Hamia kwenye habari

Hali ya Kiroho Ni Nini? Je, Ninaweza Kuwa Mtu wa Kiroho Bila Kuwa Mshiriki wa Dini?

Hali ya Kiroho Ni Nini? Je, Ninaweza Kuwa Mtu wa Kiroho Bila Kuwa Mshiriki wa Dini?

Jibu la Biblia

 Neno hilo linatumiwa katika Biblia kufafanua tamaa yenye kina na utayari wa kumpendeza Mungu na kujifunza kufikiri kama anavyofikiri. Mtu wa kiroho hujitahidi kuishi kupatana na viwango vya Mungu na kufuata mwongozo Wake wa roho takatifu. aWaroma 8:5; Waefeso 5:1.

 Mara nyingi Biblia hufafanua hali ya kiroho kwa kueleza kuhusu matendo ya watu ambao hawana hali nzuri ya kiroho. Kwa mfano, tofauti na mtu wa kiroho, “mtu wa kimwili hayakubali mambo ya roho ya Mungu,” au mafundisho ya Mungu. (1 Wakorintho 2:14-16) Tofauti na watu wa kiroho, watu wa kimwili mara nyingi huchochea “wivu na mizozo” badala ya ukarimu na amani. (1 Wakorintho 3:1-3) Na wale ambao huwachongea na kuwatenganisha marafiki wa karibu kwa maneno yao wanaitwa watu “wasio na hali ya kiroho.”—Yuda 19; Methali 16:28. b

Katika makala hii

 Hali ya kiroho inatoka wapi?

 Tuna uwezo wa kuonyesha hali ya kiroho kwa sababu tumeumbwa kwa mfano wa Mungu. (Mwanzo 1:27) Hivyo, haishangazi kwamba watu wengi wanathamini na wangependa kujifunza kuhusu vitu ambavyo hawawezi kuona au kugusa.

 Tuna uwezo wa asili wa kuonyesha sifa kama zile za Yehova c Mungu, kwa mfano amani, rehema, na kutokuwa na ubaguzi. (Yakobo 3:17) Isitoshe, Mungu huwapa roho takatifu wale wanaojitahidi kutii amri zake.—Matendo 5:32.

 Kwa nini hali ya kiroho ni muhimu?

 Hali ya kiroho huongoza kwenye “uzima na amani.” (Waroma 8:6) Hizo ni zawadi zenye thamani kubwa kutoka kwa Mungu.

  •   Uzima: Mungu anaahidi kuwapa uzima wa milele watu walio na hali nzuri ya kiroho.—Yohana 17:3; Wagalatia 6:8.

  •   Amani: Hiyo ni amani kati yetu na Mungu. Wale wanaokazia fikira mahitaji yao ya kimwili ni maadui wa Mungu. (Waroma 8:7) Mbali na hilo, Mungu huwathawabisha wale wanaositawisha hali ya kiroho kwa kuwapa “amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote.” (Wafilipi 4:6, 7) Amani kama hiyo ya moyoni huwasaidia kupata furaha maishani.—Mathayo 5:3.

 Ninaweza kusitawishaje hali ya kiroho?

  •   Jifunze na utii amri za Mungu. Unaweza kufanya hivyo kwa kusoma Biblia, ambayo ina mawazo ya Mungu yaliyoandikwa na wanadamu ambao “[waliongozwa] na roho takatifu.” (2 Petro 1:21) Mambo unayojifunza yatakusaidia kumwabudu Mungu “kwa roho na kweli,” ukiongozwa na roho takatifu na kupatana na mapenzi ya Mungu.—Yohana 4:24.

  •   Sali upate msaada wa Mungu. (Luka 11:13) Mungu atakusaidia kuonyesha sifa zinazokutambulisha kuwa mtu wa kiroho. (Wagalatia 5:22, 23) Pia kusali kunaweza kukupa hekima ya kushughulika na changamoto za maisha.—Yakobo 1:5.

  •   Shirikiana na watu wa kiroho. Watakutia moyo uimarishe hali yako ya kiroho. (Waroma 1:11, 12) Tofauti na hilo, kushirikiana na watu ambao mawazo yao yanatofautiana na ya Mungu kunaweza kudhoofisha hali yako ya kiroho.—Yakobo 4:4.

 Je, ninahitaji dini ili kuwa mtu wa kiroho?

 Kuwa tu katika dini hakumfanyi mtu kuwa na hali ya kiroho. Biblia inasema hivi: “Ikiwa mtu yeyote anafikiri yeye ni mtu wa dini lakini haudhibiti kabisa ulimi wake, anaudanganya moyo wake, na ibada yake ni ubatili.”—Yakobo 1:26, maelezo ya chini.

 Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba watu wa kiroho humwabudu Mungu kwa njia anayokubali. Wanakiri kwamba kuna “roho moja” tu—roho takatifu ya Mungu. Roho hiyo huwachochea kumwabudu Mungu kama “mwili mmoja,” kikundi kilichopangwa kinachodumisha “roho ya umoja katika kifungo cha muungano cha amani.”—Waefeso 4:1-4.

 Maoni yasiyo sahihi kuhusu hali ya kiroho

 Maoni yasiyo sahihi: Hali ya kiroho inatia ndani njia ya maisha inayomsaidia mtu kujihisi ameridhika au kufikia uwezo wake kamili.

 Ukweli: Biblia inarejelea hali ya kiroho kuwa njia ya maisha inayoongozwa na mawazo ya Mungu. Hairejelei kujaribu kuwa mtu mwema bila kumtegemea Mungu. Watu wa kiroho huishi maisha yenye kuridhisha kwa sababu wanamkubali Yehova kuwa Muumba wao na wanaishi kupatana na kusudi lake.—Zaburi 100:3.

 Maoni yasiyo sahihi: Mtu anaweza kusitawisha hali ya kiroho kwa kujinyima kabisa vitu anavyopenda au kujiumiza mwili wake.

 Ukweli: Kuudhuru mwili ni “ibada ya kujitungia wenyewe” na ni aina ya kufikiri kwa kimwili. (Wakolosai 2:18, 23) Biblia inaonyesha kwamba kuishi maisha ya kiroho kunaleta shangwe, si uchungu.—Methali 10:22.

 Maoni yasiyo sahihi: Hali ya kiroho inaweza kupatikana kwa kujihusisha kwa njia yoyote na ulimwengu wa roho, kutia ndani kuwasiliana na roho.

 Ukweli: Aina moja ya kuwasiliana na roho ni imani ya kwamba roho za wafu zinaweza kuwasiliana na watu walio hai. Hata hivyo, Biblia inafundisha kwamba wafu hawajui lolote. (Mhubiri 9:5) Kuwasiliana na roho ni kuwasiliana na viumbe wa roho ambao wanampinga Mungu. Kuwasiliana na roho ni jambo linalomkasirisha Mungu na kunamzuia mtu kuwa na hali nzuri ya kiroho.—Mambo ya Walawi 20:6; Kumbukumbu la Torati 18:11, 12.

 Maoni yasiyo sahihi: Viumbe wote kiasili wana hali ya kiroho.

 Ukweli: Kila kitu ambacho Mungu aliumba kinamletea utukufu. (Zaburi 145:10; Waroma 1:20) Hata hivyo, viumbe wa Mungu wenye akili ndio tu wanaoweza kusitawisha hali ya kiroho. Tofauti na hilo, wanyama hutenda kwa silika na hawawezi kusitawisha urafiki na Mungu. Matendo yao huongozwa hasa na mahitaji yao ya kimwili. (2 Petro 2:12) Hivyo, Biblia inatofautisha hali ya kiroho na kufikiri au tabia ya kinyama.—Yakobo 3:15; Yuda 19.

a Maneno ya lugha ya awali ya Biblia yaliyotafsiriwa “roho” yana maana ya msingi ya “pumzi.” Maana pana inarejelea kitu ambacho hakiwezi kuonekana lakini ambacho kina nguvu inayodhihirika. Biblia inamfafanua Mungu kuwa Mtu Mkuu Zaidi wa Roho. Mtu wa kiroho huchagua kuongozwa na mapenzi ya Mungu na roho takatifu ya Mungu.

b Katika Biblia neno “kimwili” linapotumiwa linarejelea wanadamu ambao kufikiri kwao na matendo yao yanaongozwa hasa na mahitaji ya mwili au ya kimwili, bila kuzingatia viwango vya Mungu.

c Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa katika Biblia.—Zaburi 83:18.