada Waliotaabika Ambao ‘Waliijenga Nyumba ya Israeli.’

  •  Juu ya kujua sababu zenye zilifanya Mungu aruhusu kwa wakati fulani mwanaume kuwa na bibi wengi kati ya watu wake wa zamani, soma habari yenye kichwa “Je, Mungu Anakubali Ndoa ya Wake Wengi?

  Maria (dada ya Marta na Lazaro)

 Maria alikuwa nani? Sawa vile ndugu yake Lazaro, na dada yake Marta, na yeye alikuwa rafiki yake na Yesu wa sana.

 Alifanya nini? Mara mingi, Maria alionyesha kama alimuona Yesu, Mwana wa Mungu, kuwa wa maana. Aliamini kama Yesu alikuwa na uwezo wa kuzuia kifo ya ndugu yake Lazaro, na alikuwa pale wakati Yesu alimufufula. Wakati Maria aliamua kumusikiliza Yesu kuliko kusaidia kufanya ma kazi ya nyumba, Marta, dada yake alimusema. Lakini Yesu alimupongeza Marta juu aliona mafundisho ya Mungu kuwa ya maana sana kuliko kitu ingine yoyote.​—Luka 10:38-42.

 Wakati ingine, Maria alionyesha ukarimu sana kwa kumwanga juu ya kichwa na migulu ya Yesu “mafuta ya bei kali na yenye marashi.” (Matayo 26:6, 7) Watu fulani wenye walikuwa pale walisema kama Maria alipoteza ile mafuta bure. Lakini Yesu alimutetea na alisema: “Kila mahali kwenye hii habari njema [ya Ufalme wa Mungu] itahubiriwa katika ulimwengu wote, jambo lenye mwanamuke huyu alifanya litasemwa pia ili kumukumbuka.”​—Matayo 24:14; 26:8-13.

 Mufano wa Maria unaweza kutufundisha nini? Maria alikomalisha imani ya nguvu. Alitia pa nafasi ya kwanza ibada ya Mungu kuliko mambo ingine ya kawaida. Na kwa unyenyekevu alimuheshimia Yesu, hata wakati iliomba makuta mingi ili kufanya vile.

  Maria (mama ya Yesu)

 Maria alikuwa nani? Alikuwa kijana mwanamuke Muyahudi. Alikuwa bikira wakati alimuzala Yesu, mwana wa Mungu, ile iliwezekana juu ilikuwa muujiza.

 Alifanya nini? Maria alifanya mapenzi ya Mungu kwa unyenyekevu. Maria alikuwa alishachumbiwa na Yosefu wakati malaika alimutokea na kumuambia kama atakuwa na mimba na atazala Masiya mwenye watu walikuwa wanangojea tangu zamani. (Luka 1:26-33) Alikubali ile mugao kwa kujipendea. Kisha Yesu kuzaliwa, Maria na Yosefu walizala watoto ine wanaume na watoto wanamuke mbili ao zaidi. Kwa hiyo Maria hakuendelea kuwa bikira. (Matayo 13:55, 56) Hata kama alipata pendeleo ya pekee, Maria hayatafutaka kusifiwa ao hakukuwaka anatendewa kwa njia ya pekee, ikuwe wakati wa utumishi wa Yesu ao wakati alikuwa mu kutaniko ya wakati wa mitume.

 Mufano wa Maria unaweza kutufundisha nini? Maria alikuwa mwanamuke muaminifu. Na alikubali kwa kujipendea daraka nzito. Alijua muzuri sana Maandiko. Inaonekana kama wakati alisema maneno yenye inapatikana mu Luka 1:46-55, Maria alitaja sehemu mbalimbali za Maandiko mara makumi mbili hivi.

  •  Juu ya kujua mambo ya mingi kuhusu Maria, soma habari yenye kichwa “Mfano wa Maria Unatufundisha Nini?

  Maria Magdalene

 Maria Magdalene alikuwa nani? Alikuwa mwanafunzi mushikamanifu wa Yesu.

 Alifanya nini? Maria Magdalene alikuwa kati ya wanamuke wengi wenye walifanya safari pamoja na Yesu na wanafunzi wake. Kwa ukarimu alitumia mali yake ili kutegemeza mahitaji yao. (Luka 8:1-3) Alimufuata Yesu mupaka mwisho wa utumishi wake na alibakia karibu na Yesu wakati aliuawa. Alipata pendeleo ya kuwa kati ya watu wa kwanza kumuona Yesu kisha kufufuliwa.​—Yohana 20:11-18.

 Mufano wa Maria unaweza kutufundisha nini? Maria Magdalene alitegemeza utumishi wa Yesu kwa ukarimu na aliendelea kuwa mwanafunzi wake mupaka mwisho.

  Marta

 Marta alikuwa nani? Alikuwa dada ya Lazaro na Maria. Na wote watatu waliishi karibu na Yerusalemu, mu kijiji ya Betania.

 Alifanya nini? Marta alikuwa rafiki yake na Yesu wa sana, na Yesu “alimupenda Marta na dada yake, na Lazaro.” (Yohana 11:5) Marta alikuwa mwanamuke mwenye kukaribisha wageni. Siku moja wakati Yesu aliwatembelea, Maria aliamua kumusikiliza Yesu wakati Marta alikuwa anahangaikia makazi ya nyumba. Marta hakufurahi kuona namna Maria hakumusaidia. Kwa upole, Yesu alirekebisha mawazo ya Marta.​—Luka 10:38-42.

 Wakati Lazaro aligonjwa, Marta na dada yake walimuomba Yesu akuje juu walijua kama angeweza kumuponyesha ndugu yao. (Yohana 11:3, 21) Lakini Lazaro alikufa. Wakati Yesu alizungumuza na Marta, ilionekana wazi kama huyu mwanamuke alikuwa anaamini ahadi ya ufufuo yenye kuwa mu Biblia na alikuwa hakika kama Yesu alikuwa na uwezo wa kumufufula ndugu yake.​—Yohana 11:20-27.

 Mufano wa Marta unaweza kutufundisha nini? Marta alikuwa mukaribishaji wageni. Alikuwa tayari kukubali mashauri. Alisema waziwazi namna alikuwa anajisikia na alionyesha waziwazi imani yake.

  •  Juu ya kujua mambo ya mingi kuhusu Marta, soma habari yenye kichwa “Nimeamini.”

  Miriamu

 Miriamu alikuwa nani? Alikuwa dada ya Musa na Haruni. Yeye njo mwanamuke wa kwanza mwenye Biblia inaita nabii mwanamuke.

 Alifanya nini? Juu alikuwa nabii, alikuwa na daraka ya kuambia wengine ujumbe wa Mungu. Alikuwa na cheo ya juu mu Israeli na aliimba wimbo wa ushindi pamoja na wanaume kisha jeshi ya Wamisri kuharibiwa mu Bahari Nyekundu.​—Kutoka 15:1, 20, 21.

 Wakati fulani kisha pale, Miriamu na Haruni walianza kusema mubaya juu ya Musa. Ni wazi kama kiburi na wivu njo viliwasukuma kufanya vile. Mungu “alikuwa anasikiliza,” na akawakemea wote wawili, Miriamu na Haruni. (Hesabu 12:1-9) Kisha, Mungu alimupiga Miriamu kwa ukoma, na inaonekana ni juu yeye njo alianzisha ile maneno ya mubaya juu ya Musa. Wakati Musa alimuomba Mungu kwa ajili ya Miriamu, Mungu alimuponyesha. Na kisha kuwa mbali na watu kwa siku saba, Miriamu aliruhusiwa kurudia mu kambi ya Israeli.​—Hesabu 12:10-15.

 Biblia inaonyesha kama Miriamu alikubali kurekebishwa. Kisha mamia ya miaka, Mungu alizungumuzia pendeleo kubwa yenye alipata wakati alikumbusha Waisraeli hivi: “Nilituma Musa, Haruni, na Miriamu mbele yenu.”​—Mika 6:4.

 Mufano wa Miriamu unaweza kutufundisha nini? Habari ya Miriamu inaonyesha kama Mungu anasikilizaka kwa uangalifu mambo yenye watumishi wake wanaambiaka wengine ao kusema juu ya wengine. Tunajifunza pia kama ili kumufurahisha Mungu, tunapaswa kuepuka kiburi na wivu. Ile ni mambo yenye inaharibishaka sifa za wengine.

  Rahabu

 Rahabu alikuwa nani? Alikuwa kahaba mwenye aliishi mu muji wa Yeriko yenye ilikua mu eneo ya Kanaani, na alifikia kuwa mutumishi wa Yehova Mungu.

 Alifanya nini? Rahabu alificha Waisraeli wawili wenye walienda kupeleleza muji wa Yeriko. Alifanya vile juu alisikia habari yenye ilionyesha namna Yehova, Mungu wa Israeli, aliokoa watu wake kutoka mu Misri na namna aliwasaidia wakati kabila la Waamori liliwashambulia.

 Rahabu aliwasaidia wale wapelelezi na aliwaomba wamulinde yeye na watu wa familia yake wakati Waisraeli wangekuja kuharibu muji wa Yeriko. Walikubali, lakini, walimuambia kama juu wafanye vile kuko mambo yenye alipaswa kufanya na yenye hakupaswa kufanya: Hakupaswa kusema na mutu yeyote juu ya kusudi ya wale wapelelezi, yeye na watu wa familia yake wangepaswa kubakia mu nyumba yake wakati Waisraeli wangeshambulia muji, na angepaswa kutia kamba ya rangi ya mwekundu yenye kuangara ku dirisha la nyumba yake juu ile nyumba itambuliwe. Rahabu alifuata mambo yote yenye balimuambia, na yeye na watu wa familia yake waliokoka wakati Waisraeli walikamata muji wa Yeriko.

 Kisha, Rahabu aliolewa na mwanaume Mwisraeli na akakuwa babu ao tate ya Mufalme Daudi na Yesu Kristo.​—Yoshua 2:1-24; 6:25; Matayo 1:5, 6, 16.

 Mufano wa Rahabu unaweza kutufundisha nini? Biblia inaonyesha kama Rahabu alikuwa na imani ya nguvu. (Waebrania 11:30, 31; Yakobo 2:25) Habari yake inaonyesha kama Mungu anakuwaka anasamehe, hana ubaguzi, anakuwaka anabariki wale wenye kumutumainia hata kama zamani walikuwa na maisha ya mubaya.

  Raheli

 Raheli alikuwa nani? Alikuwa mutoto wa Labani na bibi mwenye Yakobo, muzee wa ukoo, alipendaka sana.

 Alifanya nini? Raheli aliolewa na Yakobo na alimuzalia watoto mbili wanaume. Na wale watoto walifikia kuwa kati ya wenye walianzisha makabila 12 ya Israeli ya zamani. Raheli alikutanaka na Yakobo, mwenye alifikia kuwa bwana yake, wakati alikuwaka anachunga kondoo za baba yake. (Mwanzo 29:9, 10) Alikuwa “mwenye kuvutia sana,” lakini dada yake, Lea, hakukuwa vile.​—Mwanzo 29:17.

 Yakobo alimupenda sana Raheli, na akaitika kutumika miaka saba juu amuoe. (Mwanzo 29:18) Lakini, Labani alimudanganya juu amuoe kwanza Lea, na ni kisha pale njo alimuruhusu amuoe Raheli.​—Mwanzo 29:25-27.

 Yakobo alimupenda sana Raheli na watoto wake wawili kuliko namna alimupenda Lea na watoto wake. (Mwanzo 37:3; 44:20, 27-29) Njo maana Raheli na Lea walikuwa wanashindana.​—Mwanzo 29:30; 30:1, 15.

 Mufano wa Raheli unaweza kutufundisha nini? Raheli alivumilia matatizo mu familia na aliendelea kuwa na tumaini kama Mungu atasikiliza sala zake. (Mwanzo 30:22-24) Habari yake inaonyesha namna ndoa ya bibi wengi inaletaka magumu mu familia. Habari ya Raheli inaonyesha kama Mungu alikuwa na hekima wakati alianzisha ndoa kati ya mwanaume mumoja na mwanamuke mumoja tu.​—Matayo 19:4-6.

  •  Juu ya kujua mambo ya mingi kuhusu Raheli, soma habari yenye kichwa “Dada Waliotaabika Ambao ‘Waliijenga Nyumba ya Israeli.

  •  Juu ya kujua sababu zenye zilifanya Mungu aruhusu kwa wakati fulani mwanaume kuwa na bibi wengi kati ya watu wake wa zamani, soma habari yenye kichwa “Je, Mungu Anakubali Ndoa ya Wake Wengi?

  Rebeka

 Rebeka alikuwa nani? Alikuwa bibi ya Isaka na mama ya mapacha (mapasa), Yakobo na Esau.

 Alifanya nini? Rebeka alifanya mapenzi ya Mungu, hata wakati ilikuwa nguvu kufanya vile. Wakati alikuwa anashota maji mu kisima, mwanaume fulani alimuomba maji kidogo akunywe. Palepale Rebeka alimupatia maji na akajitolea ashote maji pia kwa ajili ya ngamia wa ule mwanaume. (Mwanzo 24:15-20) Ule mwanaume alikuwa mutumishi wa Abrahamu, na alikuwa alishafanya safari ya murefu juu ya kumutafutia, mwana wa Abrahamu, Isaka bibi. (Mwanzo 24:2-4) Tena ule mwanaume alikuwa alishasali juu Mungu amubariki. Sasa wakati aliona namna Rebeka alifanya kazi kwa bidii na alikuwa mukarimu, alitambua kama Mungu alijibia sala yake, na alikuwa anamuonyesha kama ule mwanamuke njo atakuwa bibi ya Isaka.​—Mwanzo 24:10-14, 21, 27.

 Wakati Rebeka alijua sababu yenye ilifanya ule mwanaume afanye ile safari yote, alikubali kuenda pamoja naye na kuwa bibi ya Isaka. (Mwanzo 24:57-59) Rebeka alifikia kuwa na watoto wawili wanaume mapacha. Mungu alimuambia kama mutoto mukubwa, Esau, angemutumikia ule mudogo, Yakobo. (Mwanzo 25:23) Wakati Isaka alitaka kumupatia Esau baraka ya muzaliwa wa kwanza, Rebeka alifanya mupango juu Yakobo njo apate ile baraka. Rebeka alifanya vile juu alijua kama ile njo mapenzi ya Mungu.​—Mwanzo 27:1-17.

 Mufano wa Rebeka unaweza kutufundisha nini? Rebeka alikuwa na kiasi, alitumika kazi kwa bidii na alikuwa mukarimu. Ile masifa ilifanya akuwe bibi muzuri, mama muzuri, na mutumishi muzuri wa Mungu.

  •  Juu ya kujua mambo ya mingi kuhusu Rebeka, soma habari yenye kichwa “Niko Tayari Kuenda.”

  Rutu

 Rutu alikuwa nani? Alikuwa mwanamuke Mumoabu mwenye aliacha miungu yake na inchi yake ili akuwe muabudu wa Yehova mu inchi ya Israeli.

 Alifanya nini? Rutu alimuonyesha Naomi, mama-mukwe wake, upendo wa ajabu. Naomi, pamoja na bwana yake na watoto wao wawili walikimbilia mu eneo ya Moabu juu wasikufe na njala yenye ilikuwa mu Israeli. Wale watoto wawili walifikia kuoa wanamuke Wamoabu, Rutu na Orpa. Na kisha wakati fulani bwana ya Naomi na watoto wake wawili walikufa. Naomi na bibi za watoto wake wawili, wote walibakia wajane.

 Naomi aliamua kurudia mu inchi ya Israeli, na ile wakati ukame ulikuwa umeisha. Rutu na Orpa waliamua kuenda naye. Lakini Naomi aliwaambia warudie ku mafamilia yao. Orpa alirudia. (Rutu 1:1-6, 15) Lakini Rutu, alishikamana na mama-mukwe wake. Alimupenda Naomi na alipenda kumuabudu Yehova, Mungu wa Naomi.​—Rutu 1:16, 17; 2:11.

 Juu Rutu alikuwa binti-mukwe mushikamanifu, na mufanyakazi mwenye bidii, ile ilifanya ajulikane kuwa mwanamuke muzuri mu Betlehemu, muji wa Naomi. Boazi, mwanaume tajiri mwenye alikuwa na shamba lake alishangazwa sana na Rutu, na akamupatia chakula mingi kwa ajili yake na Naomi. (Rutu 2:5-7, 20) Kisha Rutu aliolewa na Boazi na akakuwa babu ao tate ya Mufalme Daudi na pia Yesu Kristo.​—Matayo 1:5, 6, 16.

 Mufano wa Rutu unaweza kutufundisha nini? Juu alimupenda Naomi na Yehova, Rutu alikuwa tayari kuacha nyumba yake na watu wa familia yake. Alikuwa anatumika kwa bidii, alijitoa kwa uaminifu-mushikamanifu hata wakati alipata magumu mingi.

  Sara

 Sara alikuwa nani? Alikuwa bibi ya Abrahamu na mama ya Isaka.

 Alifanya nini? Sara aliacha muji wa Uru wenye ulikuwa tajiri na kwenye alikuwa na maisha ya muzuri juu aliamini ahadi zenye Mungu alimupatia bwana yake, Abrahamu. Mungu alimuambia Abrahamu atoke mu muji wa Uru na aende mu muji wa Kanaani. Mungu alimupatia ahadi ya kumubariki na kumufanya akuwe taifa kubwa. (Mwanzo 12:1-5) Ile wakati inawezekana Sara alikuwa na miaka 60 hivi. Tangu pale na kuendelea Sara na bwana yake walianza kuishi mu mahema, na maisha ya kuhama-hama.

 Hata kama maisha ya kuhama-hama ilikuwa hatari, Sara alimutegemeza Abrahamu na alifuata muongozo wa Mungu. (Mwanzo 12:10, 15) Kwa miaka mingi Sara hakukuwa anazala, ile ilimuhuzunisha sana. Hata vile, Mungu alitoa ahadi kama angebariki uzao wa Abrahamu. (Mwanzo 12:7; 13:15; 15:18; 16:1, 2, 15) Kisha wakati fulani, Mungu alimuhakikishia Sara kama atamuzalia Abrahamu mutoto. Na alifikia kuzala mutoto hata kama alikuwa alishapitisha miaka yenye mwanamuke anaweza kuzala. Ile wakati alikuwa na miaka 90, na bwana yake alikuwa na miaka 100. (Mwanzo 17:17; 21:2-5) Walimupatia jina Isaka.

 Mufano wa Sara unaweza kutufundisha nini? Mufano wa Sara unatufundisha kama sikuzote tunaweza kutumaini kama Mungu atatimiza ahadi zake, hata ahadi zenye zinaonekana kuwa haziwezi kutimia! (Waebrania 11:11) Pia mufano wake muzuri unaonyesha kama heshima ni ya lazima sana mu ndoa.​—1 Petro 3:5, 6.

  Yaeli

 Yaeli alikuwa nani? Alikuwa bibi ya Heberi, mwanaume mwenye hakukuwa Mwisraeli. Kwa uhodari, Yaeli alitegemeza watu wa Mungu.

 Alifanya nini? Yaeli alitenda kwa uhodari na bila kukawia wakati Sisera, mukubwa wa jeshi ya Wakanaani, alikuja mu hema yake. Sisera alikuwa ameshindwa mu vita yenye alipigana na Waisraeli, alikimbia na alikuwa anatafuta fasi ya kujificha. Yaeli alimualika mu hema yake juu ajifiche na apumuzike. Wakati alikuwa analala, Yaeli akamuua.​—Waamuzi 4:17-21.

 Tendo ya Yaeli ilitimiza hii unabii yenye Debora alitoa: “Yehova atamutia Sisera katika mukono wa mwanamuke.” (Waamuzi 4:9) Yaeli alisifiwa juu ya tendo yenye alifanya, na aliitwa kuwa mwenye “amebarikiwa zaidi ya wanamuke wote.”​—Waamuzi 5:24.

 Mufano wa Yaeli unaweza kutufundisha nini? Yaeli alifanya mupango na akatenda kwa uhodari. Habari yake inaonyesha vile Mungu anaweza kuongoza mambo juu ya kutimiza unabii.

  Yezebeli

 Yezebeli alikuwa nani? Alikuwa bibi ya Mufalme Ahabu wa Israeli. Hakukuwa Mwisraeli na hakukuwa anamuabudu Yehova. Lakini alikuwa anaabudu Baali, mungu wa Wakanaani.

 Alifanya nini? Malkia Yezebeli alikuwa mutu wa kupenda kuonea wengine, hakukuwa na huruma na alikuwa mukali. Alichochea watu waabudu Baali na kufanya matendo ya uasherati yenye ilikuwa sehemu ya ile ibada. Na ileile wakati alijaribu kumaliza ibada ya Mungu wa kweli, Yehova.​—1 Wafalme 18:4, 13; 19:1-3.

 Juu apate vitu vyenye alitaka, Yezebeli alikuwa anadanganya na kuua watu. (1 Wafalme 21:8-16) Vile tu Mungu alitabiri, Yezebeli alikufa mubaya na habakumuzikaka.​—1 Wafalme 21:23; 2 Wafalme 9:10, 32-37.

 Mufano wa Yezebeli unaweza kutufundisha nini? Yezebeli iko mufano mubaya. Juu alikuwa na matendo ya mubaya na alikuwa tayari kufanya kila kitu ili apate kitu yenye alitafuta. Jina yake ikafikia kuwa alama yenye kuonyesha mwanamuke mweye kukosa haya, mwenye kuwa na matendo ya mubaya, mwenye haheshimie mamlaka na mwenye hahangaikie kitu, hata kama matendo yake ni ya muzuri ao ya mubaya.

 Wanamuke wenye kutajwa mu Biblia: Majina yao kulingana na wakati wenye waliishi

  1.  Eva

  2. Garika (2370 Mbele ya Kuzaliwa kwa Yesu)

  3.  Sara

  4.  Bibi ya Loti

  5.  Rebeka

  6.  Lea

  7.  Raheli

  8. Kutoka (1513 Mbele ya Kuzaliwa kwa Yesu)

  9.  Miriamu

  10.  Rahabu

  11.  Rutu

  12.  Debora

  13.  Yaeli

  14.  Delila

  15.  Hana

  16. Mufalme wa kwanza wa Israeli (1117 Mbele ya Kuzaliwa kwa Yesu)

  17.  Abigaili

  18.  Kijana mwanamuke Mushulami

  19.  Yezebeli

  20.  Esta

  21.  Maria (mama ya Yesu)

  22. Ubatizo wa Yesu (29)

  23.  Marta

  24.  Maria (dada ya Marta na Lazaro)

  25.  Maria Magdalene

  26. Kifo ya Yesu (33)