Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

 UIGE IMANI YAO | MARIA

Alivumilia Maumivu ya Moyoni Yaliyokuwa Kama ya Upanga

Alivumilia Maumivu ya Moyoni Yaliyokuwa Kama ya Upanga

MARIA alipiga magoti, alikuwa na uchungu mwingi sana ambao ni vigumu kueleza. Lakini alisikia kilio cha mwisho cha mwana wake alipokuwa akikufa kisha kuteswa kwa muda wa saa nyingi. Giza lilikuwa limeingia, hata ikiwa ilikuwa katikati ya muchana. Sasa dunia ikatetemeka sana. (Mathayo 27:45, 51) Labda Maria aliona kwamba Yehova mwenyewe alifanya hivyo ili kuacha dunia ijue kuwa aliumizwa sana moyoni na kifo cha Yesu Kristo, kupita mutu mwengine yeyote.

Wakati mwangaza wa kipindi cha kisha midi uliondoa giza lililozunguka Golgotha, ao Mahali pa Fuvu la Kichwa, Maria alihuzunika kwa ajili ya mwana wake. (Yohana 19:17, 25) Inawezekana alikumbuka mambo mengi. Labda jambo alilokumbuka sana lilitokea miaka 33 hivi iliyopita. Wakati yeye na Yosefu walitoka tu kuonyesha mutoto wao mupendwa sana kwenye hekalu la Yerusalemu, mwanaume aliyezeeka anayeitwa Simeoni aliongozwa na roho ya Mungu kutoa unabii. Alitabiri mambo makubwa juu ya Yesu, lakini aliongeza pia kwamba siku moja, Maria angejisikia kama vile anachomwa na upanga murefu. (Luka 2:25-35) Sasa, kipindi kigumu kilipofika, ndipo Maria alielewa kabisa maana ya maneno hayo.

Maumivu yalimuchoma Maria moyoni

Imesemekana kuwa kifo cha mutoto wa mutu ndicho kibaya sana, chenye maumivu mengi, kupita kifo cha mutu mwengine yeyote mwenye mutu anaweza kupoteza. Kifo ni adui mubaya sana, na kinatuumiza sisi wote katika njia moja ao nyingine. (Waroma 5:12; 1 Wakorintho 15:26) Inawezekana kuvumilia maumivu hayo? Tunapochunguza maisha ya Maria kuanzia mwanzo wa utumishi wa Yesu mupaka wakati wa kifo chake na kisha hapo, tutajifunza mambo mengi juu ya imani iliyomusaidia Maria kuvumilia maumivu ya moyoni yaliyokuwa kama ya upanga.

‘MUFANYE LOLOTE ATAKALOWAAMBIA’

Acheni tuzungumuzie mambo yaliyotendeka miaka tatu na nusu mbele ya kifo cha Yesu: Maria alitambua kuwa kuna badiliko lenye lingekuja. Hata katika muji mudogo wa Nazareti, watu walikuwa wanazungumuza juu ya Yohana Mubatizaji na juu ya ujumbe wake wa toba uliokuwa wenye kuchochea moyo. Maria angeweza kuona kwamba mwana wake wa kwanza aliona habari juu ya Yohana kuwa alama; wakati ulikuwa umefika ili kuanza utumishi wake. (Mathayo 3:1, 13) Maria na watu wa nyumba yake waliona kuwa kukosekana kwa Yesu nyumbani kungeleta matokeo mabaya sana katika familia. Sababu gani?

Inawezekana Yosefu, bwana ya Maria, alikuwa tayari amekufa. Ikiwa ni hivyo, wakati Yesu alikufa, haikuwa mara ya kwanza Maria anafiwa. * Yesu aliitwa sasa “Mwana wa yule seremala” na pia “yule seremala.” Inawezekana Yesu ndiye alianza kufanya kazi ya baba yake na alichukua daraka la kutimiza mahitaji ya familia, iliyokuwa na watoto sita hivi waliozaliwa kisha yeye. (Mathayo 13:55, 56; Marko 6:3) Hata ikiwa Yesu alikuwa amemuzoeza Yakobo ili kuendelesha kazi hiyo, kwa sababu labda yeye ndiye alizaliwa kisha Yesu, kuondoka kwa Yesu nyumbani akiwa mutoto wa kwanza haingekuwa jambo jepesi kwa familia. Tayari Maria alikuwa na muzigo muzito; je, aliogopa badiliko hilo? Hatujue kabisa. Lakini kuna ulizo la maana sana: Angefanya nini wakati Yesu wa Nazareti angekuwa Yesu Kristo, Masiya aliyeahidiwa kwa muda murefu? Habari moja ya Biblia inafunua kitu fulani juu ya jambo hilo.—Yohana 2:1-12.

 Yesu alimuendea Yohana ili amubatize, na kisha akakuwa Mutiwa-Mafuta, ao Masiya. (Luka 3:21, 22) Kisha akaanza kuwachagua wanafunzi wake. Hata ikiwa kazi yake ilikuwa ya kufanya kwa haraka, alikuwa anapanga wakati ili kuenda kwenye matukio yenye kufurahisha pamoja na familia yake na marafiki wake. Akiwa pamoja na mama yake, wanafunzi wake, na ndugu zake wa kimwili, Yesu alienda kwenye karamu ya ndoa katika muji wa Kana, labda muji huo ulikuwa juu ya mulima kwenye kilometa 13 kutoka Nazareti. Wakati wa karamu, Maria alitambua tatizo moja. Inawezekana alitambua kwamba watu fulani wa familia ya watu waliooana waliangaliana-angaliana kwa woga na kusemezana kwa sauti ya chini inayoonyesha kuwa walikuwa na ulazima wa kitu fulani. Divai iliwaishia! Katika desturi yao, kumalizika kwa divai mbele ya karamu kuisha kungekatisha ukarimu wao, hilo lingeletea familia haya na kuharibu kabisa tukio hilo. Maria alijitia pa nafasi yao, na akazungumuza na Yesu.

Maria alimuambia mwana wake hivi: “Hawana divai.” Alipenda Yesu afanye nini? Hatujue kabisa, lakini alijua kwamba mwana wake alikuwa mutu mukubwa mwenye angefanya mambo makubwa. Labda alitumaini kwamba angeanza saa hiyo. Kwa kweli, ni kama vile alikuwa anamuambia, “Mwana wangu, tafazali fanya jambo fulani juu ya tatizo hili!” Anapaswa kuwa alishangazwa na jibu la Yesu kwa sababu Yesu alimuambia hivi: ‘Nina nini nawe, mwanamuke?’ Maneno ya Yesu hayaonyeshe kuwa alikosa heshima kwa mama yake, hata ikiwa watu fulani wameyaelewa kwa njia hiyo. Katika luga ya Kigiriki, maneno yaliyotafsiriwa hivyo yanamaanisha kwamba Yesu alikataa. Kwa kusema hivyo, alikuwa tu anamurekebisha mama yake. Yesu alimukumbusha mama yake kwamba hakuwa kabisa na jambo lolote la kusema juu ya namna alipaswa kufanya utumishi wake; hilo lilikuwa daraka la Baba yake, Yehova.

Maria alikubali rekebisho hilo la mwana wake, kwa sababu alikuwa mwanamuke mwenye kuelewa kwa vyepesi na munyenyekevu. Aliwaendea wale waliokuwa wanafanya kazi ya kugawa divai na akawaambia hivi: ‘Mufanye lolote atakalowaambia.’ Maria aliona kwamba hakuwa tena na daraka la kumuongoza mwana wake; lakini yeye na watu wengine wangepaswa kuongozwa naye. Kama mama yake, Yesu naye aliwasikilia huruma watu hao wawili waliooana siku hiyo. Kwa hiyo, alifanya muujiza wake wa kwanza, kwa kugeuza maji kuwa divai. Muujiza huo ulikuwa na matokeo gani? ‘Wanafunzi wake wakamuamini.’ Maria pia akamuamini Yesu. Hakumuona tena kama mwana wake tu lakini pia kama Bwana na Mwokozi.

Leo, wazazi wanaweza kujifunza mambo mengi kutokana na imani ya Maria. Kwa kweli, hakuna muzazi mwengine hata mumoja mwenye amelea mutoto aliye kama Yesu. Lakini wakati mutoto yeyote anakomaa, hata awe nani, badiliko hilo linaweza kuleta magumu. Muzazi anaweza kuwa na tabia ya kuendelea kumutendea kijana wake mwanaume ao mwanamuke kama mutoto mudogo, hata ikiwa namna hiyo ya kumutendea haiko tena yenye kufaa. (1 Wakorintho 13:11) Namna gani muzazi anaweza kuwasaidia watoto wake wenye kukomaa? Njia moja ni kuonyesha uhakika kabisa kwamba kijana wake mwanaume ao mwanamuke ataendelea kutumia mafundisho ya Biblia na kupata baraka za Yehova. Kwa unyenyekevu muzazi akionyesha imani na uhakika, hilo linaweza kuwasaidia sana watoto wenye kukomaa. Bila shaka Yesu alifurahia utegemezo wa Maria katika miaka yenye matukio mengi yaliyofuata.

’NDUGU ZAKE WALIKUWA HAWAMUAMINI’

Vitabu vya Injili havituambie mengi juu ya Maria katika miaka mitatu na nusu ya utumishi wa Yesu. Hata hivyo, kumbuka kwamba wakati huo inawezekana alikuwa mujane, labda alikuwa yeye mwenyewe nyumbani pamoja na watoto wake wadogo. Inaeleweka ikiwa hakuweza kumufuata Yesu alipokuwa akihubiri katika muji wake wa kuzaliwa. (1 Timotheo 5:8) Hata hivyo, Maria aliendelea kutafakari ao kufikiri sana juu ya mambo ya kiroho aliyokuwa  amejifunza kumuhusu Masiya na kuhuzuria mikutano katika sinagogi la kwao kama ilivyokuwa zoezi la familia yake.—Luka 2:19, 51; 4:16.

Kwa hiyo, inawezekana alikuwa kati ya wasikilizaji wakati Yesu alifundisha katika sinagogi la Nazareti. Lilikuwa jambo la furaha kwake kumusikia mwana wake alipotangaza kwamba unabii uliotabiriwa juu ya Masiya mamia ya miaka iliyopita ulitimizwa sasa juu yake! Hata hivyo, lilikuwa jambo la kuhuzunisha sana kuona watu wenzake wa Nazareti wanamukataa mwana wake. Walijaribu hata kumuua!—Luka 4:17-30.

Tena, lilikuwa jambo la kuhuzunisha kuona namna wana wake wengine walimuona Yesu na mafundisho yake. Andiko la Yohana 7:5 linatuonyesha kwamba ndugu ine wa Yesu hawakuwa na imani ya mama yao. Andiko hilo linasema hivi: ‘ndugu zake walikuwa hawamuamini.’ Kuhusu dada za Yesu, waliokuwa wawili hivi, Biblia haiseme jambo lolote. * Katika hali hizo zote, Maria alisikia maumivu ya pekee yanayotokana na kuishi katika nyumba kwenye watu wana maoni ya kidini yenye kutofautiana. Alipaswa kujikaza sana ili kuwa na usawaziko wa kubakia mwaminifu katika kweli wakati huohuo akijikaza kuvutia mioyo ya watu wa familia yake bila kuwakaza wala kubishana-bishana nao.

Wakati fulani, kikundi cha watu wa jamaa kiliamua kuenda ‘kumushika’ Yesu. Katika kikundi hicho, bila shaka kulikuwa pia ndugu za Yesu. Ni kama vile walikuwa wanasema: “Amerukwa na akili.” (Marko 3:21, 31) Kwa kweli, Maria hakuwa anafikiri hivyo, lakini alienda na watoto wake, pengine akiwaza kwamba watajifunza jambo fulani lenye lingewasaidia wamuamini Yesu. Je, walimuamini? Hata ikiwa Yesu aliendelea kufanya mambo ya kushangaza na kufundisha mambo mazuri, watoto wengine wa Maria hawakumuamini tu. Je, Maria alijiuliza, akiwa mwenye kuuzika, ikiwa iliomba nini ili kuwagusa mioyo?

Unaishi katika nyumba kwenye watu wana imani tofauti za kidini? Imani ya Maria inaweza kukufundisha mambo mengi. Hakuchoka na watu wa jamaa yake wenye hawakuwa wanaamini. Lakini, aliamua kuwaacha wajionee kwamba imani yake ilimuletea furaha na amani ya akili. Kwa upande mwengine, aliendelea kumuunga mukono mwana wake muaminifu. Kutokuwa na Yesu nyumbani kulimusumbua? Je, wakati fulani alikuwa anafikiri kwamba ingekuwa vizuri Yesu abakie nyumbani pamoja naye na familia yake? Ikiwa ndiyo, alikuwa anajizuia ili asifikirie sana mambo hayo. Aliona kuwa ni pendeleo kumuunga Yesu mukono na kumutia moyo. Wewe pia unaweza kuwasaidia watoto wako watie mambo ya Mungu pa nafasi ya kwanza katika maisha yao?

‘UPANGA MUREFU UTAICHOMA NAFSI YAKO’

Maria alibarikiwa kwa sababu ya imani yake katika Yesu? Yehova hakose hata kidogo kuwabariki watu wenye imani, na bila shaka hakukosa kumubariki Maria pia. (Waebrania 11:6) Jaribu kuwazia ilikuwa namna gani kwake kumusikia mwana wake akifundisha ao kusikia habari kuhusu mahubiri yake kutoka kwa watu wengine waliosikia mahubiri hayo.

Mifano mingi ya Yesu inaonyesha kwamba hakusahau mafundisho aliyopata kutoka kwa Yosefu na Maria

Katika mifano ya mwana wake, je, Maria alitambua maneno fulani yenye Yesu alijionea ao kusikia katika utoto wake alipokuwa anakomaa katika muji wa Nazareti? Wakati Yesu alisema juu ya mwanamuke aliyefagia nyumba yake ili kupata feza ya kichele iliyopotea, kusaga unga ili kutengeneza mukate, ao kuwasha taa na kuiweka juu ya kinara, je, Maria alifikiri juu ya kijana huyo mudogo aliyekuwa pembeni yake wakati alikuwa anafanya kazi hizo za kila siku? (Luka 11:33; 15:8, 9; 17:35) Wakati Yesu alisema kwamba nira yake ilikuwa laini na muzigo wake ulikuwa mwepesi, je, maria alikumbuka vipindi vizuri vya kisha midi vilivyopita wakati alikuwa anamuona Yosefu anafundisha kijana Yesu namna ya kutengeneza nira kwa uangalifu ili munyama aibebe bila shida? (Mathayo 11:30) Ni kweli kwamba Maria alitosheka kabisa alipokuwa anafikiria pendeleo lenye Yehova alimupatia katika maisha, ni kusema, pendeleo la kusaidia  kumulea na kumuzoeza mwana mwenye angekuja kuwa Masiya. Anapaswa kuwa alipata furaha ya pekee ya kumusikiliza Yesu, mwalimu mukubwa zaidi kupita wote, mwenye alitumia mifano ya vitu na hali kama hizo za kawaida ili kufundisha mambo ya maana sana!

Hata hivyo, Maria aliendelea kuwa munyenyekevu. Mwana wake hakumufanya kuwa mutu wa kusifiwa, ao wa kuabudiwa. Siku moja wakati wa utumishi wa Yesu, mwanamuke mumoja katika kikundi alisema kwa sauti kubwa kwamba mama yake alipaswa kuwa mwenye furaha kabisa kwa sababu ya kumuzaa. Yesu alijibu hivi: “Hapana, badala yake, wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!” (Luka 11:27, 28) Na wakati watu fulani katika kikundi walimuonyesha Yesu kwamba mama yake na ndugu zake walikuwa karibu, alisema kwamba watu walioamini ndio kabisa walikuwa mama na ndugu zake. Kuliko kukasirika, bila shaka Maria alielewa maana ya maneno hayo ya Yesu. Alielewa kuwa uhusiano wa kiroho ndio wa maana zaidi kupita uhusiano wa kimwili.—Marko 3:32-35.

Lakini, ni vigumu kueleza maumivu yenye Maria alisikia alipomuona mwana wake anakufa kifo chenye maumivu makali kwenye muti wa mateso. Mutume Yohana, aliyejionea kuuawa kwa Yesu, alieleza baadaye jambo hilo katika habari aliyoandika kwa kusema hivi: Wakati wa mateso hayo, Maria alikuwa anasimama ‘kando [ao pembeni] ya muti wa mateso.’ Hakuna jambo lolote lenye lingeweza kumuzuia mama huyo muaminifu na mwenye upendo kusimama pembeni ya mwana wake kwa mara ya mwisho. Yesu alimuona, na hata ikiwa alikuwa anasikia maumivu makali wakati wa kupumua na kusema, alijikaza tu kusema. Alimupatia mutume Yohana aliyependa sana daraka la kutunza mama yake. Kwa sababu ndugu za Yesu wa kimwili walikuwa hawajamuamini, hakupatia hata mumoja kati yao daraka hilo lakini akalipatia mumoja wa wafuasi wake wa kweli. Kwa kufanya hiyo, Yesu alionyesha kwamba ni jambo la maana sana mutu mwenye kuamini atunze watu wa familia yake, zaidi sana kwa kuwatimizia mahitaji yao ya kiroho.—Yohana 19:25-27.

Mwishowe, kifo cha Yesu kilipofika, Maria alipatwa na maumivu makali yaliyo kama ya upanga murefu wenye kuchoma nafsi yaliyotabiriwa zamani. Ikiwa tunaona kuwa ni vigumu kuwazia kiasi cha maumivu yake ya moyoni, ni vigumu hata zaidi kuwazia furaha aliyosikia siku tatu kisha hapo! Maria alijifunza kutokana na muujiza mukubwa zaidi kupita miujiza yote, Yesu alikuwa amefufuliwa! Na furaha yake iliongezeka, kwa sababu Yesu alimutokea Yakobo, ndugu yake nusu, alipokuwa peke yake bila shaka. (1 Wakorintho 15:7) Kukutana na Yesu kulimugusa moyo Yakobo na pia ndugu-nusu wengine wa Yesu. Mwishowe tunajifunza kwamba walifikia kuamini kuwa Yesu ndiye Kristo. Bila kukawia, walikuwa kwenye mikutano ya Kikristo pamoja na mama yao, “wakidumu katika sala.” (Matendo 1:14) Kisha, wawili kati yao, ni kusema, Yakobo na Yuda, waliandikavitabu vya Biblia..

Maria alifurahi sana kuona watoto wake wengine wanakuwa Wakristo waaminifu

Maria anatajwa kwa mara ya mwisho akiwa kwenye mikutano pamoja na wana wake, wakisali. Habari juu ya Maria inaisha vizuri sana, na anatuachia mufano muzuri! Kwa sababu ya imani yake, alivumilia maumivu ya moyoni yaliyokuwa kama ya upanga na mwishowe, alipata baraka kubwa. Ikiwa tunaiga imani yake, sisi pia tutavumilia kila aina ya maumivu yanayotupata katika dunia hii na tutapata baraka kubwa kupita zile tunazoweza kuwazia.

^ fu. 8 Yosefu anazungumuziwa katika tukio lililofanyika wakati Yesu alikuwa na miaka 12, kisha hapo, hazungumuziwe tena katika Injili. Kisha tukio hilo, mama ya Yesu na watoto wake wengine wanazungumuziwa lakini Yosefu hazungumuziwe. Pindi moja Yesu anaitwa “mwana wa Maria” bila kutaja Yosefu.—Marko 6:3.

^ fu. 16 Yosefu hakuwa baba muzazi wa Yesu, kwa hiyo ndugu na dada hao walikuwa ndugu-nusu na dada-nusu wa Yesu.—Mathayo 1:20.