Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KWANZA

“Ijapokuwa Alikufa, Bado Anasema”

“Ijapokuwa Alikufa, Bado Anasema”

1. Ni nini iliyowazuia Adamu na Eva na watoto wao kuingia katika bustani ya Edeni, na Abeli anatumaini nini?

ABELI anatazama kundi lake la kondoo wenye kula majani kwa amani kwenye mulima. Kisha, labda anaangalia mbali huko, anaona mahali fulani palipo na mwangaza mudogo kabisa. Anajua vizuri kwamba mahali hapo kuna upanga unaowaka na unaoendelea kuzunguka-zunguka ili kuzuia njia inayopeleka kwenye bustani ya Edeni. Anakumbuka kwamba wakati fulani wazazi wake waliishi mahali hapo, lakini sasa hawawezi tena kuingia mahali hapo, wala watoto wao. Wazia namna upepo wenye kutulia wa mangaribi unavyopeperusha nywele zake, huku akitazama juu na kufikiri juu ya Muumbaji wake. Labda anajiuliza ikiwa wanadamu wanaweza tena kukubaliwa katika familia ya Mungu. Abeli anatumaini kwamba jambo hilo linawezekana.

2-4. Namna gani Abeli anasema na sisi leo?

2 Unajua kwamba Abeli anasema nawe leo hii? Unaweza kumusikia? Labda unaweza kusema hivi: Jambo hilo haliwezekane. Mutoto huyo wa pili wa Adamu alikufa kumepita miaka mingi. Kumepita karibu miaka 6 000, mwili wake na mifupa yake vimekwisha kuoza na kuwa mavumbi. Pia kuhusu watu waliokufa, Biblia inatufundisha kwamba ‘hawajue lolote kamwe.’ (Mhu. 9:5, 10) Tena, hakuna neno hata moja ambalo Abeli alisema lililoandikwa katika Biblia. Sasa namna gani inawezekana aseme na sisi?

3 Mutume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu ili aandike hivi juu ya Abeli: “Ijapokuwa alikufa, bado anasema.” (Soma Waebrania 11:4.) Abeli anasema na sisi kupitia nini? Kupitia imani yake. Abeli ndiye mutu wa kwanza aliyeonyesha sifa hiyo nzuri. Alionyesha imani yenye nguvu hivi kwamba hatusahau mufano wa imani yake, na tunaweza kuiga mufano huo. Tunapojifunza juu ya imani ya Abeli na kuiga imani hiyo, hilo linaonyesha kama tunamusikiliza anaposema na sisi.

4 Kwa hiyo tunaweza kujifunza nini juu ya Abeli na imani yake, hata ikiwa Biblia haiseme mambo mengi juu yake? Acha tuzungumuzie jambo hilo.

Abeli Anakuwa “Musingi wa Ulimwengu”

5. Yesu alimaanisha nini aliposema kuwa Abeli ndiye aliyekuwa ‘musingi wa ulimwengu’? (Soma pia maelezo yaliyo chini.)

5 Abeli alizaliwa muda mufupi kisha wanadamu wa kwanza kuumbwa. Miaka mingi baadaye, Yesu alisema kuwa Abeli ndiye aliyekuwa “musingi wa ulimwengu.” (Soma Luka 11:50, 51.) Bila shaka, ulimwengu ambao Yesu anataja katika andiko hilo, ni wanadamu ambao wanatumaini la kukombolewa kutoka katika zambi. Abeli alikuwa mutu wa ine kuishi hapa duniani, lakini inaonekana kwamba yeye ndiye mwanadamu wa kwanza ambaye Mungu aliona kuwa anastahili kufaidika na ukombozi. * Ni wazi kwamba Abeli alipokuwa anakomaa, dunia haikuwa na watu wenye tabia nzuri ambao angeweza kuiga.

6. Wazazi wa Abeli walikuwa watu wa namna gani?

6 Hata ikiwa dunia haikuwa bado na watu wengi wakati huo, tayari wanadamu walianza kupambana na hali ngumu za maisha. Bila shaka, wazazi wa Abeli, ni kusema, Adamu na Eva, walikuwa watu wenye sura nzuri na wenye nguvu. Hata hivyo, walifanya zambi nzito, nao walijua jambo hilo. Waliumbwa wakamilifu na walipaswa kuishi milele. Lakini, walimuasi Yehova Mungu, na kwa hiyo, walifukuzwa katika bustani ya Edeni, ambayo ilikuwa makao yao ya Paradiso. Kwa sababu Adamu na Eva waliweka tamaa zao pa nafasi ya kwanza, kuliko hata faida za watoto wao, walipoteza ukamilifu na uzima wa milele.​—Mwa. 2:15–3:24.

7, 8. Eva alisema nini wakati Kaini alizaliwa, na inawezekana alifikiri nini?

7 Inje ya bustani, Adamu na Eva walikuwa na maisha magumu sana. Walipozaa mutoto wao wa kwanza, walimupa jina Kaini, maana yake, “Kitu Kilichotokezwa,” na Eva alisema hivi: ‘Nimezaa mwanaume kwa musaada wa Yehova.’ Maneno ya Eva yanaonyesha kwamba pengine alifikiria ile ahadi ya Yehova katika bustani ya Edeni. Yehova alitabiri kwamba mwanamuke fulani atatokeza “uzao” ambao siku moja utamuharibu yule muovu, aliyewadanganya Adamu na Eva. (Mwa. 3:15; 4:1) Je, Eva alifikiri kuwa yeye ndiye yule mwanamuke aliyetabiriwa na kwamba Kaini ndiye ule ‘uzao’ ulioahidiwa?

8 Ikiwa alifikiri hivyo, basi alijidanganya kabisa. Tena, ikiwa yeye na bwana yake waliingiza mawazo hayo katika akili ya Kaini mutoto wao alipokuwa anakomaa, basi walimufanya Kaini awe mwenye kiburi zaidi. Kisha hapo, Eva alizaa mutoto wao wa pili, lakini katika Biblia hatuone maneno kama hayo ya kumusifu-sifu mutoto huyo wa pili. Walimupatia jina Abeli, ambalo linaweza kumaanisha “Pumuzi,” ao “Bure.” (Mwa. 4:2) Je, walimupa jina hilo kwa sababu ya kuvunjika moyo, kwa kuwa hawakumutazamia zaidi Abeli kama walivyomutazamia Kaini? Inawezekana, lakini hatuna uhakika.

9. Maisha ya Adamu na Eva yanaweza kuwafundisha nini wazazi leo kuhusu watoto?

9 Maisha ya Adamu na Eva yanaweza kuwafundisha wazazi mambo mengi leo. Maneno yenu na matendo yenu yanaweza kuwafundisha watoto wenu kuwa watu wenye kiburi, wenye kutafuta mambo makubwa, na wenye kutafuta faida zao wenyewe. Pia, maneno yenu na matendo yenu yanaweza kuwafanya wamupende Yehova na kuwa marafiki wake. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba wazazi wa kwanza walishindwa kutimiza daraka lao. Hata hivyo, kulikuwa bado na tumaini kwa watoto wao.

Ni Nini Ilimusaidia Abeli Kuwa na Imani?

10, 11. Kaini na Abeli walifanya kazi gani, na Abeli alionyesha tabia ao sifa gani?

10 Kaini na Abeli walipoendelea kukomaa, bila shaka, baba yao Adamu aliwafundisha kazi ambayo ingewasaidia kutimiza mahitaji ya familia. Kaini alikuwa mulimaji, na Abeli muchungaji wa kondoo.

11 Lakini, Abeli alitimiza jambo moja la maana sana. Kwa muda wa miaka mingi alionyesha imani, na baadaye mutume Paulo aliandika kuhusu sifa hiyo nzuri. Abeli alikuwa kweli na imani! Wakati huo hapakuwa na mutu ambaye Abeli angeweza kuiga mufano wake. Ni nini basi ilimusaidia kuwa na imani katika Yehova Mungu? Acha tufikirie mambo matatu ambayo yangeweza kumusaidia Abeli kuwa na imani hiyo.

12, 13. Namna gani kuangalia uumbaji wa Yehova kulimusaidia Abeli kuwa na imani?

12 Uumbaji wa Yehova. Ni kweli kwamba Yehova alikuwa amelaani udongo, na laana hiyo ilifanya udongo uzae miba na mibaruti ambayo ilifanya kazi ya kulima iwe ngumu. Hata hivyo, udongo ulitoa chakula kingi ambacho kilisaidia familia ya Adamu kuendelea kuishi. Jambo lingine ni kwamba wanyama, ndege na samaki hawakulaaniwa; wala milima, bahari, mito; wala anga, mawingu, jua, mwezi na nyota havikulaaniwa. Kila mahali ambapo Abeli alitazama, aliona mambo yaliyoonyesha upendo, hekima na wema wa Yehova Mungu, Muumbaji wa vitu hivyo vyote. (Soma Waroma 1:20.) Bila shaka, kufikiri sana ao kutafakari juu ya uumbaji na sifa za Mungu kulifanya imani ya Abeli iwe yenye nguvu.

Uumbaji ulimusaidia Abeli kuwa na imani yenye nguvu katika Muumbaji mwenye upendo

13 Abeli alichukua wakati wa kufikiri sana juu ya Yehova. Wazia namna anavyochunga kundi lake la kondoo. Maisha ya muchungaji yanaomba kutembea sana. Muchungaji wa kondoo anawaongoza wanyama hao wapole kwenye milima, anawapitisha katika mabonde na kuvuka mito, ili kutafuta majani mazuri, na mahali pazuri palipo na maji, na mahali pazuri zaidi pa kupumuzika. Kati ya wanyama wote ambao Mungu aliumba, kondoo ni wanyama wanaoonekana kuwa zaifu zaidi, ni kama vile waliumbwa na uhitaji wa kuongozwa na kulindwa na mwanadamu. Je, Abeli pia aliona kwamba anahitaji kuongozwa, kulindwa na kutunzwa na Mutu fulani mwenye hekima na nguvu zaidi kuliko mwanadamu yeyote? Bila shaka, Abeli alieleza mambo mengi kama hayo katika sala zake, na hilo lilifanya imani yake iendelee kukomaa.

14, 15. Namna gani maneno ambayo Yehova alitabiri yalimusaidia Abeli awe na mambo mengi ya kufikiri juu ya Mungu?

14 Neno la Yehova. Adamu na Eva hawakukosa kuwaelezea watoto wao sababu ya kufukuzwa kwao katika bustani ya Edeni. Kwa hiyo, Abeli alikuwa na mambo mengi ya kufikiri sana juu ya Mungu.

15 Yehova alisema kwamba udongo umelaaniwa. Abeli alipoona miiba na mibaruti alielewa wazi kwamba ni utimizo wa maneno hayo. Pia, Yehova alisema kwamba Eva atakuwa na maumivu wakati wa mimba na kwamba atazaa kwa uchungu. Bila shaka, Abeli aliona utimizo wa maneno hayo wakati ndugu na dada zake wadogo walipozaliwa. Yehova aliona mbele ya wakati kwamba Eva atakuwa na maoni yasiyofaa kuhusu upendo wa bwana yake kwake na atataka ahangaikiwe kupita kiasi, na kwamba Adamu atamutawala. Abeli aliona mambo hayo yakitendeka kati ya mama yake na baba yake. Katika kila hali, Abeli aliona kwamba neno la Yehova ni la kweli kabisa. Kwa hiyo, alikuwa na sababu zenye nguvu za kuamini ahadi ambayo Mungu alitoa, kwamba siku fulani “uzao” utaondoa mambo yote mabaya yaliyoanzishwa katika Edeni.—Mwa. 3:15-19.

16, 17. Mufano wa makerubi wa Yehova ulimufundisha Abeli nini?

16 Watumishi wa Mungu. Kati ya wanadamu walioishi wakati huo hakukuwa na mutu ambaye Abeli angeweza kuiga. Hata hivyo, hapa duniani kulikuwa na viumbe wengine ambao Abeli angeweza kuiga imani yao. Wakati Adamu na Eva walifukuzwa katika bustani, Yehova alichukua mipango ili wao na watoto wao wasiingie katika Paradiso hiyo. Kwa hiyo, aliweka makerubi, ni kusema, malaika wa hali ya juu sana, ili kuwazuia; na pia kulikuwa na upanga wenye kuwaka moto ambao uliendelea kuzunguka​-zunguka.​—Soma Mwanzo 3:24.

17 Wazia namna Abeli alifurahia kuwaona makerubi hao tangu utoto. Bila shaka, kuonekana kwao, katika hali ya kibinadamu, kunamusaidia Abeli aone kwamba ni viumbe wenye nguvu sana. Na ule “upanga” unaoendelea kuwaka na kuzunguka​-zunguka, unamusaidia pia kuwa na woga na heshima. Anapoendelea kukomaa, je, kuna siku ameona makerubi hao wanachoshwa na kuacha mugao wao? Hata siku moja. Muchana na usiku, mwaka baada ya mwaka, malaika hao wenye akili na wenye nguvu sana, wanaendelea kutimiza mugao wao. Ni kwa njia hiyo, Abeli anajua kwamba Yehova Mungu ana watumishi waaminifu na washikamanifu. Anaona kwamba makerubi hao wana sifa ya ushikamanifu na utii kwa Yehova, sifa ambazo haone katika familia yao. Bila shaka, mufano wa malaika hao unatia imani yake nguvu.

Katika maisha yake yote, Abeli aliona kwamba wale makerubi walikuwa watumishi waaminifu na watiifu wa Yehova

18. Ni mambo gani yanayoweza kutusaidia kuwa na imani yenye nguvu leo?

18 Kupitia uumbaji, neno lake, na mifano ya watumishi wake, ni kusema, malaika zake, Yehova anajifunua. Abeli anapofikiri juu ya mambo hayo imani yake inakuwa yenye nguvu zaidi. Bila shaka, Abeli anasema na sisi kupitia mufano wake, sivyo? Mufano wa Abeli unawasaidia zaidi sana vijana wajue kwamba wanaweza kuwa na imani ya kweli katika Yehova Mungu, hata ikiwa watu fulani katika familia yao si mufano muzuri. Maajabu ya uumbaji, Biblia nzima, na pia mifano mingi ya watu wenye imani wanaotuzunguka, hayo yote yanatusaidia kuwa na imani yenye nguvu leo.

Sababu Gani Zabihu ya Abeli Ni Nzuri Zaidi?

19. Mwishowe, Abeli alielewa ukweli gani wa musingi?

19 Imani ya Abeli katika Yehova inapokomaa, anatafuta njia ya kuionyesha kwa matendo. Lakini, mutu wa udongo tu anaweza kumupatia nini Muumbaji wa ulimwengu wote? Ni wazi kwamba Mungu hana lazima ya zawadi fulani ao musaada wowote wa wanadamu. Mwishowe, Abeli anaelewa ukweli huu wa musingi: Ikiwa kwa nia njema anamutolea Yehova, kile kizuri zaidi alicho nacho, Baba yake mwenye upendo atafurahi sana.

Imani ndio ilimuchochea Abeli kumutolea Mungu zabihu; lakini haikuwa hivyo kwa Kaini

20, 21. Kaini na Abeli, kila mumoja anamutolea Yehova nini, na Yehova anakubali zabihu ya nani?

20 Abeli anaamua kumutolea Mungu kondoo fulani wa kundi lake. Anachagua kondoo wazuri zaidi, ni kusema, kati ya wazao wa kwanza wa kondoo zake, na anamutolea Mungu zabihu anazoona kuwa nzuri zaidi. Wakati huohuo, Kaini pia anatafuta kukubaliwa na kubarikiwa na Mungu, anatayarisha mavuno ya shamba ili kumutolea Mungu. Lakini, hafanye hivyo kwa nia nzuri kama Abeli. Tofauti kati ya ndugu hao wawili inaonekana wazi wakati kila mumoja anamutolea Mungu toleo lake.

21 Bila shaka, watoto hao wawili wa Adamu wanatumia kila mumoja mazabahu na moto ili kumutolea Mungu toleo, pengine makerubi, ambao wakati huo walikuwa ndio wajumbe wa Yehova duniani, wanatazama namna wanavyofanya. Na Yehova anatenda namna gani? Biblia inasema hivi: ‘Yehova alikuwa anamutazama Abeli na toleo lake kwa kibali.’ (Mwa. 4:4) Lakini, Biblia haiseme namna gani Mungu anakubali zabihu ya Abeli.

22, 23. Sababu gani Yehova anakubali zabihu ya Abeli?

22 Sababu gani Mungu anamukubali Abeli? Ni kwa sababu ya zabihu yake tu? Abeli anamutolea Mungu kiumbe kilicho na uzima, kinachopumua, na anamwanga damu ya kiumbe hicho, inayofananisha uzima. Je, Abeli anaelewa namna zabihu kama hiyo itakuwa ya maana sana? Miaka mingi kisha wakati wa Abeli, Mungu alitumia zabihu ya mwana-kondoo asiye na kilema ili kufananisha zabihu ya Mwana wake mukamilifu, “Mwana​-Kondoo wa Mungu,” ambaye damu yake isiyo na kosa itamwangwa. (Yoh. 1:29; Kut. 12:5-7) Hata ikiwa labda Abeli alijua kwamba zabihu ya kiumbe chenye uzima ni ya maana sana, hata hivyo inaonekana kwamba hakujua wala kuelewa kabisa maana ya zabihu hizo.

23 Jambo ambalo tunajua kwa uhakika ni hili: Abeli alitoa kile kizuri zaidi alichokuwa nacho. Yehova anamukubali Abeli na toleo analotoa. Abeli anatoa kwa sababu anachochewa na upendo na imani ya kweli kwa Yehova.

24. (a) Sababu gani tunasema kwamba si toleo la Kaini ndilo lilikuwa tatizo? (b) Leo, watu wengi wanafanana na Kaini namna gani?

24 Lakini Kaini hafanye hivyo. Yehova ‘hamutazame Kaini na toleo lake kwa kibali chochote.’ (Mwa. 4:5) Hapa tatizo si aina ya toleo la Kaini, kwa sababu baadaye, Sheria ya Mungu iliruhusu kumutolea toleo la mazao ya udongo. (Law. 6:14, 15) Biblia inasema kwamba “matendo yake [Kaini] mwenyewe yalikuwa maovu.” (Soma 1 Yohana 3:12.) Kaini anafikiri kama watu wengi leo, kwamba inatosha tu kuonyesha kijuu​-juu kama mutu anajitoa kwa Mungu. Matendo ya Kaini yanaonyesha mara moja kwamba hana imani ya kweli wala upendo kwa Mungu.

25, 26. Yehova alimuonya Kaini kuhusu nini, lakini Kaini anafanya nini?

25 Wakati Kaini anaona kwamba Yehova hamukubali, je, anajikaza kuiga mufano wa Abeli? Hapana. Kuliko kufanya hivyo, anamukasirikia ndugu yake na kumuchukia. Yehova anaona yale yanayopita katika moyo wa Kaini na kwa uvumilivu anajaribu kumufanya afikiri vizuri. Anamuonya Kaini kuwa hali hiyo itamuongoza kwenye zambi nzito, na anamuahidi kwamba akibadilisha kabisa mwenendo wake ‘atamuinua,’ ni kusema, atamukubali.​—Mwa. 4:6, 7.

26 Kaini anapuuza onyo la Mungu. Anamuambia mudogo yake, anayemutumainia, waende kutembea kwenye mashamba. Wanapofika huko, Kaini anamushambulia na kumuua. (Mwa. 4:8) Tunaweza kusema kwamba Abeli ndiye shahidi wa kwanza aliyeteswa na kuuawa kwa sababu ya imani yake. Ni kweli kwamba alikufa, lakini historia ya maisha yake inaendelea.

27. (a) Sababu gani tunaweza kuwa hakika kwamba Abeli atafufuliwa? (b) Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunapenda siku fulani tukutane na Abeli?

27 Kwa njia ya mufano, damu ya Abeli ilimulilia Yehova Mungu, ilimuomba alipize kisasi, ao Mungu akate jambo hilo kwa haki kwa kumuazibu yule muovu Kaini kwa sababu ya tendo lake la uuaji. (Mwa. 4:9-12) Jambo la maana zaidi ni kwamba Abeli anasema na sisi leo kupitia habari ya imani yake. Pengine Abeli aliishi tu miaka 100 hivi; hayo yalikuwa maisha mafupi sana kwa wanadamu wakati huo. Hata hivyo, alitumia maisha yake katika njia yenye kumupendeza Mungu. Alikufa akiwa mwenye kujua kwamba alipendwa na kukubaliwa na Baba yake wa mbinguni, Yehova. (Ebr. 11:4) Kwa hiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anaendelea kumukumbuka Abeli; Abeli anangojea ufufuo ili kuishi katika paradiso duniani. (Yoh. 5:28, 29) Utakutana na Abeli huko? Itawezekana ikiwa tu unaazimia kumusikiliza Abeli ambaye ijapokuwa alikufa, bado anasema, na ikiwa unaazimia kuiga imani yake ambayo ni mufano wa ajabu.

^ fu. 5 Maneno ‘musingi wa ulimwengu’ yanatoa wazo la kutupa mbegu chini, ni kusema, kuzaa. Kwa hiyo, maneno hayo, yanamaanisha kuzaliwa kwa mutoto wa kwanza wa kibinadamu. Ikiwa ni hivyo, sababu gani Yesu alisema Abeli ndiye “musingi wa ulimwengu” ijapokuwa Kaini ndiye alikuwa mutoto huyo wa kwanza? Ni kwa sababu Kaini alimuasi Yehova Mungu kimakusudi kupitia maamuzi yake na matendo yake. Kwa hiyo, inaonekana Kaini hatakuwa kati ya watu watakaofufuliwa na kufaidika na ukombozi, kama vile wazazi wake pia.