Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA MBILI

Alifarijiwa na Mungu Wake

Alifarijiwa na Mungu Wake

1, 2. Ni mambo gani yaliyotukia katika siku ya pekee maishani mwa Eliya?

ELIYA alikimbia katika mvua huku giza likiongezeka. Ingawa hakuwa na nguvu za ujana, bado alihitaji kukimbia mwendo mrefu ili afike Yezreeli. Hata hivyo, alikimbia bila kuchoka, kwa kuwa “mkono wa Yehova” ulikuwa juu yake. Kwa kweli, hakuwa amewahi kuwa na nguvu kama hizo. Nguvu hizo zilimwezesha kuwapita farasi waliokuwa wakivuta gari la Mfalme Ahabu!​—Soma 1 Wafalme 18:46.

2 Sasa, alihitaji kukimbia mwendo mrefu. Wazia mvua ikimpiga Eliya usoni huku akikimbia na kutafakari matukio ya siku hiyo ya pekee maishani mwake. Bila shaka, huo ulikuwa ushindi mkubwa kwa Mungu wa Eliya, Yehova, na ibada ya kweli. Katika giza la dhoruba hiyo, Eliya hangeweza kuuona Mlima Karmeli uliokuwa nyuma yake, ambapo Yehova alikuwa amemtumia kuangamiza kimuujiza ibada ya Baali. Mamia ya manabii wa Baali walikuwa wamefunuliwa kuwa wadanganyifu na wakauawa. Kisha, Eliya akasali kwa Yehova ili amalize ukame ambao ulikuwepo kwa miaka mitatu na nusu. Nayo mvua ikanyesha!​—1 Fal. 18:18-45.

3, 4. (a) Kwa nini huenda Eliya alikuwa na matumaini mengi alipokuwa akielekea Yezreeli? (b) Tutachunguza maswali gani?

3 Alipokuwa akikimbia zile kilomita 30 kwenda Yezreeli, huenda Eliya alikuwa na matazamio mengi. Labda aliwazia kwamba kungekuwa na mabadiliko makubwa. Ahabu alipaswa kubadilika! Baada ya matukio aliyojionea, kwa kweli Ahabu hangekuwa na la kufanya ila kuacha ibada ya Baali; kumdhibiti Yezebeli malkia wake; na kuacha kuwatesa watumishi wa Yehova.

“Eliya . . . akakimbia mbele ya Ahabu mpaka Yezreeli”

4 Ni jambo la kawaida kuwa na matumaini mambo yanapotuendea vizuri. Huenda tukawazia kwamba hali yetu itazidi kuwa bora na hata kufikiri matatizo yetu yamekwisha. Haishangazi ikiwa Eliya alihisi hivyo, kwa sababu “alikuwa mtu mwenye hisia kama zetu.” (Yak. 5:17) Hata hivyo, matatizo ya Eliya hayakuwa yamekwisha. Kwa kweli, baada ya saa chache tu Eliya angekuwa na woga mwingi na kushuka moyo sana hivi kwamba angetamani kufa. Ni nini kilichotokea, na Yehova alimsaidiaje nabii wake aimarishe imani na ujasiri wake? Acheni tuone.

Mambo Yabadilika Ghafla!

5. Baada ya matukio kwenye Mlima Karmeli, je, Ahabu alijifunza kumheshimu Yehova zaidi, na tunajuaje hilo?

5 Ahabu alipofika kwenye makao yake ya kifalme huko Yezreeli, je, alionyesha kwamba alikuwa amebadilika? Tunasoma hivi: “Ahabu akamwambia Yezebeli mambo yote ambayo Eliya alikuwa amefanya na mambo yote kuhusu namna alivyowaua manabii wote kwa upanga.” (1 Fal. 19:1) Ona kwamba Ahabu aliposimulia matukio ya siku hiyo, hakumtaja Yehova, Mungu wa Eliya. Ahabu aliona matukio ya kimuujiza ya siku hiyo kwa maoni ya kibinadamu, kama mambo “ambayo Eliya alikuwa amefanya.” Kwa kweli, hakuwa amejifunza kumheshimu Yehova Mungu. Naye mke wake mkatili alifanya nini?

6. Yezebeli alimtumia Eliya ujumbe gani, na ulimaanisha nini?

6 Yezebeli alikasirika sana! Akiwa amewaka hasira, alimtumia Eliya ujumbe huu: “Miungu na ifanye hivyo, nayo izidishe jambo hilo, ikiwa wakati kama huu hapo kesho sitaifanya nafsi yako iwe kama nafsi ya kila mmoja wao!” (1 Fal. 19:2) Huo ulikuwa ujumbe wenye kutisha. Ni kama Yezebeli alikuwa anaapa kwamba yeye mwenyewe anapaswa kufa ikiwa hatakuwa amemuua Eliya kufikia siku iliyofuata, ili kulipiza kisasi kwa ajili ya manabii wa Baali. Wazia Eliya akiamshwa kutoka usingizini, katika chumba cha kulala cha hali ya chini huko Yezreeli usiku huo wenye dhoruba kali, na kupewa ujumbe wenye kuogopesha kutoka kwa malkia. Ujumbe huo ulimwathirije?

Alemewa na Woga na Kuvunjika Moyo

7. Ujumbe wa Yezebeli ulimwathirije Eliya, naye alifanya nini?

7 Ikiwa Eliya alifikiri kwamba vita dhidi ya ibada ya Baali vilikuwa vimekwisha, mara moja alitambua kwamba haikuwa hivyo. Yezebeli hakuwa amebadilika. Tayari manabii wengi waaminifu walioishi wakati huo walikuwa wameuawa kwa agizo lake, na sasa, ilionekana kuwa zamu ya Eliya. Ujumbe wa Yezebeli ulimwathirije Eliya? Biblia inasema: ‘Eliya aliogopa.’ Je, Eliya aliwazia jinsi Yezebeli alivyokuwa anapanga kumuua kikatili? Ikiwa aliendelea kufikiria mambo kama hayo, basi alipoteza ujasiri wake. Vyovyote vile, Eliya “[alianza] kwenda kwa ajili ya nafsi yake”—alikimbia ili kuokoa uhai wake.​—1 Fal. 18:4; 19:3.

Ikiwa tunataka kudumisha ujasiri wetu, hatupaswi kuendelea kufikiria hatari tunazoogopa

8. (a) Petro alikabili tatizo gani lililofanana na tatizo la Eliya? (b) Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa Eliya na Petro?

8 Eliya hakuwa mtumishi pekee wa Yehova aliyelemewa na woga. Miaka mingi baadaye, mtume Petro alipatwa na tatizo kama hilo. Kwa mfano, Yesu alipomwezesha kutembea juu ya maji, mtume huyo alianza ‘kuitazama ile dhoruba ya upepo.’ Hivyo, Petro akapoteza ujasiri na akaanza kuzama. (Soma Mathayo 14:30.) Kwa hiyo, mfano wa Petro na Eliya unatufundisha jambo muhimu. Ikiwa tunataka kudumisha ujasiri wetu, hatupaswi kuendelea kufikiria hatari tunazoogopa. Tunahitaji kukazia fikira Chanzo cha tumaini na nguvu zetu.

“Inatosha!”

9. Eleza jinsi safari ya Eliya ilivyokuwa na hisia zake alipokuwa akikimbia.

9 Kwa sababu ya woga, Eliya alikimbia umbali wa kilomita 150 kwenda kusini-magharibi, kwenye mji wa Beer-sheba, uliokuwa karibu na mpaka wa kusini wa Yuda. Alimwacha mtumishi wake huko na akaingia nyikani peke yake. Simulizi hilo linasema kwamba alienda “safari ya siku moja,” na tunaweza kuwazia akianza safari hiyo asubuhi, bila chakula wala vitu vingine muhimu. Akiwa ameshuka moyo na kujawa na woga, alitembea katika eneo hilo kavu na lenye mawemawe huku akichomwa na jua kali. Jua lilipoanza kutua jioni, Eliya aliishiwa na nguvu. Akiwa amechoka, alikaa chini ya mti wa mretemu, mahali pekee ambapo angeweza kupumzika katika eneo hilo kame.​—1 Fal. 19:4.

10, 11. (a) Sala ya Eliya kwa Yehova ilimaanisha nini? (b) Ukitumia maandiko yaliyo mwishoni mwa fungu, eleza hisia za watu wengine waliovunjika moyo.

10 Eliya alisali akiwa amekata tamaa kabisa. Aliomba afe. Alisema: “Mimi si bora kuliko mababu zangu.” Eliya alijua kwamba mababu zake walikuwa mavumbi na mifupa katika makaburi, na hawangeweza kumfanyia mtu jambo lolote zuri. (Mhu. 9:10) Kama wao, Eliya alijihisi hafai. Haishangazi kwamba alilia hivi: “Inatosha!” Hakuona sababu ya kuendelea kuishi.

11 Je, tunapaswa kushangaa kwamba mtumishi wa Mungu angevunjika moyo hivyo? Hapana. Biblia inataja wanaume na wanawake ambao walihuzunika sana hivi kwamba wakatamani kufa, baadhi yao ni Rebeka, Yakobo, Musa, na Ayubu.​—Mwa. 25:22; 37:35; Hes. 11:13-15; Ayu. 14:13.

12. Unawezaje kuiga mfano wa Eliya unapovunjika moyo?

12 Leo, tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” na haishangazi kwamba watu wengi, hata watumishi waaminifu wa Mungu, nyakati nyingine huvunjika moyo. (2 Tim. 3:1) Ukikabili hali ngumu kama hiyo, iga mfano wa Eliya: Mweleze Mungu yote yaliyo moyoni mwako. Yehova ni “Mungu wa faraja yote.” (Soma 2 Wakorintho 1: 3, 4.) Je, alimfariji Eliya?

Yehova Amtegemeza Nabii Wake

13, 14. (a) Kupitia malaika, Yehova alionyeshaje kwamba alimjali nabii wake aliyekuwa na wasiwasi? (b) Kwa nini inafariji kujua kwamba Yehova anajua hali za kila mmoja wetu, kutia ndani udhaifu wetu?

13 Unafikiri Yehova alihisije alipotazama kutoka mbinguni na kumwona nabii wake mpendwa akiwa amelala chini ya ule mti nyikani akiomba afe? Hatuhitaji kukisia. Baada ya Eliya kulala usingizi, Yehova alimtuma malaika wake. Malaika huyo alimwamsha Eliya kwa kumgusa kwa wororo na kumwambia: “Amka, ule.” Eliya aliamka na kula, kwa kuwa malaika alikuwa amemwandalia chakula chepesi, yaani, mkate na maji. Je, Eliya alimshukuru malaika huyo? Simulizi hilo linasema tu kwamba nabii huyo alikula na kunywa, kisha akaendelea kulala. Je, alikuwa amevunjika moyo sana asiweze kuzungumza? Vyovyote vile, malaika huyo alimwamsha tena, labda wakati wa mapambazuko. Akamhimiza tena Eliya, “Amka, ule,” na kuongezea maneno haya yenye kushangaza, “kwa maana safari ni ndefu mno kwako.”​—1 Fal. 19:5-7.

14 Kwa sababu ya uwezo aliopewa na Mungu, malaika huyo alijua Eliya alikuwa akielekea wapi. Pia, alijua safari hiyo ingekuwa ndefu sana na Eliya hangeiweza kwa nguvu zake mwenyewe. Inafariji kama nini kumtumikia Mungu ambaye anajua vizuri malengo na udhaifu wetu kuliko sisi wenyewe! (Soma Zaburi 103:13, 14.) Chakula hicho kilimsaidiaje Eliya?

15, 16. (a) Chakula ambacho Yehova alimwandalia Eliya kilimsaidia kufanya nini? (b) Kwa nini tunapaswa kuthamini jinsi Yehova anavyowategemeza watumishi wake leo?

15 Tunasoma hivi: “Akaamka, akala na kunywa, naye akazidi kwenda katika nguvu za chakula kile kwa siku 40, mchana na usiku, mpaka Horebu, mlima wa Mungu wa kweli.” (1 Fal. 19:8) Kama Musa aliyeishi karne sita kabla ya Eliya na pia Yesu aliyeishi karne kumi hivi baadaye, Eliya alifunga kwa siku 40, mchana na usiku. (Kut. 34:28; Luka 4:1, 2) Mlo huo mmoja haukumaliza matatizo yake yote, bali ulimwimarisha kimuujiza. Wazia mzee huyo akitembea kwa uchovu katika nyika isiyo na njia, siku baada ya siku, juma baada ya juma, kwa karibu mwezi mmoja na nusu!

16 Leo pia, Yehova anawategemeza watumishi wake, si kwa kuwalisha chakula cha kimwili kimuujiza, bali kwa njia muhimu hata zaidi. Anawaandalia watumishi wake chakula cha kiroho. (Mt. 4:4) Kujifunza kumhusu Mungu kupitia Neno lake na machapisho yanayotegemea Biblia, hutuimarisha kiroho. Huenda chakula hicho cha kiroho kisituondolee matatizo yetu yote, lakini kinaweza kutusaidia kuvumilia mambo ambayo huenda yangetulemea. Pia, kinatusaidia kupata “uzima wa milele.”​—Yoh. 17:3.

17. Eliya alienda wapi, na kwa nini mahali hapo palikuwa muhimu?

17 Eliya alitembea kilomita 320 hivi hadi kwenye Mlima Horebu. Palikuwa mahali muhimu, kwa sababu hapo ndipo Yehova Mungu alimtokea Musa kupitia malaika katika mti wa miiba uliokuwa ukiwaka moto na baadaye Yehova akafanya agano la Sheria na Waisraeli. Eliya alikaa katika pango.

Jinsi Yehova Alivyomfariji na Kumtia Nguvu Nabii Wake

18, 19. (a) Malaika wa Yehova aliuliza swali gani, na Eliya alijibuje? (b) Ni sababu gani tatu zilizomfanya Eliya ashuke moyo?

18 Huko Horebu, “neno” la Yehova—yaelekea kupitia malaika—lilimuuliza swali hili rahisi: “Una kazi gani hapa, Eliya?” Inaelekea swali hilo liliulizwa kwa upole, kwa kuwa Eliya alitumia nafasi hiyo kusema yote yaliyokuwa moyoni mwake. Na kwa kweli alijieleza! Alisema: “Nimekuwa na wivu kwelikweli kwa ajili ya Yehova Mungu wa majeshi; kwa maana wana wa Israeli wameliacha agano lako, wamezibomoa madhabahu zako, nao wamewaua manabii wako kwa upanga, hivi kwamba ni mimi peke yangu nimebaki; nao wanaanza kuitafuta nafsi yangu ili kuiondoa.” (1 Fal. 19:9, 10) Maneno ya Eliya yanaonyesha sababu tatu hivi zilizofanya avunjike moyo.

19 Kwanza, Eliya alihisi kwamba alifanya kazi bure. Ingawa kwa miaka mingi alikuwa na “wivu kwelikweli” katika kumtumikia Yehova, akitanguliza jina takatifu la Mungu na ibada yake, aliona kama hali zilizidi kuwa mbaya. Bado watu walikuwa hawana imani na wakaidi, na ibada ya uwongo ilizidi kuenea. Pili, Eliya alihisi upweke. “Mimi peke yangu nimebaki,” akasema, kana kwamba ndiye tu mtumishi wa Yehova aliyekuwa amebaki katika taifa hilo. Tatu, Eliya aliogopa. Tayari manabii wenzake walikuwa wameuawa, na alikuwa na hakika kwamba sasa ilikuwa zamu yake. Huenda haikuwa rahisi kwa Eliya kukubali kwamba jambo hilo lilimhangaisha, lakini hakuruhusu kiburi au aibu imzuie. Alimweleza Mungu yote yaliyokuwa moyoni mwake kupitia sala, na hivyo akawawekea mfano mzuri watu wote waaminifu.​—Zab. 62:8.

20, 21. (a) Fafanua mambo ambayo Eliya alijionea akiwa kwenye mwingilio wa pango juu ya Mlima Horebu. (b) Eliya alijifunza nini kutokana na maonyesho ya nguvu za Yehova?

20 Yehova alishughulikiaje woga na mahangaiko ya Eliya? Malaika alimwambia Eliya asimame kwenye mlango wa pango. Alitii, bila kujua ni nini kingefuata. Ghafla, upepo wenye nguvu ukavuma! Ni lazima upepo huo ulikuwa na kelele nyingi, kwa sababu ulivuma kwa nguvu sana hivi kwamba ukapasua milima na miamba. Wazia Eliya akijaribu kukinga macho yake akiwa ameshikilia vazi lake gumu lenye manyoya, upepo huo ulipokuwa ukivuma. Alihitaji pia kusimama imara ili asianguke, kwa kuwa ardhi ilianza kutikisika, eneo hilo lilikuwa limekumbwa na tetemeko! Kabla hajaelewa kilichokuwa kikiendelea, moto mkubwa ukapita, na akalazimika kurudi ndani ya pango ili ajikinge dhidi ya joto kali.​—1 Fal. 19:11, 12.

Yehova alitumia nguvu zake zisizo na kifani kumfariji na kumtia moyo Eliya

21 Katika kila tukio, simulizi hilo linasema kwamba Yehova hakuwa katika maonyesho hayo yenye kustaajabisha ya nguvu za asili. Eliya alijua kwamba Yehova hakuwa mungu wa kuwaziwa kama Baali, aliyetukuzwa na waabudu wake waliodanganywa kwamba alikuwa “mwendeshaji wa mawingu,” au mleta-mvua. Yehova ndiye Chanzo halisi cha nguvu zote za asili zisizo na kifani, lakini pia ni mkuu kuliko kitu chochote alichoumba. Hata mbingu haziwezi kumtosha! (1 Fal. 8:27) Mambo hayo yote yalimsaidiaje Eliya? Kumbuka alikuwa na woga. Kwa vile Yehova Mungu mwenye nguvu nyingi sana alikuwa upande wake, Eliya hakupaswa kuwaogopa Ahabu na Yezebeli!​—Soma Zaburi 118:6.

22. (a) Ile “sauti tulivu, ya chini” ilimhakikishiaje Eliya kwamba alikuwa mwenye thamani? (b) Huenda ni nani aliyekuwa chanzo cha ile “sauti tulivu, ya chini”? (Ona maelezo ya chini.)

22 Baada ya moto kupita, kimya kikatokea na Eliya akasikia “sauti tulivu, ya chini.” Ilimwomba ajieleze tena, naye akafanya hivyo, akieleza mahangaiko yake yote kwa mara ya pili. * Labda hilo lilimtuliza. Bila shaka, Eliya alitulizwa hata zaidi na maneno ambayo ile “sauti tulivu, ya chini” iliongezea. Yehova alimhakikishia Eliya kwamba alikuwa mwenye thamani sana. Jinsi gani? Mungu alimfunulia mengi kuhusu makusudi yake ya wakati ujao ya kuangamiza ibada ya Baali katika Israeli. Ni wazi kwamba kazi ya Eliya haikuwa ya bure, kwa kuwa bado Mungu angetimiza makusudi yake. Zaidi ya hayo, Eliya alihusika katika kutimiza makusudi hayo, kwa kuwa Yehova alimtuma na kumpa maagizo hususa.​—1 Fal. 19:12-17.

23. Yehova alishughulika na hisia za upweke za Eliya katika njia gani mbili?

23 Namna gani kuhusu upweke ambao Eliya alihisi? Yehova alifanya mambo mawili kuhusu hilo. Kwanza, alimwambia Eliya amtie mafuta Elisha awe nabii ambaye baadaye angechukua mahali pake. Mwanamume huyo kijana angeshirikiana na Eliya na kumsaidia kwa miaka mingi. Hilo lilimfariji sana! Pili, Yehova alifunua habari hii yenye kuchangamsha: “Nimewaacha watu elfu saba wabaki katika Israeli, magoti yote ambayo hayakumwinamia Baali, na kila kinywa ambacho hakikumbusu.” (1 Fal. 19:18) Eliya hakuwa peke yake. Ni lazima Eliya alifurahi sana kusikia kuhusu maelfu ya watu hao waaminifu ambao hawakumwabudu Baali. Walitaka Eliya aendelee na utumishi wake kwa uaminifu na kuwa kielelezo cha ushikamanifu thabiti kwa Yehova wakati huo mgumu. Kwa kweli Eliya aliguswa moyo sana kusikia maneno hayo kutoka kwa malaika wa Yehova, ile “sauti tulivu, ya chini” ya Mungu wake.

Biblia inaweza kuwa kama ile “sauti tulivu, ya chini” ikiwa tutaruhusu ituongoze

24, 25. (a) Leo, tunawezaje kusikiliza “sauti tulivu, ya chini” inayotoka kwa Yehova? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Eliya alikubali faraja aliyopewa na Yehova?

24 Kama Eliya, huenda tumeshangazwa na nguvu za asili zinazoonekana katika uumbaji. Uumbaji unafunua wazi nguvu za Muumba. (Rom. 1:20) Bado Yehova anataka kutumia nguvu zake nyingi kuwasaidia watumishi wake waaminifu. (2 Nya. 16:9) Hata hivyo, Mungu anasema nasi kwa ukamili zaidi kupitia Neno lake, Biblia. (Soma Isaya 30:21.) Kwa njia fulani, Biblia inaweza kuwa kama ile “sauti tulivu, ya chini” ikiwa tutaruhusu ituongoze. Yehova anatumia Biblia kuturekebisha, kututia moyo, na kutuhakikishia upendo wake.

25 Je, Eliya alikubali faraja ambayo Yehova alimpa kwenye Mlima Horebu? Bila shaka! Muda si muda, alianza tena kazi, akiwa nabii mwaminifu na jasiri aliyesimama imara dhidi ya uovu wa ibada ya uwongo. Ikiwa tutatafakari kwa uzito maneno yaliyoongozwa na roho ya Mungu, yaani, “faraja kutokana na Maandiko,” tutafanikiwa kuiga imani ya Eliya.​—Rom. 15:4.

^ fu. 22 Huenda ile “sauti tulivu, ya chini” ilikuwa ya malaika aliyetumiwa kupeleka “neno la Yehova” anayetajwa katika 1 Wafalme 19:9. Katika mstari wa 15 malaika huyo anatajwa kama “Yehova.” Huenda tukakumbuka mjumbe wa Yehova aliyetumiwa kuwaongoza Waisraeli nyikani na ambaye Mungu alisema hivi kumhusu: “Jina langu limo ndani yake.” (Kut. 23:21) Bila shaka, hatuwezi kusema jambo hili kwa uhakika, lakini tunapaswa kukumbuka kwamba kabla ya kuja duniani, Yesu alikuwa “Neno,” Msemaji maalumu wa Yehova kwa watumishi wake.—Yoh. 1:1.