Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mema na Mabaya: Biblia​​—⁠Mwongozo Unaotegemeka

Mema na Mabaya: Biblia​​—⁠Mwongozo Unaotegemeka

Hatuwezi kuwa na uhakika kwamba maamuzi yetu yatakuwa na matokeo mazuri ikiwa tunategemea tu hisia zetu na za wengine. Biblia inatueleza sababu. Isitoshe, inatupatia mwongozo unaotegemeka kuhusu maadili na hilo linatuwezesha kuwa na maisha yenye furaha na yenye kuridhisha.

MWONGOZO TUNAOHITAJI

Katika Biblia, Yehova a Mungu anasema kwamba wanadamu wanahitaji mwongozo wake kwa sababu hawana uwezo wa kujiongoza. (Yeremia 10:23) Hiyo ndiyo sababu ametupatia mwongozo katika Biblia. Anawapenda wanadamu na hataki tufanye maamuzi mabaya yatakayotuumiza na kufanya maisha yetu yawe magumu. (Kumbukumbu la Torati 5:29; 1 Yohana 4:8) Zaidi ya hilo, yeye ni Muumba wetu na ana hekima na ujuzi unaohitajika ili kutupatia ushauri bora zaidi. (Zaburi 100:3; 104:24) Hata hivyo, Mungu hawalazimishi watu wafuate viwango vyake.

Yehova aliwapatia mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, kila kitu walichohitaji ili kuwa na furaha ya kweli. (Mwanzo 1:​28, 29; 2:​8, 15) Aliwapatia pia maagizo rahisi ambayo alitarajia wayatii. Hata hivyo, aliwaruhusu wajiamulie ikiwa watafuata maagizo hayo au la. (Mwanzo 2:​9, 16, 17) Kwa kuhuzunisha, Adamu na Hawa walichagua kufuata viwango vyao wenyewe badala ya viwango vya Mungu. (Mwanzo 3:6) Matokeo yalikuwaje? Je, wanadamu wamepata furaha kwa kujiamulia lililo jema au baya? Hapana. Historia ya wanadamu imethibitisha kwamba kupuuza viwango vya Mungu hakuleti amani na furaha ya kudumu.—Mhubiri 8:9.

Biblia inatupatia mwongozo tunaohitaji ili kufanya maamuzi yenye hekima licha ya malezi yetu. (2 Timotheo 3:​16, 17; ona sanduku “ Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote.”) Ona jinsi Biblia inavyofanya hivyo.

Jifunze kwa nini Biblia inastahili kuitwa “neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13. Tazama video Ni Nani Aliyeitunga Biblia? kwenye jw.org.

BIBLIA INAFUNUA MWONGOZO WA MUNGU

Biblia ina habari sahihi kuhusu jinsi ambavyo Yehova amekuwa akishughulika na wanadamu. Habari zilizomo zinatusaidia kuelewa mambo ambayo Mungu anaona kuwa mema au mabaya na mambo anayoona kuwa yenye kunufaisha au yenye madhara. (Zaburi 19:​7, 11) Isitoshe, katika Biblia tunaweza kujifunza kanuni ambazo zinatusaidia kufanya maamuzi yenye hekima maishani.

Kwa mfano, fikiria ushauri unaopatikana kwenye Methali 13:20: “Anayetembea na wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wapumbavu ataumia.” Maneno hayo ni ya kweli leo kama yalivyokuwa zamani pia. Biblia ina kanuni nyingi zinazotusaidia. —Ona sanduku “ Ushauri wa Biblia Usiopitwa na Wakati.”

Huenda ukajiuliza, ‘Ninawezaje kuwa na uhakika kwamba ushauri wa Biblia unaweza kunisaidia leo?’ Makala inayofuata itakuwa na mifano halisi maishani.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu.—Zaburi 83:18.