Kulingana na Luka 7:1-50

  • Ofisa wa jeshi mwenye imani (1-10)

  • Yesu amfufua mwana wa mjane huko Naini (11-17)

  • Yohana Mbatizaji asifiwa (18-30)

  • Kizazi kisicho na imani chashutumiwa (31-35)

  • Mwanamke mwenye dhambi asamehewa (36-50)

    • Mfano wa watu wenye madeni (41-43)

7  Alipomaliza kuzungumza na watu, akaingia Kapernaumu.  Ofisa fulani wa jeshi alikuwa na mtumwa aliyempenda sana, na ambaye alikuwa mgonjwa sana karibu kufa.+  Aliposikia kuhusu Yesu, akawatuma wazee fulani wa Wayahudi wamwombe Yesu aje kumponya mtumwa wake.  Walipofika kwa Yesu wakamsihi sana wakisema: “Mfanyie jambo hilo, anastahili  kwa maana analipenda taifa letu na yeye ndiye aliyetujengea sinagogi.”  Basi Yesu akaenda pamoja nao. Alipokaribia nyumba hiyo, yule ofisa wa jeshi alikuwa tayari amewatuma rafiki zake wamwambie: “Bwana, usijisumbue, kwa maana mimi sistahili uingie ndani ya nyumba yangu.+  Ndiyo sababu niliona sistahili kuja kwako. Lakini sema tu neno, na mtumishi wangu atapona.  Kwa maana mimi pia niko chini ya mamlaka, na nina wanajeshi walio chini yangu, nami humwambia mmoja, ‘Nenda!’ naye huenda, na mwingine, ‘Njoo!’ naye huja, na mtumwa wangu, ‘Fanya hili!’ naye hulifanya.”  Yesu aliposikia maneno hayo alishangazwa naye, akaugeukia umati uliokuwa ukimfuata na kusema: “Ninawaambia, hata katika Israeli sijaona imani kubwa kama hii.”+ 10  Na wale waliokuwa wametumwa waliporudi nyumbani, wakamkuta yule mtumwa amepona.+ 11  Muda mfupi baadaye, Yesu akasafiri pamoja na wanafunzi wake na umati mkubwa kwenda jiji linaloitwa Naini. 12  Alipokaribia lango la jiji, tazama! kulikuwa na watu waliokuwa wamebeba maiti wakiipeleka nje, yule aliyekufa alikuwa mwana pekee,* na mama yake+ alikuwa mjane. Watu wengi kutoka jijini walikuwa pamoja na yule mwanamke. 13  Bwana alipomwona yule mjane akamsikitikia+ na kumwambia: “Acha kulia.”+ 14  Akakaribia na kuligusa jeneza,* nao wale waliolibeba wakasimama. Akasema: “Kijana, ninakuambia, inuka!”+ 15  Yule mfu akaketi akaanza kuongea, naye Yesu akamkabidhi kwa mama yake.+ 16  Basi wote wakaogopa, wakaanza kumtukuza Mungu wakisema: “Nabii mkuu ameinuliwa kati yetu,”+ na, “Mungu amewakumbuka watu wake.”+ 17  Habari hizo kumhusu Yesu zikaenea katika Yudea yote na maeneo jirani. 18  Basi wanafunzi wa Yohana wakamjulisha mambo hayo yote.+ 19  Ndipo Yohana akawaita wawili kati ya wanafunzi wake akawatuma kwa Bwana wamuulize: “Je, wewe ndiye Yule Anayekuja,+ au tumtarajie mwingine?” 20  Walipofika kwa Yesu wakamwambia: “Yohana Mbatizaji alitutuma kwako tukuulize: ‘Je, wewe ndiye Yule Anayekuja au tumtarajie mwingine?’” 21  Wakati huohuo, Yesu akawaponya watu wenye magonjwa,+ maradhi hatari, na wenye roho waovu, na pia akawapa vipofu wengi zawadi ya kuona. 22  Kisha akawajibu: “Nendeni mkamwambie Yohana mambo mliyoona na kusikia. Vipofu wanaona,+ viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakaswa, viziwi wanasikia,+ wafu wanafufuliwa, na maskini wanahubiriwa habari njema.+ 23  Mwenye furaha ni mtu ambaye hapati ndani yangu sababu ya kukwaza.”+ 24  Wajumbe wa Yohana walipoondoka, Yesu akaanza kuuambia umati kumhusu Yohana: “Mlienda nyikani kuona nini? Tete likitikiswa na upepo?+ 25  Basi, mlienda kuona nini? Mtu aliyevaa mavazi laini?*+ Kwa maana wale wanaovaa mavazi maridadi na kuishi maisha ya anasa hukaa katika nyumba za kifalme. 26  Basi kwa kweli, mlienda kuona nini? Nabii? Ndiyo, ninawaambia, mtu aliye zaidi ya nabii.+ 27  Huyu ndiye ambaye imeandikwa hivi kumhusu, ‘Tazama! Ninamtuma mjumbe wangu mbele yako,* ili akutayarishie njia mbele yako.’+ 28  Ninawaambia, kati ya wale waliozaliwa na wanawake hakuna aliye mkuu kuliko Yohana, lakini mtu mdogo zaidi katika Ufalme wa Mungu, ni mkuu kuliko Yohana.”+ 29  (Watu wote na wakusanya kodi waliposikia jambo hilo, wakamtangaza Mungu kuwa mwadilifu, kwa sababu walikuwa wamebatizwa kwa ubatizo wa Yohana.+ 30  Lakini Mafarisayo na wale wenye ujuzi wa Sheria walilipuuza shauri la* Mungu,+ kwa sababu hawakuwa wamebatizwa na Yohana.) 31  “Basi, nitawalinganisha watu wa kizazi hiki na nani, wanafanana na nani?+ 32  Wao ni kama watoto walioketi sokoni ambao wanaambiana kwa sauti kubwa, wakisema: ‘Tuliwapigia filimbi, lakini hamkucheza dansi; tuliomboleza, lakini hamkulia.’ 33  Vivyo hivyo, Yohana Mbatizaji hakuja akila mkate wala kunywa divai,+ lakini mnasema: ‘Ana roho mwovu.’ 34  Mwana wa binadamu amekuja akila na kunywa, lakini mnasema: ‘Tazama! yeye ni mlafi na mwenye mazoea ya kunywa divai, rafiki ya wakusanya kodi na watenda dhambi!’+ 35  Hata hivyo, hekima huthibitishwa* kuwa yenye uadilifu kupitia watoto wake wote.”*+ 36  Mmoja wa Mafarisayo alikuwa akimwomba Yesu ale pamoja naye. Basi akaenda katika nyumba ya Farisayo huyo na akaketi mezani. 37  Tazama! mwanamke aliyejulikana jijini kuwa mtenda dhambi akapata habari kwamba Yesu alikuwa akila* katika nyumba ya Farisayo, naye akaja na chupa ya alabasta yenye mafuta ya marashi.+ 38  Akaketi miguuni pa Yesu, akalia na kulowesha miguu yake kwa machozi na kuifuta kwa nywele za kichwa chake. Pia, akaibusu kwa wororo miguu ya Yesu na kuipaka mafuta ya marashi. 39  Alipoona hivyo, yule Farisayo aliyemwalika akajiambia: “Kama kweli mtu huyu angekuwa nabii, angejua ni nani na ni mwanamke wa aina gani anayemgusa, kwamba ni mtenda dhambi.”+ 40  Lakini Yesu akamwambia: “Simoni, ninataka kukuambia jambo.” Akasema: “Sema, mwalimu!” 41  “Mtu fulani aliwakopesha watu wawili pesa, mmoja alikuwa na deni la dinari* 500, na mwingine 50. 42  Waliposhindwa kumlipa, akawasamehe kwa hiari wote wawili. Kwa hiyo, ni nani kati yao atakayempenda zaidi?” 43  Simoni akajibu: “Nadhani ni yule aliyesamehewa zaidi.” Akamwambia: “Umejibu vizuri.” 44  Ndipo akamgeukia yule mwanamke na kumwambia Simoni: “Unamwona mwanamke huyu? Niliingia katika nyumba yako; hukunipa maji ya kuosha miguu yangu. Lakini mwanamke huyu aliiosha miguu yangu kwa machozi yake na kuifuta kwa nywele zake. 45  Wewe hukunibusu, lakini mwanamke huyu hajaacha kuibusu miguu yangu kwa wororo tangu nilipoingia. 46  Hukunipaka mafuta kichwani, lakini mwanamke huyu ameipaka miguu yangu mafuta yenye marashi. 47  Kwa hiyo, ninakuambia ingawa dhambi zake ni nyingi,* amesamehewa,+ kwa sababu amependa sana. Lakini anayesamehewa kidogo, hupenda kidogo.” 48  Ndipo akamwambia mwanamke huyo: “Umesamehewa dhambi zako.”+ 49  Wale walioketi mezani pamoja naye wakaanza kuulizana: “Mtu huyu ni nani ambaye hata anasamehe dhambi?”+ 50  Lakini akamwambia yule mwanamke: “Imani yako imekuokoa;+ nenda kwa amani.”

Maelezo ya Chini

Tnn., “mwana mzaliwa pekee.”
Au “machela ya kubebea maiti.”
Au “mavazi bora?”
Tnn., “mbele ya uso wako.”
Au “mwongozo wa.”
Au “kupitia matokeo yake.”
Au “hutetewa.”
Au “alikuwa ameketi mezani.”
Au “kubwa.”