Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA SABA

“Tazama! Kijakazi wa Yehova!”

“Tazama! Kijakazi wa Yehova!”

1, 2. (a) Maria alipokea salamu gani kutoka kwa mgeni? (b) Maria alikabili uamuzi gani?

MARIA alishangaa sana, mgeni alipoingia nyumbani kwake. Mgeni huyo hakuulizia baba wala mama yake. Alikuwa amekuja kumwona yeye! Mgeni huyo hakuwa mwenyeji wa Nazareti. Katika mji mdogo kama huo ilikuwa rahisi kuwatambua wageni. Hakuwa mwanadamu wa kawaida. Alimsalimu Maria katika njia isiyo ya kawaida, akisema: “Siku njema, uliyependelewa sana, Yehova yuko pamoja nawe.”—Soma Luka 1:26-28.

2 Hivyo ndivyo Biblia inavyoanza kumtaja Maria, binti ya Heli, aliyeishi Nazareti huko Galilaya. Maria alikabili uamuzi muhimu. Alikuwa amechumbiwa na seremala aliyeitwa Yosefu, ambaye hakuwa tajiri, lakini mwenye imani thabiti. Hivyo, huenda Maria aliwazia jinsi ambavyo maisha yake yangekuwa—maisha rahisi akiwa mke wa Yosefu huku wakisaidiana kutunza familia. Bila kutarajia, alitembelewa na mgeni ambaye alikuwa amemletea mgawo kutoka kwa Mungu, jukumu ambalo lingebadili maisha yake.

3, 4. Ili tumfahamu Maria, tunahitaji kuepuka nini, na badala yake tunapaswa kuzingatia nini?

3 Watu wengi hushangaa kwa sababu Biblia haisemi mengi kumhusu Maria. Inataja mambo machache kuhusu malezi yake, utu wake, na haisemi lolote kuhusu sura yake. Hata hivyo, yale ambayo Neno la Mungu linasema yanatusaidia kumfahamu.

4 Ili tumfahamu vizuri Maria, hatupaswi tu kuamini mambo ambayo dini nyingi zinafundisha kumhusu. Kwa hiyo, acheni tusifikirie michoro mingi ya Maria. Acheni pia tusahau mafundisho yasiyoeleweka kumhusu, na majina mengi ya kumkweza kama vile, “Mama ya Mungu” na “Malkia wa Mbinguni.” Badala yake acheni tukazie fikira yale ambayo Biblia inafunua. Inatufunulia habari muhimu kuhusu imani yake na jinsi tunavyoweza kumwiga.

Atembelewa na Malaika

5. (a) Tunajifunza nini kumhusu Maria kutokana na jinsi alivyoitikia salamu ya malaika Gabrieli? (b) Tunajifunza somo gani muhimu kutokana na Maria?

5 Mgeni wa Maria hakuwa mwanadamu wa kawaida. Alikuwa malaika Gabrieli. Alipomwita “uliyependelewa sana,” Maria ‘alishtuka’ kusikia maneno hayo na kushangazwa na salamu hiyo. (Luka 1:29) Alipendelewa sana na nani? Maria hakutazamia kuwa mwanadamu aliyependelewa sana. Lakini malaika alimaanisha kwamba alipendelewa na Yehova Mungu. Maria aliona jambo hilo kuwa muhimu. Lakini hakufikiria kwa kiburi kwamba tayari alikuwa amepata kibali cha Mungu. Mfano wa Maria unatufunza kwamba tunapaswa kujitahidi kupata kibali cha Yehova, badala ya kufikiri kwa kiburi kwamba tayari tumekipata. Mungu huwapinga wenye majivuno, bali huwapenda na kuwategemeza watu wa hali ya chini na wanyenyekevu.​—Yak. 4:6.

Maria hakufikiria kwa kiburi kwamba tayari alikuwa amepata kibali cha Mungu

6. Malaika alimpa Maria pendeleo gani la pekee?

6 Maria alihitaji kuwa mnyenyekevu, kwa sababu malaika alimjulisha kuhusu pendeleo la pekee sana. Alimwambia kwamba angezaa mtoto ambaye angekuwa mwanadamu muhimu kuliko wote. Gabrieli alisema: “Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, naye atatawala akiwa mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho.” (Luka 1:32, 33) Bila shaka, Maria alijua ahadi ambayo Mungu alikuwa amempa Daudi zaidi ya miaka elfu moja mapema—kwamba mmoja wa wazao wake angetawala milele. (2 Sam. 7:12, 13) Hivyo basi, mwana huyo angekuwa Masihi ambaye watu wa Mungu walimtarajia kwa karne nyingi!

Malaika Gabrieli alimjulisha Maria kuhusu pendeleo kubwa sana

7. (a) Swali la Maria lilifunua nini kumhusu? (b) Leo vijana wanawezaje kumwiga Maria?

7 Zaidi ya hayo, malaika alimwambia kwamba mtoto wake angekuwa “Mwana wa Aliye Juu Zaidi.” Mwanamke angewezaje kuzaa Mwana wa Mungu? Kwa kweli, Maria angewezaje kuzaa mwana? Alikuwa amechumbiwa na Yosefu lakini hakuwa ameolewa. Maria aliuliza swali hili kwa unyoofu: “Hilo litawezekanaje, kwa kuwa silali na mwanamume?” (Luka 1:34) Ona kwamba Maria alizungumza kuhusu ubikira wake bila kuona aibu. Alijivunia ubikira wake. Leo, vijana wengi wako tayari kupoteza ubikira wao na hata wanawadhihaki wale ambao ni mabikira. Kwa kweli, ulimwengu umebadilika. Hata hivyo, Yehova hajabadilika. (Mal. 3:6) Kama ilivyokuwa katika siku za Maria, bado anawathamini wale wanaofuata viwango vyake vya maadili.​—Soma Waebrania 13:4.

8. Ingawa Maria hakuwa mkamilifu angewezaje kutokeza uzao mkamilifu?

8 Ingawa Maria alikuwa mtumishi mwaminifu wa Mungu, bado alikuwa mwanadamu asiye mkamilifu. Angewezaje kutokeza Mwana wa Mungu, aliye mkamilifu? Gabrieli alimfafanulia: “Roho takatifu itakuja juu yako, na nguvu za Aliye Juu Zaidi zitakufunika. Kwa sababu hiyo pia kile kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.” (Luka 1:35) Utakatifu humaanisha “usafi,” au “utakato.” Kwa kawaida watoto hurithi dhambi kutoka kwa wazazi wao. Hata hivyo, katika kisa hiki, Yehova angefanya muujiza wa pekee. Angehamisha uhai wa Mwana wake kutoka mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la Maria na kwa kutumia nguvu zake, au roho takatifu, ‘kumfunika’ Maria, ili kumkinga mtoto huyo asipate dhambi. Je, Maria aliamini ahadi ya malaika? Aliitikiaje?

Maria Aliitikiaje

9. (a) Kwa nini watu fulani wanakosea wanapotilia shaka simulizi kumhusu Maria? (b) Gabrieli aliimarishaje imani ya Maria?

9 Watu wengi kutia ndani wanatheolojia wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, hawaamini kwamba bikira angepata mtoto. Ingawa wana elimu, wameshindwa kuelewa ukweli rahisi. Kama Gabrieli alivyosema, “kwa Mungu hakuna tangazo lolote lisilowezekana.” (Luka 1:37) Maria aliamini maneno ya Gabrieli kwa sababu alikuwa mwanamke mwenye imani yenye nguvu. Hata hivyo, Maria hakuamini tu bila uthibitisho wowote. Kama ambavyo mtu yeyote mwenye akili angefanya, Maria alihitaji uthibitisho ili aamini. Malaika Gabrieli alimpa uthibitisho zaidi. Alimwambia kumhusu Elisabeti, mtu wa jamaa yake aliyezeeka, na ambaye alikuwa tasa. Mungu alikuwa amemwezesha Elisabeti kupata mimba kimuujiza!

10. Kwa nini hatupaswi kufikiri kwamba pendeleo la Maria lilikuwa rahisi?

10 Maria angefanya nini? Alikuwa amepewa mgawo na alikuwa na hakika kwamba Mungu angetimiza yote ambayo Gabrieli alikuwa amesema. Ingawa lilikuwa pendeleo kubwa, haikuwa rahisi kwa Maria. Kwanza, alikuwa mchumba wa Yosefu. Je, angekubali kumwoa ikiwa angegundua kwamba alikuwa mjamzito? Jambo lingine ni kwamba alikuwa na jukumu zito. Maria angebeba uhai wa kiumbe muhimu kuliko wote, yaani, Mwana mpendwa wa Mungu! Alipaswa kumtunza akiwa mtoto mchanga na kumlinda katika ulimwengu mwovu. Lilikuwa jambo zito kweli kweli!

11, 12. (a) Wakati mwingine watu wenye imani thabiti wameitikiaje migawo migumu kutoka kwa Mungu? (b) Maria alifunua nini kujihusu katika jibu lake kwa Gabrieli?

11 Biblia inaonyesha kwamba wakati mwingine hata watumishi waaminifu walisitasita kukubali mgawo kutoka kwa Mungu. Musa alisema kwamba hangekuwa msemaji wa Mungu kwa sababu hakuzungumza kwa ufasaha. (Kut. 4:10) Yeremia alisema kwamba alikuwa “mvulana tu,” asiyeweza kutimiza mgawo aliopewa na Mungu. (Yer. 1:6) Na Yona alikimbia mgawo wake! (Yona 1:3) Namna gani Maria?

12 Maneno yake ya unyenyekevu na utii, yanakumbukwa mpaka leo. Alimwambia Gabrieli: “Tazama! Kijakazi wa Yehova! Na itendeke kwangu kulingana na tangazo lako.” (Luka 1:38) Kijakazi alikuwa mtumishi wa hali ya chini, ambaye maisha yake yalitegemea kabisa bwana mkubwa wake. Hivyo ndivyo Maria alivyohisi kuhusu Yehova, Bwana mkubwa wake. Alijua kwamba angekuwa salama katika mikono ya yake, na kwamba ni mshikamanifu kwa wale ambao ni washikamanifu kwake, na angembariki ikiwa angejitahidi kabisa kutimiza mgawo huo mgumu.​Zab. 18:25.

Maria alijua kwamba alikuwa salama katika mikono ya Mungu wake mshikamanifu, Yehova

13. Ikiwa tunaona ni vigumu kufanya mambo ambayo Mungu anataka, tunaweza kujifunza nini kutoka kwa Maria?

13 Nyakati nyingine Mungu anaweza kutuomba tufanye jambo ambalo huenda tukaona kuwa gumu, hata lisilowezekana. Hata hivyo, katika Neno lake anatupa sababu za kumtegemea, kujiweka kwenye mikono yake, kama Maria alivyofanya. (Met. 3:5, 6) Je, tutamtegemea? Tukifanya hivyo, atatuthawabisha na hivyo kuimarisha imani yetu.

Maria Amtembelea Elisabeti

14, 15. (a) Yehova alimbarikije Maria alipowatembelea Elisabeti na Zekaria? (b) Maneno ya Maria yaliyorekodiwa kwenye Luka 1:46-55 yanafunua nini kumhusu?

14 Maneno ambayo Gabrieli alimwambia Maria yalikuwa muhimu kwake. Nani kati ya wanawake wote ulimwenguni angeelewa hali yake vizuri? Maria alielekea kwenye eneo lenye milima la Yuda, safari ya siku tatu au nne. Alipoingia nyumbani kwa Elisabeti na kuhani Zekaria, Yehova alimthawabisha kwa kumpa uthibitisho mwingine ulioimarisha imani yake. Elisabeti aliposikia salamu ya Maria, mara moja akahisi mtoto aliyekuwa katika tumbo lake akiruka kwa shangwe. Elisabeti akajawa na roho takatifu na akamwita Maria “mama ya Bwana wangu.” Mungu alikuwa amemfunulia Elisabeti kwamba mwana wa Maria angekuwa Bwana, yaani, Masihi. Zaidi ya hayo, alimpongeza Maria kwa utii na uaminifu wake, akisema: “Mwenye furaha pia ni yule aliyeamini.” (Luka 1:39-45) Naam, yote ambayo Yehova alikuwa amemwahidi Maria yangetimia!

Urafiki kati ya Maria na Elisabeti uliwaletea baraka

15 Maria akajibu. Maneno yake yamehifadhiwa katika Neno la Mungu. (Soma Luka 1:46-55.) Na hiyo ndiyo rekodi ndefu zaidi ya maneno ya Maria katika Biblia, na yanafunua mengi kumhusu. Yanaonyesha mtazamo wake wa shukrani na uthamini, alipokuwa akimtukuza Yehova kwa sababu ya baraka ya kuwa mama ya Masihi. Yanaonyesha kina cha imani yake, anaposema Yehova huwashusha wenye nguvu na majivuno na kuwasaidia watu wa hali ya chini na maskini wanaojitahidi kumtumikia. Pia, yanaonyesha ujuzi aliokuwa nao. Kulingana na kadirio fulani, alirejezea Maandiko ya Kiebrania zaidi ya mara 20! *

16, 17. (a) Maria na mwanawe walionyesha mtazamo gani ambao tunapaswa kuiga? (b) Urafiki wa Maria na Elisabeti unatukumbusha kuhusu baraka gani?

16 Ni wazi kwamba, Maria alitafakari sana Neno la Mungu. Lakini aliendelea kuwa mnyenyekevu, na kunukuu Maandiko badala ya kusema maneno yake mwenyewe. Baadaye, mwana aliyekuwa tumboni mwake angeonyesha unyenyekevu kama huo, kwa kusema: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.” (Yoh. 7:16) Tunapaswa kujiuliza: ‘Je, ninaonyesha kwamba ninaheshimu hivyo Neno la Mungu? Au je, ninaona maoni na mafundisho yangu kuwa muhimu?’ Maria alikuwa na mtazamo unaofaa.

17 Maria alikaa na Elisabeti kwa karibu miezi mitatu, na bila shaka walitiana moyo sana. (Luka 1:56) Simulizi hili la Biblia linaonyesha jinsi urafiki unavyoweza kutufaidi. Tukichagua marafiki wanaompenda kikweli Mungu wetu Yehova, tutakomaa kiroho na kumkaribia Mungu hata zaidi. (Met. 13:20) Hatimaye wakati wa Maria kurudi nyumbani ulifika. Yosefu angesema nini baada ya kujua hali yake?

Maria na Yosefu

18. Maria alimwambia Yosefu nini, naye aliitikiaje?

18 Maria hakungoja mimba yake ionekane ndipo amwambie Yosefu. Alipaswa kumwambia Yosefu. Huenda kabla ya kuzungumza naye, hakujua Yosefu angeitikiaje. Ingawa hivyo, alimfikia na kumweleza yote yaliyokuwa yametokea. Bila shaka, Yosefu alihangaishwa sana na jambo hilo. Alitaka kumwamini msichana huyo mrembo lakini ilionekana kwamba hakuwa mwaminifu. Biblia haisemi Yosefu alikuwa akiwaza nini wakati huo. Lakini inasema aliamua kumtaliki, kwa kuwa wakati huo, watu waliochumbiana walionwa kana kwamba wameoana. Hata hivyo, hakutaka kumwaibisha, basi akaamua kumtaliki kisiri. (Mt. 1:18, 19) Maria aliumia sana kumwona Yosefu akihangaishwa na hali hiyo. Licha ya hayo, Maria hakumkasirikia.

19. Yehova alimsaidiaje Yosefu kufanya uamuzi mzuri?

19 Kwa fadhili, Yehova alimsaidia Yosefu kufanya uamuzi mzuri. Katika ndoto, malaika wa Mungu alimwambia kwamba Maria alipata mimba kimuujiza. Hilo lilimtuliza Yosefu. Sasa Yosefu akafanya kile ambacho Maria alikuwa amefanya tangu mwanzoni—alimtii Yehova. Akamchukua Maria awe mke wake, na akajitayarisha kwa ajili ya jukumu la pekee la kumtunza Mwana wa Yehova.—Mt. 1:20-24.

20, 21. Wenzi wa ndoa na wale wanaofikiria kufunga ndoa, wanajifunza nini kutokana na mfano wa Maria na Yosefu?

20 Wenzi wa ndoa pamoja na wale ambao wanafikiria kufunga ndoa wanapaswa kutafakari mfano wa wenzi hawa walioishi miaka 2,000 iliyopita. Yosefu alipomwona mke wake akitimiza majukumu yake akiwa mama, bila shaka alifurahi kwamba malaika wa Yehova alikuwa amemwongoza. Aliona umuhimu wa kumtegemea Yehova wakati wa kufanya maamuzi. (Zab. 37:5; Met. 18:13) Bila shaka, aliendelea kufanya maamuzi kwa uangalifu akiwa kichwa cha familia.

21 Kwa upande mwingine, tunajifunza nini kutokana na uamuzi wa Maria wa kukubali kuolewa na Yosefu? Ingawa mwanzoni hali ilikuwa ngumu, Maria alingoja Yosefu atoe mwongozo kwa sababu yeye ndiye angekuwa kichwa cha familia. Hilo lilikuwa somo zuri kwake, kama ilivyo kwa wanawake Wakristo leo. Mwishowe, matukio hayo yaliwafundisha Yosefu na Maria umuhimu wa kuwa wanyoofu na kuzungumza waziwazi.​Soma  Methali 15:22.

22. Yosefu na Maria waliwekea ndoa yao msingi gani, na ni matarajio gani yaliyokuwa mbele yao?

22 Kwa kweli, wenzi hao wa ndoa vijana walianzisha ndoa yao kwenye msingi thabiti. Wote walimpenda Yehova Mungu na walitaka sana kumpendeza wakiwa wazazi wenye kuwajibika na wenye kujali. Bila shaka, baadaye wangepata baraka nyingi na pia wangekabili hali ngumu. Walikuwa na jukumu la kumlea Yesu ambaye baadaye angekuwa mtu mkuu zaidi aliyewahi kuishi duniani.

^ fu. 15 Miongoni mwa marejeo hayo, inaonekana Maria alimnukuu mwanamke mwaminifu Hana, ambaye pia aliwahi kupokea baraka kutoka kwa Yehova ya kupata mtoto.—Ona sanduku “Sala Mbili za Pekee,” kwenye Sura ya Sita.