Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

BIBLIA INABADILI MAISHA

Nilishindwa Mara Nyingi Kabla ya Kushinda

Nilishindwa Mara Nyingi Kabla ya Kushinda
  • ALIZALIWA: 1953

  • NCHI: AUSTRALIA

  • HISTORIA: MRAIBU WA PONOGRAFIA

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Baba yangu alihamia nchini Australia kutoka Ujerumani mwaka wa 1949. Alihamia Australia ili kutafuta kazi katika migodi na viwanda vya kuzalisha umeme na aliishi katika eneo la kijijini la Victoria. Akiwa huko alimwoa mama yangu na mimi nikazaliwa mwaka wa 1953.

Miaka michache baadaye, mama yangu alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, hivyo niliyajua mafundisho ya Biblia tangu utotoni. Baba yangu hakupendezwa na dini yoyote. Alikuwa mwenye jeuri, aliwaogopesha watu na mama yangu alimwogopa sana. Hata hivyo, mama aliendelea kujifunza Biblia kwa siri, na akapenda mambo aliyojifunza. Baba alipoondoka, mama alitufundisha mimi na dada yangu mambo aliyojifunza. Alitueleza kuhusu paradiso ya wakati ujao na jinsi ambavyo tunaweza kuwa wenye furaha ikiwa tutafuata kanuni za maadili zilizo katika Biblia.—Zaburi 37:10, 29; Isaya 48:17.

Nilipokuwa na umri wa miaka 18, nililazimika kuondoka nyumbani kwa sababu ya jeuri ya baba. Ingawa niliamini mambo ambayo mama alinifundisha kutoka katika Biblia, sikuona thamani yake. Hivyo sikuishi kulingana nayo. Nilianza kufanya kazi ya ufundi wa umeme katika migodi ya makaa ya mawe. Nilifunga ndoa nilipokuwa na umri wa miaka 20. Binti yetu wa kwanza alizaliwa miaka mitatu baadaye na nilianza kufikiria tena jambo lililokuwa muhimu katika maisha yangu. Nilijua kwamba Biblia inaweza kusaidia familia yangu, kwa hiyo nikaanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Lakini mke wangu aliwapinga sana Mashahidi. Nilipohudhuria mmoja kati ya mikutano yao, alitaka nichague jambo moja, kati ya kujifunza Biblia au familia. Nilihisi sina ujasiri wa kupinga uamuzi wake, hivyo niliacha kushirikiana na Mashahidi. Baadaye nilijutia uamuzi wangu wa kuacha kufuata mambo niliyojua kwamba ni sawa.

Siku moja, mfanyakazi mwenzangu alinionyesha ponografia. Picha hizo zilinivutia lakini pia zilinishtua na kunifanya nilemewe na hisia za hatia. Nilipokumbuka yale niliyojifunza katika Biblia, niliamini kabisa kwamba lazima Mungu atanihukumu. Hata hivyo, kadiri nilivyotazama picha hizo mara nyingi, ndivyo mtazamo wangu kuhusu ponografia ulivyobadilika. Baada ya muda, nikawa mraibu wa ponografia.

Kwa zaidi ya miaka 20, niliacha kabisa mambo niliyofundishwa na mama yangu. Mwenendo wangu ulionyesha mambo niliyokuwa nikiwaza. Nilitumia lugha chafu na nilipenda mizaha michafu. Nilisitawisha mtazamo usiofaa kuhusu ngono. Ingawa niliendelea kuishi na mke wangu, nilikuwa na uhusiano wa kingono na wanawake wengine. Badala ya kujiheshimu, nilijichukia.

Ndoa yangu ilivunjika, na maisha yangu yakaharibika. Kisha, nilisali kwa Yehova kwa moyo wangu wote. Nilianza tena kujifunza Biblia, ingawa sikuwa nimejifunza kwa miaka 20. Kufikia wakati huo baba yangu alikuwa amekufa, na mama yangu alikuwa amebatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Kulikuwa na tofauti kubwa kati ya mtindo wa maisha yangu na viwango vya juu vya Biblia. Lakini wakati huu niliazimia kuipata amani ya akili ambayo Biblia inaahidi. Niliamua kuepuka usemi wenye matusi na kuzuia hasira yangu. Pia, niliamua kuacha mwenendo wangu mpotovu, kucheza kamari, kulewa, na kumwibia mwajiri wangu.

Wafanyakazi wenzangu hawakuelewa sababu ya kufanya mabadiliko hayo makubwa. Kwa miaka mitatu, walinishawishi nirudie maisha yangu ya zamani. Ikiwa ningefanya jambo fulani dogo, kama vile kuwaka hasira au kusema neno baya, walipiga kelele na kushangilia wakisema: “Aha! Sasa Joe wa zamani amerudi.” Maneno hayo yaliniumiza sana! Mara nyingi nilihisi ni kana kwamba nimeshindwa.

Ilikuwa rahisi kupata ponografia nikiwa kazini, iwe ni kwenye vifaa vya kielektroniki au picha zilizochapishwa. Mara kwa mara wafanyakazi wenzangu walinitumia picha chafu kupitia kompyuta, kama nilivyofanya awali. Nilijitahidi kuacha zoea hilo, lakini wafanyakazi wenzangu walionekana wameazimia kunifanya nishindwe. Nilimwendea mwalimu wangu wa Biblia ili kupata msaada na kitia moyo. Kwa subira alinisikiliza nilipomweleza yaliyo moyoni mwangu. Kwa kutumia mistari hususa ya Biblia, alinionyesha jinsi ya kushinda zoea langu, na alinitia moyo kuendelea kusali kwa Yehova ili kupata msaada.—Zaburi 119:37.

Siku moja nilifanya mkutano pamoja na wafanyakazi wenzangu. Walipokusanyika, niliwaambia wawape bia wanaume wawili, ambao walijulikana kuwa waraibu wa pombe. Wote walipinga na kusema: “Hupaswi kufanya hivyo! Wanaume hawa wanajitahidi kuacha zoea hilo!” Kisha nikawajibu: “Mimi pia ninajitahidi kuacha zoea hili.” Tangu siku hiyo na kuendelea, wote walielewa jinsi nilivyojitahidi kuacha zoea la kutazama ponografia, na hawakunishawishi tena nirudie mwenendo wangu wa zamani.

Baada ya muda, kwa msaada wa Yehova nilifaulu kushinda zoea sugu la kutazama ponografia. Mwaka wa 1999, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, ninashukuru kwamba nilipewa nafasi nyingine ya kuishi maisha safi na yenye furaha.

Sasa ninaelewa kwa nini Yehova anachukia mambo ambayo nilipenda kwa muda mrefu. Akiwa Baba mwenye upendo, alitaka kunilinda kutokana na madhara ya kutazama ponografia. Maneno ya Methali 3:5, 6 ni ya kweli kabisa! Maneno hayo yanasema hivi: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.” Kanuni za Biblia ni ulinzi na pia zinatusaidia tufanikiwe.—Zaburi 1:1-3.

JINSI NILIVYOFAIDIKA:

Zamani, sikujiheshimu, lakini kwa sasa ninajiheshimu na nina amani ya akili. Ninaishi maisha safi na ninafurahia msamaha na msaada wa Yehova. Mwaka wa 2000, nilimwoa Karolin, dada Mkristo mrembo na anayempenda Yehova kama mimi. Nyumba yetu ina amani tele. Tunahisi kuwa ni pendeleo kubwa kuwa sehemu ya undugu wa Kikristo ulio safi na wenye upendo ulioenea ulimwenguni pote.