Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA SABA

‘Aliendelea Kukua Akiwa na Yehova’

‘Aliendelea Kukua Akiwa na Yehova’

1, 2. Hali ilikuwaje Samweli alipokuwa akizungumza na Waisraeli, na kwa nini alihitaji kuwasaidia watubu?

SAMWELI aliwatazama watu wake. Taifa lilikuwa limekusanyika katika mji wa Gilgali, baada ya kuitwa na mtumishi huyo mwaminifu ambaye alikuwa ametumika akiwa nabii na mwamuzi kwa miaka mingi. Ulikuwa mwezi wa Mei au Juni kulingana na kalenda ya kisasa, na majira ya kiangazi yalikuwa yameanza. Mashamba ya ngano katika eneo hilo yalikuwa meupe tayari kuvunwa. Umati uliokuwa umekusanyika ulinyamaza. Samweli angewezaje kugusa mioyo yao?

2 Watu hawakuelewa uzito wa hali iliyowakabili. Walikuwa wamesisitiza kuwa na mtawala wa kibinadamu. Hawakujua kwamba walikuwa wameonyesha ukosefu mkubwa wa heshima kwa Mungu wao, Yehova, na pia kwa nabii wake. Kwa kweli, walikuwa wanamkataa Yehova kuwa Mfalme wao! Samweli angewasaidiaje watubu?

Maisha ya Samweli alipokuwa mvulana yanaweza kutufundisha mengi kuhusu kusitawisha imani katika Yehova hata tunapozungukwa na watu waovu

3, 4. (a) Kwa nini Samweli alitaja siku za ujana wake? (b) Kwa nini mfano wa imani ya Samweli ni muhimu kwetu leo?

3 Samweli alizungumza nao. Akawaambia: “Mimi nimezeeka nami nina mvi.” Nywele zake nyeupe ziliongeza uzito wa maneno yake. Kisha akasema: “Nimetembea mbele yenu tangu ujana wangu mpaka leo hii.” (1 Sam. 11:14, 15; 12:2) Ingawa Samweli alikuwa amezeeka hakuwa amesahau siku za ujana wake. Bado alikuwa akizikumbuka. Maamuzi aliyofanya akiwa kijana, yalimsaidia asitawishe imani na kujitoa ili amtumikie Mungu wake, Yehova.

4 Samweli alihitaji kusitawisha na kudumisha imani yake, ingawa mara nyingi alizungukwa na watu wasio na imani na wasio washikamanifu. Pia leo, si rahisi kusitawisha imani, kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu usio na imani na uliopotoka. (Soma Luka 18:8.) Hebu tuone mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mfano wa Samweli, tangu alipokuwa mvulana mdogo.

‘Alihudumu Mbele za Yehova Akiwa Mvulana’

5, 6. Kwa nini maisha ya utotoni ya Samweli hayakuwa ya kawaida, lakini wazazi wake walikuwaje na hakika kwamba angetunzwa?

5 Maisha ya utotoni ya Samweli hayakuwa ya kawaida. Muda mfupi baada ya kuachishwa kunyonya, labda akiwa na miaka mitatu hivi, alianza kutumika katika maskani ya Yehova huko Shilo, umbali wa zaidi ya kilomita 30 kutoka nyumbani kwao, Rama. Wazazi wake, Elkana na Hana, walimweka wakfu kwa Yehova kwa ajili ya utumishi wa pekee na hivyo akawa Mnadhiri katika maisha yake yote. * Je, hilo lilimaanisha kuwa wazazi wa Samweli hawakumpenda wala hawakutaka kumtunza?

6 Hapana! Walijua kuwa mwana wao angetunzwa huko Shilo. Bila shaka, Kuhani Mkuu Eli alihakikisha Samweli alitunzwa kwa sababu alifanya kazi karibu naye. Pia, kuna wanawake waliofanya kazi katika maskani, na yaelekea waliifanya kwa utaratibu fulani.​—Kut. 38:8; Amu. 11:34-40.

7, 8. (a) Kila mwaka, wazazi wa Samweli walimtiaje moyo kwa upendo? (b) Leo, wazazi wanajifunza nini kutoka kwa wazazi wa Samweli?

7 Zaidi ya hayo, Hana na Elkana hawakumsahau mtoto wao wa kwanza waliyempenda, ambaye alizaliwa sala ya Hana ilipojibiwa. Hana alikuwa amemwomba Mungu mtoto wa kiume, na kuahidi kwamba angemtoa ili amtumikie Mungu katika utumishi mtakatifu. Kila mwaka, Hana alipomtembelea Samweli alimpelekea koti jipya lisilo na mikono, ambalo angetumia katika utumishi wake kwenye maskani. Kwa kweli, mvulana huyo mdogo alifurahia sana kutembelewa. Bila shaka, Samweli alifurahi wazazi wake wenye upendo walipomtia moyo na kumpa mwongozo walipokuwa wakimfundisha kwamba lilikuwa pendeleo kubwa kumtumikia Yehova katika sehemu hiyo ya kipekee.

8 Leo, wazazi wanaweza kujifunza mengi kutoka kwa Hana na Elkana. Wazazi wanapowalea watoto wao, ni rahisi kukazia fikira mahitaji ya kimwili huku wakipuuza mahitaji ya kiroho. Lakini wazazi wa Samweli walitanguliza mambo ya kiroho, na hilo lilichangia sana sifa ambazo mwana wao Samweli alikuwa nazo alipokuwa mtu mzima.​Soma  Methali 22:6.

9, 10. (a) Eleza jinsi maskani ilivyokuwa, na jinsi kijana Samweli alivyohisi kuelekea mahali hapo patakatifu. (Ona pia maelezo ya chini.) (b) Huenda Samweli alikuwa na majukumu gani, na unafikiri leo vijana wanawezaje kumwiga?

9 Alipokuwa akiendelea kukua, tunaweza kuwazia mvulana huyo akitembea huku na huku kwenye vilima vilivyozunguka Shilo. Alipotazama mji huo kutoka mlimani na pia kutazama bonde lililokuwa upande mmoja wa mji huo, yaelekea moyo wake ulijaa furaha alipoona maskani ya Yehova. Kwa kweli, maskani hiyo ilikuwa takatifu. * Ilikuwa imejengwa miaka 400 hivi iliyopita chini ya mwongozo wa Musa, na palikuwa mahali pekee pa ibada safi ya Yehova duniani kote.

10 Kijana Samweli aliipenda sana maskani. Tunasoma hivi katika simulizi aliloandika baadaye: “Samweli alikuwa akihudumu mbele za Yehova, akiwa mvulana, amejifunga efodi ya kitani.” (1 Sam. 2:18) Koti hilo lisilo na mikono linaonyesha Samweli aliwasaidia makuhani kwenye maskani. Ingawa Samweli hakuwa wa jamii ya kikuhani, alikuwa na majukumu yaliyotia ndani kufungua milango ya ua wa maskani kila asubuhi na kumsaidia Eli aliyekuwa amezeeka. Samweli alifurahia pendeleo hilo, lakini baada ya muda alianza kutaabika moyoni. Kuna uovu uliokuwa ukiendelea ndani ya nyumba ya Yehova.

Hakuathiriwa na Upotovu Uliomzunguka

11, 12. (a) Ni makosa gani makubwa ambayo Hofni na Finehasi walifanya? (b) Ni uovu na upotovu gani ambao Hofni na Finehasi walifanya katika maskani? (Ona pia maelezo ya chini.)

11 Alipokuwa mdogo, Samweli alijionea waziwazi upotovu na uovu. Eli alikuwa na wana wawili, Hofni na Finehasi. Simulizi la Samweli linasema: “Wana wa Eli walikuwa watu wasiofaa kitu; hawakumtambua Yehova.” (1 Sam. 2:12) Mawazo mawili yaliyo katika mstari huo yanapatana. Hofni na Finehasi walikuwa “watu wasiofaa kitu” kwa kuwa hawakumheshimu Yehova. Walipuuza kabisa kanuni na sheria zake za uadilifu. Na hilo liliwaongoza kwenye dhambi.

12 Sheria ya Mungu ilitaja waziwazi majukumu ya makuhani na jinsi walivyopaswa kutoa dhabihu katika maskani. Mungu alifanya hivyo kwa sababu nzuri! Dhabihu hizo ziliwakilisha mpango wa Mungu wa kusamehe dhambi ili watu wawe safi machoni pake, na kustahili kupata baraka na mwongozo wake. Lakini Hofni na Finehasi waliwaongoza makuhani wenzao kutoheshimu dhabihu zilizokuwa zikitolewa. *

13, 14. (a) Watu wanyoofu waliathiriwaje na uovu kwenye maskani? (b) Eli alishindwaje kutimiza majukumu yake kama baba na kuhani mkuu?

13 Wazia kijana Samweli akitazama uovu huo mkubwa ukiendelea bila kurekebishwa. Aliona watu wangapi—kutia ndani wapole, maskini, na waliokandamizwa—wakija katika maskani takatifu huku wakitumaini kufarijiwa na kutiwa moyo kiroho, lakini wakaondoka wakiwa wamevunjika moyo, wameumia, au kuaibishwa? Na wazia jinsi alivyohisi alipotambua kuwa Hofni na Finehasi hawakutii sheria za Yehova kuhusu ngono, kwa kuwa walilala na wanawake fulani waliokuwa wakitumika katika maskani! (1 Sam. 2:22) Labda alitazamia Eli achukue hatua fulani kuhusu jambo hilo.

Bila shaka, Samweli alisumbuliwa sana na uovu wa Eli na wanawe

14 Eli ndiye angeweza kutatua tatizo hilo lililozidi kuwa baya. Akiwa kuhani mkuu, alikuwa na jukumu la kusimamia mambo kwenye maskani. Akiwa baba, alikuwa na daraka la kuwarekebisha wanawe. Matendo yao yaliwaumiza wao wenyewe na watu wengine wengi. Hata hivyo, Eli alishindwa kutimiza majukumu yake, kama baba na kuhani mkuu. Aliwakaripia wanawe kwa unyonge. (Soma 1 Samweli 2:23-25.) Lakini wanawe walipaswa kuadhibiwa vikali. Walikuwa wakitenda dhambi zilizostahili kifo!

15. Yehova alituma ujumbe gani mzito kwa Eli, na familia ya Eli iliitikiaje onyo hilo?

15 Hali ilizidi kuwa mbaya mpaka Yehova akatuma ujumbe mzito wa hukumu kwa Eli kupitia “mtu wa Mungu,” yaani, nabii fulani ambaye hatajwi jina. Yehova alimwambia Eli hivi: “Unaendelea kuwaheshimu wana wako kuliko mimi.” Hivyo, Mungu akatabiri kuwa wana waovu wa Eli wangekufa siku moja na kwamba familia ya Eli ingeteseka sana, na hata kupoteza pendeleo la kuwa makuhani. Je, onyo hilo kali lilibadili mambo katika familia hiyo? Simulizi hilo halitaji badiliko lolote.​—1 Sam. 2:27–3:1.

16. (a) Tunasoma mambo gani kuhusu maendeleo ya kijana Samweli? (b) Je, mambo hayo yanakutia moyo? Eleza.

16 Upotovu huo wote ulimwathirije kijana Samweli? Mara kwa mara simulizi hilo linataja mambo fulani mazuri, yaani, habari njema kuhusu ukuzi na maendeleo ya Samweli. Kumbuka kitabu cha 1 Samweli 2:18 kinasema Samweli alikuwa “akihudumu [kwa uaminifu] mbele za Yehova, akiwa mvulana.” Hata katika umri huo mchanga, Samweli alikazia fikira kumtumikia Mungu. Katika mstari wa 21 wa sura hiyo tunasoma jambo lingine lenye kutia moyo hata zaidi: “Mvulana Samweli akaendelea kukua akiwa na Yehova.” Kadiri alivyoendelea kukua, ndivyo uhusiano wake na Baba yake wa mbinguni ulivyoimarika. Uhusiano huo wa kibinafsi pamoja na Yehova, ndio ulinzi hakika dhidi ya upotovu wowote.

17, 18. (a) Vijana Wakristo wanawezaje kumwiga Samweli wanapokabili upotovu? (b) Nini kinachoonyesha kwamba Samweli alichagua njia inayofaa?

17 Ingekuwa rahisi kwa Samweli kusema kwamba ikiwa kuhani mkuu na watoto wake wanafanya dhambi, hata yeye angefanya apendavyo. Lakini, upotovu unaotendwa na wengine, kutia ndani wenye mamlaka, haupaswi kuwa kisingizio cha kutenda dhambi. Leo, vijana wengi Wakristo wanaiga mfano wa Samweli na ‘kuendelea kukua wakiwa na Yehova’—hata ikiwa watu wanaowazunguka si mfano mzuri.

18 Samweli alifaidikaje kwa kumtii Yehova? Tunasoma hivi: “Na wakati huo wote mvulana Samweli alikuwa akiendelea kukua na kupendwa na Yehova na vilevile na wanadamu.” (1 Sam. 2:26) Kwa hiyo, Samweli alipendwa na watu waliokuwa na maoni yanayofaa. Yehova mwenyewe alimpenda kijana huyo kwa sababu ya uaminifu wake. Samweli alikuwa na hakika kwamba Mungu angeondoa uovu uliokuwa ukiendelea huko Shilo, lakini hakujua ni lini. Usiku moja alipata jibu.

“Sema, kwa Maana Mtumishi Wako Anasikiliza”

19, 20. (a) Eleza kilichompata Samweli usiku mmoja kwenye maskani. (b) Samweli alitambuaje chanzo cha ujumbe aliopata, na alimtendeaje Eli?

19 Asubuhi ilikuwa ikikaribia lakini bado kulikuwa na giza; nuru ya taa kubwa ya maskani ilikuwa ikiangaza. Kulikuwa kimya, Samweli aliposikia sauti ikiita jina lake. Alifikiri ni sauti ya Eli, ambaye wakati huo alikuwa mzee sana na hakuwa anaona vizuri. Samweli akaamka na ‘kukimbia’ kwenda kwa mzee huyo. Hebu wazia mvulana huyo akikimbia bila viatu ili kuona Eli anahitaji nini! Inatia moyo kuona kwamba Samweli alimheshimu na kumtendea Eli kwa fadhili. Licha ya dhambi zake, bado Eli alikuwa kuhani mkuu wa Yehova.​—1 Sam. 3:2-5.

20 Samweli alimwamsha Eli na kusema: “Mimi hapa, kwa maana umeniita.” Lakini Eli akasema hakuwa amemwita na akamwambia aende akalale. Hata hivyo, hilo lilitendeka tena na tena! Mwishowe, Eli akatambua kilichokuwa kikiendelea. Muda ulikuwa umepita tangu Yehova alipotuma maono au ujumbe wa kinabii kwa watu wake, na tunajua ni kwa nini. Lakini Eli alijua kwamba Yehova alikuwa akizungumza tena—wakati huu kupitia mvulana huyo! Eli alimwambia aende akalale na akamweleza jinsi ya kujibu atakapoitwa tena. Samweli alitii. Punde si punde, akasikia sauti ikiita: “Samweli, Samweli!” Naye akajibu: “Sema, kwa maana mtumishi wako anasikiliza.”​—1 Sam. 3:1, 5-10.

21. Tunawezaje kumsikiliza Yehova leo, na kwa nini ni muhimu kufanya hivyo?

21 Angalau sasa Yehova alikuwa na mtumishi huko Shilo ambaye alikuwa akimsikiliza. Naye Samweli akaendelea kumsikiliza Yehova maisha yake yote. Namna gani wewe? Si lazima tusikie sauti isiyo ya kawaida ikizungumza nasi usiku. Leo, kwa njia ya mfano tunaweza kusikia sauti ya Mungu wakati wowote. Nayo inapatikana katika Neno lake, Biblia. Kadiri tunavyoendelea kumsikiliza Mungu na kumtii, ndivyo imani yetu inavyoimarika. Hivyo ndivyo ilivyotokea kwa Samweli.

Ingawa Samweli aliogopa, bado alimwambia Eli kuhusu ujumbe wa hukumu kutoka kwa Yehova

22, 23. (a) Ujumbe ambao mwanzoni Samweli aliogopa kuutoa ulitimizwaje? (b) Sifa nzuri za Samweli ziliendeleaje kuongezeka?

22 Usiku huo ulikuwa wa maana sana katika maisha ya Samweli, kwa sababu alianza kumjua Yehova kwa njia ya pekee na akawa nabii na msemaji wake. Mwanzoni, mvulana huyo aliogopa kumwambia Eli ujumbe wa Yehova, kwa sababu ulikuwa ujumbe wa mwisho kwamba unabii uliohusu familia hiyo ungetimizwa. Lakini Samweli alizungumza na Eli kwa ujasiri, naye Eli akakubali kwa unyenyekevu hukumu hiyo ya Mungu. Muda si muda, kila kitu ambacho Yehova alisema kilitimizwa. Waisraeli walipigana na Wafilisti, Hofni na Finehasi wakauawa siku moja, naye Eli akafa aliposikia Sanduku takatifu la Yehova lilikuwa limetekwa.​—1 Sam. 3:10-18; 4:1-18.

23 Lakini sifa nzuri za Samweli akiwa nabii mwaminifu wa Mungu zilizidi kuongezeka. Simulizi hilo linasema, “Yehova akawa pamoja naye,” na linaongezea kuwa Yehova aliendelea kutimiza kila unabii ambao Samweli alitoa.​Soma  1 Samweli 3:19.

‘Samweli Alimwita Yehova’

24. Baada ya muda, Waisraeli walifanya uamuzi gani, na kwa nini hiyo ilikuwa dhambi nzito?

24 Hata hivyo, je, Waisraeli walifuata mwongozo wa Samweli na kuwa waaminifu kwa Yehova? Hapana. Baada ya muda, waliamua kwamba hawakutaka kuongozwa tu na nabii. Walitaka kuwa kama mataifa mengine na kutawaliwa na mfalme wa kibinadamu. Kwa mwongozo wa Yehova, Samweli aliwasikiliza. Lakini alihitaji kuwaonyesha Waisraeli uzito wa dhambi yao. Hawakuwa tu wakimkataa mwanadamu, bali Yehova mwenyewe! Kwa hiyo akawakusanya watu huko Gilgali.

Samweli alisali kwa imani, naye Yehova akajibu kwa kuleta ngurumo na mvua

25, 26. Huko Gilgali, Samweli aliyezeeka aliwasaidiaje watu wake waone uzito wa dhambi yao kwa Yehova?

25 Acheni tuone jinsi alivyozungumza na Waisraeli huko Gilgali wakati huo mgumu. Samweli aliwakumbusha Waisraeli kuhusu maisha yake ya uaminifu. Kisha, tunasoma hivi: “Samweli akamwita Yehova.” Akamwomba alete ngurumo na mvua.​—1 Sam. 12:17, 18.

26 Kwa nini aombe kuwe na ngurumo na mvua wakati wa kiangazi? Hawakuwazia kamwe jambo kama hilo! Kama watu walikuwa na shaka yoyote au walimdhihaki Samweli, hawakufanya hivyo kwa muda mrefu. Ghafla mawingu meusi yakatanda angani. Upepo ukaanza kuvuma, na kuharibu ngano shambani. Nayo radi ikatoa ngurumo kwa kishindo. Na mvua ikanyesha. Watu walifanya nini? ‘Walimwogopa sana Yehova na Samweli.’ Mwishowe, wakatambua uzito wa dhambi yao.​—1 Sam. 12:18, 19.

27. Yehova anahisije kuhusu wale wanaoiga imani ya Samweli?

27 Yehova, Mungu ndiye aliyefikia mioyo yao yenye kuasi, bali si Samweli. Tangu ujana hadi uzeeni Samweli aliweka imani yake kwa Mungu. Na Yehova alimbariki. Mpaka leo, Yehova hajabadilika. Bado huwategemeza wale wanaoiga imani ya Samweli.

^ fu. 5 Wanadhiri walikuwa chini ya nadhiri iliyowakataza kunywa pombe na kunyoa nywele zao. Wengi wao walikuwa Wanadhiri kwa muda fulani, lakini wachache kati yao kama Samsoni, Samweli, na Yohana Mbatizaji, walikuwa Wanadhiri katika maisha yao yote.

^ fu. 9 Maskani hiyo takatifu ilikuwa hema kubwa lenye umbo la mstatili, lililoshikiliwa kwa viunzi vya mbao. Hata hivyo, ilitengenezwa kwa vitu bora sana, yaani, ngozi ya sili, vitambaa maridadi vilivyopambwa, na mbao za bei ya juu zilizofunikwa kwa fedha na dhahabu. Maskani hiyo ilizungukwa na ua, na ndani ya ua huo kulikuwa na madhabahu yenye kupendeza ya kutolea dhabihu. Baadaye, yaelekea vyumba vingine vilivyotumiwa na makuhani vilijengwa kandokando ya maskani hiyo. Huenda Samweli alilala ndani ya mojawapo ya vyumba hivyo.

^ fu. 12 Simulizi hilo linatoa mifano miwili ya ukosefu wa heshima. Kwanza, Sheria ilitaja kihususa vipande vya nyama vilivyotolewa dhabihu ambavyo makuhani waliruhusiwa kula. (Kum. 18:3) Lakini katika maskani, makuhani hao waovu walifanya jambo tofauti kabisa. Waliwalazimisha wahudumu wao kuingiza uma mkubwa ndani ya chungu cha kupikia ambacho kilikuwa na nyama zilizokuwa zikitokota, na kutoa kipande chochote kizuri walichopata! Pia, watu walipoleta dhabihu zao ili ziteketezwe juu ya madhabahu, makuhani hao waovu waliwatuma wahudumu kuwasumbua watu kwa kuwaambia wawape nyama mbichi kabla ya kumtolea Yehova dhabihu ya sehemu ya mafuta.​—Law. 3:3-5; 1 Sam. 2:13-17.