Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA PILI

“Alitembea Pamoja na Mungu wa Kweli”

“Alitembea Pamoja na Mungu wa Kweli”

1, 2. Noa na familia yake walishugulika na kazi gani, na ni magumu gani fulani ambayo walipambana nayo?

NOA anajinyoosha mugongo na sehemu zingine za mwili wake wenye kuchoka. Wazia namna anavyokaa kwenye kipande cha muti mukubwa ili kupumuzika kidogo, anatazama lile jengo kubwa la safina. Anasikia harufu kali ya lami yenye kuyeyushwa inaenea katika hewa; anasikia milio ya vyombo vya kazi ya seremala vilivyotengenezwa kwa miti. Mahali hapo anapokaa anaona namna watoto wake wanavyofanya kazi kwa bidii, wanajenga sehemu mbalimbali za jengo hilo kubwa la mbao. Sasa kumepita miaka mingi tangu Noa na bibi yake mupendwa, na watoto wake na bibi za watoto wake wanafanya kazi hii ya jasho pamoja, wanapenda kuimaliza. Tayari wamejenga sehemu kubwa ya safina, lakini bado wana kazi nyingi inayobaki ili kumaliza ujenzi huo!

2 Watu wanawaza kwamba Noa na familia yake ni wapumbavu. Kadiri Noa anavyoendelea kujenga safina, ndivyo watu wanavyoendelea kumuchekelea zaidi; watu wanapuuza wazo la kwamba dunia nzima itafunikwa kwa maji ya garika. Noa anaendelea kuwaonya, lakini wao wanaona kwamba hilo ni jambo lisilowezekana, ao kwamba ni upuuzi tu! Hawaelewe sababu gani mutu kama Noa anaweza kupoteza wakati wake na wa familia yake katika kazi kama hiyo isiyo na maana. Hata hivyo, Yehova, Mungu wa Noa hamuone kuwa mupumbavu ao mutu wa wazimu.

3. Noa alitembea pamoja na Mungu katika maana gani?

3 Neno la Mungu linasema hivi: “Noa alitembea pamoja na Mungu wa kweli.” (Soma Mwanzo 6:9.) Maneno hayo yanamaanisha nini? Hayamaanishe kwamba Mungu alikuja kutembea hapa duniani, wala kwamba Noa alienda kutembea kule mbinguni. Maana yake ni kwamba Noa alimutii na kumupenda Mungu sana, hivi kwamba ingeweza kusemwa kuwa yeye na Mungu wanatembea pamoja kama marafiki. Kisha maelfu ya miaka, Biblia ilisema hivi juu ya Noa: “Kupitia imani [yake] aliuhukumu ulimwengu.” (Ebr. 11:7) Namna gani Noa aliuhukumu ulimwengu kupitia imani yake? Imani ya Noa inaweza kutufundisha nini leo?

Mutu Asiye na Kosa Katika Ulimwengu Muovu

4, 5. Katika siku za Noa, sababu gani mambo maovu yalipita kiasi?

4 Noa alikomalia katika ulimwengu ulioendelea kuharibika zaidi haraka. Ni kweli kwamba mambo yalikuwa mabaya katika siku za Enoko, kambo (ao tate) yake, ambaye alikuwa pia mutu mwenye haki aliyetembea pamoja na Mungu. Enoko alitabiri kwamba siku ya hukumu inakuja juu ya watu wa ulimwengu wasiomuogopa Mungu. Lakini sasa, katika siku za Noa watu wanatenda uovu kupita kiasi. Kwa hiyo, kulingana na maoni ya Yehova, dunia ni yenye kuharibika kwa sababu inajaa jeuri. (Mwa. 5:22; 6:11; Yuda 14, 15) Ni nini inafanya hali ya dunia iwe mbaya kupita kiasi hivyo?

5 Hali fulani ya kusikitisha ilitokea kati ya wana wa kiroho wa Mungu, ni kusema, malaika wake. Mumoja wao alikuwa amekwisha kumuasi Yehova; akawa Shetani Ibilisi kwa kumusingizia Mungu na kuwashawishi Adamu na Eva watende zambi. Katika siku za Noa, malaika wengine wanaingia pia katika uasi wa Shetani. Malaika hao wanaacha mugao wao ambao Mungu aliwapatia huko mbinguni, wanakuja hapa duniani, wanavaa miili ya wanadamu, na wanaoa wale binti warembo sana. Hao malaika waasi, wenye kiburi na wenye kutafuta faida zao wenyewe walichochea mambo mabaya sana kati ya wanadamu.​—Mwa. 6:1, 2; Yuda 6, 7.

6. Namna gani Wanefili walifanya hali ya dunia iwe mbaya zaidi, na Yehova aliamua kufanya nini?

6 Jambo lingine ni hili: malaika hao wanaovaa miili ya kibinadamu wanalala na wanawake, jambo ambalo hawaruhusiwe kufanya. Wanawake hao wanawazalia watoto wasio wa kawaida; wakubwa na warefu sana na wenye nguvu nyingi sana. Biblia inawaita Wanefili, maana yake, “Waangushaji,” ni kusema, wale wanaofanya wengine waanguke. Wanefili ni wachokozi na hawana huruma, kwa hiyo wanafanya hali ya dunia iwe yenye kuharibika zaidi. Basi, haishangaze ikiwa Muumbaji, ‘aliona kwamba ubaya wa mwanadamu ulikuwa mwingi duniani na kila muelekeo wa fikira za moyo wake ulikuwa mubaya tu wakati wote.’ Kwa hiyo, Yehova aliamua kuwafagia kabisa watu hao waovu kisha miaka 120.​—Soma Mwanzo 6:3-5.

7. Noa na bibi yake walifanya nini ili kulinda watoto wao wasiambukizwe na hali mbaya ya siku zao?

7 Wazia namna ilikuwa vigumu kulea watoto katika dunia kama hiyo! Hata hivyo, Noa anatunza vizuri familia yake. Ana mwanamuke mwema. Kisha kueneza miaka 500, bibi yake anamuzalia watoto wanaume watatu: Shemu, Hamu na Yafethi. * Wote wawili, Noa na bibi yake, walilinda watoto wao ili wasiambukizwe na hali mbaya ya ulimwengu uliowazunguka. Kwa kawaida, watoto wadogo wanavutiwa na kushangazwa na “watu wenye nguvu” na ‘watu wenye sifa,’ na Wanefili ni watu wa namna hiyo. Noa na bibi yake hawawezi kufunga watoto wao masikio ili wasisikie habari kuhusu mambo ya ajabu ambayo Wanefili hao wanafanya, lakini wanaweza kuwafundisha ukweli wenye kuvutia juu ya Yehova Mungu, ambaye anachukia mambo yote maovu. Wanapaswa kusaidia watoto wao wajue kwamba Yehova anaumizwa sana moyoni na jeuri na uasi huo ambao watu wanafanya.​—Mwa. 6:6.

Noa na bibi yake walilinda watoto wao wasiambukizwe na hali mbaya

8. Namna gani wazazi wenye hekima wanaweza kuiga mufano wa Noa na bibi yake?

8 Wazazi leo, wanaweza kuelewa vizuri hali ya Noa na bibi yake. Leo pia dunia yetu inaharibika kwa sababu ya jeuri na uasi. Mara nyingi miji mikubwa inajaa vijana wenye kupotoka wanaotenda mambo ya jeuri. Hata mambo ya kujifurahisha yanayofanywa kwa ajili ya watoto yanajaa kabisa mambo ya jeuri na uasi. Wazazi wenye hekima wanafanya yao yote ili kuwalinda watoto wao wasiambukizwe na mambo hayo, kwa hiyo, wanawafundisha kumuhusu Mungu wa amani, Yehova, ambaye siku fulani atamaliza mambo yote ya jeuri. (Zab. 11:5; 37:10, 11) Ndiyo, hata katika dunia hii mbovu, inawezekana watoto wajifunze mambo mazuri ya kufanya! Noa na bibi yake walifanikiwa. Watoto wao walikomaa vizuri na kuwa wanaume wema, na walioa wanawake ambao pia walipenda kumutia Yehova, Mungu wa kweli pa nafasi ya kwanza katika maisha yao.

‘Ujifanyie Safina’

9, 10. (a) Yehova anamupatia Noa amri gani inayobadilisha kabisakabisa maisha yake? (b) Ni mambo gani Yehova anamuambia Noa juu ya ujenzi na kusudi la safina?

9 Siku fulani, maisha ya Noa yanabadilika kabisakabisa. Yehova anamuambia mutumishi wake mupendwa kusudi lake la kuharibu dunia ya wakati huo. Mungu anamuamuru Noa hivi: ‘Ujifanyie safina ya muti wenye utomvu.’​—Mwa. 6:14.

10 Safina hiyo haikuwa mashua ya kawaida kama wengine wanavyofikiri. Ilikuwa tu kama sanduku kubwa. Haikuwa na vitu kama vile usukani kama mashua ya kawaida. Yehova anamupatia Noa vipimo kamili vya safina, na maagizo mengine kuhusu ujenzi wa safina hiyo, na pia anamuambia atie lami inje na ndani. Na anamuambia Noa hivi kuhusu kusudi la safina hiyo: ‘Tazama, mimi ninaleta garika ya maji duniani. . . . Kila kitu kilicho duniani kitakata pumuzi.’ Hata hivyo, Yehova anafanya agano na Noa, anamuambia hivi: ‘Nawe uingie ndani ya safina, wewe na wana wako na muke wako na wake za wana wako pamoja nawe.’ Noa anapaswa pia kuingiza wanyama kulingana na aina yao. Ni kila kitu tu kinachoingia katika safina ndicho kitaokoka Garika inayokuja!​—Mwa. 6:17-20.

Noa na familia yake walifanya kazi pamoja ili kutimiza maagizo ya Mungu

11, 12. Noa alipambana na kazi gani kubwa, na namna gani aliona kazi hiyo?

11 Noa anapambana na kazi kubwa sana. Safina inapaswa kuwa kubwa kabisa: inapaswa kuwa na urefu wa metre 133 hivi, upana wa metre 22 hivi, na kimo kuenda juu metre 13 hivi. Safina ilikuwa kubwa kuliko uwanja wa kabumbu. Je, Noa anajaribu kukimbia mugao huo? Je, ananungunika kuhusu magumu atakayopata katika kazi hiyo, ao anabadilisha maagizo ili kufanya kazi iwe nyepesi zaidi? Biblia inasema hivi: ‘Noa akafanya kulingana na yote ambayo Mungu alikuwa amemuamuru. Alifanya vivyo hivyo.’​—Mwa. 6:22.

12 Kazi hiyo ilichukua miaka mingi, labda miaka 40 ao 50. Iliomba kukata miti mingi, kuikokota mupaka mahali pa ujenzi, kuipasua iwe mbao ao nguzo, kuichonga vizuri na kuiunganisha. Safina ilipaswa kuwa na orofa tatu, na vyumba vingi, na mulango kwenye ubavu wake. Inaonekana kwamba ilikuwa na madirisha kwenye sehemu za juu kuizunguka, ilikuwa pia na paa lenye kuinuka kidogo katikati ili maji yaweze kumwangika haraka.​—Mwa. 6:14-16.

13. Ni kazi gani ambayo Noa anapaswa kutimiza ambayo pengine ni ngumu zaidi kuliko hata kazi ya kujenga safina, na watu wanajiendesha namna gani?

13 Kadiri miaka inavyopita, safina inaendelea kujengwa na umbo lake linaonekana, Noa ni mwenye furaha sana kuona familia yake inamuunga mukono! Kuna kazi ingine ambayo Noa anapaswa kutimiza na ambayo pengine hata ni ngumu zaidi kuliko kazi ya kujenga safina. Biblia inasema kwamba Noa alikuwa ‘muhubiri wa uadilifu.’ (Soma 2 Petro 2:5.) Basi, kwa ujasiri anakuwa mbele katika kazi hiyo ili kujaribu kuwaonya watu kwamba mwisho wa ulimwengu huo muovu, na usiomuogopa Mungu, unakaribia. Je, watu wanakubali onyo hilo? Kisha miaka mingi kupita, Kristo alikumbusha namna watu walivyojiendesha wakati huo, alisema kwamba “hawakujali.” Alisema pia kwamba walihangaikia tu mambo yao ya maisha ya kila siku: kula, kunywa, kuoa na kuolewa; hawakumusikiliza Noa hata kidogo. (Mt. 24:37-39) Walimuchekelea Noa na familia yake; labda wengine walimuogopesha na kumutendea kwa jeuri. Labda hata walijaribu kuharibu kazi ya ujenzi ao kuizuia iendelee.

Ijapokuwa ushuhuda ulikuwa wazi kwamba Mungu anamubariki Noa, watu walimuchekelea na walipuuza ujumbe wake

14. Leo, Wakristo wanaweza kujifunza nini juu ya imani ya Noa na familia yake?

14 Hata hivyo, Noa na familia yake wanaendelea kutimiza kazi yao kwa uaminifu; hata ikiwa watu wanawaza kwamba mambo wanayotia pa nafasi ya kwanza si ya lazima, ni ya upuuzi ao ya upumbavu. Kwa hiyo, leo Wakristo wanaweza kujifunza mambo mengi kuhusu imani ya Noa na familia yake. Tusisahau kwamba Biblia inaita wakati wetu “siku za mwisho” za ulimwengu huu muovu. (2 Tim. 3:1) Yesu alisema kwamba wakati wetu utakuwa kabisa kama wakati Noa alikuwa anajenga safina. Ikiwa leo watu hawapendezwe na ujumbe wa Ufalme wa Mungu, wanacheka ao kuwatesa Wakristo, ni vizuri tumukumbuke Noa. Sisi si watu wa kwanza kupambana na mambo kama hayo.

“. . .Ingia Ndani ya Safina”

15. Wakati Noa anakaribia umri wa miaka 600, anafiwa na nani?

15 Miaka inapita, polepole safina inamalizika kujengwa. Noa anakaribia sasa umri wa miaka 600, amefiwa na watu aliowapenda. Lameki baba yake, amekwisha kufa. * Kisha miaka tano, Methusela, baba ya baba ya Noa, anakufa mwenye umri wa miaka 969; huyo ndiye mwanadamu aliyeishi miaka mingi zaidi kuliko wengine wote wanaozungumuziwa katika Biblia. (Mwa. 5:27) Methusela na Lameki waliishi wakati mumoja na Adamu, mutu wa kwanza.

16, 17. (a) Ni ujumbe gani mupya Noa anapata katika mwaka wa 600 wa maisha yake? (b) Fasiria jambo lisiloweza kusahaulika ambalo Noa na familia yake wanatazama.

16 Katika mwaka wa 600 wa maisha ya Noa, muzee huyo alipata ujumbe mupya kutoka kwa Yehova: “Ingia ndani ya safina, wewe pamoja na nyumba yako yote.” Mungu alimuambia pia Noa achukue wanyama kutokana na aina yao na awaingize katika safina: saba-saba kati ya walio safi, wanaofaa kwa matumizi ya zabihu, na wawili wawili kati ya wasio safi.​—Mwa. 7:1-3.

17 Kuwatazama wanyama hao wanavyomiminika ili kuja kuingia katika safina, ni jambo lisiloweza kusahaulika. Wanamiminika maelfu: wenye kutembea, wenye kuruka, wenye kutambaa, wenye kujikokota; wanyama wenye ukubwa mbalimbali na umbo mbalimbali wenye kushangaza, na pia wenye tabia mbalimbali. Wazia namna Noa anavyojaribu kuwakusanya-kusanya, kuwasukuma-sukuma, kuwabembeleza-bembeleza ili waingie mahali palipotayarishwa kwa ajili yao katika safina. Biblia inasema kuwa “wakaingia . . . kwa Noa ndani ya safina.”​—Mwa. 7:9.

18, 19. (a) Namna gani tunaweza kujibu maulizo ya watu fulani walio na mashaka kuhusu mambo yaliyofanyika siku za Noa? (b) Njia ambayo Yehova alitumia ili kuwalinda wanyama inaonyesha namna gani hekima yake?

18 Watu fulani walio na mashaka wanaweza kuuliza hivi: ‘Hilo linawezekana namna gani? Namna gani hao wanyama wangeweza kuishi kwa amani mahali pamoja?’ Lakini tuwazie jambo hili: Ni vigumu kabisa kwa Muumbaji wa ulimwengu muzima kuwa na mamlaka juu ya wanyama, hata kuwafanya wawe watiifu ikiwa ni lazima? Usisahau kwamba ni Yehova aliyeumba wanyama. Siku nyingi baadaye, alitenganisha maji ya Bahari Nyekundu, na alifanya jua lisimame, bila kutikisika. Je, Mutu huyo hakuwa na uwezo wa kufanya kabisa kila jambo linaloelezwa katika habari ya Noa? Ndiyo, ana uwezo huo na alifanya hivyo!

19 Ni kweli kwamba Mungu angeweza kuwalinda wanyama katika njia nyingine. Lakini, njia ambayo alichagua inatukumbusha namna tangu mwanzo alimukabizi mwanadamu kila kitu kilicho na uzima hapa duniani ili akitunze. (Mwa. 1:28) Pia wazazi wengi leo wanatumia hadisi ya Noa ili kuwafundisha watoto wao kwamba Yehova anaona wanyama na wanadamu alioumba kuwa wa maana sana.

20. Juma moja mbele ya Garika kuanza, namna gani Noa na familia yake walifanya kazi kwa bidii?

20 Yehova alimuambia Noa kwamba kunabaki juma moja ili Garika ianze. Juma hilo familia ya Noa ilifanya kazi nyingi sana. Wazia jambo hili: walikuwa na kazi ya kuingiza wanyama wote katika safina na kuwapanga kulingana na aina yao, kutayarisha chakula cha wanyama hao kulingana na aina yao, na kuingiza vitu vyote vya familia. Bila shaka, bibi ya Noa na bibi ya Shemu, Hamu na Yafethi, wanashugulika sana ili kufanya mahali pao pa kuishi katika safina pawe mahali pazuri.

21, 22. (a) Watu wa siku za Noa hawakujali, kwa nini hatuwezi kushangazwa na hali hiyo? (b) Ni wakati gani watu waliomuzihaki ao kumuchekelea Noa na familia yake walinyamazishwa kabisa?

21 Sasa watu wengine wanafanya nini? Wanajionea wenyewe ushuhuda mwingi unaoonyesha kwamba Yehova anamubariki Noa na kazi yake, lakini hata hivyo “hawajali.” Hawafanye jambo lolote isipokuwa tu kutazama namna wanyama wanavyoingia kwa uwingi katika safina. Je, tunaweza kushangaa ikiwa watu walikuwa wasiojali? Hapana! Leo pia watu hawajali ijapokuwa kuna ushuhuda mwingi unaoonyesha kwamba tunaishi siku za mwisho za ulimwengu huu muovu. Na mutume Petro alitabiri kwamba katika siku za mwisho, watu wenye kuzihaki watakuja na zihaka zao, watachekelea wale wanaotii onyo la Mungu. (Soma 2 Petro 3:3-6.) Ilikuwa hivyo pia katika siku za Noa, watu walimuzihaki yeye na familia yake.

22 Je, watu hao walimuzihaki ao kumuchekelea Noa milele? Biblia inasema kwamba wakati tu Noa alimaliza kuingiza familia yake na wanyama katika safina, ‘Yehova akafunga mulango nyuma yake.’ Ikiwa hao wenye kuzihaki walikuwa hapo, basi tendo hilo la Mungu liliwafanya wafunge kinywa. Na ikiwa waliendelea kumuchekelea Noa, mvua iliwanyamazisha kabisa, kwa sababu ilinyesha kweli! Iliendelea kunyesha, kunyesha, kunyesha mupaka ikafunika dunia yote, kama Yehova alivyosema.​—Mwa. 7:16-21.

23. (a) Namna gani tunajua kwamba Yehova hakufurahi wakati watu waliharibiwa kwenye Garika? (b) Sababu gani ni jambo la hekima kuiga imani ya Noa leo?

23 Je, unawaza Yehova alifurahi wakati watu hao waovu waliharibiwa? Hapana! (Eze. 33:11) Yehova aliwapatia wakati mwingi sana wa kubadilisha mwenendo wao na kufanya yaliyo mema. Je, ingewezekana wabadilike? Maisha ya Noa yanajibu ulizo hilo. Noa alitembea pamoja na Yehova, alimutii Mungu katika mambo yote, kwa hiyo maisha ya Noa yalionyesha kwamba watu wangeweza kuokoka. Katika maana hiyo, imani yake ilihukumu ulimwengu wa siku hizo; ilionyesha wazi kwamba inawezekana kuishi maisha yanayomupendeza Mungu. Imani yake ilimuokoa yeye na familia yake. Ukiiga imani ya Noa unaweza pia kujiokoa wewe mwenyewe na kuokoa wale unaowapenda. Kama Noa, unaweza kutembea pamoja na Yehova Mungu, na anaweza kuwa Rafiki yako. Na urafiki wenu unaweza kuwa wa milele!

^ fu. 7 Katika siku hizo, watu waliishi miaka mingi sana kuliko watu wa leo. Waliishi hivyo kwa sababu walikuwa hawajapungukiwa sana na nguvu na hali ya kukamilika ambayo Adamu na Eva walikuwa nayo mbele ya kufanya zambi.

^ fu. 15 Lameki alimupatia mutoto wake jina Noa, jina ambalo pengine linamaanisha, “Pumuziko,” ao “Faraja,” na alitabiri kwamba Noa atatimiza maana ya jina lake kwa kuongoza wanadamu kwenye faraja ao pumuziko, ni kusema, hawatateseka tena kutokana na udongo uliolaaniwa. (Mwa. 5:28, 29) Lameki hakuona utimizo wa unabii wake. Inaonekana kwamba mama ya Noa, ndugu zake na dada zake, walikufa katika Garika.