Kulingana na Marko 6:1-56

  • Yesu akataliwa katika mji wa nyumbani kwao (1-6)

  • Wale 12 wapewa maagizo kuhusu huduma (7-13)

  • Kifo cha Yohana Mbatizaji (14-29)

  • Yesu alisha wanaume 5,000 (30-44)

  • Yesu atembea juu ya maji (45-52)

  • Yesu awaponya watu huko Genesareti (53-56)

6  Akaondoka huko na kwenda kwenye eneo lake la nyumbani,+ na wanafunzi wake wakamfuata.  Ilipofika siku ya Sabato, akaanza kufundisha katika sinagogi, na wengi waliomsikiliza wakashangaa na kusema: “Mtu huyu alitoa wapi mambo haya?+ Kwa nini alipewa hekima hii, na kwa nini matendo haya yenye nguvu yafanywe kupitia mikono yake?+  Je, huyu si yule seremala+ mwana wa Maria+ na ndugu ya Yakobo,+ Yosefu, Yuda, na Simoni?+ Na dada zake wapo hapa pamoja nasi, sivyo?” Basi wakaanza kukwazika kwa sababu yake.  Lakini Yesu akawaambia: “Nabii anaheshimiwa kila mahali isipokuwa katika eneo lake la nyumbani na kati ya watu wake wa ukoo, na katika nyumba yake mwenyewe.”+  Basi, hakuweza kufanya matendo yoyote yenye nguvu huko isipokuwa kuweka mikono yake juu ya wagonjwa wachache na kuwaponya.  Kwa kweli, alishangaa sana kwa sababu hawakuwa na imani. Naye akaenda akizunguka vijijini, akifundisha.+  Sasa akawaita wale 12 akaanza kuwatuma wawili wawili,+ naye akawapa mamlaka juu ya roho waovu.+  Pia, akawaagiza wasibebe chochote kwa ajili ya safari isipokuwa fimbo—wasibebe mkate, mfuko wa chakula, wala pesa* kwenye mishipi yao+  bali wavae viatu lakini wasivae mavazi mawili.* 10  Pia, akawaambia: “Mtakapoingia katika nyumba yoyote, kaeni humo mpaka mtakapoondoka huko.+ 11  Na mahali popote ambapo watu hawatawakaribisha wala kuwasikiliza, mnapoondoka kung’uteni mavumbi yaliyo kwenye miguu yenu ili kuwa ushahidi kwao.”+ 12  Basi wakaondoka na kuhubiri kwamba watu wanapaswa kutubu,+ 13  pia wakafukuza roho wengi waovu+ na kuwapaka mafuta wagonjwa wengi na kuwaponya. 14  Mfalme Herode akasikia habari hizo, kwa maana jina la Yesu lilijulikana sana na watu walikuwa wakisema: “Yohana Mbatizaji amefufuliwa kutoka kwa wafu, ndiyo sababu anafanya matendo yenye nguvu.”+ 15  Lakini wengine walikuwa wakisema: “Ni Eliya.” Pia, wengine wakasema: “Ni nabii kama manabii wa kale.”+ 16  Lakini Herode alipopata habari hizo akasema: “Yule Yohana niliyemkata kichwa, amefufuliwa.” 17  Kwa maana Herode alikuwa ameagiza Yohana akamatwe na kufungwa gerezani kwa sababu ya Herodia, mke wa Filipo ndugu yake. Kwa sababu Herode alikuwa amemwoa.+ 18  Kwa maana Yohana alikuwa akimwambia Herode: “Si halali kwako kuwa na mke wa ndugu yako.”+ 19  Basi Herodia alikuwa na kinyongo kumwelekea Yohana na alitaka kumuua, lakini hakuweza. 20  Kwa maana Herode alimwogopa Yohana kwa kuwa alijua ni mtu mwadilifu na mtakatifu,+ naye alikuwa akimlinda. Baada ya kumsikiliza, hakujua la kufanya, lakini bado aliendelea kumsikiliza kwa furaha. 21  Nafasi ilipatikana Herode alipoandaa mlo wa jioni kwenye sherehe ya sikukuu yake ya kuzaliwa.+ Akawaalika maofisa wake wa cheo cha juu, makamanda wa jeshi, na watu mashuhuri zaidi wa Galilaya.+ 22  Binti ya Herodia akaingia, akacheza dansi na kumfurahisha Herode na wageni wake.* Mfalme akamwambia msichana huyo: “Niombe chochote unachotaka, nami nitakupa.” 23  Ndiyo, akamwapia: “Chochote utakachoomba nitakupa, hata ikiwa ni nusu ya ufalme wangu.” 24  Akaondoka na kwenda kumuuliza mama yake: “Niombe nini?” Akamwambia: “Kichwa cha Yohana Mbatizaji.” 25  Akarudi haraka mbele ya mfalme na kutoa ombi lake, akisema: “Nataka unipe sasa hivi kwenye sinia kichwa cha Yohana Mbatizaji.”+ 26  Ingawa mfalme alihuzunika sana, hakutaka kupuuza ombi lake, kwa sababu ya viapo vyake na wageni wake.* 27  Mara moja mfalme akamtuma mlinzi na kumwamuru alete kichwa cha Yohana. Basi akaenda gerezani na kumkata kichwa, 28  akakileta kwenye sahani. Akampa yule msichana, na huyo msichana akampa mama yake. 29  Wanafunzi wake waliposikia jambo hilo, wakaja na kuuchukua mwili wake wakaulaza kaburini.* 30  Mitume wakamzunguka Yesu na kumwambia mambo yote waliyokuwa wamefanya na kufundisha.+ 31  Naye akawaambia: “Twendeni faraghani mahali pasipo na watu ili mpumzike kidogo.”+ Kwa maana wengi walikuwa wakija na kwenda, nao hawakuwa na wakati hata wa kula. 32  Basi wakapanda mashua na kwenda mahali pasipo na watu ili wawe peke yao.+ 33  Lakini watu wakawaona wakienda na wengi wakajua jambo hilo. Watu kutoka majiji yote wakakimbia kwa miguu wakafika huko mbele yao. 34  Basi, aliposhuka, akaona umati mkubwa, akawasikitikia,+ kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji.+ Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.+ 35  Ilipokaribia jioni wanafunzi wake wakaja na kumwambia: “Mahali hapa hapana watu, na muda umesonga sana.+ 36  Waambie waondoke, waende wakajinunulie chakula katika maeneo ya mashambani na vijiji vilivyo karibu.”+ 37  Akawajibu: “Ninyi wapeni chakula.” Nao wakamwambia: “Je, twende tukanunue mikate ya dinari* 200 na kuwapa watu wale?”+ 38  Akawaambia: “Mna mikate mingapi? Nendeni mkaangalie!” Baada ya kuhakikisha, wakasema: “Mikate mitano na samaki wawili.”+ 39  Akawaagiza watu wote waketi katika vikundi kwenye nyasi.+ 40  Basi wakaketi katika vikundi vya watu 100 na vya watu 50. 41  Akachukua ile mikate mitano na wale samaki wawili, akatazama mbinguni akatoa baraka.+ Kisha akaimega mikate na kuanza kuwapa wanafunzi ili wawape watu, naye akawagawanya wale samaki wawili kwa ajili ya watu wote. 42  Basi wote wakala wakashiba, 43  nao wakakusanya vipande vilivyobaki na kujaza vikapu 12, bila kuhesabu samaki.+ 44  Wale waliokula mikate hiyo walikuwa wanaume 5,000. 45  Kisha, bila kukawia, akawaagiza wanafunzi wake wapande mashua watangulie kuelekea Bethsaida ng’ambo ya bahari, huku yeye akiuaga umati.+ 46  Lakini baada ya kuwaaga, akaenda mlimani kusali.+ 47  Ilipofika jioni, mashua ilikuwa katikati ya bahari, lakini yeye alikuwa peke yake kwenye nchi kavu.+ 48  Alipowaona wanafunzi wake wakitaabika kupiga makasia kwa kuwa upepo ulikuwa ukivuma kinyume chao, usiku karibu kesha la nne* akawaendea akitembea juu ya bahari; lakini alitaka* kuwapita. 49  Walipomwona akitembea juu ya bahari wakafikiri: “Ni mzuka!” Nao wakapaza sauti. 50  Kwa maana wote walimwona, wakahangaika. Lakini mara moja akawaambia: “Jipeni moyo! Ni mimi; msiogope.”+ 51  Kisha akapanda kwenye mashua, na upepo ukatulia. Nao wakashangaa sana, 52  kwa maana hawakuwa wamefahamu maana ya ule muujiza wa mikate, bado mioyo yao ilikuwa mizito isiweze kuelewa. 53  Walipovuka bahari, wakafika Genesareti na kutia nanga hapo karibu.+ 54  Lakini mara tu waliposhuka kutoka kwenye mashua, watu wakamtambua. 55  Wakakimbia katika eneo hilo lote na kuanza kuleta wagonjwa wakiwa kwenye vitanda* mahali waliposikia Yesu yuko. 56  Na kila mahali alipokwenda katika vijiji, majiji, au mashambani watu waliwaweka wagonjwa sokoni, na kumsihi waguse tu upindo wa vazi lake la nje.+ Na wote waliougusa wakapona.

Maelezo ya Chini

Tnn., “shaba.”
Au “vazi la ziada.”
Au “wale waliokuwa wameketi mezani.”
Au “wale waliokuwa wameketi mezani.”
Au “katika kaburi la ukumbusho.”
Yaani, karibu saa 9 usiku hadi karibu saa 12 asubuhi.
Au “alikuwa karibu.”
Au “machela.”