Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA MUNANE

Alikutana na Hali Zenye Kuvunja Moyo, Lakini Alivumilia

Alikutana na Hali Zenye Kuvunja Moyo, Lakini Alivumilia

1. Sababu gani wakaaji wa Shilo wanalia na kuomboleza?

SAMWELI pamoja na wakaaji wa Shilo wanahuzunika sana. Ni kama vile muji wote unatoa machozi. Katika nyumba nyingi ni sauti ya maombolezo; wanawake na watoto wamepata habari kwamba bwana zao, watoto wao, baba zao, na ndugu zao hawatarudi tena nyumbani. Katika vita, Wafilisti wameshinda Waisraeli na kuua maaskari 30 000 hivi; muda mufupi tu mbele ya hapo walikuwa wameua maaskari wengine 4 000 katika pigano lingine.—1 Sam. 4:1, 2, 10.

2, 3. Ni misiba gani inayofanya muji wa Shilo upoteze heshima na utukufu wake?

2 Huo ni mwanzo tu wa misiba. Hofni na Finehasi, wana wawili waovu wa Kuhani Mukubwa Eli, wametoka inje ya muji wa Shilo wakiwa wenye kubeba Sanduku Takatifu la Agano. Kwa kawaida, sanduku hilo la maana sana, linawekwa katika patakatifu pa hema ya kukutania; sanduku hilo lilikuwa alama ya kuwapo kwa Mungu. Sasa watu wa Israeli wanachukua Sanduku la Agano na kulibeba kwenye vita, wanafikiri kwa upumbavu kuwa litatenda kama hirizi na kuwapatia ushindi. Lakini, Wafilisti wanakamata Sanduku hilo, na kuwaua Hofni na Finehasi.—1 Sam. 4:3-11.

3 Kwa miaka mingi, hema ya ibada katika muji wa Shilo iliheshimiwa kwa sababu Sanduku la Agano lilikuwa humo. Sasa limechukuliwa. Wakati Eli, ambaye ana miaka 98 anasikia habari hizo, anaanguka nyuma kutoka kwenye kiti chake na anakufa. Siku hiyo, bibi ya Finehasi, mutoto wa Eli, anakuwa mujane, na anakufa katika kuzaa. Mbele ya kufa, mwanamuke huyo anasema hivi: “Utukufu umeondoka katika Israeli kuenda uhamishoni.” Kwa kweli, Shilo haitakuwa tena kama ilivyokuwa hapo mbele.—1 Sam. 4:12-22.

4. Tutajifunza nini katika sura hii?

4 Samweli atashugulikia namna gani hali hizo zenye kuvunja moyo? Je, imani yake itakuwa nguvu ili aweze kabisa kusaidia taifa ambalo halina tena ulinzi wa Yehova na ambalo Yehova amekataa? Nyakati fulani, sisi wote tunaweza kukutana na hali zenye kuvunja moyo zinazojaribu imani yetu; kwa hiyo, acheni tuone mambo mengine ambayo mufano wa Samweli unaweza kutufundisha.

Anatimiza “Uadilifu”

5, 6. Namna gani Biblia inazungumuzia kile kipindi cha miaka 20, na ni nini inayoonyesha kwamba Samweli ana mambo mengi ya kufanya katika kipindi hicho?

5 Kisha tukio hilo, Biblia inaacha kwanza kuzungumuzia Samweli, na inazungumuzia sasa Sanduku Takatifu; inatuonyesha namna Wafilisti wanavyoteseka kwa sababu ya kukamata Sanduku hilo, na hivyo wanalazimika kulirudisha. Miaka 20 inapita, ndipo Biblia inazungumuzia tena Samweli. (1 Sam. 7:2) Samweli alikuwa anafanya nini miaka hiyo yote? Biblia inajibu ulizo hilo.

6 Biblia inasema kama mbele ya miaka hiyo 20 kuanza, “neno la Samweli likaendelea kuwajia Israeli wote.” (1 Sam. 4:1) Kisha kipindi hicho kumalizika, Samweli anakuwa na zoea la kufanya muzunguko kila mwaka ili kutembelea miji mitatu ya Israeli, kuwasaidia kumaliza mabishano yao na matatizo mengine. Na kisha anarudia kwake, huko Rama. (1 Sam. 7:15-17) Ni wazi kwamba Samweli ana mambo mengi ya kufanya, na hata katika kipindi hicho cha miaka 20.

Katika kipindi cha miaka 20 cha maisha ya Samweli ambacho Biblia haizungumuzie, Samweli alikuwa na mambo mengi ya kufanya katika utumishi wa Yehova

7, 8. (a) Kisha kufanya kazi ngumu kwa miaka 20, Samweli anawatolea Waisraeli ujumbe gani? (b) Waisraeli wanafanya nini wanaposikia ujumbe huo?

7 Mwenendo wa uasherati wa wana wa Eli na mambo mengine maovu waliyokuwa wanatenda vimeharibu imani ya Waisraeli. Inaonekana sasa kwamba watu wengi wanaanza kuabudu sanamu. Hata hivyo, kisha kufanya kazi ngumu kwa miaka 20, Samweli anawatolea Waisraeli ujumbe huu: ‘Ikiwa munarudi kwa Yehova kwa mioyo yenu yote, muondoe miungu ya kigeni iliyo katikati yenu na pia zile sanamu za Ashtorethi, nanyi muelekeze mioyo yenu kwa Yehova bila kuyumba-yumba, mukamutumikie yeye peke yake, naye atawakomboa kutoka mukono wa Wafilisti.’—1 Sam. 7:3.

8 ‘Mukono wa Wafilisti’ unawatesa Waisraeli. Kisha kushinda jeshi la Israeli, Wafilisti wanawaza kwamba wanaweza kuwatesa watu wa Mungu bila kulipizwa. Lakini Samweli anawahakikishia Waisraeli kama ikiwa tu wanamurudilia Yehova, mambo yatabadilika. Je, watapenda kufanya hivyo? Samweli anafurahi kuona Waisraeli wanaondoa sanamu zao na ‘kuanza kumutumikia Yehova peke yake.’ Anawakusanya wana wa Israeli huko Mispa, muji ulio katika eneo lenye milima, kaskazini mwa Yerusalemu. Hivyo, watu wanakusanyika, wanafunga kula chakula, na kutubu matendo yao mengi ya kuabudu sanamu.—Soma 1 Samweli 7:4-6.

Wafilisti walikusudia kushambulia watu wa Yehova wenye kutubu walipokuwa wenye kukusanyika

9. Wakati watu ni wenye kukusanyika, Wafilisti wanakusudia kufanya nini, na watu wa Mungu wanafanya nini wanapoona hatari hiyo?

9 Lakini, Wafilisti wanapata habari ya kusanyiko hilo kubwa na wanakusudia sasa kufanya jambo fulani. Wanatuma maaskari wao huko Mispa ili wawaangamize waabudu hao wa Yehova. Wakati Waisraeli wanapata habari kuhusu hatari hiyo inayokaribia, wanaogopa sana na wanamuomba Samweli asali kwa ajili yao. Anafanya hivyo na anatoa zabihu. Wakati wa ibada hiyo takatifu, Wafilisti wanashambulia muji wa Mispa. Ndipo, Yehova anajibu sala ya Samweli na kuonyesha kasirani yake. ‘Anafanya kuwe na mungurumo wa sauti kubwa siku hiyo juu ya Wafilisti.’—1 Sam. 7:7-10.

10, 11. (a) Sababu gani tunaweza kusema kwamba mungurumo ambao Wafilisti wanasikia ni mungurumo ambao hawajapata kusikia? (b) Vita ambayo inaanzia Mispa ina matokeo gani?

10 Je, unawaza kama Wafilisti hao ni kama watoto wadogo ambao wanaposikia mungurumo wa radi wanaogopa na kuenda kujificha nyuma ya mama zao? Hapana, wao ni maaskari hodari wenye kuzoea vita. Kwa hiyo basi, mungurumo wanaosikia ni mungurumo ambao hawajapata kusikia. Sababu gani mungurumo huo ni tofauti kabisa? Je, ni kwa sababu una “sauti kubwa” inayotokea katika anga lisilo na mawingu, ao ni kwa sababu ni kama unatokea pia katika milima? Iwe sababu ni gani, mungurumo huo unawatia Wafilisti katika muvurugo na wanaogopa sana. Ni wao sasa wanashambuliwa kuliko kushambulia. Wanaume Waisraeli kutoka Mispa wanawamwangikia Wafilisti, wanawashinda, na kuwakimbiza kilometre nyingi, kushuka kuelekea kusini-mangaribi mwa Yerusalemu.—1 Sam. 7:11.

11 Vita hii inabadilisha kabisa mambo. Katika muda wote ambao Samweli ni mwamuzi, Wafilisti wanaendelea kushindwa. Muji mumoja baada ya mwengine, watu wa Mungu wanakamata tena miji yao.—1 Sam. 7:13, 14.

12. Ni katika njia gani Samweli alitimiza “uadilifu,” na ni sifa gani zinazomusaidia aendelee kupata matokeo mazuri?

12 Miaka mingi baadaye, mutume Paulo anamutaja Samweli kati ya waamuzi na manabii waaminifu ambao walitimiza “uadilifu.” (Ebr. 11:32, 33) Samweli anafanya yaliyo mema na yaliyo haki mbele za Mungu na anawasaidia Waisraeli pia wafanye hivyo. Anapata matokeo mazuri kwa sababu anamungojea Yehova kwa uvumilivu, na anatimiza kazi yake kwa uaminifu hata ikiwa anakutana na hali zenye kuvunja moyo. Tena, yeye ni mutu mwenye shukrani. Kisha Waisraeli kushinda vita huko Mispa, Samweli anaomba wajenge monima ili uwe ukumbusho wa namna Yehova alivyowasaidia watu wake.—1 Sam. 7:12.

13. (a) Ni sifa gani tunazohitaji ikiwa tunataka kumuiga Samweli? (b) Wewe unawaza ni wakati gani mutu anapaswa kuanza kuonyesha sifa kama za Samweli?

13 Je, wewe pia unataka kutimiza “uadilifu”? Ikiwa ndiyo, inakuomba ujifunze kuwa na uvumilivu, unyenyekevu, na roho ya shukrani kama Samweli. (Soma 1 Petro 5:6.) Kila mumoja wetu ana lazima ya sifa hizo, sivyo? Tangu ujana wake, Samweli alikomalisha na kuonyesha sifa hizo, na hilo lilimusaidia baadaye alipokutana na hali nyingi zenye kuvunja moyo.

“Wana Wako Hawakutembea Katika Njia Zako”

14, 15. (a) Ni hali gani yenye kuhuzunisha sana inayomupata Samweli wakati “amezeeka”? (b) Je, Samweli ni baba mwenye kulaumiwa kama Eli? Eleza.

14 Biblia inapozungumuzia tena Samweli, nabii huyo tayari “amezeeka.” Sasa ana watoto wawili wakubwa, Yoeli na Abiya, na amewapa daraka la kumusaidia katika kazi ya uamuzi. Lakini kwa huzuni, amekosea kwa kuwatumainia. Hata kama Samweli ni mutu mwenye kuaminika na mwenye haki, watoto wake wanatumia madaraka yao kwa faida yao wenyewe, wanahukumu bila haki na kupokea rushwa ao kata-midomo.—1 Sam. 8:1-3.

15 Siku moja, wanaume wazee wa Israeli wanakuja kumuona nabii huyo muzee na kumuonyesha malalamiko yao, wanamuambia: ‘Wana wako hawatembee katika njia zako.’ (1 Sam. 8:4, 5) Je, Samweli ni mwenye kujua jambo hilo? Biblia haiseme jambo lolote. Ni kweli kwamba, Samweli ni tofauti na Eli, hakika yeye si baba mwenye kulaumiwa. Yehova alimukaripia Eli na kumuazibu kwa sababu alishindwa kuwakosoa watoto wake waovu, na kwa sababu aliwaheshimu zaidi watoto hao kuliko Mungu. (1 Sam. 2:27-29) Lakini, Yehova hajawahi hata siku moja kumukaripia Samweli hivyo.

Samweli alivumilia namna gani hali yenye kuvunja moyo ya kuwa na watoto waovu?

16. Wazazi wenye kuwa na watoto wenye mioyo migumu wanajisikia namna gani, na namna gani, kwa kadiri fulani, mufano wa Samweli unaweza kuwatolea faraja na muongozo?

16 Biblia haiseme ikiwa Samweli alisikia haya, ikiwa alihangaishwa, ao kuvunjika moyo aliposikia kuhusu mwenendo mubaya wa watoto wake. Hata hivyo, wazazi wengi wanaweza kuwazia jinsi alivyojisikia. Leo katika ulimwengu huu muovu, watoto wengi wanapuuza mamlaka na nizamu [disipline] ya wazazi wao. (Soma 2 Timotheo 3:1-5.) Kwa kadiri fulani, wazazi wanaokutana na matatizo kama hayo wanaweza kupata faraja na muongozo katika mufano wa Samweli. Hakuruhusu hata kidogo ukosefu wa imani wa watoto wake umuzuie kuendelea kuwa mwaminifu. Kumbuka, hata wakati maneno na nizamu haviguse tena mioyo migumu ya watoto, mufano muzuri wa wazazi unaweza kugusa mioyo hiyo migumu. Na siku zote, kama Samweli, wazazi wana nafasi ya kumufurahisha Baba yao, Yehova Mungu.

‘Tuchagulie Mufalme’

17. Wazee wa Israeli wanamuomba Samweli nini, naye anajisikia namna gani?

17 Watoto wa Samweli wanasahau kwamba mwenendo wao wa pupa na uchoyo utakuwa na matokeo mabaya juu ya watu. Wazee wa Israeli wanaendelea kumuambia Samweli hivi: ‘Sasa tuchagulie mufalme wa kutuhukumu sisi kama mataifa mengine yote.’ Je, Samweli anaona kama ombi hilo linaonyesha kama wanamukataa yeye? Kwa miaka mingi, amekuwa mwamuzi wa watu hao kwa jina la Yehova. Lakini sasa Waisraeli hawataki nabii tu, wanataka wawe na mufalme ili awe mwamuzi wao. Mataifa mengine jirani yana wafalme, Waisraeli pia wanataka wawe na mufalme. Samweli anajisikia namna gani? Tunasoma hivi: ‘Jambo hilo lilikuwa mbaya’ machoni pa Samweli.—1 Sam. 8:5, 6.

18. Yehova anamufariji Samweli namna gani, lakini anaonyesha namna gani uzito wa zambi ya Waisraeli?

18 Ona namna Yehova anamujibu Samweli wakati anamuelezea jambo hilo katika sala: ‘Sikiliza sauti ya watu kuhusu mambo yote wanayokuambia; kwa maana hawakukukataa wewe, bali wamenikataa mimi nisiwe mufalme juu yao.’ Moyo wa Samweli unatulizwa sana, hata hivyo, Waisraeli wamemukosea sana Mungu Muweza Yote! Yehova anamuambia nabii wake awaelezee Waisraeli matokeo mabaya ya kuwa na mufalme mwanadamu. Wakati Samweli anawaelezea, wanaendelea tu kusisitiza: ‘Hapana, bali mufalme atakuwa juu yetu.’ Siku zote Samweli ni mutiifu kwa Mungu wake, kwa hiyo basi, anaenda na kumutia mafuta mufalme ambaye Yehova amechagua.​—1 Sam. 8:7-19.

19, 20. (a) Namna gani Samweli anatii agizo la Yehova la kumutia Sauli mafuta awe mufalme wa Israeli? (b) Samweli anaendelea kuwasaidia watu wa Yehova namna gani?

19 Samweli anatii namna gani? Je, anatii kwa kutii tu, ao kwa kinyongo? Je, anaruhusu hali zenye kuvunja moyo ziharibishe moyo wake, na kumufanya awe mwenye uchungu? Watu wengi wangefanya hivyo katika hali hiyo, lakini hapana Samweli. Anamutia Sauli mafuta na anamukubali kuwa yeye ndiye mutu ambaye Yehova amechagua. Anamubusu Sauli ili kuonyesha kama anamukaribisha mufalme huyo mupya na kwamba atamutii. Kisha, anawaambia watu: ‘Je, mumemuona yule ambaye Yehova amechagua, kwamba hakuna yeyote kama yeye kati ya watu wote?’ —1 Sam. 10:1, 24.

20 Samweli hakaze akili juu ya hali ya kukosa kukamilika ya Sauli, lakini juu ya sifa nzuri za mutu huyu ambaye amechaguliwa na Yehova. Na kwa upande wake, anajikaza kubaki mwaminifu kwa Mungu kuliko kutafuta kukubaliwa na watu wageugeu. (1 Sam. 12:1-4) Tena, anatimiza kwa uaminifu mugawo wake; anawashauri watu wa Mungu kuhusu hatari za kiroho zinazoweza kuharibisha uhusiano wao na Yehova na kuwatia moyo waendelee kuwa waaminifu kwa Yehova. Shauri lake linawagusa moyo, nao wanamulilia asali kwa ajili yao. Samweli anawapa jibu hili zuri: ‘Kwa upande wangu, ni jambo lisilowaziwa, kwamba nimutendee Yehova zambi kwa kuacha kusali kwa ajili yenu; nami nitawafundisha ninyi katika njia iliyo njema na iliyo sawa.’—1 Sam. 12:21-24.

Mufano wa Samweli unatukumbusha kama hatupaswe kuacha hata kidogo wivu wala uchungu utawale moyo wetu

21. Mufano wa Samweli unaweza kukusaidia namna gani ikiwa umekwisha kuvunjika moyo kwa sababu mutu mwengine anachaguliwa kwa ajili ya daraka ao pendeleo fulani?

21 Je, umekwisha kuvunjika moyo kwa sababu mutu mwengine anachaguliwa kwa ajili ya daraka ao pendeleo fulani? Mufano wa Samweli unatukumbusha kama hatupaswe kuacha hata kidogo wivu wala uchungu utawale moyo wetu. (Soma Methali 14:30.) Mungu ana kazi nyingi nzuri na zenye kufurahisha kwa ajili ya kila mutumishi wake mwaminifu.

‘Ni Mupaka Wakati Gani Utamuombolezea Sauli?’

22. Sababu gani Samweli ana haki ya kutambua sifa nzuri za Sauli?

22 Samweli ana haki ya kutambua sifa nzuri za Sauli, kwa sababu Sauli ni mutu wa pekee. Sauli ni mutu murefu na mwenye sura nzuri, mwenye ujasiri na mwenye akili ya kumaliza matatizo ya watu, pia, mwanzoni Sauli anaonekana kuwa mwenye kiasi na munyenyekevu. (1 Sam. 10:22, 23, 27) Zaidi ya sifa hizo, Sauli ana zawadi yenye bei sana, ni kusema, uwezo wa kujichagulia namna ya kutumia maisha yake na kufanya maamuzi yake mwenyewe. (Kum. 30:19) Je, atatumia zawadi hiyo vizuri?

23. Sauli anaipoteza kwanza sifa gani ya maana, na anaonyesha namna gani kama anaanza kuwa na kiburi?

23 Kwa kusikitisha, mara nyingi mutu anapopata mamlaka, sifa ya kwanza anayopoteza ni kiasi. Kisha muda mufupi tu, Sauli anaanza kuwa na kiburi. Anachagua kutotii maagizo ya Yehova ambayo Samweli anamupa. Siku moja Sauli anakosa uvumilivu na anatoa zabihu ambayo Samweli alikuwa amekusudia kutoa. Samweli anamupatia shauri kali na kutabiri kama ufalme hautabaki katika familia ya Sauli. Kuliko kujifunza kutokana na karipio hilo, Sauli anaendelea kufanya mambo mengine mabaya zaidi ya kukosa utii.​—1 Sam. 13:8, 9, 13, 14.

24. (a) Katika vita kati ya Waisraeli na Waamaleki, namna gani Sauli anakosa kumutii Yehova? (b) Sauli anafanya nini anapoambiwa kama amefanya kosa, na Yehova anachukua uamuzi gani?

24 Kupitia Samweli, Yehova anamuomba Sauli apigane vita na Waamaleki. Katika maagizo ya Yehova, kuna amri ya kumuua mufalme wao muovu, Agagi. Lakini, Sauli hamuue Agagi na anachukua mali nyingi za Waamaleki ambazo zingepaswa kuharibiwa. Wakati Samweli anakuja ili kumuonyesha kosa lake, inaonekana wazi kama Sauli ameharibika kabisa. Kuliko kukubali kosa lake kwa unyenyekevu, Sauli anajitetea na anajaribu kupunguza uzito wa matendo yake. Anaepuka jambo linalozungumuziwa, na anajaribu kuonyesha kwamba kosa si lake, lakini, ni watu ndio waliofanya hivyo. Sauli anajaribu kupuuza shauri kwa kudai kwamba sehemu ya mali alizochukua itatolewa kama zabihu kwa Yehova. Wakati huo ndipo Samweli anamuambia maneno haya yenye kujulikana sana: ‘Tazama! Kutii ni bora kuliko zabihu.’ Kwa ujasiri, Samweli anamukaripia Sauli na kumuelezea uamuzi ambao Yehova amechukua: Ufalme utararuliwa kutoka kwa Sauli na kupewa mutu mwengine muzuri zaidi. *​—1 Sam. 15:1-33.

25, 26. (a) Sababu gani Samweli anamuombolezea Sauli, na namna gani Yehova anamushauri kwa upole nabii wake? (b) Samweli anapata somo gani anapoenda nyumbani kwa Yese?

25 Samweli anahuzunishwa sana na makosa ya Sauli. Anamulilia Yehova usiku kucha juu ya jambo hilo. Hata anamuombolezea Sauli. Aliwaza kama Sauli angeweza kuwa mufalme muzuri, mwenye sifa nzuri, lakini sasa hakuna tena tumaini. Mutu ambaye alijua, amebadilika kabisa, amepoteza sifa zake nzuri na amemuacha Yehova. Samweli anakataa kumuona Sauli tena. Hata hivyo, baadaye, kwa upole Yehova anamushauri Samweli hivi: ‘Ni mupaka wakati gani utamuombolezea Sauli, huku mimi, kwa upande mwengine, nimemukataa asiwe tena mufalme juu ya Israeli? Jaza pembe yako mafuta, nawe uende. Nitakutuma kwa Yese Mubethlehemu, kwa maana nimejipatia mufalme kati ya wanawe.’​—1 Sam. 15:34, 35; 16:1.

26 Kusudi la Yehova halitegemee uaminifu wenye kuyumbayumba wa wanadamu wasio wakamilifu. Mutu fulani akikosa uaminifu, Yehova atatafuta mutu mwengine ili kutimiza mapenzi Yake. Kwa hiyo, muzee Samweli anaacha kumuombolezea Sauli. Kwa agizo la Yehova, anaenda Bethlehemu, kwa Yese, huko anakutana na wana wa Yese, na kati yao kuna vijana wenye sura ya kuvutia sana. Lakini, kuanzia tu na ule wa kwanza, Yehova anamukumbusha Samweli asiangalie tu sura na umbo. (Soma 1 Samweli 16:7.) Mwishowe Samweli anamuona Daudi, mwana wa mwisho wa Yese, ni huyo ambaye Yehova amechagua!

Samweli anafikia kuona kwamba hakuna hali yenye kuvunja moyo inayoweza kumushinda Yehova; anaweza kushugulikia kila hali, na hata kuibadilisha iwe baraka

27. (a) Ni nini inayofanya imani ya Samweli iendelee kuwa nguvu? (b) Unajisikia namna gani unaposoma mufano muzuri wa Samweli?

27 Katika miaka yake ya mwisho-mwisho, Samweli anaelewa vizuri zaidi sababu gani Yehova aliamua kumuondoa Sauli na kumuweka Daudi. Sauli anakuwa na wivu unaomufanya atake kumuua Daudi na pia anakuwa muasi​-imani. Lakini, Daudi anaonyesha sifa nzuri kama vile ujasiri, uaminifu, imani, na ushikamanifu. Kadiri Samweli anavyokaribia kufa, ndivyo imani yake inavyokuwa nguvu zaidi. Anafikia kuona kwamba hakuna hali yenye kuvunja moyo inayoweza kumushinda Yehova; anaweza kushugulikia kila hali, na hata kuibadilisha iwe baraka. Mwishowe, Samweli anakufa, anaacha nyuma yake mufano wa mutu aliyejiendesha vizuri sana kwa miaka karibu mia moja. Haishangaze kuona Waisraeli wote wanamuombolezea mutu huyo mwaminifu! Hata leo, watumishi wa Yehova wanapaswa kujiuliza, ‘Je, nitaiga imani ya Samweli?’

^ fu. 24 Samweli mwenyewe anamuua Agagi. Mufalme huyo mubaya na familia yake hawastahili rehema. Miaka mingi baadaye, kati ya wazao wa Agagi kulikuwa ‘Hamani Muagagi,’ ambaye alijaribu kuangamiza watu wote wa Mungu.—Esta 8:3; soma Sura 15 na 16 ya kitabu hiki.