Kulingana na Yohana 4:1-54

  • Yesu na mwanamke Msamaria (1-38)

    • Mwabudu Mungu “kwa roho na kweli” (23, 24)

  • Wasamaria wengi wamwamini Yesu (39-42)

  • Yesu amponya mwana wa ofisa (43-54)

4  Bwana alipojua kwamba Mafarisayo walikuwa wamesikia kuwa Yesu alikuwa akifanya na kubatiza+ wanafunzi wengi kuliko Yohana—  ingawa Yesu hakubatiza bali wanafunzi wake ndio waliokuwa wakibatiza—  akaondoka Yudea na kuelekea tena Galilaya.  Lakini alipaswa kupitia Samaria.  Basi akafika katika jiji moja la Samaria linaloitwa Sikari, lililokuwa karibu na shamba ambalo Yakobo alimpa Yosefu+ mwana wake.  Kisima cha Yakobo kilikuwa hapo.+ Basi Yesu, kwa kuwa alikuwa amechoka kwa sababu ya safari, akaketi kando ya kisima hicho.* Ilikuwa karibu saa sita.*  Mwanamke Msamaria akaja kuteka maji. Yesu akamwambia: “Naomba maji ninywe.”  (Kwa maana wanafunzi wake walikuwa wameenda jijini kununua chakula.)  Kwa hiyo mwanamke huyo Msamaria akamuuliza: “Wewe ni Myahudi, nami ni mwanamke Msamaria, unawezaje kuniomba maji ya kunywa?” (Kwa maana Wayahudi hawashirikiani na Wasamaria.)+ 10  Yesu akamjibu: “Kama ungejua zawadi ya bure inayotoka kwa Mungu+ na ni nani ambaye anakuambia, ‘Naomba maji ninywe,’ ungemwomba, naye angekupa maji yaliyo hai.”+ 11  Akamwambia: “Bwana, huna hata ndoo ya kutekea maji, na kisima ni kirefu. Basi, umeyatoa wapi hayo maji yaliyo hai? 12  Je, wewe ni mkuu kuliko babu yetu Yakobo, aliyetupatia kisima hiki ambacho yeye pamoja na wanawe na mifugo yake walikunywa maji yake?” 13  Yesu akamjibu: “Kila mtu anayekunywa maji haya atakuwa na kiu tena. 14  Yeyote atakayekunywa maji nitakayompa hatakuwa na kiu kamwe,+ kwa sababu maji ambayo nitampa yatakuwa kama chemchemi ya maji ndani yake, inayobubujika ili kumpa uzima wa milele.”+ 15  Yule mwanamke akamwambia: “Bwana, nipe maji hayo ili nisiwe na kiu tena wala nisiendelee kuja hapa kuteka maji.” 16  Yesu akamwambia: “Nenda ukamwite mume wako uje naye hapa.” 17  Mwanamke huyo akajibu: “Sina mume.” Yesu akamwambia: “Umesema kweli kwamba huna mume. 18  Kwa maana umekuwa na waume watano, na mwanamume uliye naye sasa si mume wako. Hapo umesema kweli.” 19  Yule mwanamke akamwambia: “Bwana, ninaona kwamba wewe ni nabii.+ 20  Mababu zetu waliabudu katika mlima huu, lakini ninyi mnasema tunapaswa kumwabudu Mungu huko Yerusalemu.”+ 21  Yesu akamwambia: “Mwanamke, niamini, saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu wala kule Yerusalemu. 22  Ninyi mnaabudu msichokijua;+ sisi tunaabudu tunachokijua, kwa sababu wokovu huanza kwa Wayahudi.+ 23  Hata hivyo, saa inakuja, nayo ipo sasa, ambayo waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana kwa kweli, Baba anawatafuta watu wa namna hiyo wamwabudu.+ 24  Mungu ni Roho,+ na wale wanaomwabudu lazima wamwabudu kwa roho na kweli.”+ 25  Huyo mwanamke akamwambia: “Ninajua kwamba Masihi anakuja, anayeitwa Kristo. Atakapokuja, atatutangazia mambo yote waziwazi.” 26  Yesu akamwambia: “Mimi ninayezungumza nawe, ndiye.”+ 27  Ndipo wanafunzi wake wakaja, wakashangaa kwa sababu alikuwa akiongea na mwanamke. Hata hivyo, hakuna yeyote aliyemuuliza: “Unatafuta nini?” au, “Kwa nini unaongea naye?” 28  Basi, yule mwanamke akauacha mtungi wake wa maji akaenda jijini na kuwaambia watu: 29  “Twendeni mkamwone mtu aliyeniambia kila kitu nilichofanya. Je, inawezekana kwamba yeye ndiye Kristo?” 30  Wakatoka jijini wakaenda kumwona Yesu. 31  Wakati huohuo wanafunzi walikuwa wakimhimiza: “Rabi,+ kula.” 32  Lakini akawaambia: “Nina chakula ambacho hamkijui.” 33  Kwa hiyo wanafunzi wakaambiana: “Hakuna mtu aliyemletea chakula, sivyo?” 34  Yesu akawaambia: “Chakula changu ni kufanya mapenzi ya yule aliyenituma+ na kuimaliza kazi yake.+ 35  Je, ninyi hamsemi kwamba bado kuna miezi minne kabla ya mavuno? Tazama! Ninawaambia: Inueni macho yenu mtazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.+ Tayari 36  mvunaji anapokea mshahara na anakusanya matunda kwa ajili ya uzima wa milele, ili mpandaji na mvunaji washangilie pamoja.+ 37  Basi, maneno haya ni ya kweli: Mmoja ni mpandaji na mwingine ni mvunaji. 38  Niliwatuma mkavune kile ambacho hamkufanyia kazi. Wengine wamefanya kazi, nanyi mmefaidika kutokana na kazi yao.” 39  Wasamaria wengi kutoka jiji hilo wakamwamini Yesu kwa sababu yule mwanamke alitoa ushahidi kwa kusema: “Aliniambia mambo yote niliyofanya.”+ 40  Basi Wasamaria walipomjia, wakamwomba akae pamoja nao, naye akakaa huko siku mbili. 41  Kwa hiyo, wengi zaidi wakaamini waliposikia mambo aliyosema , 42  nao wakamwambia yule mwanamke: “Hatuamini kwa sababu tu ya maneno yako; kwa maana sisi wenyewe tumesikia, na tunajua kwamba kwa hakika mtu huyu ndiye mwokozi wa ulimwengu.”+ 43  Baada ya siku hizo mbili akaondoka na kwenda Galilaya. 44  Hata hivyo, Yesu alitoa ushahidi kwamba nabii haheshimiwi katika nchi yake.+ 45  Kwa hiyo, alipofika Galilaya, Wagalilaya wakamkaribisha, kwa sababu walikuwa wameona mambo yote aliyofanya huko Yerusalemu kwenye sherehe,+ kwa maana wao pia walikuwa wameenda kwenye sherehe.+ 46  Kisha Yesu akaja tena Kana ya Galilaya, ambako alikuwa amegeuza maji kuwa divai.+ Basi kulikuwa na ofisa fulani wa mfalme ambaye mwana wake alikuwa mgonjwa huko Kapernaumu. 47  Mtu huyu aliposikia kwamba Yesu ametoka Yudea na kuja Galilaya, akamwendea na kumwomba ashuke kwenda kumponya mwanawe, kwa maana alikuwa karibu kufa. 48  Lakini, Yesu akamwambia: “Msipoona ishara na maajabu, hamtaamini kamwe.”+ 49  Yule ofisa wa mfalme akamwambia: “Bwana, twende kabla mwanangu hajafa.” 50  Yesu akamwambia: “Rudi nyumbani; mwanao yuko hai.”+ Yule mtu akaamini maneno ambayo Yesu alimwambia, akaondoka. 51  Lakini akiwa njiani akakutana na watumwa wake, wakamwambia kwamba mwanawe yuko hai.* 52  Kwa hiyo akawauliza saa ambayo alipata nafuu. Wakamjibu: “Alipona homa jana saa saba.”* 53  Kwa hiyo yule baba akajua ilikuwa saa ileile ambayo Yesu alimwambia: “Mwanao yuko hai.”+ Basi yeye na watu wote wa nyumbani kwake wakaamini. 54  Huo ulikuwa muujiza wa pili+ ambao Yesu alifanya alipotoka Yudea na kwenda Galilaya.

Maelezo ya Chini

Au “chemchemi hiyo; au mabubujiko hayo.”
Yaani, karibu saa 6 mchana.
Au “alikuwa anapata nafuu.”
Yaani, karibu saa 7 mchana.