Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA MAKUMI MBILI

“Nimeamini”

“Nimeamini”

1. Eleza namna Martha anavyojisikia na sababu gani anajisikia hivyo.

MARTHA anaona akilini mahali ndugu yake amezikwa: kaburi hilo ni pango ambalo wameweka jiwe mahali pa kuingilia. Ana huzuni nyingi sana moyoni. Hajaitika kwamba ndugu yake mupendwa Lazaro amekufa. Siku ine ambazo zimepita tangu Lazaro atoe pumuzi zinaonekana kuwa kipindi kirefu cha huzuni. Katika kipindi hicho wanatembelewa na wageni wengi wanaokuja kuwafariji.

2, 3. (a) Martha anajisikia namna gani anapomuona Yesu? (b) Maneno ya maana sana ambayo Martha anasema yanaonyesha nini juu yake?

2 Na sasa Yesu, mutu ambaye ni rafiki wa sana wa Lazaro, anasimama mbele ya Martha. Kumuona Yesu kunamuongezea Martha huzuni tena zaidi, kwa sababu duniani pote ni Yesu peke yake ndiye mutu ambaye angeweza kumuokoa ndugu yake. Hata hivyo, Martha anafarijika kwa kadiri fulani kwa kuwa pamoja na Yesu inje ya muji mudogo wa Bethania ulio kwenye kilima. Kwa muda mufupi ambao Martha anapitisha pamoja na Yesu, anatiwa moyo na wema na pia huruma ya Yesu. Yesu anamuuliza maulizo ambayo yanamusaidia kukazia akili imani yake na tumaini la ufufuo. Mazungumuzo hayo yanamuchochea Martha aseme maneno haya ya maana sana: “Nimeamini kwamba wewe ndiye Kristo Mwana wa Mungu, Yule anayekuja ulimwenguni.”—Yoh. 11:27.

3 Maneno hayo yanaonyesha kama Martha alikuwa mwanamuke mwenye imani yenye nguvu. Mambo machache ambayo Biblia inazungumuzia kumuhusu, yanaweza kutusaidia tuitie nguvu imani yetu. Ili kuelewa jambo hilo, acheni tuchunguze habari ya kwanza katika Biblia inayozungumuzia Martha.

‘Kuhangaika na Kusumbuka’

4. Sababu gani tunasema kwamba Lazaro, Martha, na Maria wanafanyiza familia ya pekee, na familia hiyo ilikuwa na uhusiano gani pamoja na Yesu?

4 Turudi nyuma miezi fulani mbele ya hapo. Lazaro angali bado muzima na mwenye afya njema. Nyumba yake katika Bethania inajitayarisha kumukaribisha mugeni wa maana kuliko wote, Yesu Kristo. Lazaro, Martha, na Maria wanafanyiza familia ya pekee: dada hao wawili na ndugu yao wanaishi pamoja. Watu fulani wenye elimu ya mambo ya Biblia wanasema kama labda Martha alikuwa ndiye mukubwa kati yao, kwa kuwa ni yeye anayefanya matayarisho ya kumupokea mugeni na wakati fulani anatajwa wa kwanza. (Yoh. 11:5) Hatujue ikiwa yeyote kati yao alikuwa amefunga ndoa. Iwe hivyo ao hapana, walikuwa kabisa marafiki wa sana wa Yesu. Yesu alibaki nao katika nyumba yao huko Yudea wakati alikuwa akihubiri katika muji huo; katika muji huo Yesu alipambana na upinzani na uadui mukali. Bila shaka, alifurahia sana mahali hapo, mahali alipopata amani na kutegemezwa.

5, 6. (a) Martha anafanya nini ili kumupokea Yesu? (b) Maria anafanya nini wakati Yesu anapofundisha watu nyumbani kwao?

5 Martha ana mambo mengi ya kufanya ili mugeni ajisikie vizuri na mwenye kukaribishwa katika nyumba yao. Ni mwanamuke mwenye bidii ya kazi, na mara nyingi ana mambo mengi sana ya kufanya. Hata wakati huu ambao Yesu anawatembelea, Martha anatumika sana. Bila kukawia anapanga kutayarisha chakula cha pekee cha aina mbalimbali kwa ajili ya mugeni wao wa pekee, na labda kwa ajili ya wafuasi wa Yesu wanaosafiri pamoja naye. Wakati huo, kumukaribisha mugeni lilikuwa jambo la maana sana. Mugeni alipofika, iliomba kumukaribisha kwa kumubusu, kumuvua viatu, kumunawisha miguu, na kumupaka mafuta yenye harufu nzuri kichwani. (Soma Luka 7:44-47.) Ilikuwa desturi kuwatunza wageni vizuri, kuwatayarishia mahali pazuri pa kulala, na kuwapa chakula kizuri.

6 Martha na Maria wana kazi nyingi ili kutayarisha kumupokea Yesu. Ingawa wengi wanafikiri kwamba Maria alipendezwa sana na kujifunza ao kumusikiliza tu Yesu, inaonekana mwanzoni kwamba anamusaidia dada yake kufanya kazi. Lakini Yesu anapofika, mambo yanabadilika. Yesu anaona kwamba ni wakati muzuri wa kuwafundisha watu, na anafanya hivyo. Yesu ni tofauti na viongozi wa dini wa wakati huo, anawaheshimu wanawake na iko tayari kuwafundisha juu ya Ufalme wa Mungu, kichwa cha habari alichokuwa anakazia katika mahubiri yake. Maria anafurahia nafasi hiyo, kwa hiyo anakaa karibu ya Yesu na kumusikiliza kwa uangalifu kabisa.

7, 8. Sababu gani Martha anahangaika sana moyoni mwake, na mwishowe anasema nini?

7 Tunaweza kuwazia namna Martha anavyohangaika sana. Ni mwenye kutayarisha vyakula vya aina mbalimbali na kufanya mambo mengi kwa ajili ya wageni, kwa hiyo Martha anaendelea kuhangaika na ana wasiwasi hata zaidi. Anapopitapita huku na huku na kumuona dada yake anakaa tu bila kumusaidia, je, uso wake unaonyesha kama anakasirika, ao je, anapumua kidogo ili kuonyesha kwamba anavunjika moyo? Ikiwa alifanya hivyo, hilo haliwezi kutushangaza. Kwa kawaida, si yeye mwenyewe anayepaswa kuendelea kufanya kazi hizo zote!

8 Mwishowe, Martha hawezi kuvumilia tena hali hiyo. Anamukatiza Yesu na kusema: ‘Bwana, haujali kwamba dada yangu ameniacha peke yangu kushugulikia mambo? Kwa hiyo, umuambie aje anisaidie.’ (Lu. 10:40) Hayo ni maneno mazito. Biblia fulani zinatafsiri ulizo lake hivi: ‘Bwana, hauone vibaya . . . ?’ Kisha Martha anamuomba Yesu amuonyeshe Maria kama amekosea na amuagize ili amusaidie.

9, 10. (a) Yesu anamujibu Martha namna gani? (b) Tunajua namna gani kwamba Yesu hazarau kazi ngumu ya Martha?

9 Labda jibu la Yesu linamushangaza Martha, kama vile tangu zamani limewashangaza wasomaji wengi wa Biblia. Kwa upole Yesu anamujibu Martha hivi: ‘Martha, Martha, wewe unahangaika na kusumbuka juu ya mambo mengi. Ingawa hivyo, mambo machache ndio yanayohitajiwa, ao moja tu. Yeye, Maria alichagua fungu jema, nalo halitaondolewa kwake.’ (Lu. 10:41, 42) Yesu anataka kusema nini? Je, anataka kusema kwamba Martha anahangaikia zaidi mambo ya kimwili? Je, anazarau kazi ngumu ya Martha ya kumutayarishia chakula kizuri?

Hata kama Martha “alihangaika na kusumbuka juu ya mambo mengi,” kwa unyenyekevu alikubali shauri

10 Hapana. Yesu anajua vizuri kwamba Martha ni mwenye upendo na nia nzuri. Zaidi ya hilo, haone kwamba ni vibaya kuwa mukarimu hivyo ili kuonyesha ukaribishaji. Kumbuka kwamba alienda kwenye “karamu kubwa” ambayo Mathayo alimutayarishia wakati fulani mbele ya hapo. (Lu. 5:29) Hapa tatizo si chakula ambacho Martha anatayarisha; tatizo ni mambo ambayo anatia pa nafasi ya kwanza. Martha anahangaikia sana kutayarisha chakula kizuri cha pekee hivi kwamba anakosa kufikiria jambo la maana zaidi. Ni jambo gani hilo?

Yesu alifurahia ukarimu wa Martha, na alijua kwamba Martha alikuwa mwenye upendo na nia nzuri

11, 12. Namna gani Yesu anamushauri Martha kwa upole?

11 Yesu, Mwana muzaliwa​-pekee wa Yehova Mungu, iko hapo kwa Martha ili kufundisha kweli. Hakuna jambo la maana zaidi linaloweza kulinganishwa na kweli, hata chakula chake kizuri na matayarisho yake. Bila shaka, Yesu anahuzunika kuona namna Martha anavyopoteza nafasi hiyo ya pekee ya kujenga zaidi imani yake. Hata hivyo, Yesu anamuacha afanye yeye mwenyewe kile anachoamua. * Kwa hiyo, Martha hana haki ya kumuomba Yesu amulazimishe Maria apoteze pia nafasi hiyo.

12 Hivyo, kwa upole Yesu anamushauri Martha, anarudilia jina lake kwa utulivu ili kumutuliza asiwe mwenye kuhangaika, na anamuhakikishia kwamba hakuna lazima ya ‘kuhangaika na kusumbuka juu ya mambo mengi.’ Chakula chepesi kisichokuwa na mambo mengi kinatosha, zaidi sana wakati kuna karamu ya kiroho. Hivyo, hawezi kuondoa kwa Maria “fungu jema” ambalo amechagua, ni kusema, kufundishwa na Yesu!

13. Maneno ambayo Yesu alimuambia Martha yanaweza kutufundisha nini?

13 Habari hii fupi ya maisha ya nyumbani inaweza kutufundisha mambo mengi. Hatupaswe kuruhusu jambo lolote liwe la lazima zaidi kuliko kutosheleza ‘uhitaji wetu wa kiroho.’ (Mt. 5:3) Hata ikiwa tunapenda kuiga ukarimu wa Martha na bidii yake tunapokaribisha wageni, hatupaswe hata kidogo ‘kuhangaikia na kusumbukia’ mambo yasiyo ya maana na kupuuza mambo ya maana zaidi. Tunapokutana pamoja na waamini wenzetu, kusudi letu kabisa linapaswa kuwa kutiana moyo na kubadilishana zawadi za kiroho, lakini si kwa sababu ya chakula cha hali ya juu. (Soma Waroma 1:11, 12.) Tunaweza kupitisha pamoja wakati wenye kujenga hata ikiwa chakula ni chepesi.

Ndugu Mupendwa Anakufa, Kisha Anafufuliwa

14. Tunajua namna gani kama Martha alikubali shauri la Yesu na hivyo alituwekea mufano gani muzuri?

14 Je, Martha anakubali karipio lenye upole la Yesu na anapata somo? Jibu ni ndiyo. Wakati mutume Yohana anaanza kuandika habari yenye kufurahisha kumuhusu Lazaro, anatukumbusha hivi: ‘Basi Yesu alimupenda Martha na dada yake na Lazaro.’ (Yoh. 11:5) Miezi fulani ilikuwa imepita tangu Yesu kutembelea Bethania kama tulivyoona hapo juu. Ni wazi kwamba Martha hakumunungunikia Yesu, wala kumuwekea kinyongo kisha kushauriwa naye kwa upendo. Alikubali shauri hilo kwa moyo wote. Katika jambo hilo pia, Martha alituwekea mufano muzuri wa imani, kwa sababu mara kwa mara sisi wote tuna lazima ya shauri.

15, 16. (a) Martha anajikaza kufanya nini ndugu yake anapogonjwa? (b) Sababu gani tumaini la Martha na Maria halitimie?

15 Ndugu yake anapoanza kugonjwa, Martha anajikaza kumutunza. Anafanya yote anayoweza ili kumufariji na kumusaidia apone. Hata hivyo, hali ya Lazaro inaendelea kuwa mbaya. Kila siku dada zake wako karibu yake ili kumushugulikia. Wazia namna Martha anavyoutazama uso wenye kuchoka wa ndugu yake, anakumbuka miaka mingi waliyopitisha pamoja, furaha na taabu waliyopata pamoja!

16 Wakati Martha na Maria wanaona wazi kwamba hali ya Lazaro inazidi kuwa mbaya zaidi, wanamutumia Yesu habari. Wakati huo Yesu ni mwenye kuhubiri katika eneo linalopatikana kwenye mwendo wa siku mbili. Habari wanayomutumia Yesu ni fupi: ‘Bwana, ona! yule unayemupenda ni mugonjwa.’ (Yoh. 11:1,3) Wanajua kwamba Yesu anamupenda ndugu yao, na wana imani kwamba atafanya yote ili kumusaidia rafiki yake. Je, wana tumaini kwamba Yesu atafika mbele ya wakati? Ikiwa ni hivyo, basi tumaini lao halitimie kwa sababu Lazaro anakufa na Yesu hajafika.

17. Ni jambo gani ambalo Martha anajiuliza sana, na anafanya nini anapopata habari kwamba Yesu anakaribia muji?

17 Martha na Maria wanamuombolezea ndugu yao, wanatayarisha mazishi yake na wanapokea watu wa Bethania wanaokuja kuwafariji na wageni wengi kutoka maeneo jirani. Lakini, hawana habari yoyote kumuhusu Yesu. Inawezekana, kadiri wakati unavyopita, Martha anaendelea kujiuliza kwa nini Yesu hafike. Mwishowe, siku ine kisha Lazaro kufa, Martha anapata habari kwamba Yesu anakaribia kuingia katika muji. Sikuzote Martha ni mwanamuke mwenye bidii, hata katika kipindi hiki cha huzuni; anasimama, na bila kumuambia Maria, anakimbia kukutana na Yesu.—Soma Yohana 11:18-20.

18, 19. Martha anaonyesha kama ana tumaini gani, na sababu gani imani yake ni ya pekee?

18 Wakati Martha anamuona Yesu, anamuambia mambo ambayo yamewasumbua yeye na Maria kwa siku fulani: “Bwana, kama ungekuwa hapa ndugu yangu hangekufa.” Hata hivyo, Martha hakupoteza bado imani na tumaini. Anaongeza hivi: ‘Hata hivyo sasa ninajua kwamba mambo mengi kadiri unayomuomba Mungu, Mungu atakupa.’ Mara moja ili kutia nguvu imani ya Martha, Yesu anamuambia hivi: “Ndugu yako atafufuka.”—Yoh. 11:21-23.

19 Martha anawaza kama Yesu anazungumuzia ufufuo wa wakati ujao, kwa hiyo anajibu: “Ninajua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yoh. 11:24) Ana imani kabisa katika fundisho hilo la ufufuo. Viongozi fulani wa dini ya Kiyahudi wanaoitwa Masadukayo, walikuwa wenye kupinga fundisho hilo, ijapokuwa linaelezwa waziwazi katika Maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu. (Dan. 12:13; Mk. 12:18) Lakini Martha anajua kwamba Yesu alifundisha tumaini la ufufuo na pia aliwafufua watu, hata kama mupaka wakati huo hajawahi kumufufua mutu yeyote ambaye amekufa kwa muda murefu kama Lazaro. Martha hajue mambo ambayo yako karibu kutokea.

20. Eleza maana ya maneno ya Yesu yasiyoweza kusahaulika yanayopatikana katika andiko la Yohana 11:25-27, na pia maana ya jibu la Martha.

20 Ndipo Yesu anasema maneno haya yasiyoweza kusahaulika: “Mimi ndiye ufufuo na uzima.” Kwa kweli, Yehova Mungu amemupa Mwana wake mamlaka ya kufufua watu waliokufa duniani pote wakati ujao. Yesu anamuuliza Martha: “Je, unaamini hilo?” Ndipo Martha anatoa jibu ambalo tulizungumuzia mwanzoni mwa sura hii. Anaamini kwamba Yesu ndiye Kristo ao Masiya, kwamba ndiye Mwana wa Yehova Mungu, na ndiye ambaye manabii walitabiri kwamba atakuja duniani.—Yoh. 5:28, 29; soma Yohana 11:25-27.

21, 22. (a) Yesu anaonyesha namna gani kwamba anashiriki huzuni ya wale wanaofiwa? (b) Eleza namna ufufuo wa Lazaro unavyofanyika.

21 Je, Yehova Mungu na Yesu Kristo, Mwana wake, wanaiona imani kama hiyo ya Martha kuwa kitu cha maana? Mambo ambayo karibuni Martha atajionea yanatoa majibu yaliyo wazi kwa ulizo hilo. Martha anakimbia kumuita dada yake. Kisha anaona Yesu akiwa na huzuni sana anapozungumuza na Maria na watu wengi wanaoomboleza pamoja naye. Anaona namna Yesu anavyotokwa na machozi kwa sababu ya huzuni inayoletwa na kifo. Anasikia namna Yesu anavyotoa agizo ili jiwe linalofunga kaburi alimo ndugu yake liondolewe.​—Yoh. 11:28-39.

22 Kwa kuwa Martha ni mwanamuke asiyesita kuchukua hatua, anapinga, na anamuambia Yesu kwamba mwili unapaswa kuwa umeanza kunuka, kwa sababu Lazaro amekufa kumepita sasa siku ine. Yesu anamukumbusha hivi: “Je, sikukuambia kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu?” Martha anaamini na anaona utukufu wa Yehova Mungu. Papo hapo, Mungu anamupatia Mwana wake uwezo wa kumufufua Lazaro! Unaweza kuona kwamba huo ni wakati ambao Martha hangeweza kusahau maisha yake yote: Yesu anaita kwa sauti, ‘Lazaro, kuja huku inje!’; makelele inasikika kwa mbali ndani ya kaburi wakati Lazaro anainuka na kutembea polepole kuelekea mulango wa kaburi, akiwa bado amefungwa vitambaa vilivyotumiwa ili kuufunga mwili wake; Yesu anaagiza kwamba ‘wamufungue na kumuacha aende’; na bila shaka, Martha na dada yake Maria wanafurahi sana wanapokumbatiana na ndugu yao. (Soma Yohana 11:40-44.) Huzuni iliyokuwa katika moyo wa Martha imekwisha!

Martha alipewa zawadi kwa sababu ya imani yake katika Yesu wakati yeye na Maria waliona ndugu yao akifufuliwa

23. Yehova na Yesu wanataka kukufanyia nini, na wewe unapaswa kufanya nini?

23 Habari hiyo inaonyesha kwamba ufufuo wa watu waliokufa si jambo la kuwazia tu, ni fundisho la Biblia lenye kugusa moyo, ni jambo lililotokea kabisa wala si hadisi tu. (Ayu. 14:14, 15) Yehova na Mwana wake wanafurahia kuwapa zawadi watu wenye imani, kama walivyowafanyia Martha, Maria, na Lazaro. Wewe pia utapewa zawadi kama hiyo, ikiwa unafanya imani yako iwe yenye nguvu.

‘Martha Alikuwa Anahudumia’

24. Biblia inasema nini inapozungumuzia Martha kwa mara ya mwisho?

24 Mwanzoni mwa juma la mwisho la maisha ya Yesu hapa duniani, Biblia inamutaja tena Martha mara moja. Yesu anajua wazi hali ngumu ambayo itamupata karibuni, hivyo anachagua tena kukaa katika ile nyumba ya marafiki wake huko Bethania. Kutoka huko atatembea kilometre tatu mupaka Yerusalemu. Yesu na Lazaro wanakula katika nyumba ya Simoni mwenye ukoma, na hapo ndipo Biblia inazungumuzia Martha kwa mara ya mwisho; inasema hivi: ‘Martha alikuwa anahudumia.’—Yoh. 12:2.

25. Sababu gani makutaniko leo yamebarikiwa kuwa na dada walio kama Martha?

25 Kwa kweli, Martha alikuwa mwanamuke mwenye kutumika kwa bidii! Biblia inapomuzungumuzia kwa mara ya kwanza, yeye ni mwenye kufanya kazi, na inapomuzungumuzia kwa mara ya mwisho, tena ni mwenye kufanya kazi; alikuwa anafanya yote ambayo angeweza ili kuwashugulikia wengine. Makutaniko ya wafuasi wa Kristo leo yamebarikiwa kuwa na dada wenye bidii na wakarimu kama Martha, wanaojitoa sikuzote ili kuonyesha imani yao kwa matendo. Je, Martha aliendelea kufanya hivyo? Bila shaka. Alitenda kwa hekima na kwa hiyo imani yake ilimusaidia kuvumilia ijapokuwa matatizo.

26. Imani ya Martha ilimusaidia kufanya nini?

26 Kisha siku kidogo, Martha alipaswa kuvumilia kifo cha mateso mengi ambacho Yesu alipata. Zaidi ya hayo, wauaji walewale wanafiki ambao wamemuua Yesu, walikuwa wameazimia pia kumuua Lazaro, kwa kuwa ufufuo wa Lazaro ulitia nguvu imani ya wengi. (Soma Yohana 12:9-11.) Mwishowe, kifo kilivunja uhusiano wa upendo uliokuwa kati ya Martha na ndugu yake na pia dada yake. Hatujue kabisakabisa ikiwa hilo lilitokea wakati gani ao namna gani, lakini tunaweza kuwa hakika na jambo hili: imani yenye nguvu ya Martha ilimusaidia kuvumilia mupaka mwisho. Ndio sababu ni lazima Wakristo wa leo waige imani ya Martha.

^ fu. 11 Wayahudi wa wakati wa mitume hawakuruhusu wanawake wafundishwe mambo mbalimbali ya elimu. Wanawake walifundishwa tu kazi za nyumbani. Ndio sababu labda Martha aliona kama si jambo la kawaida kabisa mwanamuke kukaa karibu ya mwalimu ili kujifunza.