Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwa na Uhusiano Mzuri na Mungu

Kuwa na Uhusiano Mzuri na Mungu

Kama ilivyoelezwa katika makala ya kwanza ya gazeti hili, watu wengi wanaiona Biblia kuwa kitabu kitakatifu. Wanatambua kwamba wanapoisoma na kutumia mwongozo wake maishani, wanahisi wakiwa karibu na Mungu na wanaelewa kusudi la maisha.

Biblia inatumia maneno “hali ya kiroho” kurejelea mtazamo wa mtu kuelekea maisha. (Yuda 18, 19) Mtu asiyetaka kuongozwa na Mungu hutegemea maoni yake mwenyewe. Kwa upande mwingine, mtu anayetaka kuongozwa na Mungu hufuata viwango vilivyowekwa na Mungu.—Waefeso 5:1.

TUMAINI

KANUNI YA BIBLIA: “Ukivunjika moyo nyakati za taabu, nguvu zako zitakuwa chache.” —Methali 24:10, maelezo ya chini.

INAMAANISHA NINI: Kuvunjika moyo kunaweza kufanya tukose nguvu tunazohitaji ili kukabiliana na matatizo ya maisha. Kwa upande mwingine, tumaini linaweza kutupatia nguvu za kusonga mbele. Tunaweza kufarijika kwa kujua kwamba matatizo tunayokabili ni ya muda mfupi, na bila shaka tunatarajia baada ya dhiki tutapata faraja.

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA: Jitahidi kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu wakati ujao. Badala ya kuogopa mambo ambayo huenda yakatokea, au kusubiri hadi wakati mambo yatakuwa shwari, chukua hatua ili kutimiza malengo yako. Bila shaka “matukio yasiyotarajiwa” yanaweza kutokea. (Mhubiri 9:11) Hata hivyo, mara nyingi mambo hayawi mabaya kama tulivyofikiri. Ndiyo sababu Biblia inatumia mfano wa kilimo inaposema: “Panda mbegu zako asubuhi na usipumzishe mkono wako mpaka jioni; kwa maana hujui ni mbegu gani itakayofanikiwa, hii au ile, au ikiwa zote mbili zitafanikiwa.”—Mhubiri 11:6.

MAJIBU YA MASWALI MUHIMU KUHUSU MAISHA

KANUNI YA BIBLIA: “Nipe uelewaji . . . Neno lako ni kweli.”​—Zaburi 119:144, 160.

INAMAANISHA NINI: Biblia inatupatia majibu ya maswali ambayo huenda kila mtu hujiuliza. Kwa mfano, ina majibu ya maswali kama vile

  • Tulitoka wapi?

  • Kwa nini tuliumbwa?

  • Inakuwaje mtu anapokufa?

  • Je, maisha yalikusudiwa kuwa mafupi hivi?

Mamilioni ya watu ulimwenguni pote wameboresha maisha yao kwa kuchunguza majibu ya Biblia kuhusu maswali hayo na mengine mengi.

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA: Chunguza kibinafsi mambo ambayo Biblia inafundisha. Mwombe Shahidi wa Yehova akusaidie kuielewa Biblia. Tembelea tovuti yetu ya jw.org. Unaweza pia kuhudhuria mikutano yetu ambayo kila mtu anakaribishwa na hakuna kiingilio.

KANUNI NYINGINE ZA BIBLIA

Tazama video Kwa Nini Ujifunze Biblia? kwenye jw.org. Inapatikana katika lugha zaidi ya 880

TAMBUA UHITAJI WAKO WA KUMJUA MUNGU.

“Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”​—MATHAYO 5:3.

JIFUNZE MENGI ZAIDI KUMHUSU MUNGU ANAYETAJWA KATIKA BIBLIA.

‘Mtafute Mungu . . . na kwa kweli umpate . . . kwa hakika hayuko mbali na kila mmoja wetu.’​—MATENDO 17:27.

SOMA BIBLIA NA UTAFAKARI UJUMBE WAKE.

“Mwenye furaha ni mtu ambaye . . . anapendezwa na sheria ya Yehova, * naye huitafakari sheria Yake mchana na usiku . . . Kila jambo analofanya litafanikiwa.”​—ZABURI 1:1-3, maelezo ya chini.

^ fu. 23 Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa katika Biblia.