Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninafurahi kutumia wakati pamoja na vijana kutanikoni

BIBLIA INABADILI MAISHA

Nilipenda Mchezo wa Besiboli Kuliko Kitu Kingine Chochote!

Nilipenda Mchezo wa Besiboli Kuliko Kitu Kingine Chochote!
  • ALIZALIWA: 1928

  • NCHI: KOSTA RIKA

  • HISTORIA: ALIKUWA MCHEZAJI WA KULIPWA NA MRAIBU WA KAMARI

MAISHA YANGU YA ZAMANI

Nililelewa Puerto Limón, jiji lenye bandari lililopo pwani ya mashariki nchini Kosta Rika. Wazazi wangu walikuwa na watoto nane, na mimi nilikuwa mtoto wa saba. Baba yangu alikufa nilipokuwa na umri wa miaka nane. Baada ya hapo, mama alitulea akiwa peke yake.

Mchezo wa besiboli ulikuwa sehemu ya maisha yangu. Tangu nilipokuwa mtoto, niliupenda mchezo huo. Nilipokuwa tineja, nilijiunga na ligi ya wachezaji wasiolipwa. Nilipokuwa na umri wa miaka 20 hivi, wakati bado ninachezea ligi hiyo, mwakilishi wa timu fulani aliniomba niende kuwa mchezaji wa kulipwa huko Nikaragua. Hata hivyo, kwa kuwa mama alikuwa na matatizo ya afya, na mimi ndiye niliyekuwa ninamtunza, sikutaka kuhamia Nikaragua. Kwa hiyo nilikataa fursa hiyo. Baadaye, mwakilishi mwingine alinialika kwenda kuchezea timu ya taifa ya Kosta Rika, ambayo ilikuwa na wachezaji kadhaa wasiolipwa. Wakati huu nilikubali. Nilichezea timu ya taifa tangu mwaka wa 1949 hadi 1952, na tulicheza mechi nchini Kuba, Mexico, na Nikaragua. Nilicheza sehemu ya ulinzi na nilifanya vizuri sana, wakati fulani nilicheza michezo 17 mfululizo bila kufanya kosa lolote. Nilipenda kusikia mashabiki wakitaja jina langu!

Kwa kusikitisha, niliishi maisha ya upotovu wa maadili. Ingawa nilikuwa na mpenzi mmoja, nilizoea kuwa na wanawake wengine. Vilevile, nilikunywa pombe kupita kiasi. Siku moja nililewa sana hivi kwamba siku iliyofuata nilipoamka sikukumbuka jinsi nilivyorudi nyumbani! Pia, nilicheza kamari na bahati nasibu.

Wakati naendelea kuishi maisha hayo, mama akawa Shahidi wa Yehova. Alijaribu kunifundisha kuhusu imani yake, lakini hakufanikiwa kwa sababu nilikuwa nimezama kabisa katika mchezo wa besiboli. Nilipokuwa uwanjani nikifanya mazoezi, sikuhisi njaa hata ilipofika muda wa kula! Akili yangu yote ilikuwa mchezoni. Nilipenda mchezo wa besiboli kuliko kitu kingine chochote!

Hata hivyo, nilipokuwa na umri wa miaka 29, niliumia vibaya sana nilipokuwa nikijaribu kudaka mpira uwanjani. Baada ya kupona, niliacha kucheza mpira wa kulipwa. Ingawa hivyo, niliendelea kujihusisha na besiboli kwa kuwazoeza wachezaji wasiolipwa katika timu fulani karibu na nyumbani.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

Mwaka wa 1957, nilikubali mwaliko wa kuhudhuria kusanyiko ambalo lilifanywa katika uwanja niliochezea besiboli wakati fulani. Nilipokuwa nikisikiliza, niliona jinsi ambavyo Mashahidi walijiendesha kwa heshima tofauti kabisa na vurugu za mashabiki zinazokuwepo wakati wa michezo ya besiboli. Kile nilichoona katika kusanyiko hilo kilinichochea kujifunza Biblia na Mashahidi na kuanza kuhudhuria mikutano yao.

Nilivutiwa sana na mambo mengi niliyojifunza katika Biblia. Kwa mfano, Yesu alitabiri kwamba katika siku za mwisho, wanafunzi wake watahubiri habari njema za Ufalme wa Mungu duniani kote. (Mathayo 24:14) Nilijifunza pia kwamba Wakristo wa kweli hawahubiri kwa kusudi la kupata pesa. Yesu alisema: “Mlipokea bure, toeni bure.”—Mathayo 10:8.

Kadiri nilivyojifunza Biblia, nililinganisha yale niliyojifunza na mambo niliyoona kutoka kwa Mashahidi wa Yehova. Nilivutiwa sana na jinsi walivyojitahidi bila kuchoka, kutangaza habari njema za Ufalme wa Mungu duniani kote. Niliona jinsi walivyoonyesha roho ya kujitoa ambayo Yesu aliagiza Wakristo wawe nayo. Kwa hiyo niliposoma andiko la Marko 10:21 na kuona mwaliko wa Yesu unaosema, “[Njoo] uwe mfuasi wangu,” nilitaka kuwa Shahidi.

Hata hivyo, muda fulani ulipita kabla sijachukua hatua hiyo kikamili. Kwa mfano, kwa miaka mingi kila juma nilicheza bahati nasibu ya taifa kwa kutumia namba yangu ya “bahati.” Hata hivyo, katika Biblia nilijifunza kwamba Mungu hapendezwi na waabudu wa “mungu wa Bahati Njema,” na vilevile watu wenye pupa. (Isaya 65:11; Wakolosai 3:5) Hivyo, niliamua kuacha kucheza kamari. Jumapili ya kwanza baada tu ya kuacha kucheza bahati nasibu, namba yangu ya “bahati” ilishinda! Watu walinicheka kwa kuwa juma hilo sikucheza, na wakaanza kunishinikiza sana kurudia mchezo huo, lakini nilikataa. Niliacha kabisa kucheza kamari.

Nilikabili jambo lingine lililojaribu “utu [wangu] mpya” siku ileile niliyobatizwa katika kusanyiko la Mashahidi wa Yehova. (Waefeso 4:24) Jioni hiyo, nilirudi kwenye hoteli niliyokuwa nimefikia na kumkuta mpenzi wangu wa zamani akiwa kwenye mlango wa chumba changu akinisubiri. Akaanza kunishawishi akisema: “Aaah, Sammy, njoo tufurahie!” Lakini mara moja nikamjibu, “Hapana!” Nilimkumbusha kwamba sasa ninaishi kupatana na viwango vya Biblia vya maadili. (1 Wakorintho 6:18) Akasema kwa mshangao: “Eti nini?” Kisha, akadai kwamba maoni ya Biblia kuhusu ngono hayana maana yoyote , naye akasisitiza tuendeleze uhusiano wetu. Hata hivyo, niliingia chumbani na kufunga mlango. Leo, ninafurahi kusema kwamba tangu niwe Shahidi mwaka wa 1958, nimeshikamana kikamili na mabadiliko niliyofanya katika maisha yangu.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

Ninahisi kana kwamba ninaweza kuandika kitabu kuhusu manufaa niliyopata kwa sababu ya kufuata mwongozo wa Biblia! Baadhi ya manufaa hayo ni kuwa na marafiki wengi wa kweli, maisha yenye kusudi, na furaha ya kweli.

Bado ninafurahia mchezo wa besiboli, lakini sasa nimebadili mwenendo wangu. Nilipokuwa nikicheza besiboli nilipata umaarufu na pesa, lakini mambo hayo hayakudumu. Hata hivyo, uhusiano wangu na Mungu, na undugu ambao nimo ndani yake vitadumu milele. Biblia inasema hivi: “Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:17) Sasa, ninampenda Yehova Mungu na watu wake kuliko kitu kingine chochote!