Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA TATU

“Baba ya Wale Wote Walio na Imani”

“Baba ya Wale Wote Walio na Imani”

ABRAMU anatazama upande wa juu, anaona lile jengo kubwa la hekalu linaloshinda nyumba zote za muji wa Uru kwa urefu. * Anasikia wanyama wenye kulia, na anaona moshi unaopanda juu. Makuhani wa mungu​-mwezi wanamutolea tena mungu wao zabihu. Wazia namna Abramu anavyogeukia upande mwengine, anatikisa kichwa, na anakunja uso ili kuonyesha kwamba anachukizwa na jambo hilo. Anaenda nyumbani na njiani anakutana na watu wengi sana, bila shaka anafikiri juu ya ibada ya sanamu inayoenea mahali pote katika muji wa Uru. Ibada hiyo chafu na yenye kuchukiza ilianza tangu siku za Noa na imeenea duniani pote!

1, 2. Kuanzia wakati wa Noa namna gani dunia ilikuwa yenye kubadilika, na Abramu anajisikia namna gani?

2 Noa alikufa miaka miwili tu mbele ya Abramu kuzaliwa. Noa na familia yake walipotoka katika safina kisha ile Garika kubwa, muzee huyo alimutolea Yehova Mungu zabihu, naye Yehova alifanya upinde wa mvua uonekane. (Mwa. 8:20; 9:12-14) Wakati huo, duniani pote kulikuwa tu ibada safi. Lakini sasa, watu wa kizazi cha kumi kuanzia Noa mupaka Abramu, wanapoendelea kutawanyika juu ya dunia, ni watu wachache tu ndio wanaofuata ibada safi. Kila mahali watu wanaabudu miungu ya kipagani, ni kusema, sanamu. Hata Tera, baba ya Abramu ni muabudu​-sanamu, na inawezekana hata alikuwa anatengeneza sanamu za kuabudu​—Yos. 24:2.

Ni nini iliyomusaidia Abramu kuwa na imani ya ajabu hivyo?

3. Sababu gani Abramu alikuwa tofauti kabisa na watu wengine, na hilo linaweza kutufundisha nini?

3 Abramu alikuwa tofauti kabisa na watu wengine wa wakati wake, naye alikuwa hivyo kwa sababu ya imani yake. Ndio sababu, baadaye kupitia roho ya Mungu, mutume Paulo alimuita “baba ya wale wote walio na imani”! (Soma Waroma 4:11.) Acha sasa tuone kile kilichomusaidia Abramu kuwa na imani yenye nguvu. Sisi pia kupitia yeye tunaweza kujifunza mambo mengi yanayoweza kutusaidia kuwa na imani yenye nguvu.

Kumutumikia Yehova Kisha Garika

4, 5. Inaonekana Abramu alijifunza juu ya Yehova kupitia nani, na sababu gani tunaweza kusema kwamba inawezekana ilikuwa hivyo?

4 Ni nini iliyomusaidia Abramu kujifunza juu ya Yehova Mungu? Tunajua kwamba Yehova alikuwa na watumishi wake waaminifu katika siku za Abramu. Shemu alikuwa mumoja wao. Shemu si mutoto wa kwanza kati ya watoto watatu wa Noa, hata ikiwa mara nyingi ni yeye anayetajwa wa kwanza. Shemu anatajwa pa nafasi ya kwanza kwa sababu alikuwa na imani ya ajabu. * Wakati fulani kisha Garika, Noa alipozungumuzia juu ya Yehova, alisema kwamba Yehova ni “Mungu wa Shemu.” (Mwa. 9:26) Bila shaka, Shemu alimuheshimu Yehova na ibada yake safi.

5 Je, Abramu alimujua Shemu? Inawezekana. Wazia Abramu ni kijana. Bila shaka, anafurahi sana kujua kwamba ana tate ao kambo ambaye bado anaishi, na ambaye ana umri wa miaka zaidi ya 400! Shemu aliona uovu uliotendeka mbele ya Garika, namna mvua ilivyoisafisha dunia, aliona namna watu wa mataifa ya kwanza​-kwanza walivyoongezeka juu ya dunia kisha Garika, na aliona pia namna uasi ulitokea katika siku za Nimrodi kwenye Munara wa Babeli. Shemu alikuwa mutu mwaminifu, na kwa hiyo, hakujiunga na waasi hao, na hata ikiwa Yehova aliivuruga luga ya watu waliokuwa wanajenga munara wa Babeli, Shemu na familia yake waliendelea kuzungumuza ile luga ya kwanza ya wanadamu, ile luga ya Noa. Abramu alikuwa pia wa familia ya Shemu. Kwa hiyo, Abramu alipokuwa anakomaa, bila shaka alimuheshimu sana Shemu. Jambo lingine ni hili: Shemu aliishi wakati wa kutosha wa kipindi kirefu cha maisha ya Abramu. Kwa hiyo, inaonekana kwamba Abramu alijifunza juu ya Yehova kupitia Shemu.

Abramu alichukia ibada ya sanamu iliyoenea mahali pote katika muji wa Urur

6. (a)Namna gani Abramu alionyesha kwamba anaelewa vizuri kwa nini Garika iliharibu dunia? (b)Abramu na Sarai walikuwa na maisha ya namna gani?

6 Iwe ilikuwa hivyo ao hapana, Abramu anaelewa vizuri kwa nini Garika iliharibu dunia. Anajikaza pia kutembea pamoja na Mungu kama vile Noa alivyofanya. Hiyo ndio sababu Abramu ni tofauti kabisa na watu wengine wa Uru, na hata labda tofauti na watu wa jamaa yake, na ndio sababu anachukia ibada ya sanamu. Lakini, Abramu alipata mwanamuke wa ajabu sana aliyemutegemeza. Alimuoa Sarai, mwanamuke wa kweli kabisa, si kwa sababu ya urembo wake tu lakini pia kwa sababu ya imani yake kubwa katika Yehova. * Abramu na Sarai hawakuwa na mutoto, hata hivyo walipata furaha nyingi katika kumutumikia Yehova pamoja. Pia, walimulea Loti, mutoto wa ndugu ya Abramu; Loti alikuwa yatima.

7. Namna gani wafuasi wa Yesu wanapaswa kumuiga Abramu?

7 Abramu hakumuacha Yehova hata siku moja kwa sababu ya ibada ya sanamu inayopatikana katika muji wa Uru. Yeye na Sarai waliazimia kuwa tofauti kabisa na watu hao waabudu​-sanamu. Ikiwa tunataka kuwa na imani ya kweli, inatuomba kuwa na roho hiyohiyo. Sisi pia tunapaswa kuazimia kuwa tofauti. Yesu alisema kwamba wafuasi wake hawapaswe kuwa “sehemu ya ulimwengu,” na kwa hiyo, ulimwengu ungewachukia. (Soma Yohana 15:19.) Ikiwa unateseka kwa sababu watu wa jamaa yako ao watu wa mahali unapoishi wanakukataa kwa kuwa umeamua kumutumikia Yehova, kumbuka kwamba wewe si mutu wa kwanza kuchukiwa. Unaiga mufano muzuri wa Abramu na Sarai waliomutumikia pia Mungu kwa uaminifu.

‘Toka Katika Inchi Yako’

8, 9. (a) Abramu anaona jambo gani ambalo hatasahau hata siku moja? (b) Yehova anamupatia Abramu ujumbe gani?

8 Siku fulani, Abramu anaona jambo fulani ambalo hatasahau hata siku moja. Anapata ujumbe kutoka kwa Yehova Mungu! Biblia haitutolee habari zote kuhusu namna Abramu alipata ujumbe huo, lakini inasema tu kwamba “Mungu wa utukufu” alimutokea mwanaume huyo mwaminifu. (Soma Matendo 7:2, 3.) Labda kupitia malaika fulani, Abramu anapata kuona kidogo tu utukufu wa ajabu wa Mufalme Mukubwa wa ulimwengu wote. Wazia namna Abramu ni mwenye furaha kuona tofauti kati ya Mungu aliye na uzima na sanamu zisizo na uzima ambazo watu wanaabudu.

9 Yehova anamupatia Abramu ujumbe gani? ‘Toka katika inchi yako na kutoka kwa watu wa jamaa yako na uje mupaka katika inchi ambayo nitakuonyesha.’ Yehova anamuambia Abramu kwamba atamuonyesha inchi, lakini hamuambie ni inchi gani hiyo. Jambo la kwanza ambalo Abramu anapaswa kufanya ni kuacha inchi yake na watu wa jamaa yake. Kwa watu wa huko Mashariki ya Kati, jamaa ni jambo la maana sana. Mutu kuacha watu wa jamaa yake na kuhamia mbali, mara nyingi ilionekana kuwa ni laana ao mukoshi sana, na wengine waliona jambo hilo kuwa mbaya kuliko hata kufa!

10. Sababu gani tunaweza kusema kwamba Abramu na Sarai walijinyima kabisa kwa kuacha makao yao huko Uru?

10 Abramu alijinyima kwa kuacha maisha mazuri ya muji wa Uru. Kuna ushuhuda unaoonyesha kwamba muji wa Uru ulikuwa wenye utajiri na shuguli nyingi. (Soma kisanduku  “Muji Ambao Abramu na Sarai Waliacha.”) Uvumbuzi wa vitu vya zamani vilivyochimbuliwa huko, unaonyesha kwamba katika muji wa Uru ya zamani kulikuwa nyumba nzuri za starehe sana; nyumba fulani zilikuwa na vyumba kumi na mbili ao zaidi kwa ajili ya familia na watumishi, na vilijengwa kuzunguka uwanja wa ndani uliokuwa na sakafu ya mawe. Katika muji mahali popote watu wangeweza kupatikana, kama vile sokoni, kwenye maduka, kulikuwa na bomba ao mahali pa kunywea maji, wc ao musalani na mahali pa kutupia uchafu. Kumbuka pia kwamba Abramu na Sarai si vijana tena; Abramu ana zaidi ya miaka 70, na Sarai zaidi ya 60. Bila shaka, wakati huo angependa Sarai aishi bila mahangaiko na atunzwe vizuri, mambo ambayo kwa kawaida kila mwanaume mwema anamutakia bibi yake. Wazia namna wanavyozungumuza kuhusu mugao wao, bila shaka, wanajiuliza maulizo mengi na labda wana wasiwasi fulani. Abramu ni mwenye furaha sana kuona Sarai anakubaliana naye! Anakubali kuacha nyumba nzuri yenye starehe huko Uru.

11, 12. (a) Ni matayarisho gani na maamuzi gani yanapaswa kwanza kufanywa mbele ya kuondoka Uru? (b) Fasiria namna kuondoka kwao kulikuwa.

11 Abramu na Sarai wanachukua uamuzi, kwa hiyo wana mambo mengi ya kufanya. Wanapaswa kutayarisha safari na kuamua vitu ambavyo watachukua. Safari yao itawapeleka katika inchi wasiyoijua, watachukua nini na wataacha nini? Watafanya nini na watu wa jamaa yao, watumishi wao na hasa zaidi Tera baba ya Abramu, aliye muzee? Wanaamua kuenda naye na kumutunza mupaka atakapokufa. Inaonekana kwamba Tera anakubali kwa kujipendea kuenda pamoja nao, kwa sababu Biblia inaonyesha kwamba, ni yeye anayechukua familia na kuondoka Uru. Bila shaka, aliachana na ibada ya sanamu. Loti, mutoto wa ndugu ya Abramu, alikubali pia kuenda pamoja na wengine.​—Mwa. 11:31.

12 Mwishowe siku ya kuanza safari inafika. Wazia namna watu wote wa familia hiyo na vitu vyao wanakusanyika inje ya kuta na mufereji mukubwa wa muji wa Uru. Ngamia na punda ni wenye kubeba mizigo, wanyama wengine ni wenye kukusanywa, watu wa familia na watumishi wako tayari na wanafurahia kuondoka. * Labda wote wanamuangalia Abramu, wanangojea neno lake la mwisho ili kuondoka. Mwishowe, saa inafika, na wanaondoka kwa utaratibu, wanaacha muji wa Uru milele.

13. Namna gani watumishi wengi wa Yehova leo wanaonyesha roho kama ile ya Abramu na Sarai?

13 Leo, watumishi wengi wa Yehova wanaamua kuenda mahali ambapo kuna lazima kubwa ya wahubiri wa Ufalme. Wengine wanaamua kujifunza luga mupya ili wapanue utumishi wao. Ao wanaamua kujaribu ufundi mwengine wa kuhubiri ambao hawakutumia ao kufurahia hapo zamani. Mara nyingi ili kufanya hivyo inaomba mutu ajinyime, ni kusema, akubali kuachana na vitu fulani vya kimwili. Watumishi wa Yehova wanapongezwa kabisa kwa sababu ya kuonyesha roho kama hiyo ya kumuiga Abramu na Sarai! Ikiwa tunaonyesha imani kama hiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ataendelea kutupatia mengi zaidi kupita yale tuliyomupatia. Hakose hata kidogo kuwapa zawadi watumishi wake wenye imani. (Ebr. 6:10; 11:6) Alifanya hivyo kwa Abramu, sivyo?

Kuvuka Muto Efrati

14, 15. Safari ya Abramu kutoka Uru mupaka Harani ilikuwa namna gani, na ni sababu gani labda Abramu anaamua kuishi kwa muda hapo Harani?

14 Polepole watu hao na wanyama wanashika njia na kuanza safari yao. Unaweza kuwazia namna Abramu na Sarai wanavyofanya: mara mumoja anapanda juu ya munyama na mwengine anatembea kwa miguu, wanabadilishana; wanazungumuza na huku kuna makelele ya kengele zinazoninginia kwenye nira za wanyama. Hatua kwa hatua, wasafiri hao wanaanza kuzoea kujenga kambi na kuibomoa, na kumusaidia muzee Tera azoee kukaa vizuri juu ya ngamia ao punda. Wanaenda upande wa kaskazini pembeni​-pembeni ya Muto Efrati. Wanaendelea kusafiri kwa muda wa siku nyingi.

15 Mwishowe, kisha kutembea kilometre 960 wanaona vibanda vya muji wa Harani, vyenye umbo la mizinga ya nyuki; muji huo ni tajiri na unapatikana mahali barabara kubwa mbili zinakutana, wafanya biashara wanaotoka upande wa Mashariki na wale wanaotoka upande wa Mangaribi wanakutana hapo. Abramu na watu wake wanasimama hapo na wanaishi hapo muda fulani. Labda inakuwa vigumu kuendelea na safari kwa sababu ya Tera.

16, 17. (a) Abramu alifurahishwa sana na agano gani? (b) Namna gani Yehova alimubariki Abramu alipoishi katika inchi ya Harani?

16 Kisha muda murefu kupita, Tera anakufa mwenye umri wa miaka 205. (Mwa. 11:32) Abramu anafarijiwa sana wakati Yehova anazungumuza tena naye. Yehova anarudilia maagizo aliyomupatia Abramu alipokuwa katika inchi ya Uru, na anamutolea maelezo mengine kuhusu ahadi zake. Anamuelezea Abramu kwamba atakuwa “taifa kubwa,” na kwamba familia zote za dunia zitabarikiwa kupitia yeye. (Soma Mwanzo 12:2, 3.) Agano hilo kati ya Mungu na Abramu linamufurahisha sana Abramu na linamutia moyo kuendelea mbele.

17 Kwa sababu Yehova alimubariki Abramu alipoishi katika inchi ya Harani, Abramu ni mwenye kuwa na vitu vingi vya kimwili kuliko wakati alipotoka katika muji wa Uru. Biblia inataja “mali zote ambazo walikuwa wamekusanya na nafsi ambazo walikuwa wamejipatia katika Harani.” (Mwa. 12:5) Ili kuwa taifa, Abramu anapaswa kuwa na vitu vingi vya kimwili na watumishi, ni kusema, watu wengi katika nyumba yake. Si kila mara Yehova anafanya watumishi wake wawe matajiri, hata hivyo, hakose kuwapatia chochote wanachohitaji ili kutimiza mapenzi yake. Jambo hilo linamutia Abramu nguvu, na kwa hiyo, anaendelea na safari yake kuelekea mahali asipojua.

Ilikuwa ni kujinyima kabisa kwa Abramu na Sarai kuacha maisha yao mazuri katika muji wa Uru

18. (a) Ni siku gani Abramu anafikia wakati wa maana sana unaoanzisha historia ya Yehova na watu wake? (b) Miaka mingi baadaye, ni matukio gani mengi ya maana yametokea kwenye Nisani 14? (Soma kisanduku “Tarehe ya Maana Sana Katika Hesabu za Biblia.”)

18 Anatoka Harani, anasafiri muda wa siku nyingi mupaka mahali pa kuvukia Karkemishi, ni hapo vikundi vikubwa vya wasafiri na ngamia ao punda zao walikuwa wakivuka muto Efrati. Inaonekana kwamba ni hapo Abramu anafikia wakati wa maana sana unaoanzisha historia ya Yehova na watu wake. Ilikuwa tarehe 14 ya mwezi ambao ulikuja kuitwa baadaye Nisani, katika mwaka wa 1943 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, siku hiyo Abramu na watu wake walivuka muto Efrati. (Kut. 12:40-43) Inchi ambayo Yehova alimuahidi Abramu ilikuwa upande wa kusini. Kuanzia siku hiyo, agano la Mungu pamoja na Abramu lilianza kufanya kazi.

19. Ahadi ya Yehova kwa Abramu ilitaja jambo gani, na inawezekana ahadi hiyo ilimukumbusha Abramu nini?

19 Abramu anapita katikati ya inchi kuelekea upande wa kusini, yeye na watu wake wanasimama karibu ya miti mikubwa ya More, karibu na Shekemi. Hapo Abramu anapata tena ujumbe kutoka kwa Yehova. Mara hii Mungu anamuahidi kwamba uzao wake utaimiliki inchi hiyo. Je, wakati huo Abramu alifikiria unabii ambao Yehova alitoa katika Edeni, ambao ulitabiri kwamba siku fulani “uzao” utaokoa wanadamu? (Mwa. 3:15; 12:7) Inawezekana. Sasa inawezekana Abramu anaanza kuelewa kwamba ana daraka fulani katika utimizo wa kusudi kubwa la Yehova.

20. Namna gani Abramu alionyesha shukrani kwa ajili ya pendeleo ambalo Yehova alimutolea?

20 Bila shaka, Abramu ni mwenye shukrani sana kwa ajili ya pendeleo ambalo Yehova anamutolea. Kwa hiyo, Abramu anapoendelea na safari yake kupitia katikati ya inchi, anasimama karibu ya miti mikubwa ya More na anamujengea Yehova mazabahu hapo; mazabahu ya namna hiyo yalikuwa ya kwanza hapo More, karibu ya Beteli. Anafanya hivyo kwa uangalifu kwa kuwa inchi hiyo bado inaikaliwa na Wakanaani. Analiitia jina la Yehova, bila shaka, ili kuonyesha shukrani yake ya kutoka moyoni, na wakati huohuo, anafikiria namna uzao wake utakavyokuwa wakati ujao. Inawezekana aliwahubiri pia Wakanaani, waliokuwa majirani wake. (Soma Mwanzo 12:7, 8.) Abramu anakutana na mambo mengi katika maisha yake yanayojaribu imani yake. Abramu ni mutu mwenye hekima, haangalie nyumba na mambo mengine mazuri ya kimwili aliyoacha katika muji wa Uru. Anaangalia tu mbele kwenye ahadi ya Yehova. Kuhusu Abramu, andiko la Waebrania 11:10 linasema hivi: ‘Alikuwa akingojea muji ulio na misingi ya kweli, ambao mujenzi na mutengenezaji wa muji huo ni Mungu.’

21. Ni mambo gani mengi ambayo tunajua juu ya Ufalme wa Mungu ambayo Abrahamu hakujua, na tunachochewa kufanya nini?

21 Sisi tunaomutumikia Yehova leo, tunajua mambo mengi kupita Abramu kuhusu muji huo wa mufano, ni kusema, Ufalme wa Mungu. Tunajua kwamba Ufalme huo unatawala mbinguni na kwamba karibuni utaharibu ulimwengu huu muovu. Tunajua kwamba Yesu Kristo, ambaye ni Uzao ulioahidiwa tangu zamani, anatawala katika Ufalme huo. Tutakuwa na pendeleo kubwa la kumuona Abramu wakati atafufuliwa na wakati huo Abramu ataelewa vizuri kabisa namna kusudi la Yehova lilivyotimia! Wewe pia ungependa kuona namna Yehova atatimiza kila ahadi aliyotupatia, sivyo? Kwa hiyo, ni lazima uendelee kufanya kama Abramu. Achana na mambo fulani ili kumutumikia Yehova, tii mambo Yehova anakuambia, onyesha shukrani kwa ajili ya kila pendeleo ambalo Yehova anakutolea. Ukiiga imani ya Abramu, “baba ya wale wote walio na imani” atakuwa pia baba yako!

^ fu. 3 Miaka mingi baadaye, Mungu alibadilisha jina la Abramu kuwa Abrahamu, maana yake, “Baba ya Watu Wengi.”​—Mwa. 17:5.

^ fu. 4 Ni kama vile Abramu, mara nyingi anatajwa wa kwanza katika watoto wa Tera, ijapokuwa yeye hakuwa mutoto wa kwanza.

^ fu. 6 Kisha, Mungu alibadilisha jina la Sarai kuwa Sara, maana yake, “Binti ya Mufalme.”—Mwa. 17:15.

^ fu. 12 Watu fulani wenye elimu ya mambo ya Biblia wanawaza kwamba labda ngamia hawakufugwa katika siku za Abramu. Lakini, hawana ushuhuda wowote wa kuhakikisha jambo hilo. Mara nyingi Biblia inataja ngamia katika mali ya Abramu.—Mwa. 12:16; 24:35.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Abramu alichukia ibada ya sanamu iliyoenea mahali pote katika muji wa Uru