Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA NNE

“Uendako Nitaenda”

“Uendako Nitaenda”

1, 2. (a) Fafanua safari ya Ruthu na Naomi na huzuni nyingi waliyokuwa nayo. (b) Safari ya Ruthu ilitofautianaje na ya Naomi?

RUTHU alitembea pamoja na Naomi kwenye barabara iliyopita katika nyanda ndefu za Moabu. Walikuwa peke yao, watu wawili wadogo katika eneo kubwa lisilo na watu. Wazia Ruthu akitambua kwamba ni jioni, kisha anamtazama mama mkwe wake na kuwaza kama ni wakati wa kutafuta mahali pa kupumzika usiku. Alimpenda sana Naomi na alikuwa tayari kufanya lolote ili kumtunza.

2 Wote wawili walikuwa na huzuni nyingi sana. Tayari Naomi alikuwa mjane kwa miaka kadhaa, lakini sasa alikuwa akiomboleza misiba mingine, vifo vya wanawe wawili Kilioni na Maloni. Ruthu pia alikuwa akiomboleza. Maloni alikuwa mume wake. Ruthu na Naomi walikuwa wakielekea Bethlehemu, mji uliokuwa huko Israeli. Hata hivyo, safari zao zilitofautiana kwa njia fulani. Naomi alikuwa akirudi nyumbani. Naye Ruthu alikuwa akienda mahali asipopajua, huku akiacha watu wake wa ukoo, nchi yake, na tamaduni zake zote, kutia ndani miungu ya nchi hiyo.​Soma  Ruthu 1:3-6.

3. Ni majibu ya maswali gani ambayo yatatusaidia kuiga imani ya Ruthu?

3 Ni nini kingemchochea mwanamke kijana afanye mabadiliko makubwa hivyo? Ruthu angeanzaje upya maisha na angewezaje kumtunza Naomi? Tunapochunguza majibu ya maswali hayo, tutapata mambo mengi tunayoweza kuiga kuhusu imani ya Ruthu Mmoabu. (Ona pia sanduku  “Kazi Ndogo ya Usanii.”) Kwanza, acheni tuone jinsi wanawake hao wawili walivyojipata kwenye barabara hiyo ndefu ya kwenda Bethlehemu.

Familia Iliyovunjwa na Misiba

4, 5. (a) Kwa nini familia ya Naomi ilihamia Moabu? (b) Naomi alikabiliana na matatizo gani huko Moabu?

4 Ruthu alilelewa huko Moabu, nchi ndogo iliyokuwa upande wa mashariki wa Bahari ya Chumvi. Nchi hiyo ilikuwa na maeneo yaliyoinuka yenye miti michache na mabonde yenye kina kirefu. Mara nyingi, “nchi ya Moabu” ilikuwa na mazao mengi, hata nchi ya Israeli ilipokumbwa na janga la njaa. Hiyo ndiyo sababu iliyomfanya Ruthu akutane na Maloni na familia yao.—Rut. 1:1.

5 Janga la njaa katika nchi ya Israeli lilikuwa limefanya mume wa Naomi, Elimeleki, amchukue mkewe na wanawe wawili kutoka nchi yao na kwenda kuishi Moabu wakiwa wakaaji wageni. Ni lazima hatua hiyo ilijaribu imani ya kila mshiriki wa familia, kwa kuwa Waisraeli walihitaji kwenda kwa ukawaida mahali patakatifu ambapo Yehova alikuwa amechagua ili kuabudu. (Kum. 16:16, 17) Naomi alifaulu kushikilia imani yake. Hata hivyo, bado aliomboleza baada ya mumewe kufa.​—Rut. 1:2, 3.

6, 7. (a) Kwa nini huenda Naomi alihangaika wanawe walipooa wanawake Wamoabu? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba Naomi aliwatendea wake za wanawe kwa njia nzuri?

6 Huenda Naomi alihuzunika tena wanawe walipooa wanawake Wamoabu. (Rut. 1:4) Alijua kwamba babu yao, Abrahamu, alijitahidi sana ili kumtafutia mwanawe Isaka mke kutoka kwa watu wake, ambao walikuwa waabudu wa Yehova. (Mwa. 24:3, 4) Baadaye, Sheria ya Musa iliwaonya Waisraeli wasiwaruhusu wana na binti zao kufunga ndoa na watu wa mataifa ya kigeni, ili watu wa Mungu wasianze kuabudu sanamu.​—Kum. 7:3, 4.

7 Licha ya hayo, Maloni na Kilioni walioa wanawake Wamoabu. Iwe jambo hilo lilimhangaisha Naomi au kumvunja moyo, bado alijitahidi kuwatendea wake za wanawe, Ruthu na Orpa, kwa fadhili ya kweli na upendo. Labda alitazamia kwamba kama yeye, siku moja wangekuwa waabudu wa Yehova. Vyovyote vile, Ruthu na Orpa walimpenda sana Naomi. Uhusiano wao mzuri uliwasaidia walipopatwa na msiba. Hata kabla ya kuzaa watoto, wanawake hao vijana walifiwa na waume zao.—Rut. 1:5.

8. Huenda ni nini kilichomfanya Ruthu avutiwe na Yehova?

8 Je, imani ya kidini ya Ruthu ilimsaidia kukabiliana na msiba? Huenda haikumsaidia. Wamoabu waliabudu miungu mingi, na Kemoshi ndiye aliyekuwa mungu wao mkuu. (Hes. 21:29) Inaonekana dini ya Wamoabu ilikuwa pia na ukatili na mambo yenye kutisha yaliyokuwa ya kawaida siku hizo, kutia ndani kutoa watoto kama dhabihu. Kwa kweli, jambo lolote ambalo Ruthu alijifunza kutoka kwa Maloni au Naomi kumhusu Yehova, Mungu wa Israeli mwenye upendo na rehema, lilimfanya aone tofauti kubwa. Yehova alitawala kwa upendo, bali si kwa vitisho. (Soma Kumbukumbu la Torati 6:5.) Baada ya kukabili msiba mkubwa, huenda Ruthu alisitawisha uhusiano wa karibu zaidi na Naomi huku akimsikiliza mwanamke huyo mzee alipozungumza kumhusu Mungu mweza-yote, Yehova, kazi zake za ajabu, na jinsi alivyoshughulika na watu wake kwa upendo na rehema.

Ruthu alitenda kwa hekima kwa kukaa karibu na Naomi wakati wa majonzi na msiba

9-11. (a) Naomi, Ruthu, na Orpa walifanya uamuzi gani? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na misiba iliyowapata Naomi, Ruthu, na Orpa?

9 Kwa upande mwingine, Naomi alitamani sana kupata habari kutoka nyumbani kwao. Siku moja alisikia, labda kupitia mfanyabiashara anayesafiri, kwamba janga la njaa lilikuwa limekwisha huko Israeli. Yehova alikuwa amewakumbuka watu wake. Sasa mji wa Bethlehemu ulikuwa tena na maana yake kamili, yaani, “Nyumba ya Mkate.” Naomi akaamua kurudi nyumbani.​—Rut. 1:6.

10 Sasa Ruthu na Orpa wangefanyaje? (Rut. 1:7) Walikuwa wamesitawisha uhusiano wa karibu na Naomi kwa sababu ya mambo yaliyowapata. Inaonekana Ruthu alivutiwa na fadhili za Naomi na imani yake thabiti kwa Yehova. Wajane hao watatu waliondoka kuelekea Yuda pamoja.

11 Simulizi la Ruthu linatukumbusha kwamba misiba huwapata watu wote, wazuri na wabaya. (Mhu. 9:2, 11) Pia, linatukumbusha kwamba tunapokabiliana na misiba mikubwa, ni jambo la hekima kutafuta faraja na kitulizo kutoka kwa watu wengine, hasa wale ambao wanatafuta kimbilio katika Yehova, Mungu ambaye Naomi alimwabudu.​—Met. 17:17.

Upendo Mshikamanifu wa Ruthu

12, 13. Kwa nini Naomi alitaka Ruthu na Orpa warudi nyumbani kwao badala ya kuandamana naye, na mwanzoni wanawake hao wawili walitendaje?

12 Wajane hao watatu walipokuwa wakiendelea na safari yao, Naomi alianza kuhangaishwa na jambo lingine. Aliwafikiria wanawake hao wawili waliokuwa wakiandamana naye na upendo waliokuwa wamemwonyesha yeye na wanawe. Hakutaka kuwaongezea mizigo mingine. Ikiwa wangeacha nchi yao na kumfuata, angewasaidiaje huko Bethlehemu?

13 Mwishowe, Naomi akawaambia hivi: “Nendeni, rudini, kila mmoja nyumbani kwa mama yake. Yehova na awaonyeshe fadhili zenye upendo, kama vile tu mlivyowaonyesha wanaume hawa ambao sasa wamekufa na mimi pia.” Alionyesha pia kwamba alitumaini Yehova angewabariki kwa kuwapa waume wengine na waanze maisha mapya. “Kisha akawabusu,” simulizi hilo linasema, “nao wakaanza kupaaza sauti zao na kulia.” Ni rahisi kuelewa kwa nini Ruthu na Orpa walikuwa na uhusiano wa karibu na mwanamke huyo mwenye fadhili na asiye na ubinafsi. Wote wawili waliendelea kusisitiza hivi: “Hapana, bali tutarudi pamoja nawe kwa watu wako.”—Rut. 1:8-10.

14, 15. (a) Ni sababu gani iliyomfanya Orpa arudi? (b) Naomi alijaribuje kumshawishi Ruthu arudi pia?

14 Hata hivyo, Naomi hakushawishiwa kwa urahisi. Aliwasadikisha kwamba hangeweza kuwasaidia huko Israeli, kwa sababu hakuwa na mume wa kumwandalia, wala wana ambao wangewaoa, wala tumaini lolote. Aliwaambia kwamba alikuwa na uchungu mwingi kwa sababu hakuwa na uwezo wa kuwaandalia. Orpa alikubaliana na Naomi. Huko Moabu alikuwa na mama, watu wa familia, na makao. Lilikuwa jambo linalopatana na akili kwake kubaki Moabu. Hivyo, kwa shingo upande alimbusu Naomi, akamwambia kwaheri na kuondoka.—Rut. 1:11-14.

15 Namna gani Ruthu? Maneno ya Naomi yalimhusu pia. Hata hivyo, tunasoma hivi: “Bali Ruthu akashikamana naye.” Labda Naomi alikuwa ameanza kutembea tena barabarani alipotambua kwamba Ruthu alikuwa akimfuata. Akamwambia hivi: “Tazama! Shemeji yako amerudi kwa watu wake na kwa miungu yake. Rudi pamoja naye.” (Rut. 1:15) Maneno ya Naomi yanatufunulia jambo fulani muhimu. Orpa hakuwa tu amerudi kwa watu wake, bali pia kwa “miungu yake.” Alikuwa tayari kuendelea kumwabudu Kemoshi na miungu mingine ya uwongo. Je, Ruthu alihisi hivyo pia?

16-18. (a) Ruthu alionyeshaje upendo mshikamanifu? (b) Tunajifunza nini kutoka kwa Ruthu kuhusu upendo mshikamanifu? (Ona pia picha za wanawake hao wawili.)

16 Huku akimtazama Naomi wakiwa kwenye barabara hiyo isiyo na watu, Ruthu alikuwa na uhakika na utulivu moyoni. Alimpenda sana Naomi, na Mungu ambaye Naomi aliabudu. Hivyo Ruthu akasema: “Usiniombe nikuache, nigeuke nisifuatane nawe; kwa maana uendako nitaenda, na mahali utakapokaa usiku kucha nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu. Pale utakapokufa nitakufa nami, na hapo ndipo nitakapozikwa. Yehova na anitende hivyo na kuzidi ikiwa chochote isipokuwa kifo kitatutenganisha mimi na wewe.”​—Rut. 1:16, 17.

“Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu”

17 Maneno ya Ruthu yalikuwa ya pekee sana, hivi kwamba bado yanakumbukwa hata baada ya miaka elfu tatu kupita. Maneno yake yanafunua vizuri sifa yenye thamani, yaani, upendo mshikamanifu. Ruthu alikuwa na upendo wenye nguvu na wenye ushikamanifu sana hivi kwamba alikuwa tayari kushikamana na Naomi na kwenda naye popote pale. Wangetenganishwa tu na kifo. Watu wa Naomi wangekuwa watu wake, kwa kuwa Ruthu alikuwa tayari kuacha kila kitu alichokijua huko Moabu, hata miungu ya Wamoabu. Tofauti na Orpa, Ruthu alisema kwa moyo wote kwamba alitaka Yehova, Mungu wa Naomi, awe Mungu wake pia. *

18 Basi, wakaendelea na safari wakiwa wawili tu, kwenye barabara ndefu ya kwenda Bethlehemu. Inakadiriwa kwamba huenda safari hiyo ilichukua juma moja. Bila shaka, ingawa walikuwa na majonzi walifarijiana kwa kiasi fulani.

19. Unafikiri tunawezaje kuiga upendo mshikamanifu wa Ruthu katika mahusiano ya kifamilia, kirafiki, na kutanikoni?

19 Hata leo, watu wengi ulimwenguni wana majonzi. Katika Biblia, siku zetu zinaitwa “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” na hivyo tunakabili misiba na majonzi ya aina mbalimbali. (2 Tim. 3:1) Kwa hiyo, sifa aliyoonyesha Ruthu ni muhimu hata zaidi leo. Upendo mshikamanifu, yaani, upendo ambao hushikamana na mtu au kitu bila kuacha, ni sifa muhimu katika ulimwengu huu wenye misukosuko. Tunahitaji sifa hiyo katika ndoa, uhusiano wa familia, urafiki, na pia katika kutaniko la Kikristo. (Soma 1 Yohana 4:7, 8, 20.) Tunapoendelea kusitawisha upendo kama huo, tunaiga mfano bora wa Ruthu.

Ruthu na Naomi Huko Bethlehemu

20-22. (a) Naomi alipatwa na hali gani huko Moabu? (b) Naomi alikuwa na maoni gani yasiyofaa kuhusu matatizo yake? (Ona pia Yakobo 1:13.)

20 Bila shaka, ni rahisi kuzungumza kuhusu upendo mshikamanifu, lakini ni vigumu kuonyesha sifa hiyo kwa vitendo. Ruthu hakuwa tu na nafasi ya kumwonyesha Naomi upendo mshikamanifu bali pia Mungu aliyechagua kumwabudu, Yehova.

21 Hatimaye, wanawake hao wawili waliwasili Bethlehemu, kijiji kilichokuwa karibu kilomita 10 upande wa kusini wa Yerusalemu. Inaonekana Naomi na familia yake walijulikana sana katika mji huo mdogo, kwa kuwa habari za kurudi kwake zilisambaa kila mahali. Wanawake katika eneo hilo walimtazama na kuulizana, “Je, huyu ni Naomi?” Bila shaka, alikuwa amebadilika baada ya kuishi Moabu; kwa kumtazama, watu waliona kwamba alikuwa amekabiliana na matatizo na majonzi kwa miaka mingi.​—Rut. 1:19.

22 Naomi aliwafunulia wanawake hao wa ukoo na majirani wa zamani jinsi maisha yalivyokuwa machungu kwake. Hata alihisi kwamba jina lake lilipaswa kubadilishwa kutoka Naomi, linalomaanisha “Uzuri Wangu,” na kuwa Mara, linalomaanisha “Uchungu.” Maskini Naomi! Kama Ayubu aliyeishi kabla yake, alifikiri kwamba Yehova Mungu alikuwa amemletea matatizo.—Rut. 1:20, 21; Ayu. 2:10; 13:24-26.

23. Ruthu alianza kufikiria nini, na Sheria ya Musa ilitoa maandalizi gani kwa ajili ya maskini? (Ona pia maelezo ya chini.)

23 Wanawake hao walipoanza maisha mapya huko Bethlehemu, Ruthu alianza kufikiria jinsi ambavyo angetimiza mahitaji yake na pia ya Naomi. Alijifunza kwamba Sheria ambayo Yehova alikuwa amewapa watu wake huko Israeli ilitia ndani mpango wenye upendo kwa ajili ya maskini. Waliruhusiwa kwenda mashambani wakati wa mavuno na kuwafuata wavunaji, huku wakikusanya masalio na vilevile kuvuna nafaka kwenye kingo za mashamba. *Law. 19:9, 10; Kum. 24:19-21.

24, 25. Ruthu alifanya nini alipoingia katika mashamba ya Boazi, na kazi ya kukusanya masalio ilikuwaje?

24 Ulikuwa wakati wa kuvuna shayiri, inaelekea mwezi wa Aprili kulingana na kalenda ya kisasa, na Ruthu alienda mashambani ili kuona kama kuna mtu ambaye angemruhusu akusanye masalio. Aliingia katika shamba la mwanamume aliyeitwa Boazi, tajiri mwenye mashamba ambaye alikuwa mtu wa ukoo wa Elimeleki, mume wa Naomi aliyekuwa amekufa. Ingawa Sheria ilimruhusu kukusanya masalio, hakutumia maandalizi hayo vibaya, alimwomba ruhusa mwanamume aliyewasimamia wavunaji ili aanze kukusanya. Alimruhusu, na Ruthu akaanza kazi.​—Rut. 1:22–2:3, 7.

25 Wazia Ruthu akiwafuata wavunaji. Walipokuwa wakikata shayiri kwa miundu yao, aliinama ili aokote masuke waliyoangusha au kubakisha, akayakusanya katika miganda, na kuibeba mpaka mahali ambapo angeipiga-piga na kupata nafaka baadaye. Ilikuwa kazi ya polepole, yenye kuchosha, na ilizidi kuwa ngumu kadiri jua lilivyoendelea kuwa kali. Hata hivyo, Ruthu aliendelea kukusanya, akisimama kidogo tu ili kupangusa jasho usoni na kula chakula chepesi cha mchana katika “nyumba”—inaelekea ni kibanda kilichotengenezwa ili kuwapa wafanyakazi kivuli.

Ruthu alikuwa tayari kufanya kazi ngumu na ya hali ya chini ili atimize mahitaji yake na pia ya Naomi

26, 27. Boazi alikuwa mtu wa aina gani, na alimtendeaje Ruthu?

26 Inaelekea Ruthu hakutazamia mtu yeyote amtambue, lakini kuna mtu aliyemtambua. Boazi alimwona na kumwuliza msimamizi fulani kijana kuhusu mwanamke huyo. Boazi, mwanamume mwenye imani thabiti, aliwasalimu wafanyakazi wake—huenda wengine walikuwa vibarua wa siku moja au hata watu wa mataifa ya kigeni—akiwaambia: “Yehova na awe pamoja nanyi.” Nao wakamjibu kwa maneno kama hayo. Mwanamume huyo mwenye umri mkubwa aliyempenda Yehova alimtendea Ruthu kama bintiye.​—Rut. 2:4-7.

27 Huku akimwita “binti yangu,” Boazi alimshauri Ruthu aendelee kukusanya masalio kwenye mashamba yake na afanye kazi karibu na wanawake vijana wa nyumba yake ili asisumbuliwe na wafanyakazi wa kiume. Alihakikisha kwamba alipata chakula cha mchana. (Soma Ruthu 2:8, 9, 14.) Zaidi ya hayo, alitafuta nafasi ya kumpongeza na kumtia moyo. Jinsi gani?

28, 29. (a) Ruthu alijulikana kuwa mtu wa aina gani? (b) Kama Ruthu, unawezaje kupata kimbilio katika Yehova?

28 Ruthu alipomwuliza Boazi kwa nini alimtendea kwa fadhili hivyo ingawa hakuwa Mwisraeli, Boazi alimwambia alikuwa amesikia yote aliyokuwa amemfanyia Naomi, mama-mkwe wake. Inaelekea Naomi alikuwa amemsifu Ruthu aliyempenda mbele ya wanawake wa Bethlehemu, na habari hizo zilikuwa zimemfikia Boazi. Pia, alijua kwamba Ruthu alikuwa ameanza kumwabudu Yehova, kwa kuwa alisema: “Yehova na akupe thawabu kwa sababu ya jinsi unavyotenda, na upate malipo kamili kutoka kwa Yehova Mungu wa Israeli, ambaye umekuja kutafuta kimbilio chini ya mabawa yake.”​—Rut. 2:12.

29 Kwa kweli, maneno hayo yalimtia moyo sana Ruthu! Alikuwa ameamua kutafuta kimbilio chini ya mabawa ya Yehova Mungu, kama ndege mdogo anavyojificha kando ya mama yake. Alimshukuru Boazi kwa kumtia moyo. Naye akaendelea kufanya kazi mpaka jioni.—Rut. 2:13, 17.

30, 31. Tunajifunza nini kutokana na Ruthu kuhusu mazoea mazuri ya kazi, uthamini, na upendo mshikamanifu?

30 Leo, sote tunaopambana na hali ngumu za kiuchumi tunaweza kuiga imani ya Ruthu. Hakutazamia kwamba watu wengine walipaswa kumtunza, hivyo alithamini kila jambo alilofanyiwa. Hakuaibika kufanya kazi ngumu kwa saa nyingi ili kumtunza mtu aliyempenda, ingawa ilikuwa kazi ya hali ya chini. Alifanya kazi hiyo na akafuata mashauri yenye hekima ya kufanya kazi akiwa salama na kushirikiana na watu wazuri. Jambo la maana zaidi ni kwamba hakusahau kamwe kimbilio lake la kweli, yaani, Baba yake aliyemlinda, Yehova Mungu.

31 Tukionyesha upendo mshikamanifu kama wa Ruthu na kuiga mfano wake wa unyenyekevu, bidii, na kuonyesha uthamini, imani yetu pia itaigwa na wengine. Hata hivyo, Yehova aliwaandaliaje Ruthu na Naomi? Tutazungumzia jambo hilo katika sura inayofuata.

^ fu. 17 Inapendeza kuona kwamba Ruthu hakutumia tu jina la cheo “Mungu,” kama vile ambavyo watu wengi wa mataifa ya kigeni wangefanya; alitumia jina la kibinafsi la Mungu, Yehova. Kitabu The Interpreter’s Bible kinasema hivi: “Hivyo basi, mwandikaji anakazia kwamba mgeni huyo ni mfuasi wa Mungu wa kweli.”

^ fu. 23 Ilikuwa sheria ya pekee sana, tofauti kabisa na mpango wowote ambao Ruthu alijua katika nchi yao. Zamani, katika Mashariki ya Karibu, wajane walitendewa vibaya. Kitabu kimoja cha marejezo kinasema: “Baada ya kufiwa na mumewe, kwa kawaida mjane angetegemea wanawe; kama hakuwa na wana, huenda angejiuza awe mtumwa, angefanya ukahaba, au kufa.”