Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

UIGE IMANI YAO | NOA

Alilindwa “Akiwa Salama Pamoja na Wengine Saba”

Alilindwa “Akiwa Salama Pamoja na Wengine Saba”

NOA na familia yake walijikusanya pamoja wakati mvua nyingi ilikuwa ikinyesha. Wazia ukiwaona akilini mwako, wakiwa katika giza, nyuso zao zinaangazwa na nuru ya taa kubwa ya mafuta, macho yao yako wazi wanaposikia maji ya mvua yakianguka juu ya safina na kumwangika pande zote za safina hiyo. Ni wazi kwamba kulikuwa na makelele makubwa ya maji ya mvua.

Noa alipotazama nyuso za watu wa familia yake ambao alipenda sana, ni kusema, bibi yake mwaminifu na watoto wake wanaume watatu hodari pamoja na bibi zao, bila shaka moyo wake ulijaa shukrani. Katika nyakati hizo ngumu, labda alifarijiwa kwa kuona watu ambao alipenda sana walikuwa pamoja naye ndani ya safina. Wote walikuwa salama kabisa. Bila shaka, alisali pamoja na familia yake ili kumushukuru Mungu, akiinua sauti yake ili waweze kusikia kwa sababu kulikuwa makelele ya mvua.

Noa alikuwa mwanaume mwenye imani kubwa. Imani ya Noa ndiyo ilimuchochea Yehova Mungu kumulinda Noa na familia yake. (Waebrania 11:7) Lakini je, hawakuhitaji tena kuwa na imani wakati mvua ilianza kunyesha? Hapana kabisa, wangehitaji sana sifa hiyo katika siku ngumu ambazo zilikuwa mbele yao. Sisi pia tunahitaji imani katika nyakati hizi zenye misukosuko ao mivurugo. Kwa hiyo, acheni tuone mambo ambayo tunaweza kujifunza kutokana na imani ya Noa.

‘SIKU 40 MUCHANA NA USIKU’

Inje ya safina, mvua iliendelea kunyesha kwa ‘siku 40 muchana na usiku.’ (Mwanzo 7:4, 11, 12) Maji yaliendelea kupanda, na kupanda tena na tena. Kadiri maji hayo yalikuwa yakipanda, Noa angeweza kuona kwamba Yehova Mungu alikuwa akiokoa wakati huohuo watu wenye haki na kuwaazibu waovu.

Garika ilikomesha uasi ambao ulianzishwa na malaika wabaya. Wakichochewa na roho ya Shetani ya kujifikiria mwenyewe, malaika wengi waliacha “makao yao yanayofaa” huko mbinguni ili kuja kuishi na wanawake hapa duniani, na wakazaa watoto waliokuwa warefu na wakubwa sana ambao waliitwa Wanefili. (Yuda 6; Mwanzo 6:4) Bila shaka, kwa sababu mwanadamu ndiye uumbaji muzuri zaidi kati ya uumbaji wa Yehova duniani, Shetani alifurahi sana wakati uasi uliongezeka, uasi huo uliongeza hesabu ya wanadamu waovu.

Hata hivyo, maji ya garika yalipoongezeka, malaika hao waasi walilazimika kuondoa miili yao ya wanadamu na kurudi mbinguni, na tangu wakati huo wakanyanganywa uwezo wa kuvaa tena miili ya wanadamu. Waliacha bibi zao na watoto wao wakufe na maji ya garika, pamoja na wanadamu wengine waovu.

Tangu siku za Enoko, karibu miaka mia saba mbele ya Noa, Yehova alikuwa amewaonya wanadamu kwamba atawaharibu waovu, wasiomuogopa. (Mwanzo 5:24; Yuda 14, 15) Tangu wakati wa Enoko, watu waliendelea kuwa waovu zaidi, wakiharibu dunia na kuijaza na jeuri. Sasa uharibifu ulikuwa juu yao. Je, Noa na familia yake walifurahia uharibifu huo wa watu waovu?

Hapana! Na hata Mungu mwenye rehema hakufurahi pia. (Ezekieli 33:11) Yehova alifanya yote aliyoweza ili kuwaokoa wanadamu wengi kadiri ilivyowezekana. Alimuamuru Enoko aonye watu, na alimuagiza Noa ajenge safina. Noa na familia yake walifanya kazi hiyo kubwa kwa makumi ya miaka, mbele ya macho ya watu. Zaidi ya hayo, Yehova alimuongoza Noa ili afanye kazi akiwa ‘muhubiri wa uadilifu [ao haki].’ (2 Petro 2:5) Kama Enoko aliyeishi miaka mingi mbele yake alivyofanya, Noa aliwaonya watu juu ya hukumu ambayo ilikuwa karibu kutokea juu ya ulimwengu. Je, watu walimusikiliza? Yesu, ambaye aliona matukio hayo akiwa mbinguni, baadaye alisema juu ya watu wa siku za Noa hivi: ‘Hawakujali mupaka garika ikaja na kuwafagilia mbali wote.’​—Mathayo 24:39.

Wazia namna hali ya Noa na familia yake ilivyokuwa katika siku 40 za kwanza kisha Yehova kufunga mulango wa safina. Mvua kubwa ilipoendelea kumwagika juu ya safina siku baada ya siku, inaelekea watu hao munane waliendelea kufanya mambo yaleyale kila siku ndani ya safina, ni kusema, kusaidiana, kutunza mahali waliishi ndani ya safina, kushugulikia mahitaji ya wanyama. Hata hivyo, wakati fulani, safina hiyo kubwa ilitikisika na kuyumba​-yumba. Safina ikaanza kuelea juu ya maji! Ikiwa yenye kuelea juu ya maji ambayo yalikuwa yakipanda, safina hiyo iliendelea kuinuliwa juu zaidi na zaidi, mupaka “ikawa inaelea juu ya dunia.” (Mwanzo 7:17) Hilo ni jambo la ajabu sana ambalo lilionyesha nguvu za Yehova, Mungu Mweza-Yote!

Ni wazi kwamba Noa alimushukuru Yehova sana, si kwa sababu tu alimulinda salama yeye na familia yake, lakini pia kwa sababu aliwaonyesha rehema kwa kuwatumia waonye watu ambao waliangamizwa inje ya safina. Labda miaka hiyo ya kazi ngumu haikuonekana kuwa yenye faida wakati huo. Watu hawakumusikiliza hata kidogo! Wazia jambo hilo. Inawezekana Noa alikuwa na ndugu, dada, wapwa wa wanaume na wanawake ambao walikuwa wazima mbele ya Garika kuanza; lakini, kati yao hakuna mutu mumoja aliyemusikiliza isipokuwa tu watu wa familia yake, ni kusema, bibi yake, watoto wake wanaume na bibi zao. (Mwanzo 5:30) Sasa, watu hao munane walipopata usalama ndani ya safina, bila shaka walifarijiwa kwa kukumbuka wakati wote ambao walitumia kuwahubiria watu ili kuwapa nafasi ya kuokoka.

Yehova hajabadilika tangu wakati wa Noa. (Malaki 3:6) Yesu Kristo alieleza kwamba nyakati zetu za leo zinafanana sana na “siku za Noa.” (Mathayo 24:37) Siku zetu ni kipindi chenye kutiwa alama, wakati wenye muvurugo mukubwa ambao utafikia mwisho wake katika uharibifu wa ulimwengu huu muovu. Leo, watu wa Mungu pia wanatoa ujumbe wa kuonya wale wote wanaotaka kusikiliza. Wewe utasikiliza ujumbe huo? Ikiwa umekwisha kukubali kweli ya ujumbe huo wenye kuokoa uzima, je, wewe pia utajiunga na wale ambao wanatolea wengine ujumbe huo? Noa na familia yake walituwekea sisi wote mufano.

“WALICHUKULIWA SALAMA KUPITIA MAJI”

Safina ilipokuwa ikiyumba​-yumba juu ya maji hayo mengi sana yaliyokuwa kama bahari yenye mawimbi, wale waliokuwa ndani walisikia mulio wa mbao hizo kubwa ambazo zilitumiwa kujenga safina zilizokuwa zikilia sawa vile zitavunjika. Je, Noa aliogopa mawimbi hayo makubwa ao kuogopa kwamba safina inaweza kuvunjika? Hapana. Leo, watu walio na mashaka juu ya Biblia wanaweza kuwazia hivyo, lakini Noa hakuwa na mashaka. Biblia inasema hivi: ‘Kwa imani Noa . . . alijenga safina.’ (Waebrania 11:7) Imani katika mambo gani? Yehova alikuwa amefanya agano, ao mapatano pamoja na Noa kwamba atamulinda salama yeye na wote waliokuwa pamoja naye ndani ya safina ili wasikufe na Garika. (Mwanzo 6:18, 19) Je, yule ambaye aliumba ulimwengu wote, dunia, na viumbe vyote vilivyo hai juu ya dunia hangeweza kulinda chombo hicho kikubwa kisivunjike na kuzama? Bila shaka! Noa alikuwa na sababu nzuri ya kutumainia kwamba Yehova atatimiza ahadi zake. Na, kwa kweli, yeye na familia yake “walichukuliwa salama kupitia maji.”​—1 Petro 3:20.

Mwishowe, kisha siku 40 muchana na usiku, mvua iliisha. Kwenye kalenda yetu, ilikuwa siku fulani katika Mwezi wa 12, mwaka wa 2370 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu. Lakini, familia hiyo iliyokuwa ndani ya safina ingepatwa bado na mambo mengine. Chombo hicho ambacho kilikuwa na viumbe wengi walio hai kilielea ao kuenda huku na huku juu ya maji mengi yaliyokuwa kama bahari, na kilielea hata juu ya milima mirefu iliyokuwa imefunikwa na maji. (Mwanzo 7:19, 20) Tunaweza kumufikiria Noa akipanga kazi ngumu pamoja na watoto wake Shemu, Hamu, na Yafethi ili waweze kuwalisha wanyama wote, kuwasafisha na kuwatunza vizuri. Bila shaka, Mungu yuleyule aliyewafanya wanyama wa porini kuwa watulivu sana ili wakubali kuingia katika safina angeweza kuwafanya wabaki katika hali hiyo ya utulivu muda wote wa Garika. *

Ni wazi kwamba Noa alilinda akilini habari zote juu ya matukio hayo. Habari hizo zinaonyesha wakati mvua ya Garika ilianza na wakati iliisha. Pia habari hizo zinaonyesha kwamba maji yalifunika dunia muda wa siku 150. Mwishowe, maji yalianza kupunguka. Siku moja ambayo haingeweza kusahauliwa, safina ilitua kwenye “milima ya Ararati,” inayopatikana katika inchi inayoitwa leo Uturuki. Inawezekana hilo lilifanyika katika Mwezi wa 4, mwaka wa 2369 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu. Siku 73 kisha hapo, katika Mwezi wa 6, vichwa vya milima vikaanza kuonekana. Miezi mitatu kisha hapo, katika Mwezi wa 9, Noa aliamua kuondoa sehemu fulani ya juu ya safina. Bila shaka, kazi hiyo ngumu ya kuondoa sehemu hiyo ya juu ilileta matokeo mazuri kwa sababu mwangaza na hewa nzuri vilianza kuingia ndani ya safina. Mbele ya kuondoa sehemu hiyo ya juu ya safina, Noa alianza pia kuchunguza hali ya inje ili kujua ikiwa kulikuwa na usalama na ikiwa sasa wangeishi inje. Alituma ndege anayeitwa kunguru ao kibombobombo, ambaye alienda na kurudi kwa muda fulani, labda alitua juu ya safina kisha kuenda na kurudi mara nyingi; kisha akatuma njiwa, ambaye alikuwa anaenda na kurudi kwa Noa mupaka alipopata mwishowe nafasi ya kutua.​—Mwanzo 7:24–8:13.

Bila shaka, Noa aliongoza familia yake katika ibada hata katika nyakati ngumu sana

Bila shaka, mambo ya kiroho yaliendelea kuwa ya maana zaidi katika maisha ya Noa. Tunaweza kuwazia akilini familia hiyo ikikusanyika pamoja kwa ukawaida ili kusali pamoja na kuzungumuza juu ya Baba yao wa mbinguni aliyewalinda. Noa alimutegemea Yehova kila mara alipochukua uamuzi wa maana. Hata wakati Noa aliona kwamba dunia ilikuwa ‘imekauka,’ kisha kufanya zaidi ya mwaka mumoja ndani ya safina, hakufungua mulango na kutoa watu na wanyama waliokuwa ndani ya chombo hicho. (Mwanzo 8:14) Lakini alingoja agizo kutoka kwa Yehova!

Wale ambao ni baba wa familia leo wanaweza kujifunza mambo mengi kutokana na mwanaume huyo mwaminifu. Alikuwa na utaratibu, bidii, uvumilivu, na alilinda wale wote waliokuwa chini ya uongozi wake. Zaidi ya yote, aliona kwamba kufanya mapenzi ya Yehova ndilo jambo la maana zaidi kuliko mambo mengine yote. Ikiwa tunaiga imani ya Noa katika mambo hayo, tutawaletea baraka watu wote ambao tunawapenda.

‘TOKA INJE YA SAFINA’

Mwishowe, Yehova akatoa agizo. Akamuambia Noa hivi: ‘Toka inje ya safina, wewe na muke wako na wana wako na wake za wana wako pamoja nawe.’ Kwa kumutii Yehova, familia ikatoka inje na wanyama wote wakafuata. Walitoka namna gani? Je, walitoka ovyoovyo? Hapana! Habari hiyo ya Biblia inasema kwamba ‘kulingana na familia zao walitoka inje ya safina.’ (Mwanzo 8:15-19) Walipokuwa inje ya safina, wakivuta hewa nzuri ya milima na wakiangalia mbali kwenye maeneo yaliyoinuka ya milima ya Ararati, Noa na familia yake waliona dunia ambayo ilikuwa imesafishwa. Wanefili, malaika waasi, na watu wote waovu walikuwa hawako tena, na hata jeuri ilikuwa imekwisha! * Wanadamu walikuwa na nafasi ya kuanza maisha mapya.

Noa alijua jambo la kufanya. Jambo la kwanza ambalo alifanya lilikuwa kumuabudu Mungu. Alijenga mazabahu na akachukua wanyama fulani ambao Mungu aliona kuwa safi, kati ya wale ambao waliingizwa “saba saba” ndani ya safina, na akamutolea Yehova zabihu ya kuteketezwa. (Mwanzo 7:2; 8:20) Je, ibada hiyo ilimupendeza Yehova?

Biblia inajibu ulizo hilo kwa maneno haya yenye kutia moyo: “Yehova akaanza kunusa harufu ya kutuliza.” Mungu hakusikia tena hali ya uchungu ambayo alisikia wakati wanadamu walijaza jeuri duniani. Lakini sasa alijisikia kuwa mwenye kutulia na mwenye furaha kwa kuona familia ya waabudu waaminifu duniani ambao walikuwa wameazimia kuendelea kufanya mapenzi yake. Yehova hakutazamia Noa na familia yake wawe wakamilifu. Andiko hilohilo linaendelea kusema hivi: ‘Mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mubaya tangu ujana wake na kuendelea.’ (Mwanzo 8:21) Kisha tukio hilo, fikiria namna Yehova alionyesha uvumilivu wake wenye rehema kwa wanadamu.

Mungu aliondoa laana juu ya udongo. Tangu wakati Adamu na Eva waliasi, Mungu alitangaza laana hiyo ambayo ilifanya kazi ya kulima udongo iwe ngumu. Lameki, baba ya Noa, alimupatia mwana wake jina la Noa, jina ambalo labda linamaanisha “Pumuziko,” ao “Faraja,” na akatabiri kwamba mwana wake angeongoza wanadamu kwenye wakati wa pumuziko kutokana na laana hiyo. Ni wazi kwamba Noa alifurahi alipojua kuwa angeona sasa utimizo wa unabii huo na kwamba dunia ingetoa sasa mazao mengi wakati wangeulima udongo. Kwa sababu hiyo, Noa akaanza kazi ya kulima bila kukawia!​—Mwanzo 3:17, 18; 5:28, 29; 9:20.

Noa na familia yake walitoka katika safina na kurudi katika dunia iliyosafishwa

Wakati huohuo, Yehova aliwapatia wazao wote wa Noa sheria fulani zilizokuwa wazi na nyepesi ili ziwaongoze katika maisha yao. Sheria hizo zilitia ndani sheria iliyokataza kuua na kutumia damu vibaya. Pia, Mungu alifanya agano pamoja na wanadamu, na akaahidi kwamba hangeleta tena garika ili kuharibu viumbe wote ambao wanaishi duniani. Ili kuhakikisha kwamba atatimiza ahadi yake, Yehova aliwapa wanadamu ishara ya kwanza ya utukufu wake, ni kusema, aliweka upinde wa mvua katika mawingu. Mupaka leo hii, kila upinde wa mvua ambao tunaona unatufariji na kutukumbusha ahadi ambayo Yehova alitoa kwa upendo.​—Mwanzo 9:1-17.

Ikiwa habari juu ya Noa ilikuwa hadisi ya kuwazia tu, habari hiyo haingeendelea kuzungumuziwa kisha upinde huo wa mvua. Lakini Noa ni mutu ambaye aliishi kwelikweli, na maisha yake yalikuwa na magumu mengi. Kwa kuwa wakati huo watu waliishi miaka mingi, mwanaume huyo mwaminifu alipaswa kuvumilia miaka mingine 350 kisha garika, na muda wa miaka hiyo alipatwa na mambo ambayo yalimuletea uchungu mwingi. Alifanya kosa nzito wakati alilewa pombe, lakini kosa hilo liliongezeka wakati Kanaani, mujukuu wake alifanya zambi nzito zaidi, ni kusema, zambi ambayo ililetea familia ya Kanaani matokeo yenye kuhuzunisha. Noa aliishi miaka mingi na aliona wakati wazao wake walitenda zambi nzito kama vile kuabudu sanamu na jeuri katika siku za Nimrodi. Hata hivyo, jambo la kufurahisha ni kwamba, Noa aliona Shemu, mwana wake, akionyesha familia yake mufano muzuri wa imani.​—Mwanzo 9:21-28; 10:8-11; 11:1-11.

Kama vile Noa, tunahitaji kubakia waaminifu ijapokuwa tunapatwa na magumu. Wakati watu wengine wanakataa kumuamini Mungu wa kweli ao hata wanaacha kumutumikia, tunahitaji kuendelea kuwa waaminifu kama Noa. Yehova anapendezwa sana na watu ambao wanabaki waaminifu ijapokuwa magumu. Kama Yesu Kristo alivyosema, ‘yule ambaye atavumilia mupaka mwisho ndiye atakayeokolewa.”​—Mathayo 24:13.

^ Watu fulani wamesema kuwa kuna uwezekano wa kwamba Mungu alifanya wanyama hao walale usingizi muzito, unaofanana na ule wa wanyama fulani wanaolala usingizi muzito wakati wa kipindi cha baridi, na kwamba kwa kuwatia katika hali hiyo ya usingizi, Mungu alifanya wanyama hao wasihitaji kula chakula kingi. Iwe Mungu alifanya hivyo ao hapana, bila shaka alitimiza ahadi yake, kwa kuwalinda salama na kuwaokoa watu na wanyama wote ambao walikuwa ndani ya safina.

^ Pia, hapakuwa tena na alama yoyote ambayo ilionyesha mahali ambapo Bustani ya Edeni ilikuwa, bustani hiyo ilikuwa imefutiliwa mbali na maji ya Garika. Ikiwa ni hivyo, basi ni wazi kwamba makerubi waliokuwa wanalinda mwingilio wa bustani hiyo walikuwa sasa na uhuru wa kurudi mbinguni, na mugawo wao uliodumu miaka 1 600 ulikuwa umefikia sasa mwisho wake.​—Mwanzo 3:22-24.