Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wamasora walinakili Maandiko kwa uangalifu

HABARI KUU | JINSI BIBLIA ILIVYOOKOKA

Biblia Iliokoka Jitihada za Kubadili Ujumbe Wake

Biblia Iliokoka Jitihada za Kubadili Ujumbe Wake

TATIZO: Biblia imedumu licha ya upinzani na uwezekano wa kuharibika kwa vifaa vya kuandikiwa. Hata hivyo, baadhi ya wanakili na watafsiri wamejaribu kubadili ujumbe wa Biblia. Nyakati nyingine, wamejaribu kubadili ujumbe wa Biblia ili ufaane na mafundisho yao, badala ya mafundisho yao kupatana na ya Biblia. Fikiria mifano kadhaa:

  • Mahali pa ibada: Kati ya karne ya pili na ya nne K.W.K., waandishi wa Pentateuki ya Wasamaria waliongezea maneno haya katika Kutoka 20:17 “katika Mlima Gerizimu. Na huko utajenga madhabahu.” Wasamaria walikusudia Maandiko yaunge mkono ujenzi wao wa hekalu lililokuwa katika Mlima Gerizimu.

  • Fundisho la Utatu: Miaka 300 hivi baada ya Biblia kuandikwa, mwandishi wa fundisho la Utatu aliongezea maneno haya katika andiko la 1 Yohana 5:7 “mbinguni, Baba, na Neno, na Roho Mtakatifu, na watatu hawa ni umoja.” Maneno hayo hayakupatikana katika maandishi ya awali. Msomi wa Biblia Bruce Metzger anasema hivi: “Kuanzia karne ya sita na kuendelea, maneno hayo yalipatikana mara nyingi zaidi kwenye hati za Kilatini cha Zamani na Vulgate ya Kilatini.”

  • Jina la Mungu: Watafsiri wengi wa Biblia waliamua kuondoa jina la Mungu kwenye Maandiko kwa sababu ya kufuata desturi za kishirikina za Wayahudi. Badala ya kutumia jina Yehova, walitumia majina ya cheo kama vile, “Mungu” au “Bwana.” Majina hayo yanapotumiwa kwenye Biblia yanaweza kurejelea Muumba, wanadamu, vitu vinavyoabudiwa na hata Ibilisi. —Yohana 10:34, 35; 1 Wakorintho  8:5, 6; 2 Wakorintho 4:4. *

JINSI BIBLIA ILIVYOOKOKA: Baadhi ya wanakili wa Biblia walikuwa wadanganyifu au hawakuwa waangalifu, hata hivyo wanakili wengi walikuwa stadi na makini sana. Kati ya karne ya sita na ya kumi W.K., Wamasora walinakili Maandiko ya Kiebrania na kutokeza maandishi yanayojulikana kuwa maandishi ya Wamasora. Inaripotiwa kwamba Wamasora walihesabu maneno na herufi ili kuhakikisha kwamba wamenakili kwa usahihi. Walipohisi kwamba nakala za maandishi ya Kiebrania walizotumia zina makosa, waliandika makosa hayo pambizoni. Wamasora hawakubadili maandishi ya Biblia. Profesa Moshe Goshen-Gottstein aliandika hivi: “Wamasora waliona kubadili Maandiko kimakusudi kuwa uhalifu mkubwa sana.”

Pili, kwa kuwa hati nyingi za kale zinapatikana leo, wasomi wa Biblia wanaweza kutambua makosa kwa njia rahisi. Kwa mfano, kwa miaka mingi viongozi wa dini walifundisha kwamba tafsiri ya Biblia yao ya Kilatini ilikuwa sahihi. Hata hivyo, kama ilivyotajwa mwanzoni mwa makala hii waliongeza maneno yasiyo sahihi katika 1 Yohana 5:7. Makosa hayo yaliandikwa pia katika tafsiri ya Kiingereza ya King James Version! Hata hivyo, hati nyingine za kale zilizogunduliwa zilionyesha nini? Bruce Metzger aliandika: “Maneno [yaliyo kwenye 1 Yohana 5:7] hayapatikani kwenye hati zote za awali (Kisiria, Kikoptiki, Kiarmenia, Kiethiopia, Kiarabu, Kislavonia) isipokuwa kwenye tafsiri ya Kilatini pekee.” Kwa sababu hiyo, tafsiri zilizoboreshwa za King James Version na Biblia nyingine zimeondoa fungu hilo la maneno lisilo sahihi.

Chester Beatty P46, hati ya mafunjo ya Biblia ya mwaka wa 200 W.K.

Je, hati za zamani zinathibitisha kwamba ujumbe wa Biblia umeokoka? Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi vilipopatikana mwaka wa 1947, wasomi waliweza kulinganisha maandishi ya Kiebrania ya Wamasora na ya vitabu hivyo vilivyoandikwa zaidi ya miaka elfu moja iliyopita. Mhariri mmoja wa Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi alisema kwamba nakala moja “inatoa uthibitisho usiokanushika kwamba Wayahudi walionakili maandishi ya Biblia katika kipindi cha zaidi ya miaka elfu moja, walifanya kazi hiyo kwa uaminifu na uangalifu mkubwa.”

Mafunjo ya vitabu vingi vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanapatikana katika Maktaba ya Chester Beatty iliyo Dublin, nchini Ireland, kutia ndani hati za kuanzia karne ya pili W.K., miaka 100 hivi baada ya Biblia kuandikwa. The Anchor Bible Dictionary inasema hivi: “Zaidi ya kuwa na habari nyingi mpya, pia Mafunjo yanaonyesha umakini wa ajabu katika historia ya kunakili maandishi ya Biblia.”

“Tunaweza kusema kwa uhakika kwamba hakuna maandishi mengine ya kale yaliyonakiliwa kwa usahihi kama hayo.”

MATOKEO: Kupatikana kwa hati nyingi za kale za maandishi ya Biblia, kumesaidia kuiboresha badala ya kuipotosha. Sir Frederic Kenyon aliandika hivi kuhusu Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo: “Hakuna kitabu kingine cha zamani kilicho na uthibitisho mwingi na wa awali kama Biblia na hakuna msomi anayeweza kudai kwamba maandishi tuliyo nayo si ya kweli.” Naye msomi William Henry Green aliandika hivi kuhusiana na Maandiko ya Kiebrania: “Tunaweza kusema kwa uhakika kwamba hakuna maandishi mengine ya kale yaliyonakiliwa kwa usahihi kama hayo.”

^ fu. 6 Kwa habari zaidi, soma nyongeza iliyo kwenye ukurasa wa 195-197 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kinachopatikana kwenye www.pr418.com/sw.