Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JINSI BIBLIA ILIVYOOKOKA

Biblia Iliokoka Upinzani

Biblia Iliokoka Upinzani

TATIZO: Wanasiasa na viongozi wengi wa dini walikuwa na malengo yaliyopingana na ujumbe wa Biblia. Mara nyingi, walitumia mamlaka yao kuwakataza watu kumiliki, kuchapisha, au kutafsiri Biblia. Fikiria mifano miwili:

  • Karibu mwaka wa 167 K.W.K.: Mfalme Antioko Epifane wa Seleuko alijaribu kuwalazimisha Wayahudi wajiunge na dini ya Kigiriki kwa kuamuru nakala zote za Maandiko ya Kiebrania ziharibiwe. Mwanahistoria Heinrich Graetz aliandika hivi: “Maofisa wake walichana na kuchoma vitabu vya kukunjwa vya Sheria popote walipovipata, na wale wote waliosoma vitabu hivyo ili kupata faraja, waliuawa.”

  • Enzi za Kati: Baadhi ya viongozi wa Kanisa Katoliki walikasirika walipowaona watu wa kawaida wakihubiri kweli za Biblia badala ya mafundisho ya Kikatoliki. Hivyo mtu yeyote aliyemiliki vitabu vingine vya Biblia zaidi ya Zaburi ya Kilatini alionwa kuwa mwasi. Baraza moja la kanisa lilitekeleza amri hiyo kwa kuwaagiza wanaume “wawatafute waasi hao kwa uangalifu, uaminifu na bidii. . . kwa kupekua nyumba zote na vyumba vya chini walivyotilia shaka. . . . Nyumba yoyote ambayo wangempata mwasi walipaswa kuiharibu.”

Ikiwa maadui wa Biblia wangefaulu kuiangamiza, ujumbe wake ungepotea.

Tafsiri ya Kiingereza ya William Tyndale iliokoka licha ya marufuku, kuchomwa kwa Biblia na hata kuuawa kwa Tyndale mwenyewe mwaka wa 1536

JINSI BIBLIA ILIVYOOKOKA: Mfalme Antioko alielekeza kampeni zake huko Israeli, hata hivyo, Wayahudi walikuwa wametawanyika katika nchi nyingine nyingi. Wasomi wanakadiria kwamba kufikia karne ya kwanza, zaidi ya asilimia 60 ya Wayahudi hawakuishi Israeli. Wayahudi walihifadhi nakala za Maandiko katika masinagogi yao, Maandiko ambayo yalitumiwa baadaye na vizazi vyao, kutia ndani Wakristo.—Matendo 15:21.

Wakati wa Enzi za Kati, watu walioipenda Biblia walivumilia upinzani na wakaendelea kutafsiri na kunakili Maandiko. Hata kabla ya kubuniwa kwa mashine za kuchapa katikati ya karne ya 15, sehemu fulani za Biblia zilipatikana katika lugha 33 hivi. Baadaye, Biblia ilitafsiriwa na kuchapishwa kwa wingi zaidi.

MATOKEO: Licha ya upinzani kutoka kwa wafalme wenye nguvu na viongozi wa dini waliopotoshwa, Biblia imekuwa kitabu pekee kilichotafsiriwa kwa lugha nyingi na kugawanywa katika maeneo mengi. Biblia imeboresha sheria na lugha katika nchi fulani, na imewasaidia watu wengi kubadili maisha yao.