Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA TISA

Alikuwa Baba na Mume Aliyemwogopa Mungu

Alikuwa Baba na Mume Aliyemwogopa Mungu

1, 2. (a) Yosefu na familia yake walikabili mabadiliko gani? (b) Yosefu alilazimika kumwambia mke wake habari gani mbaya?

YOSEFU aliweka mzigo mwingine kwenye mgongo wa punda. Wazia akitazama huku na huku gizani katika kijiji cha Bethlehemu na kumpigapiga ubavuni mwana-punda huyo mwenye nguvu. Bila shaka, alikuwa akifikiria safari ndefu iliyokuwa mbele yao. Kwenda Misri! Nchi ya kigeni, lugha na tamaduni tofauti—familia yake ndogo ingekabilianaje na mabadiliko hayo yote?

2 Haikuwa rahisi kwa Yosefu kumwambia habari mbaya Maria, mke wake mpendwa, hata hivyo, alijikaza na kumwambia. Alimwambia kuhusu ujumbe huu kutoka kwa Mungu ambao malaika alimpa kupitia ndoto: Mfalme, Herode, alitaka kumuua mwana wao mchanga! Walipaswa kuondoka mara moja. (Soma Mathayo 2:13, 14.) Jambo hilo lilimhangaisha sana Maria. Kwa nini mtoto wake asiye na hatia auawe? Maria na Yosefu hawakuelewa sababu. Lakini waliamini ujumbe wa Yehova, basi wakajitayarisha.

3. Eleza jinsi Yosefu na familia yake walivyoondoka Bethlehemu. (Ona pia picha.)

3 Huku watu katika kijiji cha Bethlehemu wakiwa wamelala, Yosefu, Maria, na Yesu wakaondoka kimyakimya usiku. Walielekea kusini huku mwangaza ukianza kuonekana upande wa mashariki, na huenda Yosefu alijiuliza hali ingekuwaje. Seremala wa hali ya chini angewezaje kuilinda familia yake kutokana na hatari? Je, sikuzote angefaulu kuiandalia familia yake? Je, angefanikiwa kutimiza kwa uvumilivu mgawo mzito ambao Yehova Mungu alikuwa amempa, wa kumlinda na kumlea mtoto huyo wa pekee? Yosefu alikabili majaribu mengi. Tunapochunguza jinsi alivyokabiliana na kila hali, tutaona ni kwa nini akina baba leo, na sisi sote, tunahitaji kuiga imani ya Yosefu.

Yosefu Aliilinda Familia Yake

4, 5. (a) Maisha ya Yosefu yalibadilikaje kabisa? (b) Malaika alimsaidiaje Yosefu akubali mgawo mgumu?

4 Miezi kadhaa mapema, akiwa katika mji wa kwao, huko Nazareti, maisha ya Yosefu yalibadilika kabisa baada ya kumchumbia binti ya Heli. Yosefu alijua kwamba Maria alikuwa mwanamke kijana, mwaminifu, na asiye na hatia. Lakini, akatambua Maria alikuwa mjamzito! Alikusudia kumtaliki kisiri ili amlinde asipatwe na aibu. * Hata hivyo, malaika alizungumza naye katika ndoto, na kumweleza kwamba Maria alipata mimba kupitia roho takatifu ya Yehova. Pia, malaika alisema mwana ambaye angezaliwa angewaokoa “watu wake kutoka katika dhambi zao.” Kisha akamhakikishia Yosefu hivi: “Usiogope kumchukua Maria mke wako na kwenda naye nyumbani.”​—Mt. 1:18-21.

5 Yosefu, mwanamume aliyekuwa mwadilifu, alitii maneno hayo. Alikubali mgawo mgumu zaidi: kumlea na kumtunza mwana ambaye hakuwa wake lakini aliyekuwa na thamani sana kwa Mungu. Baadaye, kwa kutii agizo la serikali, Yosefu alimchukua mke wake aliyekuwa mjamzito na kwenda Bethlehemu ili kujiandikisha. Yule mtoto akazaliwa huko.

6-8. (a) Ni nini kilichosababisha mabadiliko katika maisha ya Yosefu na familia yake ndogo? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba ile “nyota” iliongozwa na Shetani? (Ona pia maelezo ya chini.)

6 Yosefu hakurudisha familia yake Nazareti. Badala yake, waliishi Bethlehemu, mji uliokuwa kilomita chache kutoka Yerusalemu. Walikuwa maskini, lakini Yosefu alijitahidi kuwatunza na kuwalinda Maria na Yesu. Baada ya muda mfupi, walianza kuishi katika nyumba ndogo. Kwa ghafula maisha yao yalibadilika tena, labda sasa Yesu alikuwa na umri mwaka mmoja hivi.

7 Kikundi cha wanajimu wa Mashariki kiliwasili, huenda wanaume hao walitoka mbali, huko Babiloni. Walikuwa wamefuata “nyota” iliyowaelekeza nyumbani kwa Yosefu na Maria na walikuwa wakimtafuta mtoto ambaye angekuwa mfalme wa Wayahudi. Wanaume hao walionyesha heshima sana.

8 Iwe walijua au la, wanajimu hao walikuwa wamehatarisha sana uhai wa Yesu. “Nyota” waliyoona iliwaelekeza kwanza Yerusalemu, bali si Bethlehemu. * Wakiwa huko walimwambia Mfalme Herode aliyekuwa mwovu kwamba walikuwa wakimtafuta mtoto ambaye angekuwa mfalme wa Wayahudi. Hilo lilimfanya mfalme huyo akasirike sana.

9-11. (a) Ni kwa njia gani nguvu zilizopita za Herode na Shetani zilikuwa zikiongoza mambo? (b) Safari ya kwenda Misri ilikuwaje tofauti na hekaya za apokrifa?

9 Hata hivyo, kuna nguvu zilizopita za Herode na Shetani ambazo zilikuwa zinaongoza mambo. Jinsi gani? Wageni hao walipomwona Yesu na mama yake, walitoa zawadi, na hawakuomba chochote. Yosefu na Maria walishangaa kama nini kupata kwa ghafula “dhahabu na ubani na manemane”—vitu vyenye thamani! Wanajimu hao walikusudia kurudi ili wamwambie Mfalme Herode mahali walipompata yule mtoto. Hata hivyo, Yehova aliingilia kati. Kupitia ndoto, aliwaagiza wanajimu hao warudi kwao wakitumia njia tofauti.​—Mathayo 2:1-12.

10 Muda mfupi baada ya wanajimu kuondoka, Yosefu alipewa onyo hili na malaika wa Yehova: “Simama, mchukue huyo mtoto mchanga na mama yake mkimbie kuingia Misri, mkae huko mpaka nikupe agizo; kwa maana Herode yuko karibu kumtafuta huyo mtoto amwangamize.” (Mt. 2:13) Kwa hiyo, kama tulivyoona mwanzoni, Yosefu alitii mara moja. Alitaka sana kumlinda mtoto wake, hivyo akaondoka na familia yake kwenda Misri. Kwa kuwa wale wanajimu wapagani waliipa familia hiyo vitu vyenye thamani, sasa Yosefu angeweza kuitunza familia ikiwa safarini na pia huko Misri.

Yosefu alichukua hatua bila ubinafsi ili kumlinda mtoto wake

11 Baadaye, mafumbo na hekaya za apokrifa zilitia chumvi safari hiyo ya kwenda Misri, na kudai kwamba mtoto Yesu alifupisha safari hiyo kimuujiza, akawashinda nguvu majambazi, na hata akafanya mitende iiname ili mama yake achume tende. * Ukweli ni kwamba walitembea mwendo mrefu wenye kuchosha.

Yosefu alijinyima starehe ili alinde familia yake

12. Wazazi wanaolea watoto katika ulimwengu huu hatari wanajifunza nini kutoka kwa Yosefu?

12 Wazazi wanaweza kujifunza mengi kutoka kwa Yosefu. Alikuwa tayari kuacha kazi yake na kujinyima starehe ili alinde familia yake kutokana na hatari. Ni wazi kwamba aliiona familia yake kuwa kitu kitakatifu na chenye thamani alichopewa na Yehova. Leo, wazazi wanalea watoto wao katika ulimwengu usio salama, uliojaa uvutano hatari wenye kupotosha, na unaoweza kuwaangamiza vijana. Inapendeza kama nini kuona wazazi ambao kama Yosefu wanachukua hatua mara moja ili kuwalinda watoto wao kutokana na uvutano hatari!

Yosefu Aliandalia Familia Yake

13, 14. Ni nini kilichofanya Yosefu na familia yake wahamie Nazareti?

13 Inaonekana familia hiyo haikuishi sana huko Misri, kwa kuwa baada ya muda mfupi malaika alimwambia Yosefu kwamba Herode alikuwa amekufa. Yosefu aliirudisha familia yake katika nchi yao. Unabii uliotolewa zamani ulitabiri kuwa Yehova angemwita Mwana wake “kutoka Misri.” (Mt. 2:15) Yosefu alishiriki kutimiza unabii huo, lakini sasa angepeleka familia yake wapi?

14 Yosefu alikuwa mwenye tahadhari. Kwa hekima alimwogopa Arkelao aliyetawala baada ya Herode, na ambaye pia alikuwa mkatili na muuaji. Mungu alimwongoza Yosefu kuipeleka familia yake upande wa kaskazini, katika eneo la nyumbani kwao huko Nazareti ya Galilaya, mbali na Yerusalemu na hila zake. Aliishi huko pamoja na familia yake.​—Soma Mathayo 2:19-23.

15, 16. Yosefu alifanya kazi gani na huenda alitumia vifaa gani?

15 Waliishi maisha rahisi, lakini yaliyokuwa magumu. Biblia inasema Yosefu alikuwa seremala, na inatumia neno ambalo linahusisha ufundi mbalimbali wa kutumia mbao, kama vile kukata miti, kuikokota, na kuikausha ili itumiwe kujenga nyumba, kutengeneza mashua, madaraja madogo, mikokoteni, magurudumu, nira, na vifaa mbalimbali vya kilimo. (Mt. 13:55) Ilikuwa kazi ngumu sana. Mara nyingi seremala katika nyakati za Biblia alifanya kazi karibu na mlango wa nyumba yake ndogo au katika kibanda kilichokuwa karibu.

16 Yosefu alitumia vifaa mbalimbali na huenda alirithi vingine kutoka kwa baba yake. Huenda alitumia filifili, timazi, uzi wenye chokaa, msumeno, shoka, nyundo ya chuma, nyundo ya mbao, patasi, kekee ambayo aliitumia kutoboa mashimo, gundi za aina mbalimbali, na labda misumari, ingawa ilikuwa ya bei ghali.

17, 18. (a) Yesu alijifunza nini kutokana na baba yake mlezi? (b) Kwa nini Yosefu alifanya kazi kwa bidii zaidi?

17 Wazia Yesu alipokuwa mvulana mdogo akimwona baba yake mlezi akifanya kazi. Alimtazama Yosefu kwa makini, na bila shaka alifurahia kuona mabega na mikono yenye nguvu iliyofanya kazi kwa ustadi, na jinsi alivyotumia busara. Labda Yosefu alianza kumzoeza mvulana wake jinsi ya kufanya kazi rahisi kama vile kusugua mikwaruzo kwenye mbao akitumia ngozi ya samaki iliyokaushwa. Inaelekea alimfundisha Yesu tofauti kati ya mbao alizotumia kama vile, mbao za mkuyu, mtini, mwaloni, au mzeituni.

Yosefu alimzoeza mwanawe kuwa seremala

18 Yesu alijua pia kwamba mikono hiyo yenye nguvu ambayo ilikata miti, kuchonga maboriti, na kuunganisha mbao ndiyo mikono iliyomgusa kwa wororo na kumfariji yeye, mama yake, na ndugu na dada zake wadogo. Ndiyo, Yosefu na Maria walikuwa na familia iliyoendelea kuongezeka ambayo mwishowe ilikuwa na angalau watoto saba kutia ndani Yesu. (Mt. 13:55, 56) Yosefu alifanya kazi kwa bidii zaidi ili kuwatunza na kuwalisha wote.

Yosefu alijua kwamba jambo muhimu zaidi lilikuwa kutunza familia yake kiroho

19. Yosefu aliitunzaje familia yake kiroho?

19 Hata hivyo, Yosefu alijua kwamba jambo muhimu zaidi lilikuwa kutunza familia yake kiroho. Hivyo alitenga wakati wa kuwafundisha watoto wake kumhusu Yehova Mungu na sheria Zake. Yeye na Maria walienda kwa ukawaida pamoja na watoto wao kwenye sinagogi, ambako Sheria ilisomwa na kufafanuliwa. Labda baadaye Yesu aliuliza maswali mengi na Yosefu alijitahidi kumsaidia mvulana huyo aelewe mambo ya kiroho. Pia, Yosefu aliipeleka familia yake kwenye sherehe za kidini huko Yerusalemu. Ili kuhudhuria sherehe ya Pasaka kila mwaka, huenda Yosefu alihitaji kusafiri kwa majuma mawili umbali wa kilomita 110, ili kusherehekea na kisha wangerudi nyumbani.

Yosefu aliipeleka familia yake kwa ukawaida kuabudu katika hekalu huko Yerusalemu

20. Wakristo ambao ni vichwa vya familia wanawezaje kuiga mfano wa Yosefu?

20 Leo, vichwa vya familia wanafanya vivyo hivyo. Wanajitolea kuwasaidia watoto wao, na wanatanguliza mazoezi ya kiroho badala ya mambo ya kimwili. Wanajitahidi kuongoza ibada ya familia nyumbani na kwenda pamoja na watoto wao kwenye mikutano na makusanyiko ya Kikristo. Kama Yosefu, wanajua hilo ndilo jambo lenye thamani zaidi wanaloweza kuwafanyia watoto wao.

“Hangaiko la Akilini”

21. Familia ya Yosefu ilifanya nini wakati wa Pasaka, na Yosefu na Maria walitambua wakati gani kwamba Yesu hakuwa pamoja nao?

21 Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12, kama kawaida Yosefu aliipeleka familia yake huko Yerusalemu. Ulikuwa wakati wa sherehe ya Pasaka, na familia kubwa zilisafiri pamoja katika misafara mirefu kwenye maeneo ya mashambani. Walipokaribia eneo lisilo na mimea karibu na jiji la Yerusalemu, wengi walianza kuimba zaburi za sifa zilizojulikana sana. (Zab. 120-134) Huenda jiji hilo lilijaa watu wengi. Baadaye, familia zilianza kurudi nyumbani zikiwa katika misafara. Wakiwa na mengi ya kufanya, labda Yosefu na Maria walidhani Yesu alikuwa akisafiri pamoja na washiriki wengine wa familia. Baada tu ya kusafiri mwendo wa siku moja kutoka Yerusalemu walitambua jambo lenye kushtua, Yesu hakuwa pamoja nao!​—Luka 2:41-44.

22, 23. Yosefu na Maria walifanya nini walipomkosa Yesu, na Maria alisema nini walipompata?

22 Kwa haraka walirudi mpaka Yerusalemu. Wazia jinsi walivyohangaika walipopita katika barabara za jiji hilo, huku wakiita jina la mwana wao. Mvulana huyo alikuwa wapi? Baada ya kutafuta kwa siku tatu, huenda Yosefu alifikiri alikuwa ameshindwa kutimiza mgawo mtakatifu aliopewa na Yehova. Mwishowe wakaenda hekaluni. Wakiwa huko, wakaona chumba fulani ambamo wanaume wengi wenye elimu, waliojua Sheria walikuwa wamekusanyika, huku kijana Yesu akiwa ameketi katikati yao! Wazia kitulizo ambacho Yosefu na Maria walipata!​—Luka 2:45, 46.

23 Yesu alikuwa akiwasikiliza wanaume hao wenye elimu na kuwauliza maswali. Wanaume hao walishangazwa na ufahamu na majibu ya mtoto huyo. Hata hivyo, Maria na Yosefu walishtuka. Kulingana na simulizi hilo, Yosefu hasemi chochote. Lakini maneno ya Maria yanaonyesha jinsi walivyohisi: “Mtoto, kwa nini umetutendea hivi? Tazama, baba yako nami tumekuwa tukikutafuta tukiwa na hangaiko la akilini.”​—Luka 2:47, 48.

24. Biblia inatuonyeshaje kihalisi hali ambazo wazazi hukabili?

24 Hivyo, kwa ufupi, Neno la Mungu linatuonyesha kihalisi hali ambazo wazazi hukabili. Si rahisi hata kama mtoto ni mkamilifu! Wazazi katika ulimwengu huu hatari wanaweza kupatwa na “hangaiko la akilini” kwa kiwango kikubwa, lakini wanafarijika kujua kwamba Biblia inakubali kwamba si rahisi kulea watoto.

25, 26. Yesu aliwajibuje wazazi wake, na huenda Yosefu alihisije kuhusu maneno ya mwanawe?

25 Yesu alibaki mahali pekee ambapo alijihisi akiwa karibu zaidi na Baba yake wa mbinguni Yehova, huku akijitahidi kujifunza mengi iwezekanavyo. Aliwajibu wazazi wake hivi kwa unyoofu: “Kwa nini mlilazimika kunitafuta? Je, hamkujua kwamba ni lazima niwe katika nyumba ya Baba yangu?”​—Luka 2:49.

26 Bila shaka, Yosefu alifikiria maneno hayo tena na tena. Labda yalimfurahisha. Kwa kweli, alikuwa amejitahidi kumfundisha Yesu ahisi hivyo kumwelekea Yehova Mungu. Akiwa bado mvulana, tayari Yesu alitambua maana ya neno “baba”—hasa huenda kwa sababu ya kushirikiana na Yosefu.

27. Kama wewe ni baba una pendeleo gani, na kwa nini unapaswa kuiga mfano wa Yosefu?

27 Ikiwa wewe ni baba, je, unatambua pendeleo lako la kuwasaidia watoto wako waelewe maana ya kuwa baba mwenye upendo na mwenye kujali? Vilevile, ikiwa unawalea watoto ambao si wako, kumbuka mfano wa Yosefu na umtendee kila mmoja kwa njia ya pekee na kumthamini. Wasaidie wamkaribie zaidi Baba yao wa mbinguni, Yehova Mungu.​Soma  Waefeso 6:4.

Yosefu Alivumilia kwa Uaminifu

28, 29. (a) Maneno yaliyo kwenye Luka 2:51, 52 yanafunua nini kumhusu Yosefu? (b) Yosefu alimsaidiaje mwanawe azidi kupata hekima?

28 Biblia inafunua habari nyingine chache kuhusu maisha ya Yosefu, lakini ni vizuri tuzichunguze kwa makini. Tunasoma kwamba Yesu “aliendelea kujitiisha” kwa wazazi wake. Pia, tunasoma kwamba “Yesu alizidi kufanya maendeleo katika hekima na ukuzi wa kimwili, akipata kibali kwa Mungu na wanadamu.” (Soma Luka 2:51, 52.) Maneno hayo yanafunua nini kumhusu Yosefu? Mambo kadhaa. Tunajifunza kwamba Yosefu aliendelea kuiongoza familia yake, kwa kuwa mwanawe mkamilifu aliheshimu mamlaka ya baba yake na akaendelea kujitiisha kwake.

29 Pia, tunajifunza kwamba Yesu alizidi kuwa na hekima. Bila shaka, Yosefu alimsaidia mwanawe kupata hekima hiyo. Siku hizo, Wayahudi walikuwa na methali waliyopenda sana. Bado inapatikana leo katika vitabu. Ilisema kwamba wanaume walioishi maisha ya starehe ndio tu waliokuwa wenye hekima, na watu wenye ustadi kama vile maseremala, wakulima, na wahunzi, “hawakujua sheria na hukumu; na hawangepatikana mahali ambapo mafumbo yalitolewa.” Baadaye, Yesu alithibitisha kwamba methali hiyo ilikuwa ya uwongo. Akiwa mvulana, Yesu alimsikia baba yake mlezi akifundisha kwa ustadi kuhusu “sheria na hukumu” za Yehova, ingawa alikuwa seremala maskini. Na kwa kweli alimsikia mara nyingi.

30. Yosefu aliwawekeaje vichwa vya familia mfano mzuri?

30 Vilevile, tunaona kwamba Yosefu alimsaidia Yesu kukomaa kimwili. Kwa sababu ya malezi mazuri, Yesu alikomaa na kuwa mwanamume mwenye afya na nguvu. Zaidi ya hayo, Yosefu alimzoeza mwanawe kuwa fundi stadi. Yesu hakujulikana tu kama mwana wa seremala, bali pia kama “yule seremala.” (Marko 6:3) Hivyo, mazoezi ya Yosefu yalikuwa na matokeo mazuri. Kwa hekima, vichwa vya familia wanamwiga Yosefu, kwa kuwatunza watoto wao na kuhakikisha kwamba wanaweza kujitegemea.

31. (a) Uthibitisho unaonyesha Yosefu alikufa lini? (Tia ndani sanduku  box.) (b) Yosefu alituwekea mfano gani?

31 Baada ya Biblia kutaja kuhusu kubatizwa kwa Yesu alipokuwa na umri wa miaka 30, Yosefu hatajwi tena. Uthibitisho unaonyesha kwamba Maria alikuwa mjane Yesu alipoanza huduma yake. (Ona sanduku “ Yosefu Alikufa Lini?”) Hata hivyo, Yosefu aliweka mfano bora wa baba ambaye aliilinda familia yake, akawaandalia, na kuvumilia kwa uaminifu mpaka mwisho. Kila baba, kila kichwa cha familia, na Mkristo yeyote, anapaswa kuiga imani ya Yosefu.

^ fu. 4 Siku hizo, uchumba ulionwa kuwa jambo zito kama ndoa.

^ fu. 8 “Nyota” hiyo haikuwa nyota halisi, wala haikutumwa na Mungu. Ni wazi kwamba Shetani alitumia tukio hilo lisilo la kawaida ili amwangamize Yesu.

^ fu. 11 Biblia inaonyesha waziwazi kwamba Yesu alifanya muujiza wake wa kwanza baada ya kubatizwa.—Yoh. 2:1-11.