Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA ISHIRINI NA MBILI

Alikuwa Mshikamanifu Licha ya Majaribu

Alikuwa Mshikamanifu Licha ya Majaribu

1, 2. Petro alitarajia nini Yesu alipokuwa akizungumza huko Kapernaumu, lakini nini kilichotokea?

PETRO alitazama kwa wasiwasi nyuso za watu waliokuwa wakimsikiliza Yesu. Walikuwa katika sinagogi la Kapernaumu. Petro aliishi katika mji huo; alifanya biashara yake ya kuvua samaki kwenye Bahari ya Galilaya; rafiki zake, watu wa ukoo, na watu aliofanya nao biashara waliishi katika eneo hilo. Bila shaka, Petro alitamani watu wa mji huo wawe na maoni kama yake kumhusu Yesu na wafurahie kujifunza kuhusu Ufalme wa Mungu kutoka kwa mwalimu mkuu zaidi. Lakini inaonekana siku hii mambo yangekuwa tofauti.

2 Wengi walikuwa wameacha kumsikiliza. Baadhi yao walikuwa wakinung’unika kwa sauti na kupinga ujumbe wa Yesu. Lakini, kilichomsumbua Petro zaidi ni jinsi baadhi ya wanafunzi wa Yesu walivyoitikia. Nyuso zao hazikuonyesha msisimko wowote unaotokana na kujifunza jambo jipya, wala shangwe ya kujifunza ukweli. Sasa walionekana wenye hasira na uchungu. Baadhi yao walisema maneno ya Yesu yalikuwa yenye kushtua. Walikataa kumsikiliza, wakatoka kwenye sinagogi, na hata wakaacha kumfuata.​—Soma Yohana 6:60, 66.

3. Mara nyingi, imani ya Petro ilimsaidia kufanya nini?

3 Ulikuwa wakati mgumu kwa Petro na mitume wenzake. Petro hakuelewa kikamili mambo ambayo Yesu alisema siku hiyo. Bila shaka, alijua kwa nini maneno ya Yesu yangeeleweka vibaya ikiwa hayangefafanuliwa. Petro angefanya nini? Haikuwa mara ya kwanza kwa ushikamanifu wa Petro kwa Bwana wake kujaribiwa, wala haingekuwa mara ya mwisho. Acheni tuone jinsi imani ya Petro ilivyomsaidia kukabili majaribu hayo na pia kudumisha ushikamanifu.

Adumisha Ushikamanifu Huku Wengine Wakishindwa

4, 5. Yesu alitendaje kinyume na matarajio ya wengi?

4 Mara nyingi, Petro alishangazwa na Yesu. Tena na tena, Bwana wake alitenda na kusema kinyume na matarajio ya watu. Siku iliyotangulia, Yesu alikuwa amelisha kimuujiza maelfu ya watu. Baada ya hapo, wakajaribu kumfanya awe mfalme. Lakini aliwashangaza wengi alipoondoka na kuwaagiza wanafunzi wake wapande mashua kwenda Kapernaumu. Wanafunzi wake walipokuwa wakisafiri kwa mashua usiku, Yesu aliwashangaza tena kwa kutembea juu ya Bahari ya Galilaya yenye dhoruba, na Petro alijifunza jambo muhimu kuhusu imani.

5 Asubuhi, walitambua kwamba umati ulikuwa umepanda mashua na kuwafuata. Lakini, inaelekea watu hao walitamani kulishwa tena kimuujiza na Yesu, bali hawakutamani kumsikiliza akifundisha. Yesu aliwakemea kwa sababu ya mwelekeo wao wa kupenda vitu vya kimwili. (Yoh. 6:25-27) Aliendelea kufundisha katika sinagogi huko Kapernaumu, na kwa mara nyingine, Yesu alitenda kinyume na matarajio ya watu alipojaribu kuwafunza ukweli muhimu, lakini mgumu kueleweka.

6. Yesu alitoa mfano gani, na wasikilizaji wake waliitikiaje?

6 Yesu hakutaka watu wamwone kuwa mwandalizi wa chakula cha kimwili, bali kama mkombozi ambaye Mungu alimtoa ili kupitia kifo chake wanadamu wapate uzima wa milele. Hivyo, akatoa mfano akijilinganisha na mana, mkate uliotoka mbinguni siku za Musa. Watu fulani walipopinga, alitumia mfano ulio wazi zaidi na kuwaeleza kwamba ilikuwa lazima wale mwili na damu yake ili wapate uzima. Hapo ndipo watu walipompinga vikali. Wengine wakasema: “Maneno hayo yanashtua; ni nani ambaye anaweza kuyasikiliza?” Wengi kati ya wanafunzi wa Yesu wakaamua kumwacha. *Yoh. 6:48-60, 66.

7, 8. (a) Ni nini ambacho bado Petro hakuelewa kuhusu jukumu la Yesu? (b) Petro alijibuje swali ambalo Yesu aliwauliza mitume?

7 Petro angefanya nini? Yeye pia hakuelewa maneno ya Yesu. Hakujua kwamba ilikuwa lazima Yesu afe ili atimize mapenzi ya Mungu. Je, Petro alishawishiwa kumwacha Yesu kama wanafunzi hao wasio na msimamo? Hapana; tofauti na watu hao Petro alikuwa na sifa fulani muhimu. Ni sifa gani hiyo?

8 Yesu aliwageukia mitume wake na kuwauliza: “Je, ninyi pia mnataka kwenda?” (Yoh. 6:67) Aliwauliza mitume wote 12, lakini Petro ndiye aliyejibu. Alizoea kufanya hivyo. Huenda Petro ndiye aliyekuwa na umri mkubwa zaidi kati yao. Vyovyote vile, kwa hakika Petro ndiye aliyezungumza waziwazi kati ya mitume, na mara nyingi hakusita kusema alichofikiria. Katika kisa hiki, alisema maneno haya mazuri ambayo bado yanakumbukwa: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.”—Yoh. 6:68.

9. Petro alionyeshaje ushikamanifu wake kwa Yesu?

9 Kwa kweli, maneno hayo yanagusa moyo. Imani ya Petro katika Yesu ilimsaidia kusitawisha sifa muhimu ya ushikamanifu. Petro aliamini kwamba Yesu ndiye Mwokozi pekee aliyekuwa ametumwa na Yehova, na kwamba Yesu aliwaokoa watu kupitia mafundisho yake kuhusu Ufalme wa Mungu. Petro alijua kwamba hata kama hakuelewa mambo fulani, hakuna mahali pengine ambapo angepata kibali cha Mungu na pia uzima wa milele.

Tunahitaji kuwa washikamanifu kwa mafundisho ya Yesu hata tunapohisi kwamba ni kinyume cha matarajio au mapendezi yetu

10. Leo, tunawezaje kuiga ushikamanifu wa Petro?

10 Je, unahisi hivyo? Kwa kusikitisha, watu wengi leo wanadai kwamba wanampenda Yesu, lakini si washikamanifu kwake. Ili tuwe washikamanifu kwa Kristo, kama Petro tunapaswa kupenda mafundisho yake. Tunahitaji kuyajua, kuyaelewa, na kuishi kulingana nayo, hata tunapohisi kwamba ni kinyume cha matarajio au mapendezi yetu. Tukiwa washikamanifu, tunaweza kutumaini kupata uzima wa milele ambao Yesu anataka tuufurahie.​—Soma Zaburi 97:10.

Alidumisha Ushikamanifu Aliporekebishwa

11. Yesu aliwaongoza wafuasi wake kwenda wapi? (Ona pia maelezo ya chini.)

11 Muda mfupi baadaye, Yesu aliongoza mitume na baadhi ya wanafunzi wake, katika safari ndefu kuelekea kaskazini. Nyakati nyingine, Mlima Hermoni wenye theluji, ulio upande wa kaskazini mwa Nchi ya Ahadi, ulionekana kutoka kwenye Bahari ya Galilaya. Kadiri walivyokaribia mlima huo ulizidi kuonekana wazi, huku wakipanda kuelekea vijiji fulani karibu na Kaisaria Filipi. * Wakiwa katika mandhari hii yenye kuvutia, ambapo waliona sehemu kubwa ya Nchi ya Ahadi upande wa kusini, Yesu aliwauliza wafuasi wake swali muhimu.

12, 13. (a) Kwa nini Yesu alitaka kujua maoni ya umati kumhusu? (b) Petro alionyeshaje imani ya kweli alipomjibu Yesu?

12 Akawauliza: “Umati unasema mimi ni nani?” Tunaweza kuwazia Petro akimtazama Yesu kwa makini, na kwa mara nyingine akitambua jinsi Bwana wake alivyokuwa mwenye fadhili na hekima. Yesu alitaka kujua maoni ya wasikilizaji wake kuhusu mambo waliyoona na kusikia. Wanafunzi wa Yesu walijibu swali hilo na kutaja maoni yaliyoenea yenye makosa kuhusu utambulisho wa Yesu. Lakini Yesu alitaka kujua mengi zaidi. Je, wafuasi wake wa karibu walikuwa na maoni kama hayo? Basi akawauliza, “Ingawa hivyo, ninyi mnasema mimi ni nani?”​—Luka 9:18-20.

13 Kwa mara nyingine, Petro alijibu bila kukawia. Alitaja waziwazi na kwa ujasiri maoni ya wafuasi waliokuwepo. Alisema: “Wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.” Tunaweza kuwazia Yesu akitabasamu na kumpongeza Petro kwa shauku. Yesu alimkumbusha Petro kwamba si mwanadamu bali ni Yehova Mungu aliyefunua kweli hiyo muhimu kwa watu wenye imani ya kweli. Petro alikuwa amesaidiwa kutambua kweli muhimu zaidi ambayo Yehova alikuwa amefunua, yaani, utambulisho wa Masihi, au Kristo, aliyeahidiwa!​—Soma Mathayo 16:16, 17.

14. Yesu alimpa Petro majukumu gani ya pekee?

14 Huyu ndiye Kristo ambaye unabii wa kale ulimwita jiwe ambalo wajenzi wangekataa. (Zab. 118:22; Luka 20:17) Akikumbuka unabii huo, Yesu alifunua kwamba Yehova angeanzisha kutaniko juu ya jiwe hilo au mwamba, ambao Petro alikuwa ametoka tu kuutambulisha. Kisha akampa Petro mapendeleo muhimu sana katika kutaniko hilo. Hakumpa Petro mamlaka mengi kuliko mitume wengine, kama watu wengine wanavyofikiri, lakini alimpa majukumu fulani. Alimpa Petro “funguo za ufalme wa mbinguni.” (Mt. 16:19) Petro angekuwa na jukumu la kufungulia vikundi vitatu vya wanadamu tumaini la kuingia katika Ufalme wa Mungu—kwanza Wayahudi, pili Wasamaria, na mwishowe Watu wa Mataifa, au watu wasio Wayahudi.

15. Kwa nini Petro alimkemea Yesu, na alisema nini?

15 Lakini, baadaye Yesu alisema kwamba wale wanaopewa mengi wanadaiwa mengi, na ukweli wa maneno hayo unaonekana katika kisa cha Petro. (Luka 12:48) Yesu aliendelea kufunua kweli muhimu kumhusu Masihi na akasema kwamba baada ya muda mfupi ingekuwa lazima ateseke na kufa huko Yerusalemu. Mambo hayo yalimtia Petro wasiwasi. Alimchukua Yesu kando na kumkemea akisema: “Jitendee kwa fadhili, Bwana; wewe hutapatwa hata kidogo na jambo hili.”​—Mt. 16:21, 22.

16. Yesu alimrekebishaje Petro, na tunapata ushauri gani katika maneno ya Yesu?

16 Petro hakuwa na nia mbaya, lakini bila shaka jibu la Yesu lilimshangaza. Yesu alimgeuzia Petro mgongo na kuwatazama wanafunzi wengine—ambao labda walikuwa na maoni kama ya Petro—na kusema: “Nenda nyuma yangu, Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa sababu wewe unafikiri, si fikira za Mungu, bali za wanadamu.” (Mt. 16:23; Marko 8:32, 33) Maneno ya Yesu ni ushauri mzuri kwetu sote. Ni rahisi sana kutanguliza maoni ya kibinadamu badala ya maoni ya Mungu. Tukifanya hivyo, hata kama tuna nia nzuri, tunaweza bila kukusudia kumuunga mkono Shetani badala ya Mungu. Hata hivyo, Petro aliitikiaje?

17. Yesu alimaanisha nini alipomwambia Petro ‘aende nyuma’ yake?

17 Bila shaka, Petro alijua kwamba Yesu hakumaanisha yeye ni Shetani Ibilisi. Yesu hakuzungumza na Petro jinsi alivyozungumza na Shetani. Yesu alimwambia Shetani: “Nenda zako”; lakini alimwambia Petro: “Nenda nyuma yangu.” (Mt. 4:10) Yesu hakuwa akimfukuza mtume huyo ambaye alikuwa na sifa nyingi nzuri, bali alirekebisha tu maoni yake yenye makosa kuhusu jambo hilo. Hivyo, Petro alihitaji kuacha kuwa kama jiwe la kukwaza mbele ya Bwana wake, na badala yake, awe mfuasi wake mshikamanifu.

Tutakuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yesu Kristo na Baba yake, Yehova Mungu, tukikubali nidhamu na kujifunza kutokana nayo

18. Petro alionyeshaje ushikamanifu, na tunawezaje kumwiga?

18 Je, Petro alibishana, alikasirika, au kununa? La; kwa unyenyekevu alikubali kurekebishwa. Hivyo, akaonyesha tena sifa ya ushikamanifu. Mara kwa mara wafuasi wote wa Kristo wanahitaji kurekebishwa. Tutakuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yesu Kristo na Baba yake, Yehova Mungu, tukikubali nidhamu na kujifunza kutokana nayo.​—Soma Methali 4:13.

Petro aliendelea kuwa mshikamanifu hata aliporekebishwa

Athawabishwa kwa Sababu ya Ushikamanifu

19. Yesu alisema maneno gani yenye kushangaza, na huenda Petro alifikiri nini?

19 Muda si muda, Yesu alisema maneno mengine yenye kushangaza: “Kwa kweli ninawaambia ninyi kwamba kuna baadhi ya wale wanaosimama hapa ambao hawataonja kifo kamwe mpaka kwanza wamwone Mwana wa binadamu akija katika ufalme wake.” (Mt. 16:28) Bila shaka, maneno hayo yalimfanya Petro atake kujua mengi zaidi. Yesu alimaanisha nini? Labda Petro aliwaza kwamba hangepata pendeleo kama hilo la pekee kwa sababu Yesu alikuwa ametoka tu kumkemea vikali.

20, 21. (a) Fafanua maono ambayo Petro alishuhudia. (b) Mazungumzo ya watu waliokuwa katika maono yalimsaidiaje Petro kubadili maoni yake?

20 Hata hivyo, juma moja hivi baadaye, Yesu alimchukua Yakobo, Yohana, na Petro na kupanda juu “katika mlima mrefu”—labda Mlima Hermoni, uliokuwa karibu. Inaonekana ilikuwa usiku, kwa sababu wanaume hao watatu walikuwa wakipambana na usingizi. Lakini Yesu alipokuwa akisali, jambo fulani lilitokea na kuwafanya wawe macho kabisa.​—Mt. 17:1; Luka 9:28, 29, 32.

21 Yesu akaanza kubadilika mbele ya macho yao. Uso wake ukaanza kung’aa na kuwa mwangavu kama jua. Mavazi yake pia yakaanza kumetameta. Kisha watu wawili wakatokea na kusimama pamoja naye, mmoja akiwakilisha Musa na mwingine Eliya. Walizungumza naye kuhusu ‘kuondoka kwake ambako kungetimia huko Yerusalemu,’ yaani, kifo na ufufuo wake. Ilikuwa wazi kwamba Petro alikuwa amekosea alipofikiri Yesu hakupaswa kuteseka na kufa!​—Luka 9:30, 31.

22, 23. (a) Petro alionyeshaje uchangamfu na shauku? (b) Petro, Yakobo, na Yohana walithawabishwaje tena usiku huo?

22 Petro alitamani kushiriki kwa njia fulani katika maono hayo yenye kustaajabisha, na labda hata afanye yawe marefu. Kisha ikaonekana kwamba Musa na Eliya walikuwa wakimwacha Yesu. Hivyo, Petro akasema: “Mwalimu, ni vizuri kwetu kuwa hapa, kwa hiyo na tusimamishe mahema matatu, moja lako na moja la Musa na moja la Eliya.” Bila shaka, watu hao wawili ambao katika maono waliwakilisha watumishi wa Yehova waliokufa zamani, hawakuhitaji mahema. Kwa kweli, Petro hakujua alichokuwa akisema. Hata hivyo, je, huvutiwi na uchangamfu na shauku yake?​—Luka 9:33.

Petro, Yakobo, na Yohana walithawabishwa kwa kushuhudia maono yenye kustaajabisha

23 Petro, Yakobo, na Yohana walithawabishwa tena usiku huo. Wingu lilitokea na kuwafunika. Kisha, sauti ikatoka katika wingu hilo, sauti ya Yehova Mungu! Alisema: “Huyu ni Mwanangu, ambaye amechaguliwa. Msikilizeni.” Maono hayo yakaisha, nao wakabaki na Yesu mlimani.​—Luka 9:34-36.

24. (a) Maono ya mgeuko-umbo yalimsaidiaje Petro? (b) Maono ya mgeuko-umbo yanawezaje kutusaidia leo?

24 Maono hayo ya mgeuko-umbo wa Yesu yalikuwa thawabu iliyoje kwa Petro na kwetu pia! Miaka mingi baadaye, Petro aliandika kuhusu pendeleo alilopata usiku huo la kuwa mmoja wa “mashahidi wa kujionea fahari yake,” yaani, kumwona Yesu kimbele akiwa Mfalme mwenye utukufu mbinguni. Maono hayo yalithibitisha unabii mwingi wa Neno la Mungu na kuimarisha imani ya Petro ambayo baadaye ilimsaidia kukabili majaribu. (Soma 2 Petro 1:16-19.) Imani yetu pia inaweza kutusaidia ikiwa, kama Petro, tutaendelea kuwa washikamanifu kwa Bwana ambaye Yehova amemweka juu yetu, kujifunza kutoka kwake, kukubali nidhamu na marekebisho yake, na kumfuata kwa unyenyekevu sikuzote.

^ fu. 6 Tunaweza kuona badiliko la mtazamo wa umati tunapolinganisha jinsi walivyotenda waliposikia maneno ya Yesu katika sinagogi na jinsi walivyomwita kwa furaha nabii wa Mungu siku iliyotangulia.​—Yoh. 6:14.

^ fu. 11 Safari hiyo ya kilomita 50, ilihusisha kuondoka kwenye fuo za Bahari ya Galilaya, zilizo mita 210 hivi chini ya usawa wa bahari na kupanda mpaka eneo lililo mita 350 hivi juu ya usawa wa bahari kupitia maeneo yenye kuvutia sana.