Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA TANO

‘Mwanamuke Mwema Sana’

‘Mwanamuke Mwema Sana’

1, 2. (a) Ruthu anaendelea kufanya kazi ya namna gani? (b) Ruthu amejifunza nini kuhusiana na Sheria ya Mungu na watu wake?

RUTHU anapiga magoti karibu ya fungo la miganda ya nafaka ya shayiri ambayo aliokota muchana muzima. Bethlehemu kunaanza kuwa giza katika mashamba, na wafanyakazi wengi wanaanza kurudi polepole kwenye mulango wa muji mudogo ulio juu ya kilima kilicho karibu. Ruthu ni mwenye kuchoka sana, alifanya kazi ngumu tangu asubuhi; hata hivyo, anaendelea kutumika, anatumia fimbo ao kipande cha muti ili kupiga​-piga miganda yake ili kupata mbegu za nafaka. Hata ikiwa kazi ni ngumu, hiyo ni siku nzuri kabisa kwake kuliko alivyowazia.

2 Inaonekana hali ya mujane huyo kijana inaanza kubadilika. Kama tulivyoona katika sura ya 4, Ruthu aliamua kushikamana na Naomi, mama​-mukwe wake, na aliapa kama atabaki naye na kumufanya Yehova, Mungu wa Naomi awe Mungu wake. Wajane hao wawili walitoka katika inchi ya Moabu na sasa wamefika Bethlehemu, na Ruthu, mwanamuke Mumoabu, amejifunza kwamba Sheria ya Yehova ina mipango fulani mizuri, ambayo inawafanya masikini na wageni katika Israeli waonekane kuwa pia watu. Na sasa anajionea mwenyewe kwamba watu wa Yehova wanatii Sheria hiyo na wanaonyesha wema. Jambo hilo linamugusa na kutuliza kabisa moyo wake wenye kuumia.

3, 4. (a) Namna gani Boazi alimutia Ruthu moyo? (b) Namna gani mufano wa Ruthu unaweza kutusaidia wakati huu wa matatizo ya feza?

3 Boazi ni mumoja kati ya watu hao, tajiri mwenye mashamba, na Ruthu anaokota masalio katika shamba lake. Siku hiyo, mwanaume huyo mwenye kuzeeka anamutendea kama Baba. Ruthu anafurahi sana moyoni mwake, anakumbuka maneno mazuri ya kumupongeza ambayo Boazi alimuambia kwa sababu anamushugulikia Naomi na namna alivyoamua kuja kutafuta kimbilio chini ya mabawa ya Yehova, Mungu wa kweli.​—Soma Ruthu 2:11-14.

4 Hata hivyo, labda Ruthu anajiuliza sana namna ataishi miaka ijayo. Kwa sababu yeye ni mugeni na masikini, hana bwana wala mutoto, yeye na Naomi wataishi namna gani miaka ijayo? Kuokota tu masalio kutawatimizia mahitaji yao yote? Na ni nani atamutunza atakapozeeka? Ikiwa anahangaishwa na mambo hayo, inaeleweka. Leo pia ni vigumu kupata feza, na watu wengi wanajiuliza maulizo kama hayo. Kujifunza namna imani ya Ruthu ilimusaidia kushinda mahangaiko hayo, kunaweza kutusaidia tuige imani yake katika njia nyingi.

Familia Ni Nini?

5, 6. (a) Kumuhusu Ruthu, sababu gani tunaweza kusema kwamba siku yake ya kwanza ya kuokota masalio ni siku nzuri? (b) Naomi anajisikia namna gani anapomuona Ruthu?

5 Ruthu anapomaliza kupiga​-piga mbegu zake na kuzikusanya zote, anashangaa kuona kwamba ameokota karibu efa moja ya nafaka ya shayiri, ni kusema, litre 22. Labda muzigo wake una uzito wa kilo karibu 14! Anaufunga muzigo huo labda ndani ya vazi, anaunyanyua na kuutia kwenye kichwa, na kisha anakamata njia yake mupaka Bethlehemu, wakati huo usiku unaanza kuingia.​—Rut. 2:17.

6 Naomi anafurahi sana kumuona binti wake mukwe, na labda anashituka na kushangaa anapoona muzigo huo muzito wa nafaka ya shayiri. Ruthu analeta pia chakula chake kilichobaki kutokana na chakula walichokula wakati Boazi aliwapatia wafanyakazi chakula cha muchana, na wote wawili wanachangia chakula hicho. Sasa Naomi anamuuliza: “Uliokota masalio wapi leo, nawe ulifanya kazi wapi? Yule aliyekuona na abarikiwe.” (Rut. 2:19) Naomi ni muangalifu kabisa; anatambua kwamba Ruthu hakupata chakula kingi hivyo kwa nguvu zake mwenyewe, kunapaswa kuwa na mutu fulani aliyemuhangaikia na kumuonyesha wema.

7, 8. (a) Naomi anaona kwamba wema wa Boazi unatoka wapi, na sababu gani? (b) Namna gani Ruthu anaonyesha tena upendo mushikamanifu kwa mama​-mukwe wake?

7 Katika mazungumuzo yao, Ruthu anamuelezea Naomi wema ambao Boazi alimuonyesha. Naomi anaguswa moyo, kwa hiyo anasema: ‘Abarikiwe huyo na Yehova, ambaye hakuacha kuonyesha fazili zake zenye upendo kwa walio hai na wafu.’ (Rut. 2:20) Naomi anaona kwamba ni Yehova aliyemuchochea Boazi ili amuonyeshe Ruthu wema huo. Ni Yehova anayewachochea watumishi wake kuwa wakarimu na anaahidi kwamba atawabariki kwa sababu ya wema wanaoonyesha. *—Soma Methali 19:17.

8 Naomi anamushauri Ruthu akubali mambo ambayo Boazi alimuambia: aendelee kuokota masalio katika shamba la Boazi na kubaki karibu na wanawake vijana wa nyumba yake ili wanaume waliokuwa wanafanya kazi ya kuvuna wasimusumbue. Ruthu anakubali shauri hilo. Pia, ‘anaendelea kukaa na mama​-mukwe wake.’ (Rut. 2:22, 23) Maneno hayo yanatusaidia tena kuona sifa kubwa ya Ruthu, ni kusema, upendo mushikamanifu. Je, sisi pia tunashikamana na watu wa familia zetu kwa kuwategemeza kwa ushikamanifu na kuwasaidia wanapohitaji musaada? Yehova hakose hata kidogo kuona upendo mushikamanifu kama huo!

9. Mufano wa Ruthu na Naomi unaweza kutufundisha nini kuhusu familia?

9 Je, tunaweza kusema kwamba watu hao wawili tu, Ruthu na Naomi, waliunda familia? Katika sehemu zingine, ili familia iitwe kweli familia, kunapaswa kuwa bwana, bibi, mutoto mwanaume, mutoto mwanamuke, tate (nkambo) na wengine. Lakini mufano wa Ruthu na Naomi unatufundisha kwamba familia za watumishi wa Yehova zinaweza kuwa na furaha, kuonyeshana wema na upendo, hata ikiwa ni familia ndogo sana. Je, wewe unapendezwa na watu wa familia yenu, iwe ni wengi ao wachache? Yesu aliwakumbusha wafuasi wake kwamba hata wale wasio na familia kati yao wanaweza kupata familia katika kutaniko la Kikristo.​—Mk. 10:29, 30.

Ruthu na Naomi walisaidiana na kutiana moyo

‘Yeye Ni Mumoja wa Wakombozi Wetu’

10. Naomi anapenda kumusaidia Ruthu apate nini?

10 Ruthu anaendelea kuokota masalio katika shamba la Boazi kuanzia mavuno ya shayiri, Mwezi wa 4 hivi, mupaka mavuno ya ngano, Mwezi wa 5 hivi. Majuma yanapita, na bila shaka, Naomi iko anawaza kile anaweza kumufanyia binti-mukwe wake. Walipokuwa katika inchi ya Moabu, Naomi alisema kwa uhakika kwamba hakuwa na tumaini lolote la kumusaidia Ruthu apate bwana. (Rut. 1:11-13) Lakini, sasa anaanza kuwaza kama jambo hilo linawezekana. Anamuambia Ruthu hivi: ‘Binti yangu, je, sipaswe kukutafutia mahali pa kupumuzika?’ (Rut. 3:1) Katika siku hizo, wazazi walikuwa na desturi ya kuwatafutia watoto wao bwana ao bibi. Na kwa sababu Ruthu anakuwa kama binti yake, Naomi anapenda kumutafutia Ruthu ‘mahali pa kupumuzika,’ ni kusema, usalama na ulinzi ambao mwanamuke anapata katika nyumba ya bwana yake. Lakini sasa Naomi atafanya nini?

11, 12. (a) Naomi anaposema kama Boazi ni ‘mukombozi,’ anafikiria mupango gani unaopatikana katika Sheria ya Mungu? (b) Je, Ruthu alikubali ao alikataa shauri la mama​-mukwe wake?

11 Wakati Ruthu anataja tu jina la Boazi, Naomi anasema: ‘Mwanaume huyo ni wa jamaa yetu. Yeye ni mumoja wa wakombozi wetu.’ (Rut. 2:20) Alipenda kusema nini? Sheria ambayo Mungu aliwapatia Waisraeli ilikuwa na mipango fulani kwa faida ya familia ambazo zilikuwa katika hali mbaya kwa sababu ya umasikini ao kufiwa. Mujane aliyekuwa bila watoto alikuwa katika hali ya taabu sana, kwa sababu jina la bwana yake lingepotea kabisa na hangekuwa na muriti katika vizazi vinavyokuja. Kwa hiyo, Sheria ya Mungu ilimuruhusu ndugu ya bwana kuoa mujane huyo ili aweze kuzaa muriti ambaye angeendeleza jina la bwana yake na kuchunga uriti wa familia. *​—Kum. 25:5-7.

12 Naomi anamuelezea Ruthu mupango alio nao. Tunaweza kuwazia namna Ruthu anavyofungua macho kwa mushangao, mama​-mukwe wake anapomuelezea mupango huo. Sheria hiyo ni jambo jipya kwa Ruthu; na bila shaka, hajue desturi nyingi za Sheria hiyo. Kwa hiyo, Ruthu anasikiliza kwa uangalifu kila neno Naomi anamuambia; Ruthu ni mwenye kumuheshimu sana Naomi. Jambo ambalo Naomi anamushauri kufanya ni jipya kwake, ao la haya, ni kusema, linaomba mutu ajishushe sana, hata hivyo, Ruthu anakubali. Kwa upole anasema hivi: “Yote ambayo umeniambia nitafanya.”​—Rut. 3:5.

13. Ruthu alikubali shauri kwa unyenyekevu, mufano wake unatufundisha nini kuhusu kukubali shauri la watu waliozeeka? (Soma pia Ayubu 12:12.)

13 Wakati fulani ni vigumu kwa vijana kukubali mashauri ya watu waliozeeka ao waliokwisha kuona mambo mengi katika maisha. Ni vyepesi kwao kuwaza kwamba watu hao wenye kuzeeka hawaelewe kabisa magumu na hali yao. Mufano wa unyenyekevu wa Ruthu unatukumbusha kwamba kusikiliza hekima ya watu hao wanaotupenda na wanaotaka tuwe vizuri kunaweza kutuletea baraka. (Soma Zaburi 71:17, 18.) Lakini, ni shauri gani Naomi alimupatia Ruthu, na je, Ruthu alibarikiwa kabisa kwa kufuata shauri hilo?

Kwenye Uwanja wa Kupigia-pigia Nafaka

14. Uwanja wa kupigia -pigia nafaka ni mahali pa namna gani, na namna gani watu walitumia mahali hapo?

14 Mangaribi hiyohiyo, Ruthu anaenda kwenye uwanja wa kupigia​-pigia nafaka: mahali penye kulala vizuri, penye udongo mugumu ambapo watu wenye mashamba wanaleta nafaka zao ili kuzipiga​-piga na kuzipepeta (ao kuzipepula). Mara nyingi uwanja huo unapatikana kwenye mulima ao juu ya mulima, mahali ambapo upepo unavuma sana kisha midi na mangaribi. Ili kupepeta nafaka, wafanyakazi wanatumia chombo kama kanya kubwa ao lupao: wanatupa hewani mbegu zenye kuchanganywa na makapi na kisha upepo unapeperusha makapi (ao maganda ya mbegu) na mbegu zinaanguka chini kwa sababu ni nzito kuliko makapi.

15, 16. (a) Mambo yalikuwa namna gani hapo kwenye mahali pa kupigia-pigia nafaka wakati Boazi anamaliza kazi yake mangaribi. (b) Namna gani Boazi anafikia kujua kama Ruthu analala kwenye miguu yake?

15 Kazi inaanza kumalizika, Ruthu anamuchungulia Boazi mahali alipo. Boazi anasimamia kazi ya kupepeta nafaka zake, ambazo sasa ni marundo makubwa. Anapomaliza kula kwa hamu nyingi, anajilaza kwenye rundo moja la nafaka. Wakati huo watu walizoea kufanya hivyo, labda ili kulinda mavuno yao yasiibwe. Ruthu anaona mahali Boazi anajitayarisha kulala. Anaona kwamba sasa huo ndio wakati wa kutumikisha shauri la Naomi.

16 Ruthu anakaribia sana, moyo wake unapigapiga. Iko hakika kama Boazi ni mwenye kulala kabisa. Anaenda kwenye miguu ya Boazi, anaifunua na kulala hapo pembeni ya miguu yake; anafanya kabisakabisa vile Naomi alivyomuambia. Kisha anangojea. Wakati unapita. Bila shaka, Ruthu anaona kama wakati unakawia sana. Mwishowe, karibu na katikati ya usiku, Boazi anaanza kutikisika. Anaanza kutetemeka kwa sababu ya baridi, anaamuka ili kufunika tena miguu yake. Lakini, anasikia kwamba kuna mutu fulani hapo. Biblia inasema hivi: ‘Tazama! Mwanamuke alikuwa amelala miguuni pake!’​—Rut. 3:8.

17. Wale wanaosema kwamba Ruthu alikuwa na mawazo yasiyofaa wanasahau mambo gani mawili?

17 Boazi anamuuliza: “Wewe ni nani?” Labda kwa sauti yenye kutetemeka, Ruthu anamujibu hivi: ‘Mimi ni Ruthu kijakazi wako, basi mufunike kijakazi wako kwa upindo wa nguo yako, kwa maana wewe ni mukombozi.’ (Rut. 3:9) Watu fulani wanaofasiria mambo ya Biblia leo wanasema kwamba tendo na maneno ya Ruthu vilikuwa na kusudi la kumushawishi Boazi ili alale naye. Lakini, watu hao wanasahau mambo mawili: Kwanza, Ruthu alitenda kulingana na desturi za siku hizo ambazo kwa leo zinaweza kueleweka vibaya. Kwa hiyo, ni kosa kumuhukumu Ruthu kulingana na namna tunavyoona mambo leo. Ni kweli, leo mwanamuke akifanya hivyo ataonekana kuwa ni kahaba (ao malaya). Jambo la pili, jibu la Boazi linaonyesha waziwazi kama aliona mwenendo wa Ruthu kuwa safi na wenye kusifika sana.

Ruthu alipomuendea Boazi hakuwa na mawazo mabaya wala hakuwa anatafuta faida zake mwenyewe

18. Boazi anasema nini ili kumufariji Ruthu, na namna gani Ruthu alionyesha fazili zenye upendo mara mbili?

18 Sauti pole ya Boazi na yenye kutuliza inamufariji Ruthu sana. Anamuambia hivi: ‘Yehova na akubariki, binti yangu. Umeonyesha fazili zako zenye upendo kwa njia bora zaidi mara hii ya mwisho kuliko mara ya kwanza. Haukuwafuata vijana, wawe ni wa hali ya chini ao matajiri.’ (Rut. 3:10) Ruthu alionyesha upendo mushikamanifu kwa “mara ya kwanza,” kwa kukubali kumusindikiza Naomi aliporudi Israeli na kumushugulikia. Amefanya hivyo “mara hii ya mwisho” kwa kitendo anachofanya sasa. Boazi anajua kwamba kijana mwanamuke kama Ruthu angeweza kutafuta zaidi bwana aliye kijana, awe masikini ao tajiri. Lakini, anataka tu kumutendea Naomi mema na pia baba yake mukwe aliyekufa, ili jina lake lisiondolewe katika inchi. Mwanamuke huyo kijana hatafute faida zake mwenyewe, ndio sababu Boazi anavutiwa naye.

19, 20. (a) Sababu gani Boazi hamuoe Ruthu mara moja? (b) Ni nini inayoonyesha kama Boazi anamutendea Ruthu kwa wema na kwamba anamuelewa, pia hatake Ruthu asemwe vibaya?

19 Boazi anaendelea kumuambia: ‘Basi sasa, binti yangu, usiogope. Yote utakayosema nitakufanyia, kwa maana kila mutu aliye katika lango la watu wangu anajua kwamba wewe ni mwanamuke bora [ao mwema] sana.’ (Rut. 3:11) Wazo la kumuoa Ruthu linamufurahisha Boazi sana; labda hashangazwe kabisa Ruthu anapomuomba awe mukombozi. Hata hivyo, Boazi ni mutu mwenye haki, na kwa hiyo, hataki kutenda kama anavyopenda. Anamuambia Ruthu kama kuna mutu aliye ndugu zaidi katika jamaa ya bwana ya Naomi ambaye ana haki ya kwanza ya kuwa mukombozi; Boazi anapaswa kwanza kumuona mwanaume huyo na kumupatia nafasi ya kuwa bwana ya Ruthu.

20 Boazi anamuambia Ruthu aendelee kulala mupaka asubuhi mapema; kisha ataondoka bila mutu kumuona. Hapendi watu waseme vibaya juu yake na juu ya Ruthu, kwa sababu wanaweza kuwaza kama walifanya jambo fulani mbaya. Ruthu anaendelea kulala kwenye miguu ya Boazi, inawezekana yeye ni mwenye kutulia sasa kwa sababu Boazi anamujibu vizuri. Sasa usiku unaanza kucha, Ruthu anaamuka. Boazi anajaza kwa ukarimu vazi la Ruthu nafaka nyingi. Ruthu anarudi, anashi ka njia yake mupaka Bethlehemu.​—Soma Ruthu 3:13-15.

21. Ni nini inayofanya Ruthu ajulikane sana kuwa ‘mwanamuke mwema sana,’ na namna gani tunaweza kumuiga?

21 Ruthu anafurahi sana anapofikiria maneno ambayo Boazi alimuambia, kama yeye anajulikana kuwa ‘mwanamuke mwema sana’! Bila shaka, alijulikana hivyo sanasana kwa sababu alitaka kumujua Yehova na kumutumikia. Pia, alimuonyesha Naomi na watu wake upendo mwingi; kwa sababu bila kulazimishwa alijipatanisha na desturi ambazo hakujua hapo mbele. Tukiiga imani ya Ruthu, tutawaheshimu wengine sana hata ikiwa hali yao ya maisha iko namna gani ao desturi zao. Tukifanya hivyo, sisi pia tunaweza kujulikana kuwa watu wazuri.

Mahali pa Kupumuzika

22, 23. (a) Vipimo sita ambavyo Boazi anamupatia Ruthu vinaweza kumaanisha nini? (Soma pia maelezo yaliyo chini.) (b) Sasa Naomi anamupatia Ruthu shauri gani?

22 Ruthu anafika nyumbani, Naomi anamuuliza: “Wewe ni nani, binti yangu?” Labda Naomi anauliza hivyo kwa sababu kungali bado giza na hivyo hamuone vizuri, ao anapenda kujua ikiwa mambo yamemuendea Ruthu vizuri na kwa hiyo kuna tumaini la kuolewa. Mara moja Ruthu anamuelezea jinsi mambo yalivyopita kati yake na Boazi. Pia anamuonyesha zawadi ya ukarimu, ni kusema, nafaka ambayo Boazi alimutumia Naomi. *​—Rut. 3:16, 17.

23 Naomi anamupatia Ruthu shauri la hekima: kubaki nyumbani siku hiyo kuliko kuenda kuokota masalio katika shamba. Anamuhakikishia Ruthu hivi: ‘Mwanaume huyo hatapumuzika mupaka amalize jambo hilo leo.’​—Rut. 3:18.

24, 25. (a) Namna gani Boazi anaonyesha kama yeye ni mutu wa haki na asiyetafuta faida zake mwenyewe? (b) Ruthu anabarikiwa namna gani?

24 Naomi hadanganyike. Siku hiyohiyo, Boazi anaenda kwenye mulango wa muji, mahali ambapo wazee wa muji wanazoea kukutana, na anangojea mupaka yule mwanaume wa jamaa ya karibu ya Elimeleki anapopita hapo. Mbele ya mashahidi, Boazi anamupatia nafasi ya kuwa mukombozi na kumuoa Ruthu. Lakini, mwanaume huyo anakataa, anaonyesha kwamba akifanya hivyo atapoteza uriti wake mwenyewe. Kisha, mbele ya mashahidi hao wanaokusanyika kwenye mulango wa muji, Boazi anaonyesha kwamba yeye atakuwa mukombozi huyo; atanunua shamba la Elimeleki, bwana ya Naomi, na kumuoa Ruthu, bibi ya Maloni, mutoto wa Elimeleki. Boazi anaonyesha sababu: Anataka ‘kumuinulia mwanaume aliyekufa jina katika uriti wake.’ (Rut. 4:1-10) Kwa kweli, Boazi ni mwanaume mwenye haki na asiyetafuta faida zake mwenyewe.

25 Boazi anamuoa Ruthu. Kisha, Biblia inasema hivi: ‘Yehova akamuwezesha kupata mimba naye akazaa mwana.’ Wanawake wa Bethlehemu wanamubariki Naomi na kumusifu Ruthu kwa sababu alimufaa Naomi kuliko watoto saba wanaume. Mwishowe, mutoto wa Ruthu akawa nkambo ao tate wa Mufalme Daudi. (Rut. 4:11-22) Na kisha Yesu Kristo akatokea katika uzao wa Daudi.​—Mt. 1:1. *

Yehova alimubariki Ruthu kwa kumupa pendeleo la kuwa nkambo ao tate wa Masiya

26. Mifano ya Ruthu na Naomi inatukumbusha nini?

26 Ruthu alibarikiwa kweli, na Naomi pia, ambaye alisaidia kumulea mutoto huyo kama mutoto wake. Maisha ya wanawake hao wawili yanatukumbusha kabisa kwamba Yehova Mungu anaona wale wote, ambao kwa unyenyekevu, wanatumika kwa bidii ili kutegemeza familia zao na pia wanatumika kwa uaminifu pamoja na watu wake. Yehova hakose kamwe kuwabariki watu waaminifu, kama vile Boazi, Naomi, na Ruthu.

^ fu. 7 Naomi alitambua kwamba Yehova haonyeshe wema wake kwa watu walio wazima tu; anafanya hivyo hata kwa watu waliokufa. Naomi alipoteza bwana yake na watoto wake wawili. Ruthu pia alipoteza bwana yake. Bila shaka, wanaume hao walipendwa sana na wanawake hao. Kwa hiyo, kumuonyesha Naomi na Ruthu wema ni kuwaonyesha wanaume hao wema, kwa sababu wangekuwa wazima wangependa kuona wanawake hao wanatendewa vizuri.

^ fu. 11 Haki ya kumuoa mujane ilikuwa kwanza ya ndugu za mwanaume aliyekufa na kisha wanaume wengine wa jamaa ya karibu wangeweza kufanya hivyo, ilikuwa hivyo pia kuhusu haki ya uriti.​—Hes. 27:5-11.

^ fu. 22 Boazi anamupatia Ruthu vipimo sita, lakini vipimo hivyo havijulikane ikiwa ni vya namna gani. Labda alifanya hivyo kwa sababu kulikuwa siku ya Sabato kisha siku sita za kazi; Ruthu ni mujane na alifanya kazi ngumu kwa siku sita. Siku ya Ruthu ya kupumuzika ilikuwa inakaribia; ‘pumuziko’ ambalo mwanamuke anapata katika nyumba ya bwana yake. Labda pia vipimo sita vinaonyesha tu kiasi ambacho Ruthu angeweza kubeba kwenye kichwa.

^ fu. 25 Ruthu ni mumoja kati ya wanawake watano ambao Biblia inataja katika ukoo wa Yesu. Mwanamuke mwengine ni Rahabu, mama ya Boazi. (Mt. 1:3, 5, 6, 16) Yeye pia hakuwa Muisraeli.

Mifano ya Ruthu na Naomi inatukumbusha kwamba tunapaswa kufurahia familia yetu

Ruthu alijulikana kuwa mwanamuke mwema sana kwa sababu aliwatendea wengine kwa upendo na heshima