Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA TANO

“Mwanamke Bora Sana”

“Mwanamke Bora Sana”

1, 2. (a) Ruthu alikuwa akifanya kazi gani? (b) Ruthu alitambua mambo gani mazuri kuhusu Sheria ya Mungu na watu wake?

RUTHU alipiga magoti kando ya vishina vya shayiri ambavyo alikuwa amekusanya mchana. Giza lilikuwa likiingia kwenye mashamba huko Bethlehemu, na tayari wafanyakazi wengi walikuwa wakielekea kwenye lango la jiji dogo lililokuwa juu ya bonde ambalo lilikuwa karibu. Ruthu alihisi maumivu ya uchovu baada ya kufanya kazi mchana kutwa. Lakini, aliendelea kupiga vishina akitumia ufito mdogo au gongo ili apatenafaka. Ingawa hivyo, ilikuwa siku njema, kuliko jinsi alivyotazamia.

2 Je, mambo yalikuwa yameanza kumwendea vema mjane huyo kijana? Kama tulivyoona katika sura iliyotangulia, alikuwa amemfuata mama-mkwe wake, Naomi, na akaapa kushikamana naye na kumfanya Yehova, Mungu wa Naomi, awe Mungu wake. Wajane hao wawili walikuwa wamekuja Bethlehemu kutoka Moabu, na Ruthu Mmoabu alitambua kwamba Sheria ya Yehova ilikuwa yenye faida, iliandaa mpango uliowastahi maskini huko Israeli, kutia ndani wageni. Na sasa alitambua kwamba baadhi ya watu wa Yehova, ambao walifuata Sheria na kuzoezwa nayo, walionyesha fadhili na walimpenda Yehova na hilo liligusa moyo wa Ruthu uliokuwa umeumia.

3, 4. (a) Boazi alikuwa amefanya nini ili kumtia moyo Ruthu? (b) Mfano wa Ruthu unawezaje kutusaidia katika siku hizi zenye matatizo ya kiuchumi?

3 Mmoja kati ya watu hao ni Boazi, mwanamume tajiri mwenye umri mkubwa ambaye Ruthu alikuwa akikusanya masalio katika mashamba yake. Siku hiyo, mwanamume huyo alikuwa amemtendea kama bintiye. Ruthu alitabasamu alipofikiria maneno ya Boazi yenye fadhili alipomsifu kwa kumtunza Naomi aliyezeeka na kwa kuchagua kutafuta kimbilio chini ya mabawa ya Mungu wa kweli, Yehova.​Soma  Ruthu 2:11-14.

4 Lakini bado huenda Ruthu alihangaikia maisha yake ya baadaye. Akiwa mgeni maskini asiye na mume wala mtoto, angewezaje kujitegemeza na kumtunza Naomi katika miaka ya baadaye? Je, angeendelea kukusanya masalio? Na ni nani angemtunza yeye mwenyewe wakati wa uzee? Inaeleweka ikiwa Ruthu alihangaishwa na mawazo kama hayo. Leo, katika nyakati hizi zenye matatizo ya kiuchumi, wengi hupambana na mahangaiko kama hayo. Tunapochunguza jinsi imani ya Ruthu ilivyomsaidia kukabiliana na matatizo hayo, tutajifunza mengi kutoka kwake.

Ni Nani Wanaofanyiza Familia?

5, 6. (a) Ruthu alifanikiwa kupata nini siku yake ya kwanza ya kukusanya masalio kwenye mashamba ya Boazi? (b) Naomi alitendaje alipomwona Ruthu?

5 Ruthu alipomaliza kupura nafaka na kuikusanya, alitambua kwamba alikuwa amekusanya shayiri karibu kipimo kimoja cha efa. Huenda mzigo wake ulikuwa na uzito wa kilo 14! Akainua mzigo wake, labda akiwa ameufunga kwa kitambaa na kuubeba kichwani, kisha akatembea kuelekea Bethlehemu huku jua likitua.​—Rut. 2:17.

6 Naomi alifurahi kumwona binti-mkwe wake mpendwa na labda alishangaa alipoona mzigo mzito wa shayiri ambao Ruthu alikuwa amebeba. Ruthu pia alileta chakula alichobakisha ambacho Boazi alikuwa amewaletea wafanyakazi wake, na hivyo wakala pamoja. Naomi akauliza: “Uliokota masalio wapi leo, nawe ulifanya kazi wapi? Yule aliyekuona na abarikiwe.” (Rut. 2: 19) Naomi alitazama kwa makini; akatambua mzigo mzito wa Ruthu ulioonyesha kwamba mtu fulani alikuwa amemwona mjane huyo kijana na kumtendea kwa fadhili.

7, 8. (a) Naomi aliona fadhili za Boazi kuwa zinatoka kwa nani, na kwa nini? (b) Ruthu alimwonyeshaje tena Naomi upendo mshikamanifu?

7 Wakaanza kuzungumza, na Ruthu akamwambia Naomi jinsi Boazi alivyomtendea kwa fadhili. Akichochewa na jambo hilo, Naomi akajibu: “Na abarikiwe huyo na Yehova, ambaye hakuacha kuonyesha fadhili zake zenye upendo kwa walio hai na wafu.” (Rut. 2:20) Aliona fadhili za Boazi kuwa zilitoka kwa Yehova, ambaye huchochea watumishi wake wawe wakarimu na ambaye ameahidi kuwathawabisha watu wake kwa sababu ya fadhili wanazoonyesha. *Soma  Methali 19:17.

8 Naomi alimhimiza Ruthu akubali ombi la Boazi la kuendelea kukusanya masalio katika mashamba yake na kukaa karibu na wanawake vijana wa nyumba yake ili asisumbuliwe na wavunaji. Ruthu alifuata ushauri huo. Pia, ‘aliendelea kukaa na mama-mkwe wake.’ (Rut. 2: 22, 23) Maneno hayo yanaonyesha tena sifa kuu ya Ruthu—upendo mshikamanifu. Mfano wake unaweza kutuchochea kujichunguza kama tunaheshimu vifungo vya familia, na kuwaunga mkono kwa ushikamanifu wapendwa wetu na kuwasaidia wanapohitaji msaada. Yehova hakosi kamwe kuona upendo mshikamanifu kama huo.

Mfano wa Ruthu na Naomi unatukumbusha kwamba tunapaswa kuthamini familia zetu

9. Tunajifunza nini kutoka kwa Ruthu na Naomi kuhusu familia?

9 Je, kweli Ruthu na Naomi walifanyiza familia? Watu fulani wanaamini kwamba ni lazima familia “kamili” iwe na mtu wa kutimiza kila daraka, yaani, kuwe na mume, mke, mwana, binti, babu, nyanya (au bibi), na kadhalika. Lakini Ruthu na Naomi wanatukumbusha kwamba watumishi wa Yehova wanaweza kufungua mioyo yao na kufanya hata familia ndogo zaidi ziwe na uchangamfu, fadhili, na upendo. Je, unathamini familia yenu? Yesu aliwakumbusha wafuasi wake kwamba kutaniko la Kikristo linaweza kuwa familia hata kwa wale wasio na familia.​—Marko 10:29, 30.

Ruthu na Naomi walisaidiana na kutiana moyo

“Yeye Ni Mmoja wa Wakombozi Wetu”

10. Naomi alitaka kumsaidiaje Ruthu?

10 Kuanzia wakati wa kuvuna shayiri karibu mwezi wa Aprili mpaka wakati wa kuvuna ngano karibu Juni, Ruthu aliendelea kukusanya masalio katika mashamba ya Boazi. Majuma yalipozidi kusonga, bila shaka Naomi alifikiria zaidi jambo ambalo angemfanyia binti-mkwe wake mpendwa. Huko Moabu, Naomi alikuwa na hakika kwamba hangeweza kamwe kumsaidia Ruthu kupata mume mwingine. (Rut. 1:11-13) Hata hivyo, sasa alikuwa ameanza kufikiria kwa njia tofauti. Alimkaribia Ruthu na kumuuliza: “Binti yangu, je, sipaswi kukutafutia mahali pa kupumzika?” (Rut. 3:1) Siku hizo, wazazi walikuwa na desturi ya kuwatafutia watoto wao wenzi, na sasa Ruthu alikuwa kama binti halisi wa Naomi. Alitaka kumtafutia Ruthu “mahali pa kupumzika”—akimaanisha usalama na ulinzi ambao angepata kwa kuwa na nyumba na mume. Lakini Naomi angefanya nini?

11, 12. (a) Naomi aliposema Boazi ni “mkombozi,” alikuwa akizungumzia mpango gani wa Sheria ya Mungu? (b) Ruthu aliitikiaje ushauri wa Naomi?

11 Ruthu alipomtaja Boazi kwa mara ya kwanza, Naomi alisema: “Mwanamume huyo ni wa jamaa yetu. Yeye ni mmoja wa wakombozi wetu.” (Rut. 2: 20) Alimaanisha nini? Sheria ya Mungu kwa Waisraeli ilikuwa na mpango wenye upendo kwa familia ambazo ziliteseka kwa sababu ya umaskini au kufiwa. Ikiwa mwanamke angekuwa mjane asiye na mtoto, alikatishwa tamaa kwa sababu jina la mume wake, yaani, uzao wake, haungejulikana na vizazi vya wakati ujao. Hata hivyo, Sheria ya Mungu ilimruhusu ndugu ya mwanamume huyo amwoe yule mjane ili amzalie mrithi ambaye angeendeleza jina la mume aliyekufa na kutunza mali ya familia. *​—Kum. 25:5-7.

12 Naomi akamwambia Ruthu kuhusu mpango wake. Tunaweza kuwazia mwanamke huyo kijana akiwa na mshangao, mama-mkwe wake alipokuwa akizungumza. Sheria ya Mungu kwa Waisraeli ilikuwa bado mpya kwa Ruthu; na hakujua desturi nyingi za Sheria hiyo. Hata hivyo, alimheshimu sana Naomi hivi kwamba alisikiliza kwa makini kila neno alilosema. Huenda jambo ambalo Naomi alimshauri afanye lilionekana kuwa lisilo la kawaida au lenye kuaibisha na labda lingemfedhehesha, hata hivyo, Ruthu alikubali. Alisema hivi kwa upole: “Yote ambayo umeniambia nitafanya.”—Rut. 3:5.

13. Tunajifunza nini kutoka kwa Ruthu kuhusu kukubali ushauri wa watu wenye umri mkubwa? (Ona pia Ayubu 12:12.)

13 Nyakati nyingine ni vigumu kwa vijana kusikiliza ushauri kutoka kwa watu wenye umri mkubwa na wenye uzoefu mwingi. Ni rahisi kufikiri kwamba watu wenye umri mkubwa hawaelewi kabisa matatizo yanayowakabili vijana. Mfano wa unyenyekevu wa Ruthu unatufundisha kwamba kusikiliza hekima kutoka kwa watu wenye umri mkubwa wanaotupenda na kututakia mema kunaweza kuwa na matokeo mazuri sana. (Soma Zaburi 71:17, 18.) Lakini Naomi alimshauri Ruthu afanye nini, na je, kweli alibarikiwa kwa kutii?

Ruthu Kwenye Uwanja wa Kupuria

14. Uwanja wa kupuria ulikuwa nini, na ulitumiwaje?

14 Siku hiyo jioni, Ruthu alienda kwenye uwanja wa kupuria, mahali penye udongo mgumu uliotandazwa ambapo wakulima walipeleka nafaka zao ili kuzipura na kuzipepeta. Kwa kawaida, mahali palipochaguliwa palikuwa kando ya mlima au juu ya kilima, ambapo palikuwa na upepo wenye nguvu wakati wa alasiri na jioni. Ili kutenganisha nafaka na makapi, wafanyakazi walitumia uma mkubwa au sepetu kurusha mchanganyiko huo juu kwenye upepo, ambao ulipeperusha makapi yaliyokuwa mepesi na kuruhusu nafaka yenye uzito ianguke sakafuni.

15, 16. (a) Eleza jinsi mambo yalivyokuwa kwenye uwanja wa kupuria Boazi alipomaliza kufanya kazi jioni. (b) Boazi alitambuaje kwamba Ruthu alikuwa amelala miguuni pake?

15 Ruthu alitazama kwa busara watu walipokuwa wakifunga kazi wakati wa jioni. Boazi alisimamia kazi ya kupepeta nafaka zake, ambazo zilikusanywa katika rundo kubwa. Baada ya kula na kushiba, alilala upande mmoja wa rundo hilo. Inaonekana hilo lilikuwa zoea la kawaida, labda ili kulinda mavuno hayo yenye thamani yasiibiwe na wezi na wavamizi. Ruthu alimwona Boazi akianza kulala. Wakati ulikuwa umefika wa kufanya kama alivyoagizwa na Naomi.

16 Ruthu akatambaa na kukaribia, huku moyo ukimpigapiga. Alitambua kwamba mwanamume huyo alikuwa amelala fofofo. Hivyo, kama alivyoambiwa na Naomi, akaenda kwenye miguu ya Boazi, akaifunua, na kulala kando ya miguu yake. Kisha akangoja. Muda ukapita. Huenda Ruthu aliona kipindi hicho kuwa kirefu sana. Mwishowe, karibu saa sita usiku, Boazi akaanza kusogea-sogea. Akiwa anatetemeka kwa sababu ya baridi, alijinyoosha labda ili kufunika miguu yake. Lakini akatambua kulikuwa na mtu hapo. Simulizi hilo linasema: “Tazama! mwanamke alikuwa amelala miguuni pake!”​—Rut. 3:8.

17. Wale wanaodai kwamba Ruthu alitenda kwa njia iliyopotoka kiadili wanapuuza mambo gani mawili?

17 Akamuuliza: “Wewe ni nani?” Ruthu alijibu hivi labda sauti yake ikitetemeka: “Mimi ni Ruthu kijakazi wako, basi mfunike kijakazi wako kwa upindo wa nguo yako, kwa maana wewe ni mkombozi.” (Rut. 3:9) Wafafanuzi fulani wa kisasa wamesema kwamba kulikuwa na hisia za kimapenzi katika matendo na maneno ya Ruthu lakini wanapuuza mambo mawili muhimu. Kwanza, Ruthu alikuwa akitenda kulingana na desturi za siku hizo, na nyingi kati yazo hazipo leo. Hivyo, ingekuwa kosa kufafanua matendo yake kwa kutegemea maoni ya leo yaliyopotoka kiadili. Pili, Boazi alitenda kwa njia iliyoonyesha wazi kwamba mwenendo wa Ruthu ulikuwa safi kiadili na uliokubalika kabisa.

Ruthu alimtafuta Boazi akichochewa na tamaa inayofaa na hakuwa na ubinafsi

18. Boazi alisema nini ili kumfariji Ruthu, na alizungumzia pindi gani mbili ambazo Ruthu alionyesha fadhili zenye upendo?

18 Boazi alizungumza, na bila shaka sauti yake ya upole na yenye kutuliza ilimfariji Ruthu. Alisema: “Yehova na akubariki, binti yangu. Umeonyesha fadhili zako zenye upendo kwa njia bora zaidi mara hii ya mwisho kuliko mara ya kwanza. Hukuwafuata vijana, wawe ni wa hali ya chini au matajiri.” (Rut. 3:10) Aliposema “mara ya kwanza” alimaanisha upendo mshikamanifu ambao Ruthu alionyesha kwa kumfuata na kumtunza Naomi aliporudi Israeli. ‘Mara ya mwisho’ ilikuwa wakati huu. Boazi alitambua kwamba mwanamke kijana kama vile Ruthu angetafuta kwa urahisi mume kati ya wanaume vijana, iwe ni matajiri au maskini. Badala yake, Ruthu alitaka kufanya mema si kwa Naomi tu bali pia kwa mume wake aliyekufa, yaani, kuendeleza jina la mwanamume huyo katika nchi ya Israeli. Inaeleweka kwa nini Boazi alipendezwa na mwanamke huyo kijana ambaye hakuwa na ubinafsi.

19, 20. (a) Kwa nini Boazi hakumwoa Ruthu moja kwa moja? (b) Boazi alimwonyeshaje Ruthu fadhili na ufikirio?

19 Boazi aliendelea kusema: “Basi sasa, binti yangu, usiogope. Yote utakayosema nitakufanyia, kwa maana kila mtu aliye katika lango la watu wangu anajua kwamba wewe ni mwanamke bora sana.” (Rut. 3:11) Alipendezwa na wazo la kumwoa Ruthu; labda hakushangaa sana alipoombwa kuwa mkombozi wake. Hata hivyo, Boazi alikuwa mwanamume mwadilifu na hangefanya tu alivyopenda. Alimwambia Ruthu kwamba kulikuwa na mkombozi mwingine ambaye alikuwa mtu wa ukoo wa karibu zaidi wa familia ya Naomi. Boazi angezungumza na mwanamume huyo kwanza na kumpa nafasi ya kuwa mume wa Ruthu.

Kwa sababu Ruthu aliwatendea wengine kwa fadhili na heshima, alijulikana kuwa mwanamke bora

20 Boazi alimhimiza Ruthu alale na kupumzika mpaka asubuhi ilipokaribia; kisha angeondoka kimyakimya bila kuonekana. Alitaka kulinda jina la Ruthu na jina lake pia, kwa kuwa watu wangefikiria kimakosa kwamba walikuwa wamejihusisha na upotovu wa maadili. Ruthu alilala karibu na miguu ya mwanamume huyo tena, labda sasa akiwa ametulia akilini baada ya Boazi kusikiliza ombi lake kwa fadhili. Kisha, kulipokuwa bado na giza, Ruthu akaamka. Boazi akajaza ushungi wake kwa zawadi ya ukarimu ya shayiri na akaondoka kwenda Bethlehemu.​Soma  Ruthu 3:13-15.

21. Ni nini kilichomsaidia Ruthu ajulikane kuwa “mwanamke bora sana,” na tunawezaje kuiga mfano wake?

21 Kwa kweli, Ruthu aliridhika sana alipotafakari mambo ambayo Boazi alikuwa amemwambia, kwamba alijulikana na watu wote kuwa “mwanamke bora sana”! Bila shaka, tamaa yake ya kutaka kumjua Yehova na kumtumikia ilimsaidia sana ajulikane kwa njia hiyo. Pia, alikuwa amemtendea Naomi na watu wake kwa fadhili na ufikirio sana, akifuata kwa hiari njia na desturi ambazo hakuzijua mwanzoni. Tukiiga imani ya Ruthu, tutajitahidi kuwaheshimu wengine na pia kuheshimu njia na desturi zao. Tukifanya hivyo, huenda sisi pia tukajulikana kuwa watu bora sana.

Ruthu Apata Mahali pa Kupumzika

22, 23. (a) Huenda zawadi ambayo Boazi alimpa Ruthu ilimaanisha nini? (Ona pia maelezo ya chini.) (b) Naomi alimhimiza Ruthu afanye nini?

22 “Wewe ni nani, binti yangu?” Naomi akamuuliza Ruthu alipofika nyumbani. Labda alimuuliza hivyo kwa sababu kulikuwa na giza, lakini Naomi alitaka pia kujua ikiwa bado Ruthu alikuwa mjane yuleyule au kama sasa alitarajia kuolewa. Ruthu akamweleza haraka mama-mkwe wake mambo yote yaliyokuwa yametukia kati yake na Boazi. Kisha akampa zawadi ya ukarimu ya shayiri ambayo Boazi alikuwa amemwambia ampe Naomi. *Rut. 3:16, 17.

23 Kwa hekima, Naomi alimhimiza Ruthu akae nyumbani siku hiyo na kutulia badala ya kwenda kukusanya masalio mashambani. Alimhakikishia Ruthu hivi: “Mwanamume huyo hatapumzika mpaka amalize jambo hilo leo.”​—Rut. 3: 18.

24, 25. (a) Boazi alionyeshaje kwamba alikuwa mwanamume mnyoofu na asiye na ubinafsi? (b) Ruthu alibarikiwaje?

24 Naomi alisema kweli kumhusu Boazi. Siku hiyo, Boazi alienda kwenye lango la jiji mahali ambapo wazee wa jiji walikutana kwa ukawaida, akasubiri mpaka mwanamume ambaye alikuwa mtu wa ukoo wa karibu zaidi wa familia ya Naomi alipopita. Mbele ya mashahidi, Boazi alimpa mwanamume huyo nafasi ya kuwa mkombozi na kumwoa Ruthu. Hata hivyo, yule mwanamume alikataa akidai kwamba kufanya hivyo kungeharibu urithi wake. Kisha, mbele ya mashahidi kwenye lango la jiji, Boazi akasema angekuwa mkombozi, angenunua shamba la mume wa Naomi aliyekufa, Elimeleki, na angemwoa Ruthu, mjane wa Maloni mwana wa Elimeleki. Boazi alitumaini kwamba kwa kufanya hivyo ‘angemwinulia mwanamume aliyekufa jina katika urithi wake.’ (Rut. 4: 1-10) Kwa kweli, Boazi alikuwa mwanamume mnyoofu na asiye na ubinafsi.

25 Boazi akamwoa Ruthu. Baadaye, tunasoma hivi: “Yehova akamwezesha kupata mimba naye akazaa mwana.” Wanawake wa Bethlehemu walimbariki Naomi na kumsifu Ruthu kwa kuwa bora kwa Naomi kuliko wana saba. Baadaye, tunajifunza kwamba mwana wa Ruthu alikuwa babu ya Mfalme Daudi. (Rut. 4:11-22) Kisha, ukoo wa Daudi ukamtokeza Yesu Kristo.​—Mt. 1:1. *

Yehova alimbariki Ruthu kwa kumpa pendeleo la kuwa nyanya ya Masihi

26. Mfano wa Ruthu na Naomi unatukumbusha nini?

26 Ruthu alibarikiwa sana, na vilevile Naomi ambaye alimsaidia kumlea yule mtoto kana kwamba alikuwa wake. Maisha ya wanawake hao wawili yanatukumbusha kwamba Yehova Mungu anatambua wale wanaojitahidi kwa unyenyekevu kuandalia familia zao, na ambao wanamtumikia kwa ushikamanifu pamoja na watu wake waliochaguliwa. Hakosi kamwe kuwathawabisha watu waaminifu, kama vile Boazi, Naomi na Ruthu.

^ fu. 7 Kama Naomi alivyosema, Yehova hawaonyeshi tu fadhili walio hai; bali pia wafu. Naomi alikuwa amefiwa na mumewe na wanawe wawili. Naye Ruthu alikuwa amefiwa na mumewe. Bila shaka, wanaume hao watatu walipendwa sana na wanawake hawa wawili. Fadhili zozote ambazo Ruthu na Naomi walionyeshwa, zilikuwa fadhili kuelekea wanaume hao ambao wangetaka wanawake hawa wapendwa watunzwe.

^ fu. 11 Inaelekea ndugu za mwanamume aliyekufa ndio waliopewa kwanza haki ya kuoa mjane huyo kisha mtu wa ukoo wa karibu zaidi, kama ilivyokuwa na haki ya kupokea urithi.—Hes. 27:5-11.

^ fu. 22 Boazi alimpa Ruthu vipimo sita vya uzito usiojulikana, labda kuonyesha kwamba kama vile siku sita za kufanya kazi zilivyofuatwa na pumziko la Sabato, ndivyo siku za Ruthu za kuteseka akiwa mjane zingefuatwa na “pumziko” ambalo angepata kwa kuwa na nyumba na mume. Au huenda vipimo sita—labda vilivyochotwa kwa sepetu—ndio uzito pekee ambao Ruthu angeweza kubeba.

^ fu. 25 Ruthu ni mmoja kati ya wanawake watano ambao Biblia inaorodhesha kwenye ukoo wa Yesu. Mwingine ni Rahabu, ambaye alikuwa mama ya Boazi. (Mt. 1:3, 5, 6, 16) Kama Ruthu, yeye pia hakuwa Mwisraeli.