Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nikihubiri pamoja na mke wangu, Tabitha

BIBLIA INABADILI MAISHA

Niliamini Hakuna Mungu

Niliamini Hakuna Mungu
  • ALIZALIWA: 1974

  • NCHI: JAMHURI YA KIDEMOKRASIA YA UJERUMANI

  • HISTORIA: ALIAMINI HAKUNA MUNGU

MAISHA YANGU YA ZAMANI

Nilizaliwa katika kijiji fulani kwenye jimbo la Saxony, katika nchi ambayo wakati huo iliitwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Ujerumani (GDR). Familia yetu ilikuwa yenye upendo, na wazazi wangu walinifundisha kuwa na maadili mazuri. GDR ilikuwa nchi ya Kikomunisti, hivyo, watu wengi katika jimbo la Saxony hawakuiona dini kuwa muhimu. Na mimi niliamini kwamba hakuna Mungu. Niliongozwa na falsafa mbili tangu utotoni hadi nilipofikisha umri wa miaka 18: Ukomunisti na kutoamini uwepo wa Mungu.

Kwa nini nilipendezwa na Ukomunisti? Kwa sababu nilipenda wazo la kwamba watu wote ni sawa. Kwa kuongezea, niliamini kuwa mali zote zinapaswa kugawanywa kwa usawa, kwa sababu kufanya hivyo kungeondoa tofauti kubwa iliyopo kati ya matajiri na maskini. Kwa hiyo nilishirikiana sana na shirika la vijana wa Kikomunisti. Nilipokuwa na umri wa miaka 14, nilitumia muda mwingi katika mradi wa kutunza mazingira kwa kurejesha ubora wa karatasi zilizotumika. Wakazi wa Aue walithamini sana jitihada zangu na hata wenye mamlaka wakanipatia tuzo. Ingawa bado nilikuwa na umri mdogo, nilifahamiana na baadhi ya wanasiasa mashuhuri nchini. Nilihisi nipo katika njia sahihi kabisa na kwamba ningekuwa na maisha mazuri wakati ujao.

Lakini ghafla mambo yakabadilika. Mwaka wa 1989 Ukuta wa Berlin ulianguka, na wakati huohuo muungano wa Kikomunisti wa Ulaya Mashariki ukafa. Pigo moja lilisababisha pigo lingine. Baada ya muda mfupi niligundua kwamba suala la upotoshaji wa haki lilikuwa la kawaida nchini GDR. Kwa mfano, watu ambao hawakuunga mkono Ukomunisti walitendewa kama raia duni. Hilo liliwezekanaje? Wakomunisti tunaamini kwamba watu wote ni sawa, sivyo? Je, inawezekana kwamba Ukomunisti ni falsafa ya kuwaziwa tu? Nilijawa na wasiwasi.

Kwa hiyo, nilibadili mwelekeo na kuanza kukazia fikira muziki na sanaa. Kwa kuwa nilipata nafasi ya kusoma kwenye shule ya muziki, nikiwa na matarajio ya kupata elimu ya chuo kikuu baadaye, nilikuwa na ndoto ya kuwa mwanamuziki na mchoraji. Kwa kuongezea, nilitupilia mbali maadili niliyofundishwa utotoni. Jambo lililokuwa muhimu wakati huo ni kufurahia maisha. Hilo lilihusisha kuwa na wapenzi wengi kwa wakati mmoja. Hata hivyo, muziki, sanaa, na maisha ya kujiachilia hayakuondoa wasiwasi niliokuwa nao. Hata picha nilizochora zilionyesha hofu niliyokuwa nayo moyoni. Mambo yatakuwaje wakati ujao? Na maisha yana kusudi gani?

Hatimaye, nilishangazwa sana na majibu niliyopata. Jioni moja nilipokuwa shuleni, nilijiunga na baadhi ya wanafunzi na tulizungumza kuhusu wakati ujao. Mandy * alikuwa mmoja wa wanafunzi hao na pia alikuwa Shahidi wa Yehova. Jioni hiyo alinipatia ushauri mzuri sana. Alisema hivi: “Andreas, ikiwa unataka kupata majibu ya maswali yako kuhusu maisha na wakati ujao, ichunguze Biblia kwa makini.”

Ingawa bado nilikuwa na shaka, niliamua kutafuta majibu kwenye Biblia. Mandy aliniambia nisome Danieli sura ya 2, na mambo niliyosoma yalinistaajabisha sana. Unabii huo unazungumzia mfuatano wa serikali kuu za ulimwengu, ambazo utendaji wake ungeathiri hali za wakati wetu. Mandy alinionyesha unabii mwingine wa Biblia unaozungumzia wakati wetu ujao. Hatimaye nilianza kupata majibu ya maswali yangu! Hata hivyo, ni nani aliyeandika unabii huo, na ni nani ambaye angeweza kutabiri wakati ujao kwa usahihi hivyo? Je, inawezekana kwamba kuna Mungu?

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

Mandy alinitambulisha kwa Horst na Angelika, wenzi wa ndoa Mashahidi ambao walinisaidia kuelewa vizuri Neno la Mungu. Mara moja nilitambua kwamba Mashahidi wa Yehova ndio dini pekee ambayo hufundisha na kutumia jina la Mungu la kibinafsi, Yehova. (Zaburi 83:18; Mathayo 6:9) Nilijifunza kwamba Yehova Mungu amewapa wanadamu tumaini la kuishi milele kwenye dunia paradiso. Zaburi 37:9 inasema hivi: “Wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia.” Nilipendezwa na wazo la kwamba mtu yeyote anayejitahidi kuishi kupatana na viwango vya Mungu vilivyo kwenye Biblia, anaweza kuwa na tumaini hilo.

Hata hivyo, haikuwa rahisi kubadili njia yangu ya maisha ili ipatane na Biblia. Mafanikio katika sanaa na muziki yalinifanya niwe na kiburi, hivyo nilipaswa kujifunza kuwa mnyenyekevu. Vilevile, haikuwa rahisi kuacha kabisa mwenendo mpotovu wa maadili. Ninashukuru sana kwamba Yehova huonyesha subira, rehema, na fadhili kwa wale wanaojitahidi kadiri wanavyoweza kuishi kupatana na mafundisho ya Biblia!

Tangu utotoni hadi nilipofikisha umri wa miaka 18, Ukomunisti na imani ya kwamba hakuna Mungu ndio falsafa zilizoniongoza; baada ya hapo Biblia imeendelea kubadili maisha yangu. Mambo niliyojifunza yameondoa wasiwasi niliokuwa nao na yamenisaidia kupata kusudi maishani. Mwaka wa 1993, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, kisha mwaka wa 2000 nilifunga ndoa na Tabitha, mwamini mwenzangu mwenye bidii. Tunatumia muda mwingi kadiri tuwezavyo ili kuwasaidia wengine waielewe Biblia. Watu wengi tunaokutana nao ni Wakomunisti na wanaamini kwamba hakuna Mungu, kama mimi nilivyokuwa zamani. Ninahisi uradhi wa hali ya juu ninapowasaidia wamjue Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

Nilipoanza kushirikiana na Mashahidi wa Yehova, wazazi wangu walishtuka sana. Hata hivyo, tangu wakati huo, wamejionea jinsi ambavyo kushirikiana na Mashahidi kumeboresha maisha yangu. Ninafurahi kwamba sasa wao husoma Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova.

Mimi na Tabitha tuna maisha mazuri ya ndoa kwa sababu tunajitahidi kufuata ushauri ambao Biblia inatoa kwa wenzi wa ndoa. Kwa mfano, kufuata ushauri kuhusu uaminifu katika ndoa kunaendelea kuimarisha ndoa yetu.—Waebrania 13:4.

Sasa sina hofu ya maisha wala wasiwasi kuhusu wakati ujao. Ninajiona kuwa sehemu ya familia ya ulimwenguni pote ya waamini wenzangu, ambayo inafurahia amani ya kweli na umoja. Katika familia hii, sisi sote ni sawa. Hilo ni jambo ambalo nimekuwa nikiamini na kutamani kulipata maisha yangu yote.

^ fu. 12 Jina limebadilishwa.