Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA ISHIRINI

“Nimeamini”

“Nimeamini”

1. Eleza jinsi Martha alivyohuzunika na sababu ya huzuni yake.

MARTHA aliendelea kufikiria kaburi la ndugu yake—pango lililokuwa limefunikwa kwa jiwe. Alikuwa na huzuni nyingi. Hangeweza kuamini kuwa ndugu yake mpendwa Lazaro amekufa. Siku nne zilikuwa zimepita tangu Lazaro afe na kilionekana kuwa kipindi kirefu cha kuomboleza na kutembelewa na wageni waliowafariji.

2, 3. (a) Martha alitendaje alipomwona Yesu? (b) Maneno ya Martha yalifunua nini kumhusu?

2 Hatimaye Yesu, rafiki wa karibu wa Lazaro, alikuwa amesimama mbele ya Martha. Inaelekea alipomwona Yesu alihuzunika hata zaidi, kwa sababu Yesu pekee ndiye angeweza kuzuia kifo chake. Hata hivyo, Martha alifarijika kwa kadiri fulani alipokutana na Yesu nje ya mji mdogo wa Bethania uliokuwa kwenye kilima. Baada ya kuwa pamoja na Yesu kwa muda mfupi, Martha alitiwa moyo kutokana na fadhili na huruma za Yesu. Martha aliulizwa maswali ambayo yalimsaidia kufikiria tumaini la ufufuo. Mazungumzo hayo yalimfanya atamke maneno haya muhimu: “Nimeamini kwamba wewe ndiye Kristo Mwana wa Mungu, Yule anayekuja ulimwenguni.”​—Yoh. 11:27.

3 Maneno hayo yanaonyesha kwamba Martha alikuwa mwanamke mwenye imani thabiti. Mambo machache ambayo Biblia inatuambia kumhusu yanaweza kutusaidia kuimarisha imani yetu. Ili kuelewa jambo hilo, acheni tufikirie simulizi la kwanza katika Biblia kumhusu Martha.

‘Alihangaika na Kusumbuka’

4. Kwa nini familia ya akina Martha ilikuwa ya pekee, na walikuwa na uhusiano gani na Yesu?

4 Miezi kadhaa mapema, Lazaro alikuwa hai na mwenye afya njema. Alitazamia kumkaribisha Yesu Kristo, mgeni muhimu kuliko wote, nyumbani kwake Bethania. Lazaro, Martha, na Maria walikuwa familia ya pekee—watu wazima watatu walioishi pamoja. Wasomi fulani wanasema huenda Martha ndiye aliyekuwa mkubwa kati yao, kwa vile alifanya maandalizi kwa ajili ya wageni na nyakati nyingine anatajwa kwanza. (Yoh. 11:5) Si rahisi kujua ikiwa yeyote kati yao alikuwa amefunga ndoa. Vyovyote vile, walikuwa marafiki wa karibu wa Yesu. Wakati wa huduma yake huko Yudea, ambako alipingwa na kuchukiwa sana, Yesu aliishi katika nyumba yao. Bila shaka, alithamini sana utulivu na utegemezo aliopata katika nyumba hiyo.

5, 6. (a) Kwa nini Martha alikuwa na shughuli nyingi Yesu alipowatembelea? (b) Maria alifanya nini Yesu alipowatembelea?

5 Martha alichangia sana hali nzuri na ukarimu katika nyumba yao. Alikuwa mwenye bidii, na mara nyingi alijishughulisha na mambo mengi. Ilikuwa hivyo hata Yesu alipowatembelea. Mara moja alipanga kutayarisha mlo wa pekee, yaani, vyakula mbalimbali kwa ajili ya mgeni wao maalumu, na pia labda watu walioandamana naye. Siku hizo, lilikuwa jambo muhimu sana kuonyesha ukarimu. Mgeni alipowasili, alikaribishwa kwa busu, akavuliwa viatu, akaoshwa miguu, na kupakwa mafuta yenye marashi kichwani. (Soma Luka 7: 44-47.) Mgeni alipewa chakula bora na mahali pazuri pa kulala.

6 Martha na Maria walifanya matayarisho mengi. Bila shaka, Maria ambaye mara nyingi anaonekana kuwa msikivu na mwenye kujali zaidi, alimsaidia kwanza dada yake. Lakini Yesu alipofika, mambo yalibadilika. Yesu alitumia pindi hiyo kufundisha, na alifundisha kwelikweli! Tofauti na viongozi wa kidini wa nyakati hizo, Yesu aliwaheshimu wanawake na aliwafundisha kuhusu Ufalme wa Mungu, ambao ulikuwa kichwa kikuu cha mahubiri yake. Maria alifurahia pindi hiyo, hivyo akakaa miguuni pa Yesu na kumsikiliza kwa makini.

7, 8. Kwa nini Martha alikuwa na mkazo, na mwishowe alisema nini?

7 Tunaweza kuwazia mkazo ambao Martha alikabili. Alikuwa akitayarisha vyakula mbalimbali na kufanya mambo mengi kwa ajili ya wageni wake, na hivyo hakukazia fikira mambo muhimu. Alipokuwa akipita huku na huku na kumwona dada yake akiwa ameketi bila kumsaidia, je, alikasirika na kushusha pumzi kwa nguvu, au hata kukunja uso? Inawezekana alifanya hivyo. Kwa sababu, hangeweza kufanya kazi zote peke yake.

8 Mwishowe, Martha alishindwa kuvumilia. Alimkatiza Yesu na kufoka: “Bwana, hujali kwamba dada yangu ameniacha peke yangu kushughulikia mambo? Kwa hiyo, mwambie aje anisaidie.” (Luka 10:40) Hayo yalikuwa maneno mazito. Baadhi ya Biblia hutafsiri swali lake hivi: “Bwana, hujali  . . . ?” Kisha akamwomba Yesu amrekebishe Maria na kumwagiza amsaidie kazi.

9, 10. (a) Yesu alimjibuje Martha? (b) Tunajuaje kwamba Yesu hakuwa akipuuza kazi ngumu ya Martha?

9 Huenda jibu la Yesu lilimshangaza Martha, na pia linawashangaza wasomaji wengi wa Biblia. Kwa upole alisema: “Martha, Martha, wewe unahangaika na kusumbuka juu ya mambo mengi. Ingawa hivyo, mambo machache ndiyo yanayohitajiwa, au moja tu. Yeye, Maria alichagua fungu jema, nalo halitaondolewa kwake.” (Luka 10:41, 42) Yesu alimaanisha nini? Je, alimaanisha Martha alihangaikia sana vitu vya kimwili? Je, alikuwa akipuuza kazi yake ngumu ya kutayarisha mlo mzuri?

Ingawa Martha ‘alihangaika na kusumbuka juu ya mambo mengi’ alikubali kwa unyenyekevu aliporekebishwa

10 Hapana. Yesu alijua Martha alichochewa na upendo na nia nzuri. Zaidi ya hilo, hakuona kwamba ilikuwa vibaya kuonyesha ukarimu mwingi hivyo. Alikuwa amehudhuria kwa hiari “karamu kubwa” ambayo Mathayo alikuwa amemwandalia mapema. (Luka 5:29) Tatizo halikuwa mlo wa Martha; badala yake, ni jambo alilotanguliza. Alizingatia sana mlo wake uliohusisha mambo mengi hivi kwamba akasahau jambo lililokuwa muhimu zaidi. Jambo gani hilo?

Yesu alithamini ukarimu wa Martha, na alijua kwamba alichochewa na upendo na nia nzuri

11, 12. Yesu alimrekebishaje Martha kwa upole?

11 Yesu, Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova Mungu, alikuwa katika nyumba ya Martha akifundisha kweli. Hilo lilikuwa jambo muhimu zaidi kuliko mlo na matayarisho ya Martha. Bila shaka, Yesu alihuzunika kwamba Martha alikuwa akipoteza nafasi muhimu ya kuimarisha imani yake, lakini hakumlazimisha. * Hata hivyo, Martha hakupaswa kumwomba Yesu amwamuru Maria akose nafasi hiyo pia.

12 Kwa upole, Yesu alimrekebisha Martha, akirudia jina lake kwa utulivu, na akamhakikishia kwamba hakupaswa ‘kuhangaika na kusumbuka juu ya mambo mengi.’ Mlo usiohusisha mambo mengi ungetosha, hasa kwa sababu kulikuwa na karamu ya kiroho. Hivyo, hangemnyang’anya Maria “fungu jema” ambalo alikuwa amechagua, yaani, kufundishwa na Yesu!

13. Tunajifunza nini kutokana na jibu la Yesu kwa Martha?

13 Leo, Wakristo wanaweza kujifunza mengi kutokana na simulizi hili. Hatupaswi kamwe kuruhusu chochote kitunyime nafasi ya kutosheleza ‘uhitaji wetu wa kiroho.’ (Mt. 5:3) Ingawa tungependa kuiga ukarimu na bidii ya Martha, hatupaswi kamwe ‘kuhangaika na kusumbuka’ sana kuhusu mambo yasiyo muhimu tunapokaribisha wageni. Lengo la kushirikiana na waamini wenzetu hasa ni kutiana moyo na kupeana zawadi za kiroho, bali si kufurahia milo mikubwa. (Soma Waroma 1:11,12.Hata chakula kisichohusisha mambo mengi kinaweza kufanya pindi hizo ziwe zenye kujenga.

Ndugu Mpendwa Afa—Na Kufufuliwa

14. Kwa nini Martha aliweka mfano mzuri kwa kukubali kurekebishwa?

14 Je, Martha alikubali kurekebishwa na Yesu? Ndiyo. Anapoanza kusimulia kuhusu ndugu ya Martha, mtume Yohana anasema: “Basi Yesu alimpenda Martha na dada yake na Lazaro.” (Yoh. 11:5) Miezi kadhaa ilikuwa imepita tangu Yesu alipotembelea Bethania. Ni wazi kwamba Martha hakukasirika wala kuweka kinyongo baada ya kushauriwa na Yesu. Alikubali kurekebishwa. Kuhusu jambo hilo pia, Martha alituwekea mfano mzuri wa imani, kwani mara kwa mara sote tunahitaji kurekebishwa.

15, 16. (a) Inaelekea Martha alifanya nini ndugu yake alipoanza kuugua? (b) Kwa nini matumaini ya Martha na Maria hayakutimia?

15 Ndugu yake alipoanza kuugua, kwa kweli Martha alijitahidi kumtunza. Alifanya kila alichoweza ili kumsaidia apone. Hata hivyo, hali ya Lazaro ilizidi kuzorota. Kila siku, dada zake walikaa kando yake na kumtunza. Hebu wazia Martha akiutazama uso mchovu wa ndugu yake, na kukumbuka miaka mingi waliyoishi pamoja!

16 Hali ya Lazaro ilipozidi kuwa mbaya, Martha na Maria walimtumia Yesu ujumbe. Yesu alikuwa akihubiri katika eneo lililokuwa umbali wa siku mbili. Ujumbe wao ulikuwa mfupi: “Bwana, ona! yule unayempenda ni mgonjwa.” (Yoh. 11:1, 3) Walijua Yesu alimpenda ndugu yao, na waliamini kwamba angefanya chochote ili kumsaidia rafiki yake. Je, walitumaini kwamba Yesu angewasili kabla ndugu yao hajafa? Ikiwa ndivyo, tumaini lao halikutimia. Lazaro alikufa.

17. Ni nini kilichomshangaza Martha, na alitendaje aliposikia Yesu alikuwa akikaribia kuingia mjini?

17 Martha na Maria walimwombolezea ndugu yao, wakapanga mazishi yake na kupokea wageni wengi kutoka Bethania na maeneo jirani. Hata hivyo, Yesu hakuwa amefika. Bila shaka, huenda Martha alizidi kuwa na wasiwasi. Hatimaye, siku nne baada ya Lazaro kufa, Martha alisikia kwamba Yesu alikuwa akikaribia kuingia mjini. Akiwa mwenye bidii kama kawaida, hata katika pindi hiyo ya huzuni, Martha aliinuka na bila kumwambia Maria, akakimbia kukutana na Yesu.​—Soma Yohana 11:18-20.

18, 19. Martha alikuwa na tumaini gani, na kwa nini imani yake ilikuwa imara?

18 Alipomwona Yesu, akasema mambo yaliyokuwa yakimsumbua yeye na Maria kwa siku kadhaa: “Bwana, kama ungekuwa hapa ndugu yangu hangekufa.” Lakini bado Martha alimwamini na kumtumaini Yesu. Akaongeza hivi: “Hata hivyo sasa ninajua kwamba mambo mengi kadiri unayomwomba Mungu, Mungu atakupa.” Mara moja Yesu akasema maneno haya ili kuimarisha imani yake: “Ndugu yako atafufuka.”—Yoh. 11:21-23.

19 Martha alifikiri kwamba Yesu anazungumzia ufufuo wa wakati ujao, hivyo akajibu: “Ninajua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yoh. 11:24) Imani yake katika ufufuo ilikuwa imara. Viongozi fulani wa dini ya Kiyahudi walioitwa Masadukayo, hawakuamini fundisho la ufufuo ingawa lilikuwa katika Maandiko yaliyoongozwa na roho. (Dan. 12:13; Marko 12:18) Martha alijua kwamba Yesu alifundisha kuhusu tumaini la ufufuo na hata alifufua watu—ingawa hakuwa amemfufua mtu aliyekufa kwa muda mrefu kama Lazaro. Hakujua jambo ambalo lingefuata.

20. Eleza maana ya maneno yanayojulikana sana ya Yesu kwenye Yohana 11:25-27 na maana ya jibu la Martha.

20 Kisha, Yesu akasema maneno haya yanayojulikana sana: “Mimi ndiye ufufuo na uzima.” Kwa kweli, Yehova Mungu amempa Mwana wake mamlaka ya kufufua watu duniani wakati ujao. Yesu alimuuliza Martha: “Je, unaamini hilo?” Martha akatoa jibu lililotajwa mwanzoni mwa sura hii. Aliamini Yesu ndiye Kristo, au Masihi, kwamba ndiye Mwana wa Yehova Mungu, na kwamba ndiye manabii walikuwa wametabiri angekuja ulimwenguni.​—Yoh. 5:28, 29; soma Yohana 11:25-27.

21, 22. (a) Yesu alionyeshaje kwamba anaelewa hisia za wale wanaoomboleza? (b) Fafanua ufufuo wa Lazaro.

21 Je, Yehova Mungu na Mwana wake, Yesu Kristo, wanathamini imani kama ya Martha? Mambo yaliyofuata yalijibu swali hilo. Martha alikimbia kumwita dada yake. Kisha akaona Yesu akiwa na huzuni sana alipokuwa akizungumza na Maria na waombolezaji wengi waliokuwapo. Akamwona Yesu akitokwa na machozi kwa sababu ya huzuni inayoletwa na kifo. Akamsikia Yesu akiagiza jiwe lililokuwa limefunika kaburi la ndugu yake liondolewe.​—Yoh. 11: 28-39.

22 Martha alipinga na kusema mwili ulikuwa unanuka, kwa kuwa siku nne zilikuwa zimepita tangu Lazaro afe. Ndipo Yesu akamkumbusha: “Je, sikukuambia kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu?” Martha akaamini na akaona utukufu wa Yehova Mungu. Papo hapo, Mungu akamwezesha Mwana wake kumfufua Lazaro! Fikiria tukio hili ambalo Martha aliendelea kulikumbuka maishani: Yesu aliagiza, “Lazaro, njoo huku nje!”; sauti ikasikika ndani ya pango Lazaro alipoinuka, akiwa bado amefungwa vitambaa, na kutembea polepole kuelekea mlango wa pango; Yesu akaagiza ‘wamfungue na kumwacha aende’; kisha, wazia msisimuko ambao Martha na Maria walikuwa nao walipomkumbatia ndugu yao. (Soma Yohana 11:40-44.) Martha akaacha kuhuzunika!

Imani ya Martha katika Yesu ilithawabishwa wakati yeye na dada yake Maria walipoona ndugu yao akifufuliwa

23. Yehova na Yesu wanataka kukufanyia nini, na unahitaji kufanya nini?

23 Simulizi hili linaonyesha kuwa ufufuo wa wafu si ndoto, bali ni fundisho la Biblia lenye kuchochea na ni jambo hakika ambalo limewahi kutokea. (Ayu. 14:14, 15) Yehova na Mwana wake wanapenda kuwathawabisha watu wenye imani, kama walivyofanya katika kisa cha Martha, Maria, na Lazaro. Pia, watakuthawabisha wewe ikiwa utaonyesha imani yenye nguvu.

“Martha Alikuwa Akihudumu”

24. Simulizi la Biblia linasema nini kuhusu mara ya mwisho ambayo Martha anatajwa?

24 Baada ya hapo Biblia inamtaja tena Martha mara moja tu. Lilikuwa juma la mwisho kabla ya kifo cha Yesu. Akijua hali ngumu ambayo angekabili, Yesu aliamua tena kukaa katika ile nyumba yenye amani na utulivu huko Bethania. Kutoka hapo angetembea kilomita tatu hadi Yerusalemu. Yesu na Lazaro walikuwa wakila katika nyumba ya Simoni mwenye ukoma, na ndipo tunaposoma kumhusu Martha kwa mara ya mwisho: “Martha alikuwa akihudumu.”​—Yoh. 12:2.

25. Kwa nini makutaniko yamebarikiwa kuwa na wanawake kama Martha?

25 Kwa kweli, mwanamke huyo alikuwa na bidii! Anapotajwa mara ya kwanza katika Biblia, anafanya kazi; anapotajwa mara ya mwisho, bado anafanya kazi, akijitahidi kuwahudumia wengine. Makutaniko ya wafuasi wa Kristo leo yamebarikiwa kuwa na wanawake kama Martha—wenye bidii na wakarimu, siku zote wakionyesha imani yao kwa kuwasaidia wengine. Je, Martha aliendelea kufanya hivyo? Inaelekea alifanya hivyo. Ikiwa ndivyo, alitenda kwa busara, kwa kuwa bado angekabili matatizo mengine.

26. Imani ya Martha ilimsaidiaje?

26 Baada ya siku chache, Martha alihuzunika Yesu alipouawa. Zaidi ya hayo, wauaji walewale wanafiki ambao walimuua Yesu waliazimia kumuua Lazaro pia, kwa kuwa ufufuo wa Lazaro ulikuwa unaimarisha imani ya wengi. (Soma Yohana 12:9-11.) Na bila shaka, mwishowe kifo kilimtenganisha Martha na ndugu na dada yake. Hatujui walikufa wakati gani au jinsi gani, lakini tunaweza kuwa na uhakika kwamba imani yenye thamani ya Martha ilimsaidia kuvumilia hadi mwisho. Hivyo, leo Wakristo wanapaswa kuiga imani ya Martha.

^ fu. 11 Wayahudi wengi wa karne ya kwanza waliwatenga wanawake ilipohusu mambo ya elimu. Wanawake walifundishwa tu kuhusu mambo ya nyumbani. Hivyo, huenda Martha hakuona umuhimu wa Maria kuketi miguuni pa Yesu ili kujifunza.